Habari za Punde

Hafla ya kuwapongeza watumishi waliostaafu OMKR

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Dkt Omar D. Shajak akimkabidhi Bw Ali Omar Ali, Jokofu kufuatia utumishi uliotukuka kwa kusimamia vyema kazi za ulinzi katika taasisi tofauti hadi anastaafu kwenye Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais – Zanzibar
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Dkt Omar D. Shajak akimkabidhi Bw Ali Omar Ali cheti cha shukurani kufuatia utumishi uliotukuka kwa kusimamia vyema kazi za ulinzi katika taasisi tofauti hadi anastaafu kwenye Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais – Zanzibar 
 


Na Raya Hamad - OMKR                                                                                                                                                               

Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar Dkt Omar D. Shajak amesema kila mtumishi ni muhimu katika nafasi yake aliyoajiriwa hivyo ni wajibu wake kuwajibika ipasavyo na kuwa muadilifu ili wakati wa kustaafu ukifika awache alama nzuri ya utendaji

Dkt Shajak ameeleza hao wakati wa hafla ya kuwapongeza, kuwashukuru na kuwaaga watumishi wawili wa kada ya ulinzi wa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais ambao ni Bw Ali Omar Ali na Bw Silima Khamis Machano iliyofanyika kwenye ukumbi wa mkutano migombani

Amesema kuwa kila anaeajiriwa lazima afahamu kuwa ipo na siku ya kustaafu hivyo ni vyema watendaji na watumishi wengine kuiga mema na mazuri yaliyoachwa na wastaafu hao kwa kujifunza uadilifu, uwajibikaji katika kutekeleza majukumu yao pamoja na kuwatakiwa afya njema

Akitoa wasia kwa wastaafu hao Dkt Shajak amewakumbusha kuwa kuvunjika kwa koleo sio mwisho wa uhunzi bali maisha yaendelee wakati wakiwa uraiani pamoja na kuthamini na kuitunza zawadi waliopewa ili iwe ni ushuhuda na kumbukumbu nzuri ya maisha kutokana na mchango wao walioutoa katika Utumishi.

Akisoma risala kwa niaba ya wafanyakazi wa Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Bi Fatma Mohamed amesema mfanyakazi sehemu kubwa ya maisha yake yapo kazini kwa wafanyakazi wenziwe hivyo subira, mashirikiano na upendo waliouonesha wastaafu hao umepelekea kuwaaga wakiwa na furaha.

“Kwa kweli kuagana nao ni huzuni kubwa na majonzi kwetu, kwani tayari tulikuwa tumejenga familia iliyokuwa na upendo na ushirikiano wa kutosha inayoitwa Familia ya Ofisi wa Makamu wa Kwanza wa Rais”alitilia mkazo

Mkurugenzi Uendeshaji na Utumishi Ndg. Juma Ali Simai amesema utaratibu wa kuwaaga wafanyakazi wastaafu ni takwa la kikanuni na kisheria ambapo kanuni ya 132 inaelezea kuwaandaa kwa kuwapa mafunzo maalum kabla ya kustaafu na kuwaaga wakati wa wastaafu pale inapobidi

Nae Bw Ali Omar Ali kwa niaba ya mwenzake ameushukuru uongozi wote wa Ofisi pamoja na Serikali kwa ujumla kwa kuwalea hadi kufikia muda wa kustaafu, amesema kwenye utendaji kazi lazima utangulize subira, kuithamini na kupenda  kazi yako na kutekeleza vyema majukumu ndipo utaweza kufurahia maendeleo ya kazi yako.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.