HOTUBA YA MHESHIMIWA DKT. PHILIP ISDOR MPANGO, MAKAMU WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI UFUNGUZI WA MAONESHO YA TATU YA SHIRIKA LA KUHUDUMIA VIWANDA
VIDOGO (SIDO) KITAIFA YANAYOFANYIKA KATIKA
UWANJA
WA UMOJA, WILAYA YA KASULU MKOANI
KIGOMA
22 SEPTEMBA, 2021
Mheshimiwa Dkt. Kitila A. Mkumbo, (Mb.), Waziri
wa Viwanda na Biashara;
Mheshimiwa Kamishna wa Polisi Thobias E. M. Andengenye, Mkuu wa Mkoa wa Kigoma na Mwenyeji wa Maonesho ya Mwaka huu;
Waheshimiwa Mawaziri mliopo;
Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile (Mb.), Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira;
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania!
1. Napenda nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema na fadhili kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kushiriki kwenye ufunguzi wa maonesho haya ya Shirika la kuhudumia Viwanda Vidogo (SIDO) yanayofanyika Kitaifa hapa Kasulu, katika Mkoa wetu wa Kigoma.
2. Pili, nichukukue fursa hii kukushukuru wewe binafsi Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo
(Mb.), Waziri wa Viwanda na Biashara pamoja na Uongozi wa SIDO kwa kunialika
katika ufunguzi wa maonesho haya. Pia, napenda kuwapongeza
waandaaji wote wa maonesho haya, hususan Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma na
timu yako, kwa kuratibu maandalizi haya. Napenda niwapongeze pia SIDO kwa
kubuni na kuanzisha utaratibu huu wa kuwa na maonesho ya SIDO Kitaifa. Vilevile, na kwa umuhimu wa pekee nawashukuru washiriki
wote, Wajasiriamali, Makampuni, Taasisi Binafsi na za Serikali kwa kushiriki kwenye
maonesho haya yaliyosheheni bidhaa za viwanda vyetu zinazozalishwa na Watanzania.
Ninawashukuru pia wadhamini wote wa
maonesho haya kwa jinsi walivyojitoa kuwezesha kufanikiwa kwa tukio hili muhimu
kwa maendeleo ya nchi yetu. Asante sana! kwa kutuunga mkono.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
3.
Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
imedhamiria kujenga uchumi shindani wa viwanda na kuifikisha nchi kwenye kipato
cha kati cha juu. Azma hii ya Uchumi wa
Viwanda, imeelezwa vizuri katika Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano
(2021/22-2025/26), ambapo Serikali imeazimia kuwa takribani asilimia 9 ya pato
la Taifa litokane na viwanda ifikapo mwaka 2025/26 ukilinganisha na asilimia
8.2 kwa mwaka 2020/21. Kwa upande wa ajira, Serikali imeweka lengo la asilimia 13
ya ajira yote itokane na viwanda ifikapo 2025/26 ukilinganisha na asilimia 6.7
kwa mwaka 2020/21. Mchango wa sekta ya viwanda katika mauzo ya nje (exports)
unakusudiwa ufikie asilimia 19 ukilinganisha na asilimia 17.1 ya sasa.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
4.
Nimefurahishwa
na Kaulimbiu ya Maonesho haya ya SIDO ya mwaka huu inayosema “Pamoja
Tujenge Viwanda Kwa Uchumi na Ajira Endelevu” Kaulimbiu hii, inalenga kutambua mchango wa
Sekta ya Viwanda hususan viwanda vidogo na vya kati katika kuchochea uzalishaji
kwenye Sekta mbalimbali za Kiuchumi ili kukuza biashara ya ndani na nje,
kuongeza ajira na hivyo kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa Taifa letu. Ni ukweli kuwa, ili tuweze kujenga uchumi
shindani, ni lazima tuwekeze katika ujenzi wa Viwanda vinavyotumia malighafi
zinazozalishwa hapa nchini. Pia, kufanya uwekezaji kwenye Sekta zinazochangia
upatikanaji wa malighafi hizo ikiwemo Sekta ya Kilimo. Tumekuwa na maneno
mazuri sana katika kupamba maonesho/maadhimisho mbalimbali lakini kiuhalisia
utekelezaji wake hauendani na yale tunayoyapanga ama kuyazungumza. Hivyo, natoa
rai kuwa kila maonesho yanapofanyika ni
vema itolewe tathmini ya utekelezaji wa kaulimbiu husika ya kipindi/mwaka
uliotangulia.
Ndugu Washiriki, Mabibi na
Mabwana;
5.
Maonesho ya viwanda vidogo na vya kati yana faida
na umuhimu wa pekee. Maonesho haya yanawawezesha wenye viwanda kupanua wigo wa
masoko ya bidhaa zao na hivyo kuongeza uzalishaji na kupelekea viwanda kukua.
Maonesho haya yanatoa fursa kwa wenye viwanda kubadilishana ujuzi na uzoefu na
hatimaye kuboresha bidhaa kulingana na mahitaji ya walaji na soko. Lakini pia maonesho ni fursa kwa
wajasiriamali na wananchi kujionea wenyewe mashine mbalimbali, vipuri na bidhaa
ambazo zinatengenezwa hapa nchini, wapi zinapatikana na kwa bei gani. Kwa sababu hizo nimefarijika
kuona mmefika kwa wingi katika maonesho haya. Hii inaashiria wazi kuwa mna nia
ya dhati ya kukuza masoko ya bidhaa zenu na kujifunza mambo mbalimbali kutoka
miongoni mwenu na kutoka kwa wataalamu wa Taasisi zilizoshiriki. Maonesho haya
yametudhihirishia kuwa si kweli kwamba kila kilicho bora lazima kiwe kimetoka
nje ya nchi yetu.
Ni imani yangu kuwa wajasiriamali wetu mtatumia fursa hii ya maonesho
kuzielewa na hatimaye kufanya juhudi kujipatia mashine/bidhaa zinazotengenezwa
hapa nchini.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
6.
Mara
tu nilipofika nimepata fursa ya kutembelea baadhi ya mabanda katika maonesho
haya. Nimefurahia sana kujionea wabunifu mbalimbali wa teknolojia zinazoweza
kutumika kwa uzalishaji viwandani.
Mathalani, nimeona wabunifu wanaojishughulisha na uzalishaji katika
mnyororo wa thamani wa mazao mbalimbali ya kilimo. Napenda kuchukua fursa hii kwa
niaba ya Serikali kuwatia moyo katika jitihada zenu. Ni matarajio yangu, kuwa SIDO
mtazidi kuwahamasisha na kutoa mafunzo kwa wananchi wengi zaidi ili kuwaongezea
uthubutu wa kuingia katika shughuli zinazotumia teknolojia rahisi na nafuu
hususan katika uzalishaji na uongezaji thamani wa mazao na bidhaa mbalimbali.
Hata hivyo, napenda kuwasisitiza mhakikishe
kuwa mashine, vipuri na bidhaa mnazozizalisha, ziwe zinakidhi viwango na hata
kushindana na zile zinazotoka nje lakini muhimu ziwe za gharama nafuu ili wale ambao
wanaoagiza mashine, vipuri na bidhaa za kutoka nje hivi sasa wavutiwe kununua zinazozalishwa
hapa hapa nchini.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
7.
Nimefurahi pia kuona bidhaa za mafuta ya kula
zikiwemo za mawese, alizeti na karanga pamoja na Asali kushamiri katika
maonesho haya. Kama nilivyosema hapo awali, nchi yetu inatumia fedha nyingi
kuagiza bidhaa kutoka nje. Kwa mfano, kutokana na upungufu wa uzalishaji wa
mafuta ya kula, nchi hutumia takribani shilingi bilioni 470 kwa mwaka kuagiza
mafuta ghafi. Natoa wito kwa wananchi kuungana na Serikali ya Awamu ya Sita
katika kuhakikisha tunaondokana na upungufu wa mafuta ya kula nchini haraka
iwezekanavyo kwa kuongeza uwekezaji katika kilimo na uchakataji wa mbegu za
mafuta. Nichukue fursa hii pia kuipongeza TARI na Uongozi wa Mkoa kwa ujumla kwa
uendelezaji wa mnyororo wa thamani wa zao la mchikichi. Natambua jitihada za TARI
kuwezesha kuzalisha mbegu za kisasa za michikichi 6,645,000 na tayari mbegu
4,410,000 zimeoteshwa na ekari 6,019 zimepandwa. Na katika hili, ninampongeza
sana Mheshimiwa Kassim M. Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa kuwa mstari wa mbele kuhamasisha kilimo cha michikichi katika mkoa
wetu wa Kigoma.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
8.
Madhumuni ya kuanzishwa kwa SIDO
kama yalivyopitishwa kwa sheria namba 28 ya Bunge ya mwaka 1973 bado yana
umuhimu wa pekee kwa maendeleo ya nchi.
Niwakumbushe tu, madhumuni hayo ni pamoja na:
(i)
Kushawishi, Kuhamasisha na Kusimamia
uanzishwaji wa Viwanda Vidogo nchini;
(ii)
Kuongeza thamani ya rasilimali
zilizoko nchini;
(iii)
Kuwezesha kutengeneza bidhaa za
kutosheleza mahitaji ya wananchi;
(iv)
Kuendeleza na kutumia teknolojia
rahisi inayopatikana nchini;
(v)
Kutoa kipaumbele kwa miradi ya uzalishaji inayotumia zaidi
nguvukazi; na
(vi)
Kutoa huduma kwa viwanda vidogo nchini.
9.
Pamoja na mafanikio kadhaa
yaliyoelezwa hapa ambayo SIDO wameyapata tangu kuanzishwa kwake takriban miaka
48 sasa, kwa maoni yangu mchango wa viwanda vidogo katika uchumi wa Taifa bado ni
mdogo! Bidhaa zinazotengenezwa na viwanda vidogo hazikidhi mahitaji ya wananchi
na baadhi kutokidhi viwango vya soko! Bado tunaagiza mashine ndogondogo, vipuri
na bidhaa nyingi kutoka nje ambapo kama SIDO wangejipanga vizuri naamini bidhaa
hizo zingekuwa zinatengenezwa hapa nchini na kukidhi mahitaji ya soko la ndani.
Napata shida sana ninapoona hata panga tunaagiza kutoka nje ya nchi! SIDO
mnakwama wapi? Tunazo taasisi nyingi za ufundi, utafiti na teknolojia kama DIT,
TEMDO, KMT nk mnakwama wapi? Hata vifungashio jamani kwa nini tunaendelea
kuagiza kutoka nje? Kwa nini tuendelee kuwatengenezea ajira nchi nyingine wakati
sisi tunazihitaji?
10.
Nimewakumbusha hapa madhumuni ya
kuanzishwa kwa SIDO, na nina hakika watanzania wangependa wajue madhumuni ya
kuanzishwa kwa SIDO yametekelezwa kwa kiwango gani na tuko wapi tangu
kuanzishwa kwa SIDO miaka 48 iliyopita na mwelekeo ni upi?. Kuna jitihada gani
za kuinua viwanda vidogo na kuviwezesha kuzalisha bidhaa zenye kiwango kinachokidhi
mahitaji ya soko la ndani na la nje?. Hivyo, ninaitaka Wizara ya Viwanda na
Biashara ifanye tathmini ya kweli (candid assessment) kuhusu SIDO imefanikiwa
ama imeshindwa kiasi gani katika kutekeleza malengo ya kuanzishwa kwake ili kuja
na mapendekezo ya mikakati mipya itakayopelekea Tanzania kuweza kukidhi
mahitaji ya uchumi wa kati ya mashine ndogo/za kati, vipuri, bidhaa, huduma n.k
katika karne ya 21. Waziri wa Viwanda na Biashara uhakikishe na usimamie
utekelezaji wa zoezi hilo na unipatie mrejesho kupitia kwa Waziri Mkuu.
11.
Ndugu Wananchi, Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana;
Uchumi wa Taifa letu
unategemea na utaendelea kutegemea kilimo kwa miaka mingi ijayo. Hivyo, SIDO na Taasisi nyingine zote (za Umma
na Binafsi) zinazojihusisha na maendeleo ya viwanda na teknolojia ya viwandani,
ninazitaka zifikirie na kuchukua hatua za dhati kuanzia sasa na kujiwekea
malengo ya kulinyanyua Taifa katika uchakataji wa mazao ya kilimo na kuongeza
thamani (agro-processing) kwa kutumia teknolojia rahisi, zikiwemo:
· Mashine za bei nafuu za kukamua na
kutakasa mafuta ya alizeti, mawese, ufuta, pamba, karanga, parachichi n.k;
· Mashine za kusaga nafaka na kuweka kwenye
mifuko, kutengeneza chakula cha samaki/mifugo/kuku n.k;
· Mashine za mkono za kuvuna nafaka/mazao au
kukamua maziwa hata chikichi na kuhifadhi maziwa/mazao;
·
Mashine
za kukata na kufunga majani/kukausha chakula bora cha mifugo; na
·
Mashine
za kutengeneza vifungashio, mizani nk.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
12.
Nafahamu kuwa kumekuwa na changamoto kubwa
ya kupata mitaji kwa ajili ya kuanzisha na kuendeleza viwanda vidogo. Wakati
natembelea mabanda nimeelezwa baadhi ya vikwazo vinavyopelekea wajasiliamali
hawa kushindwa kupata mikopo. Vikwazo hivyo ni pamoja na kukosa dhamana zinazokubalika
ambazo zimeandikishwa rasmi na kuwa na Hati. Vilevile, baadhi ya taasisi za
fedha zinakopesha lakini kwa riba kubwa mno ya asilimia 18 na hata zaidi. Ni
ukweli ulio wazi kuwa hatuwezi kushinda vita dhidi ya umaskini kama
wajasiriamali wadogo wanaendelea kukosa mitaji ya kukuza shughuli zao.
Utegemezi kwenye akiba zao wenyewe pekee hauwezi kuwawezesha kukuza uzalishaji
kwa kasi itakayo waongezea motisha ya faida kukua na hivyo kupanua biashara zao
zaidi na hata kuajiri wengine! Hali ilivyo sasa inawafanya wajasiliamali hawa
kubaki kwenye mzingo wa umaskini. “Biashara inakuwa ndogo kwa vile mtaji ni
mdogo, na mtaji ni mdogo kwa vile faida ni ndogo na akiba ni ndogo pia”!
13.
Napenda kutumia jukwaa hili kuzitaka Benki
na Taasisi nyingine za Kifedha kubuni namna bora zaidi ya kuwawezesha wananchi
wetu hawa. Aidha, ni muhimu pia huduma hizo ziende sambamba na kutoa elimu kwa
Wateja hasa kuhusu ubora wa miradi, usimamizi wa miradi na matumizi adili ya Mikopo
inayotolewa. Taasisi za Fedha mkiweka utaratibu mzuri wa kutoa Mikopo kwa
wajasiriamali wadogo na kwa riba nafuu wanaweza kabisa kuongeza uzalishaji, ajira
na Kupunguza Umaskini. Na kwa upande wa wajasiliamali wetu, hakikisheni kuwa
fedha zote mnazokopeshwa zinarejeshwa kwa wakati na kwa viwango mlivyokubaliana
na mabenki ili ziende tena kwenye mzunguko wa kukopa zaidi na kukopesha
wengine.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
14.
Nafahamu kuwa SIDO ina Mfuko wa Taifa
wa Kuendeleza Wajasiriamali (NEDF) na pia natambua uwepo wa SANVN Viwanda Scheme ambao ni mpango wa
kuwezesha wananchi kiuchumi ili wajasiriamali wadogo na wa kati kufikia
wajasiriamali wakubwa kwa kuwasaidia kupata elimu, ujuzi, taarifa, mtaji na
kuibua wajasiriamali wabunifu, kuwalea na kuwakuza wengine na kubwa zaidi
kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu. Pamoja na jitihada hizo za kuwa na
mifuko hiyo, bado kuna kazi ya kufanya kwa SIDO na hasa kutangaza fursa hizi
kwa wananchi na kuhakikisha mnailea na kuikuza mifuko hiyo ili kuweza kikidhi
mahitaji yaliyopo. Ongezeni wigo wa vyanzo vya fedha ili kutunisha mfuko wa NEDF.
15.
Nimefurahishwa sana na taarifa kuwa, SIDO inashirikiana na Benki ya CRDB kutoa
mikopo kwa viwanda vinavyochakata mazao na pia Mfuko wa NSSF kupitia SANVN
Viwanda scheme nao wanatoa huduma mbalimbali za kuwawezesha wajasiliamali wetu.
Huu ni mfano mzuri na wa kuigwa kwa Taasisi zetu za fedha kushiriki moja kwa
moja kuunga mkono juhudi za Serikali za kuongeza ajira na kupunguza umaskini
kwa wanachi wetu. Nitumie fursa hii kuziomba taasisi nyingine za fedha kujitokeza
na kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuwawezesha wajasiliamali wadogo.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
16.
Ninapokaribia kuhitimisha hotuba yangu, napenda
kuwaelekeza Wizara ya Viwanda na Biashara na SIDO watumie Balozi zetu nje ya nchi katika kupata teknolojia rafiki,
mitaji na fursa ya kujifunza namna wenzetu wanavyosimamia taasisi inayofanana
na SIDO yetu pamoja na kutafuta masoko. Zipo nchi nyingi sana ambazo wameweza
kutumia vizuri viwanda
vidogo katika kukuza ajira na kuchangia kikamilifu katika ukuaji wa uchumi.
Tujifunze kutoka huko wamewezaje! Mfano
nchi ya China asilimia 90 ya viwanda vyake ni viwanda vidogo na vya kati
ambavyo kwa wastani vinachangia asilimia 60 kwenye Pato la Taifa (GDP) na
asimia 80 ya ajira. Kwa upande wa India, Viwanda vidogo na vya kati vinachangia
asilimia 95 ya pato la Taifa na asilimia 45 ya mauzo nje; na kwa upande wa Balozi zetu, kupitia Wizara
ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ninawaelekeza kuhakikisha
kwamba utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi una lenga pia katika kukuza na
kuendeleza viwanda vidogo na vya kati hapa nchini kwa kutoa kipaumbele katika:
(i) Kuvutia
uwekezaji wa viwanda vidogo na vya kati;
(ii) Kuratibu
upatikanaji wa teknolojia zinazofaa
katika mazingira ya nchi yetu na masoko ya bidhaa za Viwanda vidogo;
(iii) Kuratibu
upatikanaji wa mitaji kutoka kweye mifuko au taasisi zinazofanya hivyo katika
maeneo yenu ya uwakilishi hususan taasisi zinazotoa mikopo nafuu kwa SMEs;
(iv) Kuiunganisha
Sekta ya Viwanda Vidogo na Biashara Ndogo (SMEs) na zile za nje kwa madhumuni
ya kubadilishana uzoefu na taarifa za masoko pamoja na kuziwezesha kuingia
makubaliano ya ushirikiano (MOU) katika masuala mbalimbali ikiwa ni pamoja na
teknoligia na ubunifu; na
(v) Kuiunganisha
Sekta ya Viwanda Vidogo na Biashara Ndogo na taasisi zinazotoa elimu na kujenga
uwezo kwa ajili ya SMEs zetu kuuza katika masoko ya kimataifa kwa kujua
taratibu na kanuni za masoko hayo.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
17.
Kwa upande wa Serikali napenda niwahakikishie
kuwa tutaendelea kuboresha mazingira ya Biashara na uwekezaji ili bidhaa
zinazozalishwa na viwanda vidogo nchini ziweze kuwa na bei nafuu na kupanua
soko lake ili kukuza viwanda vya ndani. Aidha, Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea
kusimamia agizo la utengaji maeneo ya viwanda katika kila Halmashauri ya Wilaya
ili kuongeza ufanisi wa viwanda vyetu kuzalisha katika mazingira bora. Serikali imeweka kipaumbele katika kutekeleza
miradi ya kimkakati ya kuhakikisha tunakuwa na nishati ya uhakika ikiwa ni
pamoja na Mradi wa Bwawa la kufua umeme wa maji la Mwalimu Nyerere mto Rufiji,
mradi wa kuunganisha mikoa yote na Grid ya Taifa na mradi wa kuvipatia vijiji
vyote umeme ifikapo 2025. Ninawaagiza wakuu wote wa mikoa kupitia Kamati za
Maendeleo za mikoa kujiwekea malengo ya kuongeza viwanda vidogo kila Wilaya
hususan vinavyochakata mazao ya kilimo. Aidha, ninazitaka Wizara za Kilimo,
Viwanda na Biashara, Elimu, Teknolojia & Mafunzo ya Ufundi na Wizara ya
Fedha na Mipango kutoa kipaumbele kwa utafiti na maendeleo (R & D) katika
sekta hii muhimu.
Ndugu Wananchi, Wageni Waalikwa, Mabibi
na Mabwana;
18.
Nimalizie hotuba yangu kwa kuwapongeza tena
Viongozi, Washiriki, Wafadhili mbalimbali na wenyeji wetu wananchi wa Mkoa wa
Kigoma na hususan wa hapa Kasulu waliotukaribisha na wale wote walioshiriki kwa
namna moja au nyingine kufanikisha maonesho haya. Aidha, niwasihi watanzania
wenzangu kuwa tuthamini na kupenda bidhaa zinazozalishwa hapa nchini kwani zina
ubora na viwango vinavyostahili.
Waswahili wanasema “Kipende chako”.
19.
Baada
ya kusema hayo, kwa heshima na taadhima,
natamka kuwa maonesho
haya ya Tatu ya SIDO Kitaifa hapa Kasulu, Mkoani Kigoma yenye kaulimbiu “Pamoja
Tujenge Viwanda kwa Uchumi na Ajira Endelevu” yamefunguliwa rasmi leo
tarehe 22/09/2021”
KIGOMA OYEE! KASULU OYEE!
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, KAZI IENDELEE
MUNGU
AWABARIKI, ASANTENI KWA KUNISIKILIZA
No comments:
Post a Comment