Habari za Punde

Balozi Seif akutana na ujumbe wa wafanyabiashara kutoka Marekani

 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Ujumbe wa Wafanyabiashara wenye Asili ya Afrika Kutoka Mji wa Sacramento Jimboni California Nchini Marekani.
Mazungumzo yao hayo yamefanyika hapo Ofisini kwake Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa katika Picha ya pamoja na Ujumbe wa Wafanyabiashara wenye Asili ya Afrika Kutoka Mji wa Sacramento Jimboni California Nchini Marekani mara baada ya mazungumzo yao.
Kushoto ya Balozi Seif ni Rais na Mkuu wa Jumuiya hiyo Bibi Zizia Davis Goines.
Rais na Mkuu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wenye Asili ya Afrika kutoka Mji wa Sacramento Jimboni California Nchini Marekani Bibi Azizia Davis Goines akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alipofika Ofisini kwa Balozi Seif yeye na ujumbe wake kuonana naye.
Picha na Hassan Issa wa - OMPR – ZNZ .
Na Othman Khamis Ame, OMPR
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Wawekezaji Vitega uchumi ndani na nje ya nchi ili kuona fursa zilizowekwa na Serikali katika kuimarisha uchumi na ustawi wa Jamii zinafanikiwa.
Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakati alipofanya mazungumzo na Ujumbe wa Viongozi sita wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wenye asili ya Afrika kutoka Mji wa Sacramento Jimboni California Nchini Marekani.
Balozi Seif aliuambia Ujumbe huo hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar kwamba Visiwa vya Zanzibar vimebarikiwa kuwa na mazingira mazuri ya uwekezaji hasa katika maeneo ya Utalii na Viwanda.

Alifahamisha kwamba Zanzibar hivi sasa inahitaji kuwa na viwanda mbali mbali vitakavyosaidia kukuza uchumi wa Taifa sambamba na kutoa ajira kwa Vijana ambao ndio walio wengi katika Jamii.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliupongeza ujumbe huo kwa uamuzi wake wa kuangalia mazingira ya uwekezaji na kuwaomba kuitumia fursa hiyo katika kuona eneo gani wanaweza kuwekeza.
“ Zanzibar ina fursa kadhaa za uwekezaji viteda uchumi kama sekta ya Utalii pamoja na Viwanda ambayo kama itatumiwa vyema inaweza kusaidia kubadilisha pato la wananchi na kunyanyua kwa haraka uchumi wake “. Alisisitiza Balozi Seif.
Mapema Rais ambae pia ni Mtendaji Mkuu wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wenye asili ya Afrika kutoka Mji wa Sacramento Jimboni California Bibi Azizia Davis Goines alisema Taasisi yao imeamua kufungua ukurasa mpya katika kuona inaendeleza mashirikiano na nchi rafiki.
Bibi Azizia alisema utaalamu uliopo ndani ya Jimbo la California hasa kwenye masuala ya kilimo unaweza kutumiwa katika kusaidia Taasisi na Jumuiya nyengine rafiki hasa Barani Afrika katika kujinyanyua kiuchumi na uwezeshaji.
Ujumbe huo wa Viongozi sita wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wenye asili ya Afrika kutoka mji wa Sacramento Jimboni California Nchini Marekani ukiwa pamoja na Mkurugenzi wa Diasfora Zanzibar Nd. Khamis Ali na baadhi ya Maofisa wake utapata fusa ya kuangalia maeneo ambayo wanaweza kuwekeza hapa Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.