Habari za Punde

SMZ Imeipongeza ZRA Kwa Jitihada za Kuimarisha Ukusanyaji wa Mapato Nchini kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza katika Kilele cha Maadhimisho ya Mwezi wa Shukrani na Furaha kwa Walipakodi wa Zanzibar 2023, hafla hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Zanzibar Uwanja wa Ndege Kiembesamaki Wilaya ya Magharibi “B” Unguja Jijini Zanzibar leo 29-12-2023
 

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar, imeipongeza Mamkaka ya Mapato Zanzibar (ZRA) kwa jitihada za kuimarisha ukusanyaji wa mapato nchini hasa kwa mwaka wa fedha 2023/ 2024.

Pia Serikali imetoa pongezi hizo kwa kufanikiwa kuvuka lengo la makusanyo ya kodi zaidi yaliyowekwa kila mwezi na kuwa na ukuaji mzuri wa mapato ikilinganishwa na mwaka jana.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameyasema hayo ukumbi wa hoteli ya Golden Tulip, Uwanja wa ndege Mkoa wa Mjini Magharibi, kwenye sherehe za kilele za mwezi wa Shukurani na furaha kwa walipa kodi wa Zanzibar.

Alisema, kwa kipindi cha miezi mitano (5) kutoka Julai hadi Novemba 2023, ZRA ilikadiriwa kukusanya jumla ya shilingi bilioni 276.063 na imefanikiwa kukusanya makusanyo halisi shilingi bilioni 288.251, sawa na ufanisi wa asilimia 104.42. hivyo, kufanikiwa kuongeza ukusanyaji mapato kwa asilimia 21.93 ikilinganishwa na makusanyo ya shilingi bilioni 236.407 ya kipindi kama hicho cha mwaka jana.

Alisema, hali hiyo inajenga imani ya uwezekano wa kukusanya mapato zaidi na zaidi. Aidha, Rais Dk. Mwinyi aliwataka wafanyakazi wa ZRA, kufanyakazi ya ukusanyaji wa mapato kwa uadilifu na uaminifu mkubwa ili waepukane na vishawishi kutoka kwa wafanyabiashara wachache wasiokuwa waadilifu.

Pia, alitoa indhari na kueleza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitomvumilia mfanyakazi yeyote wa ZRA na TRA Zanzibar, atayekwenda kinyume na maadili ya Utumishi wa Umma wakati wa kutekeleza majukumu yake ya kila siku. Alionya, mfanyakazi yeyote atakaebainika kukwepesha mapato ya Serikali, hatua kali za kiutumishi na kijinai zitachukuliwa dhidi yake.

Katika hali nyengine Rais Dk. Mwinyi aliwaahidi watumishi wa ZRA kuwa Serikali itaendelea kuyaangalia maslahi yao kama walivyoangaliwa wafanyakazi wengine wa Serikali ili kuongeza hamasa ya ukusanyaji wa mapato pamoja na kuiwezesha ZRA kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa.

Hivyo, Dk. Mwinyi aliziagiza Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Utumishi washirikiane na Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Fedha na Mipango, kukamilisha marekebisho stahiki ya mishahara ya watumishi wa ZRA, ili wapate faraja na waendelee na ufanisi katika kazi zao.

Kwa upande wa wafanyabiashara wote waliopo Zanzibar na wanaokuja kuwekeza, Dk. Mwinyi aliwahakikishia kwamba Serikali imeimarisha mfumo wa kodi iliyo rafiki itakayorahisisha biashara kwa kuimarisha mfumo wa kodi ulio sawa kwa kila mfanyabiashara.

“Hakuna atakayependelewa wala kuonewa. Tutaendelea kuimarisha mfumo wa kodi ulio rahisi kuutumia (convenient) kwa kuwekeza zaidi kwenye mifumo ya kidigitali na kuwafikia walipakodi wengi zaidi kwa kuimarisha Ofisi za kodi” Dk. Mwinyi, aliwahakikikisha wafanyabiashara hao.

Vile vile Rais Dk. Mwinyi, aliitaka mikoa na wilaya zote nchini kuendelea kuimarisha mfumo wa kodi unaotabirika (certainty) kwa kuendelea kutoa elimu ya kodi ili kila mfanyabiashara ajue aina ya kodi anayostahiki kulipa kwa wakati husika.

Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Saada Mkuya Salum, akizungumza kwenye hafla hiyo alisema, kipindi hiki cha maadhimisho ya miaka 60 ya Mapinduzi ya Zanzibar Maendeleo makubwa yamefikiwa kutokanana ukusanyaji mzuri wa mapato yaliyosaidia kutekelezwa kwa miradi mikubwa ya maendeleo.

Alisema Maendeleo hayahitaji vikwazo, ufinyu wa Maendeleo unatokana na kukosa maono, alieleza Zanzibar imejifunza utayari kutoka kwa Rais Dk. Mwinyi wakitafakari zaidi bila kuweka vikwanzo vya Maendeleo.

Alisema pamoja na mafanikio makubwa yaliyofikiwa nchini ni jitihada za Mhe. Rais Dk. Mwinyi kushajihisha ulipaji bora wa kodi za kielektroniki.

Naye, Mwenyekiti wa bodi ya Mamlaka ya ZRA, Prof. Hemed Rashid Hikmany, alieleza miongozi mwa majukumu ya bodi hiyo ni kuhakikisha wanafanyakazi wanafanyakazi kwa mujibu wa sheria zilizopo na kuhakikisha walipa kodi wanalipa kwa hiari, kuhakikisha wanafanyakazi kwa ukaribu na weledi ili kufikia malengo ya Serikali ya ukusanyaji bora wa mapato.

Kamishna Mkuu wa ZRA, Yussuf Juma Mwenda naye alieleza mafanikio makubwa yaliyofikiwa na ZRA ikiwemo kushajihisha walipakodi kwa ufanisi kupitia mfumo wa kisasa wa ZIDRAS unaowarahisishia walipakodi wa aina zote, wakubwa, wakati hadi wadogo kulipakodi na kurejesha marejesho ya kodi (returns) kwa wakati kupitia teknolojia ya kisasa.

Alisema, ZRA pia imefanikiwa kutoka makusanyo ya Shilingi bilioni 565 kwa mwaka jana ikilinganishwa na bilioni 374 za kipindi kilichopita.

Pia alieleza ZRA imeanza kuchukuakoti za majengo ya ghorofa ikiwemo mahoteli ambao wamekuwa na mwitikio mkubwa kwa serikali, alisema nyumba ndogo hazihusiki na kodi hiyo.

IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.