Habari za Punde

Serikali yafanya maamuzi magumu kuziuza Meli zote za shirika la Meli la Zanzibar - Dk Mwinyi

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Wananchi wa Wilaya ya Mkoani baada ya kuzindua Boti za Wananchi wa Visiwa vya Kisiwapanza na Makoongwe kwa ajili ya kuvukia. 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, amesema kuwa Serikali imeamua kuchukua maamuzi magumu ya kuziuza meli zote za Shirika la Meli la  Zanzibar kutokana na gharama kubwa za uendeshaji.

Akitoa hotuba yake katika majumuisho ya ziara yake kwa mikoa miwili ya Pemba, yaliyofanyika katika ukumbi wa kiwanja cha kufurahishia watoto Gombani, Chake Chake Pemba, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa uamuzi huo umekuja kutokana na gharama kubwa za uendeshaji wa meli hizo za Serikali.

Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa meli hizo za Serikali zilizo chini ya Shirika la Meli la Zanzibar zitauzwa kwa lengo la kununua meli ambazo hazitokuwa na gharama kubwa za uendeshaji.

Aidha, Rais DK. Mwinyi alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itachukua juhudi za makusudi katika kuhakikisha inaimarisha uchumi wake ikiwa ni pamoja na kuendelea kuliimarisha na kulipa hadhi yake zao la karafuu.

Akizungumzia juu ya suala la udhalilishaji, Rais Dk. Mwinyi alitilia mkazo kwamba wale wote wanaotenda vitendo hivyo waendelee kutopewa dhamana na hata mahabusu ikijaa basi wapelekwe katika vyuo vya mafunzo wakisubiri kesi zao.

Pamoja na hayo, aliwataka viongozi wa Mikoa na Wilaya kusikiliza kesi za wananchi waliodhulumiwa haki zao huku akisisitiza kwamba watumishi wote ambao hawawajibiki ataendelea kuwachukulia hatua wakiwemo wale wabadhirifu na wezi wa mali za umma ataendelea kwuafukuza.

Mapema asubuhi akizungumza na wanannchi wa Wilaya ya Mkoani  mara baada ya hafla ya kukabidhi boti kwa ajili ya wananchi wa Kisiwa cha Makongwe na Kisiwapanza alisema kuwa Serikali itafanya juu chini kuweza kuwaletea maendeleo wananchi kama ilivyowaahidi wakati wanapita kwa wananchi kuomba ridhaa ya kuchaguliwa na kuwa tena Madarakani.

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa anatambuwa kikwazo kikubwa cha maendeleo katika kipindi kilichopita ni kukosekana  umoja wa wananchi na mshikamano na ndio Serikali ya awamu ya nane imetengeneza serikali ya Umoja wa kitaifa ikiwa na lengo la kuleta amani na umoja utakaokuza maendeleo ya haraka.

Alifahamisha kuwa ni jambo la kushukuru kuwa nchi kwa sasa imetulia ina amani na hakuna sababu kusipatikane maendeleo na aliwapongeza wananchi kwa kuunga mkono juhudi hizo zilizochukuliwa na viongozi wao.

Aliongeza kuwa hatua aliyoichukua ya kuwakabidhi  boti za kusafiria  wananchi wanaoishi ndani ya visiwa vidogo ndogo vilivyoko  Pemba ni kutokana na kuwa na haja ya kusaidiwa ili waweze kupata vivuko vya uhakika badala ya kutumia vivuko visivyo na uhakika vyenye kuhatarisha maisha yao.

Alieleza vivuko hivyo viwili amevikabidhi katika bandari hiyo kwa niaba ya visiwa vyengine vitano (5) vya Zanzibar, ni wazi kuwa wananchi hao wanaoishi visiwani watapata usafiri wa uhakika  na kuwaomba  wavitunze  vizuri ili vitowe huduma kwa wananchi  mbali mbali .

Akizungumzia uimarishaji wa Bandari ya Mkoani alitowa agizo kuwa wakati umefika wa kuziimarisha Bandari zote hapa Zanzibar na hakuna sababu kwa meli zinatoka Mombasa zikateremshe bidhaa Unguja  na ndipo ziende  Pemba.

Hata hivyo, alisema hakuna sababu meli kutoka Dar-es-Salaam zikateremshe mzigo Unguja na  ndipo ziende kisiwani  Pemba hali ambayo inaongeza gharama ya usafirishaji  na inapelekea  bidhaa Pemba kuwa ghali.

Dk. Mwinyi alieleza kuwa ameliagiza mamlaka ya  Bandari sasa waanze kuweka mtaji wao (fedha ) ili Bandari hizi ziweze kupokea meli kutoka nje moja kwa moja na kuna habari  njema kuwa kuna meli kadhaa zimeshaonesha nia yakuzileta moja kwa moja kutoka Dar-es-salaam na Mombasa mpaka Bandari ya Mkoani Pemba.

Sambamba na hayo Dk. Mwinyi alisema, kuna kila sababu sasa ya kuweka mazingiza ya kusubiria usafiri abiria kuwa bora zaidi kwani faida tayari imeweza kupatikana baada ya kufunga mianya ambayo imekua ikipoteza fedha hivyo, aliitaka Wizara ya bandari kuzitumia fedha hizo kwa matengenezo ya bandari zote ikiwemo Mkoani na Wete.

Wakati huo huo, Dk. Mwinyi alitembelea hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani na kuwapongeza Madaktari wa kichina wanaomaliza muda wao kwa vile wanatowa huduma katika hiyo na kusema mchango wao ni mkubwa unathaminiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwani kuna baadhi ya huduma bila ya mchango wao zengeyumba.

Aidha Dk, Mwinyi aliwapongeza wafadhili waliotowa misaada ya vifaa mbali mbali kwa ajili ya Hospitali ya Abdalla Mzee, Mkoani akiwemo Said Bopar na kusema kuwa misaada hiyo  ni muhimu sana.

Aidha,  alimpongeza na kumshukuru Mwakilishi wa Jimbo la Mkoani Mhe.Abdalla Hussein Kombo kwa kukabidhi gari la kubebea wagonjwa katika Hospitali hiyo ya Abdalla Mzee Mkoani na kuisaidia Serikali yake kwani kwa Hospitali kama hiyo ni muhimu kuwa na gari ya aina hiyo.

Dk, Mwinyi aliwashukuru wafanyakazi wa Hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani kwa kufanya kazi katika mazingira magumu na kusema amesikia matatizo mbali mbali wanayokabiliana nayo kutoka kwa mganga  mkuu wa Hospitali hiyo Dk, Haji Mwita.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi leo aliungana na waumini wa Dini ya Kiislamu katika Msikiti wa Ibadhi, Mkanjuni Chake Chake Pemba katika sala ya Ijumaa na kusisitiza suala zima la amani, umoja na mshikamano wakati akitoa salamu kw awaumini hao.

Rais Dk. Mwinyi amemaliza ziara yake ya siku tano kisiwani Pemba na kurudi Unguja ambapo katika ziara hiyo alifutana na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serrikali akiwemo Mama Mariam Mwinyi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.