Habari za Punde

Balozi Seif akemea Wana CCM kukienzi chama wakiwa madarakani tu

Na Othman Khamis Ame OMKR
 
Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi Balozi Seif Ali Iddi amekemea tabia ya baadhi ya Wana CCM kuachana na tabia ya kujijengea mazingira ya kukiona chama hicho kizuri wakati wanapokuwa madarakani tu.
 
Alitoa kemeo hilo wakati akiufungua mkutano Mkuu wa uchaguzi CCM wa Mkoa wa Kusini Unguja hapo katika ukumbi wa Tamarind Beach Hotel iliyopo Uroa Mkoa wa Kusini Unguja.


Balozi Seif ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alisema tabia hiyo inayoonekana kuanza kuchipua ndani ya Chama ni ya hatari na inafaa Viongozi kama hao wakaepukwa kabisa.
 
Alisema Chama cha Mapinduzi hakiwezi kuendelea kuwa na makundi ya wanachama ambayo hatimae husababisha mvutano wa Viongozi na hatiae kushindwa kutetea na kulinda Sera za Chama hicho.
 
Alitahadharisha kwamba Viongozi wanaoweka maslahi mbele ndio wenye hulka ya kuogolea zaidi katika rushwa inayopigwa vita na kukemewa kabisa ndani ya sera na ilani ya Chama cha Mapinduzi.
 
Alionya kuwa uongozi hauombwi kwa rushwa na kuwataka wanachama kuwakimbia watu wanaoendeleza tabia hiyo ambayo ni mbaya kabisa inayoweza kuwajengea muelekeo mbovu wa chama hicho.
 
Balozi Seif alisisitiza kwamba katika kukabiliana na tatizo la rushwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inakusudia kuunda chombo kitakachokuwa na uwezo wa kusimamia udhibiti wa rushwa ili kupunguza au kuondosha dhambi hiyo mbaya.
Balozi Seif alitoa mfano wa Kiongozi bora ni yule anayejiamini kwa kutumia nguvu, busara na hekima katika kuwaongoza wanachama na Jamii iliyomzunguuka.
 
“ Wapo baadhi ya wanachama wenye tabia ya Mchwa ndani ya Chama ambao huitafuna miradi kadhaa ya chama hicho ambayo inauwezo kabisa ya kukiendesha chama kiuchumi”. Alifafanua Balozi Seif.
 
Akizungumzia suala la demokrasia nchini Balozi Seif alisema fursa hiyo imekuwa ikitumiwa vibaya na baadhi ya watu na hata vikundi vya dini kwa kuilazimisha jamii au wafuasi wao kufuata yale matakwa wanayoyahitaji bila ya kuzingatia uhuru wa mtu.
 
Alisema tabia hiyo haitoi ile haki halisi ya Demokrasia inayohitajika ambayo ipo kwa mujibu wa Katiba na Sheria za Nchi.
 
“ Kwa nini leo Demokrasia ipo tena ndani ya vyama vya siasa na hata katika Taasisi za Kijamii halafu wanakuwepo baadhi ya watu au vikundi vya jumuiya za Kiraia zilazimishe yale wanayoyataka wao tena kwa nguvu ?”. Alihoji Balozi Seif.
 
Aliwapongeza Wananchi wa Mkoa wa Kusini Unguja kwa kupitisha mchakato wa katiba mpya ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kwa njia ya amani na usalama.
 
Mapema akimkaribisha Balozi Seif Mwenyekiti wa CCM aliyemaliza kipindi cha
miaka mitano iliyopita Mkoani humo Ndugu Haji Ussi Gavu alisema Mkoa wa Kusini Unguja umepata Heshima kubwa ndani ya Mikoa yote ya Tanzania Kisiasa.
 
Ndugu Gavu alisema heshima hiyo imekuja kutokana na umadhubuti wa wanachama na Viongozi wa Mkoa huo uliopelekea kuwa ngome imara ya Chama cha Mapinduzi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.