Habari za Punde

Vijana Watakiwa Kuzitumia Fursa Zilizopo na Zitakazotolewa na Serikali na Wadau wa Maendeleo - Dk.Hussein

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akikabidhiwa zawadi maalum na Mkurugenzi Mkaazi wa USAID Nchini Tanzania Bi. Kate Somvongsiri na (kushoto kwake) Naibu Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Taasisi ya T-Marc Bw.Alex Mgongolwa, wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Mradi wa Kijana Nahodha Tanzania, uliozinduliwa viwanja vya mpira Maisara Suleiman Wilaya ya Mjini Unguja leo 22-2-2023.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amewataka vijana kuzitumia fursa  zilizopo na zitakazoletwa na Serikali na Wadau mbalimbali wa Maendeleo kwa ajili ya Maendeleo na Ustawi wao na Taifa kwa ujumla.

Alisema vijana ni nguvu kazi kwa taifa lolote duniani, ambayo inahitaji kuandaliwa vema kwa faida za baadae.

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo huko Maisara Wilaya ya Mjini, Mkoa wa Mjini Magharibi alipozungumza na vijana wa makundi tofauti kwenye uzinduzi wa mradi wa “Kijana Nahodha” unaofadhiliwa na Shirika la USAID la Marekani.

Alisema mradi huo unaunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hasa kwenye utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya kitaifa ikiwemo dira ya 2050, mpango wa taifa wa maendeleo 2026 na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2020 -2025.

Alisema kundi kubwa la vijana duniani kote limekuwa likikabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo ukosefu wa ajira, matumizi ya dawa za kulevya, mimba na ndoa za umri mdogo, UKIMWI, Afya ya Akili, ukatili na udhalilishaji wa kijinsia pamoja na matumizi mabaya ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA).

Dk. Mwinyi alizitaka Wizara zote zinazoguswa na mradi huo kushiriki na kufuatilia kwa karibu utekelezaji wake ili kufikia malengo yaliyokusudiwa kwa kuwaandaa na kuwasimamia vijana kuhakikisha shughuli watakazozianzisha zinakua endelevu hata baada ya kukamilika Mradi.

Akizungumzia mabaraza ya vijana Dk. Mwinyi alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inasimamia uendeshaji wa Baraza la Vijana la Zanzibar kuanzia ngazi ya Shehia hadi taifa pia alisema baraza hili ni chombo kinachowaunganisha vijana nchini ili kupaza sauti zao kwenye masuala mbalimbali yanayohusu maslahi yao pamoja na kuchochea maendeleo ya jamii.

Alieleza mabaraza hayo yamechangia kuanzishwa vituo vya mafunzo ya vijana maeneo ya Bweleo na Pangeni kwa Unguja na Weni na Mjini Ole kwa Pemba kwa kuwaandaa vijana kupata maarifa na  umahiri wa kukabiliana na changamoto kwenye makuzi yao.

Akizungumzia fedha za  ahueni ya Uviko isiyo na riba, Rais Dk. Mwinyi alieleza Serikali ilitoa fedha hiyo kwaajili ya mikopo ya kuwawezesha wananchi kiuchumi, kujenga vituo maalumu vya wajasiriamali kwa kila Wilaya pamoja na kuwapatia wananchi vifaa vya uvuvi zikiwemo boti na vifaa vyengine vya uvuvi wa kisasa, vifaa kwa wakulima wa mwani kwa vijana na kinamama. Alisema Serikali imeongeza uwekezaji wa miradi mbalimbali ikiwemo ya binafsi, uimarishaji wa shughuli za uchumi wa buluu ikiwemo kuendeleza sekta ya utalii, kukuza uchumi wa nchi na kuongeza fursa za ajira ambazo vijana ni miongoni mwa walengwa wakuu.

Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Tabia Maulid Mwita aliwaomba wadau wa maendeleo kuendelea kuiungamkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuwekeza zaidi kwenye miradi inayowahusisha vijana ili kuwakomboa na changamoto zinazowakabili ikiwemo ukosefu wa ajira wapate kujitegemea.

Naye, Mkuu wa Mradi wa Kijana Nahodha, Dk. Tuhuma Tuli alieleza mradi ni sekta mtambuka amabao utahusisha ajira kwenye sekta za elimu, kilimo, utawala bora na afya kwa unalengo la kuwajengea uwezo vijana wenye umri kati ya miaka 15-25.

Alisema mradi pia imelenga kuwajengea uwezo vijana, kuwasaidia upatikanaji ubora wa stadi mbalimbali ikiwemo mafunzo ya ufundi, kuboresha uelewa wa afya ya akili kupitia zana za elimu ya kidijitali zinazoongozwa na watu binafsi na kuimarisha njia za wazi za mawasiliano kati ya vijana na serikali ili kuinua sauti za vijana katika maisha ya kiraia, siasa, na utungaji sera.

Kwa upande wake Mkururgenzi Mkazi wa USAID, Kate Somvongsiri alisema, kupitia mradi wa Kijana Nahodha, vijana watakuwa na uwezo wa kujifunza masuala mbalimbali, kuongeza maarifa na stadi za kuendesha biashara, misaada kutoka kwa familia zao, jamii, na serikali ili wapate fursa kupitia elimu.

Mradi wa Kijana Nahodha wenye kaulimbiu “Kijana Nahodha mpango mzima”. Unatarajia kuwafikia vijana 45,000 kwa Tanzania nzima ambapo kwa Zanzibar unatarajiwa kuwafikia vijana 15,000 Unguja na Pemba.

IDARA YA MAWASILIANO  IKULU, ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.