Habari za Punde

TAARIFA MAALUM YA MHESHIMIWA MUDRIK RAMADHAN SORAGA WAZIRI WA NCHI, AFISI YA RAIS KAZI, UCHUMI NA UWEKEZAJI YA KUADHIMISHA SIKU YA KIMATAIFA YA USALAMA NA AFYA KAZINI TAREHE 28 APRIL 2022

Ndugu Wananchi, Mabibi na Mabwana.                                              

Asalam Alaykum

Awali ya yote tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaaliya afya njema na kutuwezesha kuifikia siku hii ya leo tarehe 28 April 2022, ambayo ni siku ya Maadhimisho ya Kimataifa Usalama na Afya Kazini.

Ndugu Wananchi,   Siku hii imewekwa maalum na Shirika la Kazi Duniani (ILO) ili kuhamasisha ukingaji wa ajali na maradhi yatokanayo na sehemu za kazi, duniani kote. Nia hasa ni kwa Waajiri, Wafanyakazi na Serikali, kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa usalama na afya na mabadiliko yanayotokea katika sehemu za kazi.

Ndugu Wananchi, kila mfanyakazi anatakiwa kuwa salama na mwenye afya njema kimwili na kiakili kwenye  sehemu yake ya kazi kwa muda wote anapokuwepo kazini.

Hivyo mazingira ya kazi yanapokuwa hatarishi kwa usalama au afya humfanya mfanyakazi kuwa dhaifu. Hali hii inapotokea humuathiri mfanyakazi mwenyewe kiusalama na kiafya, na hushindwa kutoa huduma inavyotakiwa. Jamii inashauriwa kujenga utamaduni wa kutunza   mazingira ya kazi yasiharibike na kuleta madhara.

Ndugu Wananchi, ukuwaji wa sayansi na teknolojia unaonekana kurahisisha uzalishaji na utoaji huduma kwa upande mmoja, lakini kwa upande mwengine umeleta changamoto nyingi zinazohatarisha usalama na afya za wafanyakazi.      

 

Changamoto kubwa zaidi ni madhara ya kiafya yanayoweza kuonekena mara moja na yale yanayochukua miaka mingi kujulikana.

Ndugu Wananchi, Kauli Mbiu ya Siku ya Kimataifa ya Usalama na Afya Kazini kwa mwaka huu 2022 ni “Act Together to Build a Positive Safety and Health Culture” yaani “Tushiriki Pamoja Katika Kujenga Utamaduni Chanya wa Usalama na Afya kazini.

Kaulimbiu hii inalenga kuweka mikakati ya kuimarisha mifumo ya kitaifa ya usalama na afya (OSH) ili kujenga uimara wa kukabiliana na hatari zilizopo   na zinazoweza kutokea kwa  siku zijazo, kama ambavyo tulivyojifunza na kupata uzoefu   kutokana na  Janga la UVIKO-19.

Janga hili limegusa karibu kila sehemu ya ulimwengu wa kazi, kutoka hatari ya kuambukiza virusi katika maeneo ya kazi, hadi hatari za usalama na afya kazini  ambazo zimeibuka kama matokeo ya hatua zilizochukuliwa za kupunguza kuenea kwa virusi.  

Ndugu Wananchi,

Usalama na afya kazini ni muhimu   kimaadili, kisheria na kiuchumi. Taasisi zote ziwe za umma au binafsi zina  wajibu wa kuhakikisha kwamba, wanawatunza wafanyakazi na mtu mwingine yeyote ambaye anaweza kuathiriwa na sehemu zinazofanyiwa kazi, wanabaki salama wakati wote.

Wajibu wa kimaadili utahusisha ulinzi wa maisha na afya ya mfanyakazi. Hatua za kisheria za usimamizi wa Usalama na Afya pahali pa kazi ziimarishwe na zizingatie  kuzuia,   kuadhibu na  kufidia ili kuhakikisha zinalinda usalama na afya ya mfanyakazi.

 

Hii itamsaidia kila muhusika kujua haki na wajibu wake na taathira inayoweza kutokea pale taratibu za Usalama na Afya Kazini zitakapokiukwa.

Ndugu Wananchi, Afisi ya Raisi, Kazi, Uchumi na Uwekezaji   itaendelea kushirikiana na  wadau wengine wanaohusika na masuala ya kazi Kimataifa na Kitaifa  kuhakikisha matatizo yanayowakabili wafanyakazi kwenye sekta zote za kiuchumi yanapewa umuhimu unaostahiki.

Usimamizi wa masuala haya unaweza kufikiwa kwa kushirikiana pamoja kukuza utamaduni wa kuimarisha viwango vya usalama na afya kazini ili tupate  mazingira ya kazi yaliyo salama, na kukuza ajira zenye staha.  

Napenda kuchukua fursa hii, kuwaomba viongozi wa Taasisi zote za kazi za umma na binafsi, kushirikiana na Serikali kuweka mfumo mzuri wa utawala wa usalama na afya kazini. Tuweke rasilimali za kutosha katika mipango kazi yetu ili kukinga ajali na maradhi kwenye maeneo yetu ya kazi kwa kuzingatia kwamba muda mwingi wa wananchi wetu unatumika kazini.

Hivyo, tuwashirikishe wafanyakazi wenyewe katika kufanya tathmini za hatari zinazowakabili katika kazi zao, utoaji wa taarifa za hatari na katika  kupanga hatua madhubuti za   kukabiliana na hatari hizo, bila ya kuacha kuwapatia elimu ya kutosha juu ya namna bora ya kujikinga na ajali na maafa mbalimbali yanayoweza kutokea wakiwa kazini   pamoja na athari za kiafya zinazohusishwa na  kazi wanazozifanya.

Ndugu Wananchi, Afisi ya Raisi, Kazi, Uchumi na Uwekezaji    inaungana na Jamii ya Kimataifa kuadhimisha siku hii inayoadhimishwa kila ifikapo tarehe 28 Aprili kwa kusimama imara kuendelea kupambana na ajira mbaya   katika maeneo ambayo bado suala la kuwalinda wafanyakazi   na hatari za usalama na afya, halipewi umuhimu   kwa ustawi wa maisha yao, familia zao na nchi kwa jumla kiuchumi na kijamii ili kufikia malengo   yaliyokusudiwa.

Utekelezaji wa Kauli mbiu ya mwaka huu, utaleta   mafanikio   na tija katika kutekeleza Sera ya Uchumi wa Buluu, ambayo katika utekelezaji wake tunaweza kupata changamoto nyingi za kiusalama na kiafya.

Hivyo, kwa pamoja tunahitaji kuwa na mikakati na mipango madhubuti katika kujenga utamaduni wa usalama na afya kazini Kuepuka ajali na maradhi katika maeneo ya kazi, ikiwa ni sehemu ya kuengeza mapato kwa wafanyakazi, Waajiri na  Serikali kwa jumla.

Ahsanteni kwa kunisikiliza.     

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.