Habari za Punde

Serikali yaandaa mwongozo wa biashara ya hewa ya ukaa

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo wakati akijibu swali Bungeni.

Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais inaandaa mwongozo wa Kitaifa wa Biashara ya Hewa Ukaa utakaotumiwa na wawekezaji, taasisi na watu binafsi wenye nia kufanya biashara hii hapa nchini.                                                                                        

Hayo yamesemwa leo bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo wakati akijibu swali la Mbunge wa Kilolo Mhe. Justine Nyamoga aliyetaka kufahamu mpango wa Serikali wa kuomba fedha katika mifuko ya kupunguza hewa ukaa duniani na kuwalipa wananchi wanaopanda na kutunza misitu katika Wilaya ya Kilolo.

Dkt. Jafo alisema hewa ukaa ni moja ya gesijoto ambazo mrundikano wake angani husababisha mabadiliko ya tabianchi na moja ya njia zinazotumika kupunguza hewa hiyo chini ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi ni misitu ambayo hunyonya hewa ukaa wakati mimea inapotengeneza chakula.

Alifafanua kuwa Mkataba huo hauna Mfuko mahsusi wa kulipa miradi ya hifadhi ya misitu inayotekelezwa katika nchi wanachama zinazoendelea kwa ajili ya kupunguza hewa ukaa. Badala yake, Mkataba huo umeweka utaratibu wa kibiashara ambapo makampuni kutoka nchi zilizoendelea ambazo zinawajibika chini ya Mkataba huo kupunguza gesijoto hulipa miradi ya kupunguza hewa ukaa kupitia hifadhi ya misitu katika nchi zinazoendelea.

Alitolea mfano wa kampuni kutoka nchi zilizoendelea ni Carbon Tanzania kutoka Uingereza ambayo hugharamia miradi ya MKUHUMI katika mikoa ya Manyara na Katavi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.