Mhandisi Goodluck Rulagora kutoka Chuo cha Uvuvi Bagamoyo (FETA) akitoa ufafanuzi kuhusu matumizi ya vipimo sahihi vya kemikali vinavyotumika katika vifaa mbalimbali ikiwemo mitungi ya gesi kwa mawakala wa forodha wakati wa mafunzo ya siku. Mafunzo hayo yanaendeshwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.
Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya siku ya mbili kwa Mawakala wa Forodha wanaohusika na udhibiti na usimamizi wa kemikali na vifaa vya kemikali vinavyomong’onyoa tabaka la ozoni. Mafunzo hayo yanafanyika katika Ukumbi wa Taasisi za Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) Jijini Dar es Salaam. Mafunzo hayo yanaendeshwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.
Serikali
imewataka mawakala wa forodha wanaoandaa nyaraka za kuingizia nchini na kupokea
mizigo ikiwemo kemikali zinazodhibitiwa kuzingatia ukomo wa matumizi wa
kemikali hizo zinazochangia mmong’onyo wa tabaka la
ozoni na kusababisha mabadiliko ya tabia nchi.
Wito
huo umetolewa Machi 1, 2023) jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Msaidizi Idara
ya Mazingira, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Catherine Bamwenzaki wakati akifungua
mafunzo kwa mawakala wa forodha kuhusu udhibiti na usimamizi wa kemikali na
vifaa vya kemikali vinavyomong’onyoa tabaka la ozoni.
Amebainisha
kuwa kemikali au gesi zinazotumika katika mojokofu, viyoyozi, vifaa vya kuzimia
moto, usafirishaji chuma, ufukizaji wa udongo katika vitalu vya tumbaku, kuwa iwapo
hatua hazitachukuliwa zinaweza kuingizwa nchini kupitia mipaka na kusababisha
madhara kwa binadamu na mazingira.
Mhandisi
Bamwenzaki amesema uchunguzi wa angahewa uliofanywa na wanasayansi
umethibitisha kuwa Tabaka la Ozoni limekuwa likimong'onyoka kwa kasi ya
asilimia tano (5) kila muongo ambapo matokeo ya uharibifu huo ni pamoja na
kuruhusu mionzi zaidi ya urujuani kufika katika uso wa dunia.
Akifafanua
zaidi Mhandisi Bamwenzaki amesema matokeo ya uvumbuzi huo yalisababisha Shirika
la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) kufanya tathimini ya kisayansi na kuamua
kuchukua hatua madhubuti katika kulinda tabaka hilo la Ozoni.
“Chini ya Programu ya Taifa,
Serikali imeandaa na inatekeleza Mpango wa Kuondosha Kemikali Zinazomong’onyoa Tabaka la
Ozoni ifikapo mwaka 2030 ambapo moja ya shughuli zinazotelekezwa ni pamoja
na kutoa elimu kwa mawakala wa forodha na wasimamizi wa Sheria kuhusu Kanuni za
Usimamizi wa Mazingira za mwaka 2022” amesema Mhandisi Bamwenzaki.
Akiwasilisha Mada kuhusu Udhibiti wa
uingizaji wa kemikali zinazodhibitiewa chini ya Itifaki ya Montreal, Afisa
Mwandamizi wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, Mhandisi George Ngoso amesema
suala udhibiti wa kemikali na vifaa vya kemikali linahitaji nguvu ya pamoja
vaina ya wadau waliopo katika mnyororo wa thamani ili kulinda afya za binadamu
na mazingira.
Mhandisi Ngoso amesema ni wajibu wa
mawakala wa forodha waliopo mipakani kujifunza teknolojia mpya ya ukaguzi wa
mizigo ikiwemo bidhaa za kemikali kuendelea na usimamizi na udhibiti wa kemikali
zinazodhibitiwa kwa kuzingatia ukomo wa matumizi wa kemikali hizo.
“Mnapaswa kuwa wazalendo na
kutanguliza maslahi ya taifa na jamii inayowazunguka, madhara ya uingizaji wa
bidhaa hizi unaweza kuleta athati kuwa kwa afya za binadamu na mazingira, hivyo tunapaswa kuhakikisha
kuwa tunadhibiti kemikali hizi kutoweza kuingia katika jamii yetu” amesema
Ngoso.
Kwa upande wake Wakala wa Forodha
kutoka Kampuni ya Freight Forwarders James Mramba ameishukuru Ofisi ya Makamu
wa Rais kwa kuendesha mafunzo hayo na kusema yataongeza tija katika utekelezaji
wa majukumu yao sehemu za kazi na kuhimiza mafunzo hayo kuwa endelevu ili
kuwafikia wanufaika wengi zaidi.
“Naahidi kuwa Balozi kwa wenzangu
kwa kushirikiana na watumishi wenzangu pamoja na taasisi nyingine za serikali
ili kuhakikisha kuwa kunakuwepo na udhibiti wa kutosha wa uingizaji wa kemikali ambazo zina athari kubwa kwa jamii na
mazingira yetu” amesema Mramba.
Katika mafunzo hayo washiriki hao walielimishwa
kuhusu Sheria ya Usimamizi wa Mazingira (Kanuni za Kudhibiti Kemikali
zinazoharibu Tabaka la Ozoni) za mwaka 2022, Udhibiti wa Uingizaji wa Kemikali
zinazodhibitiwa chini ya Itikafi ya Montreal, na Taratibu za maombi ya vibali
vya usimamizi wa kemikali.
Jumla ya Mawakala wa forodha 25 walishiriki mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoanza Machi 01 hadi 03, 2023 na kuandaliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais.
No comments:
Post a Comment