Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi Ameipongeza Timu ya Taifa ya U-17 ya Serengeti Girls kwa Kufuzu Fainali Kombe la Dunia.

 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameipongeza timu ya taifa ya wanawake chini ya miaka 17 “Serengeti Girls”, kwa kufuzu kucheza michuano ya Kombe la Dunia itakayofanyika Oktoba mwaka huu huko nchini India.

Katika salamu hizo za pongezi, Rais Dk. Mwinyi alieleza kufurahishwa na juhudi kubwa zilizochukuliwa na timu hiyo tokea yalipoanza mashidano hayo hadi kufuzu kucheza michuano ya Kombe la Dunia itakayofanyika huko nchini India.

Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara yake husika ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo chini ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF) itaendelea kuiunga mkono timu hiyo katika kuhakikisha inaendelea kufanya vizuri kwa kupata ushindi zaidi katika mashindano yajayo.

Alieleza kwamba hiyo ni faraja kubwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweka historia ya timu ya vijana ya wanawake walio chini ya umri wa miaka 17 “Serengeti Girls”, kufuzu kucheza michuano hiyo ya Dunia.

Aliongeza kuwa hatua hiyo itaendelea kulijengea sifa Taifa na kuendelea kuitangaza Tanzania kimichezo na kiutalii duniani kote hasa ikizingatiwa kwamba mashindano hayo yanaendelea kupata washabiki wengi zaidi na kuendela kupendwa duniani.

“Naipongeza sana timu yetu ya “Serengeti Girls” kwa kuweza kufuzu kucheza michuano ya Kombe la Dunia itakayofanyika Oktoba mwaka huu huko nchini India, tunaitakia kila la kheria na matarajio yetu kwamba itaendelea kufanya vizuri katika mashindano hayo na sisi tutaendelea kuiunga mkono na kuiombea dua timu yetu hii”, alisema Dk. Mwinyi.

Hivyo, timu hiyo ya Tanzania imeungana na Morocco na Nigeria kuiwakilisha Afrika na kukamilisha idadi ya timu 16 zitakazoshiriki fainali hizo za Dunia kati ya Oktoba 11-30 mwaka huu katika miji mitatu nchini India zikiwa fainali za saba tangu michuano hiyo ilipoasisiwa mnamo mwaka 2008.

Hii ni mara ya kwanza kwa Tanzania kufuzu fainali hizo kwa timu ya soka ambapo mpaka timu hiyo ya “Serengeti Girls” inafuzu mashindano hayo ilizing’oa Botswana, Burundi na kumalizia kwa kuitoa Cameroon baada ya kuibuka na ushindi wa jumla wa mabao 5-1 dhidi ya nchi hiyo.

Katika kuonesha ushirikiano kati ya ZFF na TFF kwa kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo ya Zanzibar timu hiyo ya “Serengeti Girls” iliweza kufunga kambi yake hapa Zanzibar kwa takriban wiki mbili ikijiandaa katika mashindano hayo pamoja na kucheza mchezo wa marudiano katika uwanja wa Amaan Zanzibar kati yake na Cameroon ambao ulimaliza kwa kutoka sare ya mabao 1-1 huku wa awali uliochezwa nchini Cameroon “Serengeti Gilrs” ilimaliza kwa mabao 4-1.

Imetayarishwa na Idara ya Mawasiliano,

Ikulu Zanzibar. OF RESPONSIBILITY

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.