Habari za Punde

Hotuba ya bajeti ya Waziri wa nchi ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la mapinduzi


1.       Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu likae kama Kamati kwa madhumuni ya kupokea, kujadili na hatimae kuidhinisha makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi (ORMBLM) kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
 
2.       Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuwa wazima wa afya na hivyo kutekeleza majukumu yetu yakiwemo ya kustawisha maisha ya jamii ya Wazanzibari.
 
3.       Mheshimiwa Spika, naomba pia kutumia nafasi hii kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein kwa umahiri wake katika kuiongoza nchi yetu. Chini ya uongozi wake, Serikali imeendelea kutekeleza Mipango Mikuu ya Kitaifa ikiwemo MKUZA II na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2010-2015,  sambamba na ahadi alizozitoa kwa wananchi katika nyakati tofauti na hasa wakati wa ziara zake  Mikoani. Utekelezaji wa mipango hiyo, imesaidia Serikali kutoa huduma muhimu kwa jamii na kuongeza imani ya wananchi kwa Serikali yao.
 
4.       Mheshimiwa Spika, nakupongeza wewe binafsi na Naibu wako kwa kuendelea kuliongoza Baraza letu Tukufu kwa mujibu wa kanuni na taratibu tulizojiwekea. Uvumilivu wako umekuwa ni mfano katika kuimarisha demokrasia ndani ya Baraza hili. Hata hivyo, uvumilivu huo haujawa kikwazo kwako katika kufikia maamuzi sahihi. Aidha, ninawapongeza Naibu Spika na Waheshimiwa Wenyeviti wa Baraza ambao wanakusaidia kuliendesha Baraza hili. Ninawashukuru pia Waheshimiwa Wawakilishi wote kwa ushirikiano mzuri wanaonipa katika kutekeleza majukumu yangu ya kila siku. Hii ni Ofisi inayowajumuisha na kuwaunganisha jamii na wananchi wote, hivyo mashirikiano makubwa kati yenu Waheshimiwa Wawakilishi na Ofisi hii ni suala la msingi sana.

5.       Mheshimiwa Spika, nampongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Baraza la Wawakilishi ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu, Mheshimiwa Hamza Hassan Juma, Mwakilishi wa kuchaguliwa wa wananchi wa Jimbo la Kwamtipura ambaye pia ni Mwenyekiti wa Wenyeviti. Nampongeza sana Mheshimiwa Hamza kwa kuchaguliwa tena kuwa Mwenyekiti wa Kamati hii. Naamini umahiri wake katika kuiongoza Kamati hii katika kipindi kilichopita ndio kigezo kikubwa kilichowafanya Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati anayoiongoza kumchagua tena kwa kipindi cha pili mfululizo. Aidha, napenda kuchukua fursa hii kuwapongeza Waheshimiwa Wajumbe wote walioteuliwa kuingia kwenye Kamati hii, nawaahidi kwamba mimi binafsi pamoja na watendaji wenzangu wote tutaendelea kutoa ushirikiano wa hali ya juu kwao kwa kipindi chote cha utendaji wa majukumu yetu.
 
6.       Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee naomba niwapongeze Wajumbe wote wa Kamati iliyopita kwa ushirikiano waliouonesha na utekelezaji mzuri wa kazi zao. Mafanikio ya Ofisi yangu yametokana zaidi na miongozo na ushauri wao waliokuwa wakitupatia mara kwa mara. Naamini kwa wale Wajumbe ambao hawajarejea katika Kamati hii, kwa kutumia uzoefu walioupata katika kipindi cha miaka miwili na nusu, wataendelea kutoa mchango wao mkubwa katika kufanikisha ufanisi wa utendaji wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Nitakuwa sijatenda haki kama sitompongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Kusimamia Hesabu za Serikali Mheshimiwa Omar Ali Shehe Mwakilishi wa Jimbo la Chake Chake kwa kuchaguliwa tena kuiongoza Kamati hiyo na pia nawapongeza Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati hii.
 
7.       Mheshimiwa Spika, siku za hivi karibuni kumejitokeza wimbi kubwa la baadhi ya wananchi nchini mwetu kutotii Sheria za nchi. Watu wengine wamefikia kuhatarisha usalama na amani ya nchi, kuwadhuru wengine na hata kufikia kuuwawa. Hali hii si ya kawaida nchini mwetu na ni wajibu wetu sote kuvipiga vita vitendo vyote vya kihalifu. Vile vile, ni wajibu wetu sote kulinda amani na usalama wa nchi yetu. Uzoefu wa nchi nyingi umeonesha kwamba amani ikipotea si rahisi kuirejesha tena kwa haraka lakini baya zaidi ni matokeo na hasara zinazoambatana na matokeo ya mifarakano.
 
8.       Mheshimiwa Spika, kabla sijamaliza salamu zangu za pongezi naomba kuchukua fursa hii kumpongeza kwa dhati Mwakilishi wa Jimbo la Bububu Mheshimiwa Hussein Ibrahim Makungu (Bhaa) kwa kuchaguliwa na wananchi wa Jimbo hili kupitia Chama Cha Mapinduzi. Kuchaguliwa kwake kunaonesha matumaini waliyonayo wananchi wa Jimbo hilo kwake katika kuwaletea maendeleo.
 

B. SHABAHA YA OFISI YA RAIS NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI

9.       Mheshimiwa Spika, Shabaha kuu ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ni:-
(i)          Kudumisha Amani, Ulinzi na Usalama
(ii)        Kuwafanya vijana wawe na maadili mema na mtazamo wa kujiajiri wenyewe
(iii)       Kustawisha haki za Wanafunzi waliohalifu Sheria
(iv)      Kutoa Huduma bora kwa Jamii
(v)        Kuimarika kwa Maendeleo ya Zanzibar

C. MWELEKEO WA BAJETI NA MALENGO YALIYOWEKWA KWA MWAKA WA FEDHA WA 2013/2014

10.   Mheshimiwa Spika, hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa mwaka wa fedha 2013/2014 inatoa muelekeo wa jumla wa utekelezaji wa mipango ya Idara na Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi zikiwemo Mamlaka za Serikali za Mikoa na Serikali za Mitaa pamoja na Idara Maalum za SMZ. Katika hotuba hii, ili malengo na utekelezaji yaweze kuonekana vizuri na Waheshimiwa Wajumbe nimeamua kwa makusudi kuweka viambatanisho vinavyoeleza kwa ufasaha kwa njia ya vitabu mambo yafuatayo:-
(i)       Utekelezaji wa Maagizo ya Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Yaliyotolewa Wakati wa Kuwasilisha Bajeti ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Juni 2012,
(ii)     Utekelezaji wa Malengo ya Bajeti ya Serikali za Mitaa kwa mwaka wa fedha 2012/2013 na Malengo ya Bajeti kwa mwaka wa fedha 2013/2014 na,
(iii)    Maelezo ya Bajeti Inayotumia “Program Based Budget” (PBB) Kwa Mwaka wa Fedha 2013/2014 Katika Baraza la Wawakilishi.
 
11.   Mheshimiwa Spika, kufuatia uamuzi wa Serikali wa kutaka kubadilisha mfumo wa bajeti wa sasa wa “Line Budget Item” kwenda “Program Based Budget” (PBB), Ofisi yangu imeanza maandalizi hayo kwa kupanga shughuli zote za mwaka ujao katika programu nne. Programu hizo ni:- Programu ya Ushirikiano wa Kikanda, Kimataifa na Wazanzibari Wanaoishi nje ya nchi, Programu ya Uongozi na Utawala wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Programu ya Mipango ya Ulinzi na Huduma za Urekebishaji na Uwezeshaji Kiuchumi na Programu ya Usimamizi na Utawala Katika Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Muundo wa PBB unaonekana katika Kiambatanisho Nambari 1.
12.   Mheshimiwa Spika, kutokana na Programu nilizozitaja hapo juu, Ofisi yangu inaazimia kutekeleza malengo makuu matano ambayo ni kuimarisha Ulinzi na Usalama, Kuwafanya vijana wawe na maadili mema na mtazamo wa kujiajiri wenyewe, kuimarisha Utawala Bora na Haki za Binaadamu, kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato na ushirikishwaji wa Wazanzibari walioko nje katika maendeleo ya Zanzibar. Kwa ufafanuzi zaidi angalia Kiambatanisho Nambari 2.
13.   Mheshimiwa Spika, ifikapo Januari mwakani, nchi yetu itaadhimisha Miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ambayo yaliasisiwa na Jemedari Hayati Mzee Abeid Amani Karume, Rais wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yakiwa na lengo la kumkomboa Mzanzibari kutoka katika madhila ya Wakoloni. Mapinduzi hayo, yameiwezesha Zanzibar kupiga hatua kubwa katika nyanja za kiuchumi, kijamii na kisiasa. Katika kufanikisha maadhimisho hayo, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi imejipanga kutekeleza shughuli mbali mbali kupitia Idara na Taasisi zake. Miongoni mwa mambo ambayo Ofisi inatarajia kuyatekeleza ni kuandaa na kurusha hewani vipindi mbali mbali vya TV na Redio vinavyoelezea mafanikio ya Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar na kuzindua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbali mbali ya maendeleo ya wananchi Mikoani.
14.   Mheshimiwa Spika, Ofisi itafanya tathmini ya vyanzo vya mapato vya Idara Maalum za SMZ ambayo itatoa mapendekezo ya kuimarisha misingi ya ukusanyaji wa mapato na kuvitambua vyanzo vyote vya mapato kwa usahihi. Aidha, Ofisi yangu inaendelea kuvifanyia mapitio vyanzo vya mapato vya Serikali za Mitaa sambamba na kutayarisha upya Sheria ya Serikali za Mitaa ambayo itaelekeza kwa uwazi utaratibu bora wa ukusanyaji mapato katika Serikali za Mitaa pamoja na kuainisha vyanzo vya mapato yake.
 
15.   Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo, tunakusudia kuharakisha mchakato wa ukusanyaji wa Kodi ya Mali (Property Tax), kurasimisha kisheria ada zinazokusanywa na Masheha na utozaji wa ada wa vitambulisho vya wageni. Kwa hatua ya awali, Wataalamu wa Serikali za Mitaa wamefanya ziara ya kimafunzo Jijini Dar es Salaam Wilaya ya Ilala kujifunza juu ya utaratibu bora wa ukusanyaji wa Kodi ya Mali. Kimsingi, Halmashauri ya Wilaya ya Ilala imekubali kushirikiana nasi na kubadilishana utaalamu katika kufanikisha zoezi hili.
 
16.   Mheshimiwa Spika, Serikali inaandaa utaratibu wa kuanzisha Shirika litakalosimamia Miradi ya Idara Maalum. Aidha, Serikali inategemea kufanya marekebisho ya Sheria ya Idara Maalum ya Kikosi cha Zimamoto na Uokozi ili kuweka ulazima kwa vyombo vya moto vya biashara kuwa na vifaa vya kuzimia moto na kufanyiwa ukaguzi na Kikosi cha Zimamoto na Uokozi. Azma hii itakapoanza kutekelezwa, inakusudia kuongeza usalama wa kujikinga na majanga ya moto.
 
17.   Mheshimiwa Spika, Mikoa itatoa kipaumbele katika kutumia ulinzi shirikishi ili kuhakikisha kuwa uhalifu unapungua katika mitaa na vijiji. Aidha, Serikali inakusudia kuweka mfumo maalum wa kamera za ulinzi (CCTV) sambamba na kuweka taa za kuongozea gari katika baadhi ya barabara. Kwa hatua za mwanzo, maeneo ya Malindi, Mkunazini na Kwamchina Mwanzo yatashughulikiwa. Mpango huu utakuwa chini ya Wizara ya Mawasiliano na Miundombinu kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkoa wa Mjini Magharibi.
 
18.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi itaendesha utafiti unaokusudia kuangalia kwa umakini majukumu ya Sheha katika mfumo wa mageuzi ya Serikali za Mitaa. Hii itasaidia katika zoezi la kupanga majukumu ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa katika muundo mpya wa Serikali ambao unalenga kupunguza baadhi ya madaraka kutoka Serikali Kuu kwenda kwa wananchi (Decentralization by Devolution) ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa jamii.
 
19.   Mheshimiwa Spika, utendaji kazi katika ngazi za Mikoa na Wilaya nao utaimarishwa ili kuweza kutoa huduma bora kwa jamii, azma hiyo inaenda sambamba na uwepo wa vitendea kazi katika Taasisi hizo. Jumla ya gari kumi na moja zitanunuliwa katika mwaka wa fedha wa 2013/2014, gari hizo zitasaidia sana katika kazi za usimamizi na ufuatiliaji wa shughuli mbali mbali zinazotekelezwa katika ngazi za Wilaya na Mikoa. Aidha, Ofisi inaazimia kuwawekea mazingira bora ya makaazi Viongozi wa Mikoa na Wilaya kwa kuanza ujenzi na kuzifanyia matengenezo makubwa nyumba wanazoishi. Jumla ya TZS. 458.7 milioni zimetengwa kwa kazi hiyo ya ujenzi na matengenezo ya nyumba za Wakuu wa Mikoa na Wilaya pamoja na Ofisi zao.
 
20.   Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu sasa suala la kuwa na eneo la kudumu la kutupia taka limekuwa ni tatizo kubwa. Napenda kuliarifu Baraza lako Tukufu kuwa hivi sasa Serikali imo katika hatua za mwisho za kukabidhiwa eneo la kudumu la kutupia taka lilioko Kibele Wilaya ya Kati ambalo lina ukubwa wa hekta 15. Hatua za kupimwa na kupatiwa hatimiliki kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati zinaendelea vizuri. Kupatikana eneo hilo kutatatuwa tatizo sugu la kukosekana eneo la kudumu la kutupa taka zinazozalishwa katika Manispaa ya Zanzibar na maeneo jirani.
21.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi imekuwa ikiendelea na juhudi za kuimarisha usafi katika Manispaa ya Zanzibar ambapo utaratibu maalum utaandaliwa wa kusafisha Mji wakati wa usiku ambao utatoa wasaa mzuri wa wasafishaji kuweza kuusafisha Mji kwa urahisi na kwa utulivu mkubwa. Zoezi hili litakuwa rahisi baada ya kupatikana kwa taa katika barabara zetu. Baraza la Manispaa litaendelea na utaratibu wa kuwaondoa watu wanaofanya biashara kiholela katika maeneo yasiyoruhusiwa, pia kutenga maeneo kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo wadogo.
 
22.   Mheshimiwa Spika, baada ya kuonesha mafanikio makubwa ya mradi wa majaribio wa uwekaji wa taa za barabarani wenye kutumia nguvu za jua ambao ni ufadhili wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na mazungumzo na Serikali ya Jamhuri ya Watu ya China kwa kuanza awamu ya pili ya Mradi huu ambao utahusisha barabara ya Kiembe Samaki hadi Mnazi Mmoja, Kiembe Samaki hadi Mwanakwerekwe, Amani hadi Mtoni na Mtoni hadi Malindi. Aidha, barabara za Mji wa Chake Chake nazo zimeingizwa katika mpango huu.
 
23.   Mheshimiwa Spika, matayarisho ya utekelezaji wa mradi wa Mpango wa Kuimarisha Huduma za Miji Zanzibar (Zanzibar Urban Service Program – ZUSP), awamu ya kwanza (Hatua ya maandalizi) imefikia asilimia 97. Katika awamu hiyo, jumla ya Washauri Elekezi wanane wametafutwa ambao watashiriki katika utekelezaji wa kazi mbali mbali zilizopangwa kufanyika katika maeneo ya Manispaa ya Mji wa Zanzibar na Mabaraza ya Miji ya Pemba   (maelezo ya kina yapo katika kiambatanisho nambari 14).
 
24.   Mheshimiwa Spika, awamu ya pili ya mradi wa ZUSP (Hatua ya utekelezaji) imefikia asilimia 30 inayojumuisha shughuli za ujenzi na upatikanaji wa vifaa imeanza kutekelezwa kwa kuzingatia sehemu kuu tatu ambazo ni kupatikana kwa Washauri Elekezi wa Mradi (Consultancy Services), shughuli za ukarabati na ujenzi wa miundombinu (Physical Works) na ununuzi wa vifaa. Miongoni mwa vifaa vilivyonunuliwa hadi sasa ni gari tano aina ya ‘Double Cabin’ za Wakuu wa Idara za Baraza la Manispaa na gari nne za Mabaraza ya Miji Pemba pamoja na Idara ya Uratibu Pemba, vespa 25, pikipiki saba, magari matatu ya kuchukulia  vikapu vya taka kwa Mabaraza ya Miji Pemba, gari moja ya Idara ya Mipango Miji, gari moja ya kuchukulia maji machafu ya Mabaraza ya Miji Pemba na vitendea kazi vikiwemo kompyuta, samani, printer, projector na scanner. Jumla ya programu tano zitaanza kutekelezwa katika mwaka unaokuja baada ya taratibu za mikataba na upatikanaji wa Wakandarasi kukamilika.
 
25.   Mheshimiwa Spika, Programu zinazotarajiwa kutekelezwa ni pamoja na ujenzi na ukarabati wa msingi wa maji ya mvua katika mitaa ya Sebleni na Ziwa la Kwa-Binti Hamrani ambao utekelezaji wake utaanza mwezi Januari 2014. Programu ya uwekaji taa za barabarani katika maeneo ya Shangani, Mkunazini, Kiponda na Amani – Kwabiziredi, utekelezaji wake utaanza mwezi Oktoba 2013. Ukarabati wa jengo la Ofisi Kuu ya Baraza la Manispaa Darajani na ukarabati wa Karakana ya Saateni, utekelezaji wake utaanza mwezi Agosti 2013. Programu ya kuongeza uwezo wa Baraza la Manispaa itaanza mwezi Agosti 2013. Aidha, Programu ya uendelezaji wa Mpango Mkuu wa Mji inatarajiwa kukamilika katika miezi 18 ijayo.
 
26.   Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha miundombinu ya kuzima moto katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid Amani Karume, utaratibu wa kupata eneo jengine kwa ajili ya shughuli za kituo cha Kikosi cha Zimamoto umekamilika ambapo kwa sasa eneo jipya limeshapatikana na michoro ya jengo la kituo hicho imeshatayarishwa. Aidha, katika kukabiliana na tatizo la uhaba na uchakavu wa vifaa vya kuzimia moto, Kikosi cha Zimamoto na Uokozi kimetiliana saini mkataba na Kampuni ya NN Engeneering ya nchini Uholanzi kwa ajili ya ununuzi wa magari manne ya Zimamoto na vifaa mbali mbali vya uokozi vyenye thamani ya EURO 2,054,852.
 
27.   Mheshimiwa Spika, mbali na juhudi zinazochukuliwa kuwahamasisha Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi kuchangia maendeleo katika sekta za Kijamii na Kiuchumi, bado juhudi hizi zinakabiliwa na changamoto mbali mbali. Miongoni mwa Changamoto hizo ni: Kutokuwepo kwa muongozo wa uratibu wa shughuli za maendeleo zinazofanywa na Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi, kutokuwepo kwa mfumo maalum unaoratibu utumaji wa fedha kutoka nje na kutokuwepo kwa mfumo unaoratibu utumiaji mzuri wa rasilimali walizonazo Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi ikiwemo fedha, elimu, utaalamu na teknolojia. Katika kutatua changamoto zilizotajwa na nyengine, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi inaandaa Sera ya Diaspora ambayo itatoa miongozo na mikakati itakayowashajihisha Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi kushiriki katika mipango ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya Zanzibar. Sera hiyo ya Diaspora inatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha wa 2013/2014.
28.   Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliunda Kamati ya kuchunguza uendeshaji, usimamizi na faida zinazopatikana kutoka katika Mradi wa Shamba la Mfano la Pamoja linaloendeshwa kwa ubia kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Misri. Tayari ripoti ya uchunguzi imetolewa ambapo imeonesha changamoto mbali mbali zilizopo katika mradi huo na imetoa mapendekezo juu ya namna ya kukabiliana na changamoto hizo. Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi tayari imeshaanza kuyafanyia kazi mapendekezo yaliyomo kwenye ripoti hiyo ambayo yameoneshwa katika Kiambatanisho Nambari 3. Vile vile, Baraza lako Tukufu liliunda Kamati Teule ya Kuchunguza Utendaji wa Baraza la Manispaa Zanzibar. Naomba kukujuilisha rasmi kwamba Serikali imeipokea ripoti ya Kamati hiyo na inaendelea kuifanyia kazi na itaiwasilisha rasmi taarifa ya utekelezaji katika kikao kijacho cha Baraza la Wawakilishi.
29.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014, itatekeleza mradi makhsusi wa Ukarabati wa Ikulu Kuu Zanzibar. Jengo hili kwa sasa halipo katika hali ya kuridhisha hasa ukitilia maanani ni jengo lenye umri wa miaka 108 lililojengwa katika mwaka 1905. Kazi ya ujenzi wa kuzuia mmong’onyoko nyuma ya Ikulu ndogo ya Mkoani nayo itafanyika sambamba na ujenzi na matengenezo ya nyumba za mapumziko za Micheweni na Chwaka. Aidha, Ofisi itaendelea kutekeleza miradi saba ambayo inatekelezwa katika mwaka huu wa 2012/2013. Pia, itatekeleza mradi wa Mpango wa Kuimarisha Huduma za Miji Zanzibar na “Capacity for Reform Implementation Management Program” ambayo kiutawala inasimamiwa na Ofisi ya Rais Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo.
30.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kupitia Halmashauri za Wilaya, Mabaraza ya Miji na Baraza la Manispaa imejidhatiti katika suala zima la kuimarisha masoko yetu. Tayari soko la Mombasa limefunguliwa upya, halikadhalika na soko la Qatar Chake Chake Pemba. Serikali inajitahidi sana kuongeza huduma za masoko kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya soko kwa wananchi. Pia, Serikali inazingatia kubadili mwenendo mzima wa uendeshaji wa masoko kwa kuongeza muda wa kazi wa masoko yote baada ya kubainika kwamba sehemu kubwa ya wafanyakazi wanafanya manunuzi ya mahitaji yao nyakati za jioni.

D. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO WA BAJETI 2012/2013 NA MALENGO KWA MWAKA 2013/2014

31.   Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi wa hapo juu, sasa naomba kueleza utekelezaji wa malengo ya bajeti ya mwaka 2012/2013 pamoja na mwelekeo wa bajeti ya mwaka wa fedha 2013/2014 kwa Idara na Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

OFISI YA FARAGHA YA RAIS

32.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha ya Rais imeendelea kuratibu shughuli za kila siku za Mheshimiwa Rais, kufuatilia ahadi na maagizo anayoyatoa kwa wananchi na Taasisi mbali mbali, kusimamia upatikanaji wa huduma za kila siku za Mheshimiwa Rais, pamoja na kuweka kumbukumbu za mazungumzo ya Mheshimiwa Rais na viongozi mbali mbali wakiwemo Mabalozi. Kadhalika, Ofisi imeweza kuratibu safari za ndani na nje za  Mheshimiwa Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na vile vile kutekeleza jukumu lake la utunzaji na ukarabati wa nyumba zote za Ikulu Unguja, Pemba, Dar es Salaam na Dodoma. Nyumba zilizopo katika dhamana ya Ofisi hii ni Ikulu Kuu ya Mnazimmoja, Ikulu ndogo iliyopo Kikwajuni, Ikulu ndogo iliyopo Migombani, Ikulu ndogo iliyopo Kibweni  na Ikulu ndogo iliyopo Mkokotoni. Nyengine ni nyumba ya mapunziko ya Mazizini I, Mazizini II na Bwefoum. Aidha,  Ofisi hii ina dhamana ya Ikulu ndogo iliopo Chake Chake na Mkoani pamoja na Nyumba ya Mapumziko ya Micheweni. Nyengine ni Ikulu ndogo ya Laiboni Mjini Dar es Salaam, Ikulu ndogo pamoja na nyumba ya Wageni Mjini Dodoma. Aidha, Ofisi hii imetekeleza wajibu  wake wa kuwasiliana na vyombo vya habari na kutoa taarifa sahihi za Mheshimiwa Rais  kwa wakati unaotakiwa kwa lengo la kuwafikishia wananchi na wahusika wote. Vile vile, Ofisi hii inajukumu la kuwaendeleza wafanyakazi wake kwa kuwapatia fursa za masomo katika vyuo na Taasisi mbali mbali ndani na nje ya nchi.
 
33.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Faragha ilitengewa jumla ya TZS 1,908.3 milioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida ikiwemo mishahara na hadi kufikia Machi 2013, Ofisi hii iliingiziwa TZS 1,265.0 milioni sawa na asilimia 66.3 ya makadirio.
 
34.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha imetekeleza vizuri jukumu lake la kutoa  huduma kwa Mheshimiwa Rais na wageni rasmi mbali mbali. Katika kipindi hiki, Mheshimiwa Rais amekutana na kufanya mazungumzo na mabalozi na viongozi kadhaa kutoka nchi mbali mbali kama inavyoonekana katika Kiambatanisho Nambari 4. Mazungumzo hayo yalilenga kuimarisha urafiki kati ya Zanzibar na nchi hizo, pia kuongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kutafuta maendeleo ya haraka kwa wananchi wake na kwa jumla  yalijumuisha sekta zote za uchumi, siasa na ustawi wa jamii. Wengi wa wageni hao, wamevutiwa sana na jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kukuza uchumi na kuimarisha umoja, amani, utulivu na mshikamano. Kutokana na juhudi hizo viongozi hao wamekuwa wakiunga mkono na kutoa ushirikiano wao  katika juhudi za kuleta maendeleo kwa njia mbali mbali ikiwemo kuhamasisha wawekezaji kutoka katika nchi zao kuja kuwekeza Zanzibar.
 
35.   Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha unaomalizika, Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi amefanya ziara mbili katika nchi za Mashariki ya Mbali zenye mafanikio makubwa. Katika mwezi wa Novemba, 2012 alitembelea Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam na hivi karibuni, katika  mwezi wa Mei, 2013 alitembelea Jamhuri ya Watu wa China. Katika ziara yake ya Vietnam, Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein alikutana na Mheshimiwa Truong Tan Sang, Rais wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam, Mheshimiwa Bibi Nguyen Thi Doan, Makamu wa Rais wa nchi hiyo na Mheshimiwa  Nguyen Tan Dung, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Vietnam pamoja na viongozi wa Taasisi mbali mbali nchini humo. Ziara hiyo ilikuwa ni ya mafanikio kwani ujumbe wa Zanzibar ulijifunza namna ambavyo nchi ya Vietnam imeweza kupiga hatua kubwa ya kujiletea maendeleo katika muda mfupi ikiwemo kuzalisha mpunga kwa wingi. Vile vile, Zanzibar ilifaidika kwa kuona na kufikia maelewano ya kushirikiana katika shughuli mbali mbali za kiuchumi katika sekta ya kilimo hasa uimarishaji wa ukulima wa mpunga kwa njia za kisasa na kukubaliana na Wizara ya Kilimo na Maendeleo ya Vijijini ya Vietnam iwe na ushirikiano wa karibu na Wizara ya Kilimo na Mali Asili ya Zanzibar. Aidha, wataalam wa kilimo na Uvuvi wa Vietnam watembelee Zanzibar na kutoa ushauri wao wa kitaalamu. Maeneo mengine ambayo Vietnam itashirikiana na Zanzibar ni katika sekta ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambapo wananchi watashajihishwa kufuga samaki na mazao ya baharini kupitia vikundi vya ushirika pamoja na kunyanyua shughuli za akina mama wajasiriamali.  Ujumbe wa Zanzibar ulitumia ziara hiyo kuitangaza Zanzibar kwa wawekezaji wa nchi hiyo.
 
36.    Mheshimiwa Spika, katika ziara yake katika Jamhuri ya Watu wa China, Mheshimiwa Rais alipata fursa ya kukutana na kufanya  mazungumzo na Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Mheshimiwa Xi Jinping kwa mara ya pili ndani ya mwaka huu, baada ya kukutana nae mjini Dar es Salaam mnamo mwezi wa Machi, mwaka huu. Katika mazungumzo yao yaliyotawaliwa na  hisia za kirafiki na kindugu, viongozi hao walizungumzia  na kukubaliana juu ya uimarishaji wa uhusiano wa kihistoria uliodumu tokea mwaka 1964, ulioanzishwa na Hayati  Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume na Mwenyekiti Mao TseTung. Vile vile, Jamhuri ya Watu wa China imesisitiza kuendeleza urafiki wake na Zanzibar pamoja na kukuza ushirikiano katika nyanja za kiuchumi na kijamii zikiwemo sekta za kilimo, uvuvi, afya, mafunzo mbali mbali, utafiti na utalii. Aidha, miradi kadhaa ya maendeleo illizungumzwa. Vile vile, Mheshimiwa Rais alitumia fursa hiyo kuelezea kwamba Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliyo katika Muundo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa ina dhamira ya kweli ya kuwahudumia na kuwaletea maendeleo wananchi wake ambao wanaishi kwa amani na utulivu
 
37.   Mheshimiwa Spika, Wakati huo huo, Mheshimiwa Rais alikutana na kufanya mazungumzo na Mheshimiwa Li Yuamchao Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China. Pia, Mheshimiwa Rais, alipata heshima kubwa ya kuwa miongoni mwa viongozi wa nchi nne, Singapore, Fiji, Sri Lanka na Zanzibar katika ufunguzi rasmi wa maonesho ya kimataifa ya biashara na huduma mjini Beijing, wakiwa pamoja na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Watu wa China Mheshimiwa Li Keqiang. Viongozi wengine ambao Mheshimiwa Rais alipata fursa ya kukutana na kuzungumza nao ni pamoja na Naibu Waziri wa Biashara ambapo Wizara yake ilitia saini makubaliano ya ujenzi wa kitengo cha wagonjwa mahututi katika Hospitali ya Mnazi Mmoja na utoaji wa mafunzo kwa maofisa wa habari pamoja na maofisa wa bajeti wa Zanzibar. Makubaliano mengine yaliyotiwa saini ni ushirikiano katika Sayansi na Teknolojia ya Baharini ikiwemo utafiti wa kisayansi katika bahari. Vile vile, alikutana na Kiongozi wa Mji wa Nanjing katika jimbo la Jiangsu Mheshimiwa Li Xueyong pamoja na madaktari waliowahi kufanya kazi Zanzibar kwa miaka tofauti ambapo suala la kuwapeleka wagonjwa kutoka Zanzibar  katika hospitali ya Drum Tower lilizungumzwa. Katika mazungumzo yake na Meya wa Mji wa Xiamen katika jimbo la  Fujian, Mheshimiwa Liu Keqing ilikubalika kwamba Jimbo hilo litaleta Zanzibar ujumbe wa Viongozi wa Jimbo na makampuni mbali mbali hivi karibuni, kwa ajili ya hatua za uwekezaji na mashirikiano katika maeneo mbali mbali. Aidha, Mheshimiwa Rais alikutana na viongozi wa makampuni na Taasisi mbali mbali yakiwemo Mashirika yanayojishughulisha na ujenzi, utalii na mahoteli, usafiri wa baharini, uvuvi, teknolojia na viwanda ambapo wote wameonesha moyo mkubwa wa kuwekeza na kushirikiana na Zanzibar. Ujumbe wa Rais kwa upande wake, ulitoa taaluma kwa makampuni na wawekezaji mbali mbali wa China juu ya vivutio vya uwekezaji na utalii vilivyopo Zanzibar. Aidha, Mheshimiwa Rais alitumia fursa ya kuwepo kwake nchini China kuzungumza na wananchi wa  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanaoishi nchini humo na kuwaeleza  juu ya hali ya maendeleo pamoja na amani na utulivu iliyopo nchini. Aliwataka wanafunzi wanaochukua masomo mbali mbali nchini China kusoma kwa bidii na kurejea nyumbani kuungana na wananchi wenzao katika shughuli za maendeleo mara tu watakapomaliza masomo yao.
 
38.   Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa ziara za ndani, Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amekuwa akiendeleza utaratibu wa kufanya ziara za Mikoa na Wilaya  zote za  Zanzibar kila mwaka kwa lengo la kukutana na wananchi katika maeneo yao na kuwaunga mkono katika juhudi za kuleta maendeleo. Katika kipindi hiki, Mheshimiwa Rais alifanya ziara ya Mikoa ya Unguja na Pemba tarehe 5 hadi 21 Machi 2013, ambapo alipokea taarifa za Mikoa hiyo na kufanya majumuisho katika kila Mkoa baada ya kumaliza ziara ya Mkoa husika. Katika ziara hizo ambapo Mheshimiwa Rais hufuatana na viongozi mbali mbali, wananchi hupata fursa ya kuwasilisha ana kwa ana masuala muhimu yanayowagusa katika maisha yao ya kila siku. Aidha, ziara hizo zimekuwa zikitoa mchango mkubwa na kuhamasisha viongozi na wananchi kushiriki kikamilifu katika harakati za maendeleo, kuwakurubisha viongozi kwa wananchi wanaowaongoza na katika jitihada za kufufua ari ya utamaduni wa kujitolea katika kutekeleza mipango muhimu ya maendeleo. Katika ziara za mwaka huu miradi mbali mbali ya kilimo, afya, maji, elimu ilikaguliwa, kuwekewa mawe ya msingi na myengine kuzinduliwa. Juhudi za wajasiriamali ziliungwa mkono na changamoto mbali mbali kupatiwa ufumbuzi na baadhi yake kutolewa maelekezo.
 
39.   Mheshimiwa Spika, Katika kuimarisha maendeleo ya jamii, Ofisi imewatembelea wananchi mbali mbali Unguja na Pemba na kufanya tathmini  juu ya mahitaji yao ya msingi kwa lengo la kuwasaidia na kuwaunga mkono katika juhudi zao za kuleta maendeleo.
 
40.   Mheshimiwa Spika, Ofisi iliendelea kuimarisha Ikulu ya Mnazi Mmoja kwa kujenga na kukamilisha jengo jipya linalojumuisha Stoo na Ofisi. Kadhalika, Ofisi imefanikisha ufungaji wa mashine tatu za kufulia katika Ikulu ya Migombani, mashine tatu za vipoza hewa katika ukumbi wa Baraza la Mapinduzi na kupaka rangi jengo la Ikulu. Kwa upande wa Ofisi ya Ikulu ndogo ya Laibon ilioko Dar es Salaam, Ofisi imefunga mashine ya kipoza hewa, kufanya matengenezo ya vyoo na kufanya malipo ya huduma za umeme na maji. Aidha, Ofisi imeendelea kuimarisha huduma katika Ikulu ndogo ya Dodoma kwa kuvifanyia matengenezo makubwa vyoo vitano pamoja na sehemu ya kufulia.
 
41.   Mheshimiwa Spika, pamoja na utekelezaji wa mambo yaliyoainishwa, Ofisi ya Faragha ya Rais, vile vile imetekeleza majukumu yake mengine kama ifuatavyo:-
(i)        Ofisi imeendelea kuwaendeleza wafanyakazi wake katika kada mbali mbali. Kati ya wafanyakazi watano waliokuwa masomoni katika mwaka wa fedha uliopita, wafanyakazi wawili wamemaliza mafunzo yao kwa ufanisi katika ngazi ya Stashahada kwenye masomo ya Uongozi katika Utoaji Huduma katika Chuo cha Maendeleo ya Utalii Maruhubi. Wafanyakazi wengine wawili wanaendelea na mafunzo kama hayo katika ngazi ya Shahada na mwengine mmoja anaendelea na mafunzo ya Stashada katika fani ya Rasilimali Watu katika Chuo cha Utawala wa Umma, Tunguu. Aidha, Ofisi ya Faragha imewapatia nafasi za mafunzo ya Uongozi katika Utoaji Huduma, katika ngazi ya Stashada, wafanyakazi wengine wawili katika Chuo cha Maendeleo ya Utalii Maruhubi katika mwaka huu wa fedha. Jumla ya madereva wawili wamemaliza mafunzo ya muda mfupi ya kuendesha gari za viongozi na Ofisa mmoja ameshiriki katika mafunzo mafupi ya Sheria. Vile vile, Ofisa mmoja ameshiriki mafunzo ya muda mfupi ya Uchumi na Maendeleo ya Jamii katika Jamhuri ya Watu wa China yaliyofadhiliwa na Serikali ya nchi hiyo.
(ii)     Matengenezo makubwa ya maktaba ya Mheshimiwa Rais yamekamilika. Hatua inayofuata ni ununuzi wa samani pamoja na kuongeza vitabu kwa ajili ya maktaba hiyo.
(iii)    Ofisi imeendelea kuchapisha vitabu vya Hotuba mbali mbali za Mheshimiwa Rais, pamoja na kuweka kumbukumbu za hotuba na ziara mbali mbali za Rais katika DVD na CDs.
(iv)   Ofisi imetoa huduma zinazohitajika kwa wageni rasmi pamoja na kufanikisha sherehe mbali mbali zinazohusiana na Ofisi ya Faragha.
 
42.   Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2013/2014, Ofisi ya Faragha ya Rais inatarajia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha huduma za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
(ii)      Kuimarisha mazingira ya kazi;
(iii)    Kuendelea na matengenezo madogo madogo ya majengo ya Ikulu za Zanzibar; na
(iv)   Kujenga uwezo kwa wafanyakazi sita katika ngazi ya Stashahada na watatu ngazi ya Cheti.
 
43.   Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Faragha iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 2,197.2 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.
 

OFISI YA BARAZA LA MAPINDUZI

44.   Mheshimiwa Spika, Baraza la Mapinduzi ndio chombo kikuu cha kumsaidia na kumshauri Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika masuala mbali mbali ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Shughuli za Baraza la Mapinduzi zinaratibiwa na kusimamiwa na Ofisi ya Baraza la Mapinduzi chini ya Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi. Ofisi hii pia inajukumu la kuratibu na kusimamia vikao vya Kamati mbali mbali za Baraza la Mapinduzi ikiwa ni pamoja na Kamati ya Kitaalamu ya Makatibu Wakuu (Inter-Ministerial Technical Committee). Aidha, Baraza la Mapinduzi limeunda Kamati mbili kutoka kwenye Wajumbe wake, Kamati hizi zinaitwa Kamati ya Maendeleo ya Jamii na Kamati ya Fedha na Uchumi.
 
45.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi  ilitengewa TZS. 1,362.0  milioni kwa matumizi ya kawaida na hadi kufikia Machi 2013, Ofisi hii iliingiziwa TZS. 848.0 milioni sawa na asilimia 62.3 ya makadirio.
 
46.   Mheshimiwa Spika, Ofisi imeandaa semina mbili, moja kwa Masheha na Madiwani wote katika Kisiwa cha Pemba na nyengine kwa Viongozi Wakuu wa Serikali. Semina hizo zilikuwa na lengo la kutathmini utendaji kazi wa Serikali na kuwajuilisha Viongozi hasa katika Mikoa, Wilaya na Shehia juu ya dhamana zao, majukumu yao ya kila siku na nini hawapaswi kufanya. Jumla ya vikao 22 vya Baraza la Mapinduzi na 30 vya Kamati ya Makatibu Wakuu vimefanyika. Aidha, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi imeratibu mikutano 35 ya pamoja kati ya Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Viongozi na watendaji wa Wizara mbali mbali za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Kupitia vikao na mikutano hiyo masuala mbali mbali yaliweza kujadiliwa na ushauri kutolewa.
 
47.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi pia imefanya matengenezo ya jengo la Ofisi ikiwa ni pamoja na kukamilisha kazi ya kuezeka paa la Ofisi, matengenezo ya varanda (corridor), vyumba vinne na kuweka samani (shelves na viti) katika ukumbi wa mkutano unaotumika kwa mikutano ya Kamati ya Makatibu Wakuu.
 
48.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi, imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuendelea kuandaa vikao vya kujadili Rasimu za Sera, Sheria na Nyaraka mbali mbali zinazowasilishwa katika vikao vya Baraza la Mapinduzi na Kamati zake;
(ii)     Kuimarisha na kuendeleza ustawi wa Ofisi na kuimarisha mazingira ya kazi;
(iii)    Kuwajengea uwezo watumishi ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo; na
(iv)   Kutunza na kuhifadhi nyaraka na kumbukumbu muhimu za Ofisi.
49.   Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Baraza la Mapinduzi iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 1,379.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida.

IDARA YA MIPANGO, SERA NA UTAFITI

50.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti imeendelea na jukumu lake la kuratibu na kusimamia uandaaji wa Sera, Sheria na Mipango ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Aidha, Idara imeendelea na utekelezaji wa jukumu la kufanya tafiti mbali mbali pamoja na kufanya ufuatiliaji na tathmini ya miradi ya maendeleo.
 
51.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti, ilitengewa TZS. 466.9 milioni kwa ajili ya utekelezaji wa kazi za kawaida na TZS. 906.0 milioni kwa ajili ya miradi minne ya maendeleo. Hadi kufikia Machi 2013, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti imeingiziwa TZS. 188.0 milioni sawa na asilimia 40.3 ya makadirio ya matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 372.9 milioni kwa kazi za maendeleo sawa na asilimia 41.2.
 
52.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti imeratibu mikutano mitatu ya robo mwaka kwa ajili ya kufanya tathmini ya utekelezaji wa malengo ya bajeti, utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi na uandaaji wa ripoti. Aidha, Idara imefanya mapitio ya Muongozo wa Mpango wa Muda wa Kati wa Bajeti (MTEF) na Mipango Kazi ya Taasisi zote za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Unguja na Pemba.
 
53.   Mheshimiwa Spika, Idara imewawezesha watumishi watatu kuhudhuria mafunzo ya muda mrefu katika Shahada ya kwanza ya mipango ya maendeleo, Stashahada ya Teknologia ya Habari na Mawasiliano na Shahada ya pili ya Sheria. Aidha, wafanyakazi watano wamepatiwa mafunzo ya muda mfupi katika fani za Uchambuzi wa Bajeti na Uchumi, Sera na Udereva. Vile vile, Idara imetoa mafunzo ya siku mbili kuhusu Usimamizi na Tathmini ya Miradi ya Maendeleo kwa Maofisa Mipango 25 wa Taasisi za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
 
54.   Mheshimiwa Spika, Idara imeratibu utafiti kuhusu maoni ya wananchi juu ya taarifa zinazotolewa na Idara ya Mawasiliano - Ikulu ili kubaini mafanikio na changamoto ziliopo. Sambamba na hilo katika kuimarisha mfumo wa takwimu wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Idara imekamilisha mchakato wa kumpata Mshauri Elekezi wa kufanya utafiti juu ya mahitaji ya takwimu katika Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Hatua hii ya kuelewa mahitaji ya takwimu itaiwezesha Ofisi kujua mahitaji sahihi ya takwimu zake na namna ya kukusanya na kuzitumia takwimu hizo. Aidha, Idara imeendesha semina kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuhusu Sera mpya ya Serikali za Mitaa ya Zanzibar.
 
55.   Mheshimiwa Spika, Idara pia imeandaa taarifa jumuishi za utekelezaji wa malengo ya bajeti ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa mwaka wa fedha 2012/2013 za robo mwaka ya kwanza, ya pili na ya tatu za Taasisi zote za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Taarifa imeonesha kuwa utekelezaji kwa ujumla ni asilimia 70. Aidha, katika kipindi hiki Idara imekiimarisha kitengo cha kutunzia nyaraka kwa kukipatia vitendea kazi vikiwemo samani.
 
56.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha uwezo wa Idara katika Mipango, kuandaa na kuchambua Sera, kufanya Utafiti na shughuli za uratibu;
(ii)     Kuanzisha mfumo wa ufuatiliaji na tathmini;
(iii)    Kuimarisha uwezo wa watendaji wa Idara na wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
(iv)   Kuimarisha huduma za Teknolojia ya Habari na Mawasiliano; na
(v)     Kuimarisha mazingira ya kufanyia kazi ili kutoa huduma bora.
 
57.   Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Mipango, Sera na Utafiti iweze kutekeleza malengo yake ipasavyo, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 522.4 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 1,250.0 milioni kwa matumizi ya kazi za maendeleo.

IDARA YA UTUMISHI NA UENDESHAJI

58.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Utumishi na Uendeshaji ina jukumu la kusimamia shughuli za Utawala na Utumishi za siku hadi siku zikiwemo kusimamia Sheria na Kanuni za Utumishi kwa watendaji pamoja na kuweka mazingira mazuri ya utendaji kazi, kuratibu na kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Manunuzi na Ugavi, kuwaendeleza wafanyakazi kielimu pamoja na kusimamia maslahi yao.
 
59.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Utumishi na Uendeshaji, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, iliidhinishiwa TZS. 1,247.3 milioni kwa kazi za kawaida. Hadi kufikia Machi 2013, Idara hii iliingiziwa TZS. 680.0 milioni sawa na asilimia 54.5 ya makadirio ya matumizi ya kawaida.
 
60.   Mheshimiwa Spika, Idara imelipa stahili mbali mbali za wafanyakazi zikiwemo mishahara, michango ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii, likizo kwa wafanyakazi, posho la kujikimu, gharama za safari za ndani na sare kwa wafanyakazi. Aidha, Idara imenunua vifaa mbali mbali vya kuandikia na vifaa vya usafi. Vile vile, Idara imesimamia utekelezaji kivitendo wa Sheria ya Manunuzi na Ugavi kwa kuendesha vikao vinane vya Bodi ya Zabuni pamoja na vikao vya Kamati ya Ukaguzi wa Ndani.
 
61.   Mheshimiwa Spika, wafanyakazi wamejengewa uwezo kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu wafanyakazi watatu katika ngazi ya Shahada ya Uzamili na wafanyakazi watano Stashahada. Vile vile, Idara imewapatia mafunzo ya muda mfupi wafanyakazi watatu katika fani ya Udereva, Uongozi wa Rasilimali Watu na Lugha za Alama pamoja na kuwapatia semina wafanyakazi 80 juu ya maadili ya kazi na utunzaji wa siri za Ofisi na Uimarishaji wa masjala za Ofisi. Sambamba na hayo, Idara imeratibu mafunzo ya muda mrefu na mfupi kwa Wafanyakazi 207 wa Idara na Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Kiambatanisho Nambari 5 kinatoa ufafanuzi zaidi.
 
62.   Mheshimiwa Spika, katika kuyapatia hati miliki majengo ya Ikulu na nyumba za Serikali, gharama za upimaji wa maeneo ya majengo zimelipwa kwa lengo la kuyatafutia hati miliki. Jengo la Ikulu ya Mnazi Mmoja limeshapatiwa hati miliki na majengo yaliyobakia hati zake zimeshafanyiwa uhakiki na zitapatikana hivi karibuni. Sambamba na hayo, Idara imeandaa Makisio ya mishahara na Mipango ya Matumizi ya Rasilimali Watu (Norminall Roll) pamoja na kufanya mapitio na marekebisho ya Miundo ya Utumishi (Scheme of Service) na kuwasilishwa Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa hatua ya kufanyiwa kazi.
 
63.   Mheshimiwa Spika, Idara inaendelea na kazi ya uhakiki wa mahitaji na kuandaa Mpango wa Mafunzo wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambapo kazi hiyo inategemewa kukamilika katika mwaka wa fedha 2013/2014.
 
64.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ya Utumishi na Uendeshaji inakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)            Kuongeza ufanisi wa kazi kwa kuimarisha mazingira ya utendaji kazi na maslahi ya wafanyakazi;
(ii)          Kutekeleza Sheria ya Manunuzi kwa kuendesha vikao 12 vya Bodi ya Zabuni na vikao vinne vya Kamati ya Ukaguzi wa ndani;
(iii)         Kuwajengea uwezo wafanyakazi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu na mfupi ndani na nje ya nchi;
(iv)        Kuendeleza uhusiano wa kimichezo kwa wafanyakazi;
(v)          Kuratibu masuala mtambuka pamoja na kupima afya za wafanyakazi ili kubaini mienendo ya hali zao na kupatiwa ushauri wa kinga na matibabu kwa wakati;
(vi)        Kuandaa makisio ya mishahara na kupanga matumizi ya Rasilimali Watu ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi; na
(vii)       Kusimamia utendaji na uwajibikaji wa wafanyakazi.
 
65.   Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Utumishi na Uendeshaji iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 1,274.6 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

IDARA YA MAWASILIANO - IKULU

66.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Mawasiliano - Ikulu imeendelea na utekelezaji wa majukumu yake ya msingi ya kupokea na  kutoa taarifa za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuhusu utekelezaji wa Sera na Mipango ya Serikali. Aidha, Idara ya Mawasiliano – Ikulu imepewa jukumu la kuhakikisha kuwa taarifa za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi zinazotolewa kwa wananchi ni sahihi na katika wakati muafaka.
67.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Mawasiliano – Ikulu ilitengewa jumla ya TZS. 174.9 milioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na hadi kufikia Machi 2013,  iliingiziwa TZS. 132.0 milioni sawa na asilimia 75.5 ya makadirio ya matumizi.
 
68.    Mheshimiwa Spika, Idara ya Mawasiliano – Ikulu imeendelea kuimarisha mawasiliano baina ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Taasisi za Serikali na wananchi na imeandaa na kurusha hewani vipindi 44 vya Televisheni katika Shirika la Utangazaji la Zanzibar (ZBC). Vipindi hivyo vilihusu ziara za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ndani na nje ya nchi na hotuba za Mheshimiwa Rais. Aidha, Idara imeandaa na kurusha hewani vipindi 17 vya Redio kupitia Shirika la Utangazaji la Zanzibar, vipindi ambavyo vilizungumzia masuala ya utalii kwa wote, uwezeshaji wananchi kiuchumi na uwajibikaji kwa wafanyakazi. Orodha ya vipindi vilivyorushwa hewani inaoneshwa katika Viambatanisho Nambari 6 na 7.
 
69.   Mheshimiwa Spika, Idara pia, imeandaa na kuchapisha nakala 3,000 za kalenda zenye kuonyesha shughuli zinazotekelezwa na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika nyanja za kijamii, kiuchumi na kidiplomasia. Vile vile, Idara iliandaa na kuchapisha matoleo matatu ya Jarida la ‘IKULU’ lenye kuonyesha shughuli mbali mbali za maendeleo pamoja na utekelezaji wa ahadi za Mheshimiwa Rais alizozitoa kwa wananchi katika nyakati tofauti.
 
70.   Mheshimiwa Spika, Idara imeendelea kuwajengea uwezo wa kiutendaji watumishi wake ili kuimarisha ueledi katika fani ya mawasiliano. Katika kufanikisha azma hii, Idara imelipia gharama za mafunzo ya muda mfupi na mrefu kwa watumishi watatu katika fani za Ukatibu Muhtasi, Matumizi ya Kompyuta na namna ya kuandaa majarida.
 
71.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ya Mawasiliano – Ikulu imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)      Kuendeleza taswira nzuri ya Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
(ii)    Kuimarisha mazingira ya kazi katika Idara ili iweze kutoa huduma nzuri; na
(iii)   Kuwajengea uwezo wafanyakazi wa Idara ya Mawasiliano.
 
72.   Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Mawasiliano – Ikulu iweze kutekeleza majukumu yake ipasavyo, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 242.7 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

IDARA YA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA NA URATIBU WA WAZANZIBARI WANAOISHI NJE YA NCHI

73.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Uratibu wa Wazanzibari Wanaoishi Nje ya Nchi imeendelea na majukumu yake ya kuratibu ushiriki wa Zanzibar katika mikutano mbali mbali ya Kikanda na Kimataifa na kuhakikisha kwamba Zanzibar inafaidika na ushiriki huo na fursa zinazotokana na mikutano hiyo. Aidha, Idara ina jukumu la kuwatafuta, kuwatambua na kuwashajihisha Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi (Diaspora) ili kuchangia katika kujenga uchumi mzuri na kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii Zanzibar.
 
74.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Uratibu wa Wazanzibari Wanaoishi Nje ya Nchi, ilitengewa TZS. 884.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida na hadi kufikia Machi 2013, iliingiziwa TZS. 364.8 milioni sawa na asilimia 41.3 ya makadirio ya matumizi.
 
75.   Mheshimiwa Spika, Zanzibar imeshiriki kikamilifu katika mikutano ya Kikanda ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) na Mkutano wa Nchi Zinazozungukwa na Bahari ya Hindi (IOR). Idara kwa kushirikiana na Wizara za SMZ inafuatilia maamuzi ya vikao hivyo kwa manufaa ya Zanzibar. Wizara ya Mifugo na Uvuvi tayari inafuatilia miradi ya uvuvi inayotokana na makubaliano ya mkutano uliofanyika India mwezi Novemba 2012. Aidha, Ofisi inaendelea kufuatilia hatua za mwisho za kuanzisha Taasisi ya Kiswahili ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wamesharidhia kuanzishwa kwa Taasisi hiyo hapa Zanzibar na kazi iliyobaki sasa ni utayarishaji wa makubaliano na Makao Makuu ya Jumuiya.
76.   Mheshimiwa Spika, Idara pia, ilishiriki katika mkutano wa Diaspora uliofanyika nchini Oman kufuatia ziara ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Mrisho Kikwete. Katika mkutano huo ajenda kuu ilikua ni kujadili namna ambavyo Wazanzibari wanaoishi Oman na nchi za Mashariki ya Kati wanavyoweza kushiriki na kuchangia maendeleo ya Zanzibar. Matokeo ya mikutano hiyo imepelekea Benki ya Watu wa Zanzibar kuingia mkataba na Benki ya Muscat kufungua akaunti maalum ambayo itawezesha Diaspora hao kutuma fedha zao Zanzibar bila ya usumbufu kupitia akaunti hiyo.
 
77.   Mheshimiwa Spika, matayarisho ya Sera ya Diaspora yameanza baada ya kupatikana Mshauri Elekezi, pamoja na hatua hiyo muhimu, Shirika la Uhamiaji la Kimataifa (IOM) limeahidi kuipitia Rasimu ya Sera hiyo kila baada ya hatua na kutoa ushauri wa kitaalamu. Kazi hiyo inatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2013/2014.
 
78.   Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, Idara imeendelea kuwajengea uwezo wa kiutendaji watumishi wawili, mmoja katika ngazi ya Shahada ya Uzamili (Uhasibu) na mwengine katika Stashahada (Utawala wa Umma).
 
79.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Uratibu wa Wazanzibari Wanaoishi Nje ya Nchi imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)      Kuhakikisha kuwa Zanzibar inashiriki kikamilifu katika mikutano mbali mbali ya Kikanda na Kimataifa;
(ii)    Kuwashajihisha Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi kuchangia katika maendeleo ya kiuchumi na kijamii;
(iii)   Kuwajengea uwezo Wazanzibari katika sekta mbali mbali kupitia wataalamu wa Kizanzibari wanaoishi nje ya nchi (Diaspora);
(iv)  Kuitangaza dhana ya Diaspora ndani na nje ya nchi;
(v)    Kuandaa Programu maalum itakayorahisisha upatikanaji wa taarifa kwa Diaspora kuhusu maendeleo yanayopatikana katika nchi yao;
(vi)  Kuandaa programu maalum ya mafunzo ya kuongeza uwezo wa wataalamu wa Serikali katika majadiliano ya Kikanda; na
(vii) Kuwaongezea uwezo wafanyakazi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na mrefu.
 
80.   Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Uratibu wa Wazanzibari Wanaoishi Nje ya Nchi iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 873.0 milioni kwa matumizi ya kawaida.

KITENGO CHA USALAMA WA SERIKALI (GSO) ZANZIBAR

81.   Mheshimiwa Spika, Kitengo cha Usalama wa Serikali kimeendelea kufanya kazi zake kama kilivyopangiwa kwa mujibu wa Sheria. Kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Kitengo cha Usalama wa Serikali kilitengewa TZS. 54.9 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi kufikia mwezi Machi 2013, kiliingiziwa TZS. 29.0 milioni sawa na asilimia 52.8 ya makadirio ya matumizi.
 
82.     Mheshimiwa Spika, kazi kubwa za kitengo hiki ni za kufanya upekuzi endelevu kwa wafanyakazi wanaotaka kuajiriwa. Katika mwaka wa fedha 2012/2013, Kitengo cha Usalama wa Serikali (GSO) kimefanya ukaguzi katika Taasisi tisa za Serikali. Taasisi hizo ni Kamisheni ya Utalii Zanzibar, Wizara ya Biashara Viwanda na Masoko – Unguja na Pemba, Kituo cha Matrekta Macho Mane – Pemba, Wizara ya Kilimo na Mali Asili – Pemba, Shirika la Bima – Unguja na Pemba, Chuo cha Kilimo Kizimbani – Unguja, Viwanja vya Ndege – Unguja na Pemba,  Mamlaka ya Kusimamia Uvuvi wa Bahari Kuu – Unguja na Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati. Aidha, katika kipindi hiki Kitengo kilifanya upekuzi wa kiusalama kwa wafanyakazi 168 wa Taasisi mbali mbali za Serikali na kutoa ushauri wa kiusalama kwa Taasisi hizo. Taasisi zilizokaguliwa zimeoneshwa kwenye Kiambatanisho Nambari 8.
 
83.   Mheshimiwa Spika, Kitengo kimeendesha mafunzo ya utunzaji wa nyaraka na siri za Serikali kwa watumishi wa Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko. Mafunzo hayo yalihusu udhibiti wa siri za Serikali na kuelimisha watumishi juu ya umuhimu wa nyaraka na kumbukumbu za Serikali. Aidha, Kitengo kimeendesha mafunzo kama hayo katika Chuo cha Kilimo Kizimbani, Wahudumu, Madereva, Maafisa masjala wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Makatibu Muhtasi wa Mawaziri na Makatibu Wakuu wa Wizara zote za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
 
84.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/214, Kitengo cha Usalama wa Serikali kimepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha shughuli za upekuzi kwa watumishi kabla na baada ya kuajiriwa;
(ii)     Kuimarisha ukaguzi wa majengo, miundombinu na mali za Serikali;
(iii)    Kuwajengea uwezo watumishi juu ya utunzaji na udhibiti wa siri za Serikali;
(iv)   Kufanya tathmini ya utekelezaji wa maelekezo yanayotolewa kwa Wizara/Taasisi wakati wa ukaguzi; na
(v)                 Kuimarisha mazingira ya kufanyia kazi
85.   Mheshimiwa Spika, ili Kitengo cha Usalama wa Serikali (GSO) kiweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 61.6 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

OFISI YA USAJILI NA KADI ZA UTAMBULISHO

86.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho imefanya kazi zake kwa ufanisi kwa mujibu wa Sheria. Kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho iliidhinishiwa TZS. 1,593.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi mwezi Machi  2013, iliingiziwa TZS. 1,086.9 milioni sawa na asilimia 68.2 ya makadirio.  
 
87.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho imefanya usajili wa Wazanzibari wakaazi 26,594 waliotimiza masharti ya usajili ikiwa ni ongezeko la asilimia 151 ukilinganisha na idadi ya Wazanzibari Wakaazi 10,578 waliosajiliwa katika mwaka 2011/2012. Aidha, Ofisi imetengeneza vitambulisho vipya 18,532 vilivyomaliza muda wake wa matumizi na imetengeneza vitambulisho 5,178 kwa wananchi waliopoteza na walioomba kufanya marekebesho halali ya taarifa zao binafsi.
 
88.   Mheshimiwa Spika, Ofisi imeendelea kutengeneza vitambulisho vya wafanyakazi wa Serikali na Taasisi zake ambapo jumla ya vitambulisho 2,410 vimetengenezwa. Aidha, jumla ya vitambulisho 1,347 vya Mashirika ya Serikali na 2,188 vya Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar vimetengenezwa.
 
89.   Mheshimiwa Spika, naomba kutoa taarifa kuwa Sheria Namba 7/2005 imefanyiwa marekebisho kuwa Sheria Namba 14/2012 ili kuruhusu kutoa vitambulisho maalumu kwa wageni wanaoishi Zanzibar. Utaratibu wa kutoa vitambulisho umekamilika na Serikali inategemea kuanzisha rasmi utoaji wa vitambulisho hivyo katika mwaka ujao wa fedha wa 2013/2014.
 
90.   Mheshimiwa Spika, katika kuongeza uelewa wa wananchi juu ya umuhimu wa matumizi bora ya Kitambulisho cha Mzanzibari, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho imeandaa na kurusha hewani jumla ya vipindi 18 kupitia Shirika la Utangazaji la Zanzibar. Aidha, Ofisi imeendelea kuwajengea uwezo wa kitaaluma wafanyakazi wake katika ngazi za Cheti, Stashahada na Shahada.
 
91.   Mheshimiwa Spika, Ofisi imefanyiwa ukaguzi na Shirika la Viwango vya Kimataifa (I Q Net) juu ya mfumo na viwango. Taarifa ya ukaguzi huo imethibitisha kuwa mfumo na taratibu zinazotumika ziko katika kiwango kinachokubalika Kimataifa. Sambamba na hilo, Ofisi imenunua seti 15 za mashine za kisasa za usajili. Mashine hizo zinategemewa kusaidia shughuli za usajili katika Ofisi za Wilaya.
 
92.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho inakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuwasajili Wazanzibari Wakaazi waliotimiza masharti kwa mujibu wa Sheria na kuwapatia vitambulisho;
(ii)     Kutunza taarifa za waliosajiliwa katika database maalum;
(iii)    Kuwasajili na kutoa vitambulisho maalum kwa wageni wanaoishi Zanzibar kwa ruhusa maalum;
(iv)   Kuzishajihisha Taasisi za Serikali kutumia taarifa zilizowekwa katika “Database” ya Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho kwa usalama na kiuchumi;
(v)     Kuratibu masuala mtambuka pamoja na kutoa elimu ya kujikinga na maambukizi mapya ya UKIMWI kwa wafanyakazi;
(vi)   Kuendelea kuwajengea uwezo kielimu wafanyakazi wa Ofisi; na
(vii)  Kuongeza ufanisi kazini ikiwa ni pamoja na kuwapatia wafanyakazi stahili zao.
 
93.   Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 2,055.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida.

OFISI YA OFISA MDHAMINI – PEMBA

94.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Ofisa Mdhamini – Pemba ina jukumu la kuratibu na kusimamia shughuli za utawala na huduma za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Pemba. Aidha, Ofisi ya Ofisa Mdhamini inawajibu wa kuratibu na kusimamia ziara za Viongozi  Wakuu wa Kitaifa na Kimataifa Kisiwani Pemba.
 
95.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Ofisa Mdhamini – Pemba iliidhinishiwa jumla ya TZS. 462.4 milioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida na hadi kufikia Machi 2013, iliingiziwa TZS. 385.2 milioni sawa na asilimia 83.3 ya makadirio ya matumizi.
 
96.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Ofisa Mdhamini Pemba imeendelea kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Pemba kwa kufanya ufuatiliaji na tathmini ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Taasisi za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Pemba. Aidha, Ofisi imeratibu na kuwawezesha maofisa kushiriki katika mikutano na vikao mbali mbali vilivyofanyika Unguja vikiwemo vikao vya Bodi ya Zabuni, Bajeti, na Uwasilishaji wa Ripoti za Utekelezaji.
97.   Mheshimiwa Spika, Ofisi imewawezesha wafanyakazi watatu kupata mafunzo ya Stashahada katika fani ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano na Vyakula na Vinywaji. Vile vile, mfanyakazi mmoja amepatiwa mafunzo ya muda mfupi juu ya zabuni za majengo na ukandarasi. Aidha, Ofisi iliandaa mafunzo ya siku moja kwa wafanyakazi 50 wa Taasisi za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi - Pemba juu ya utunzaji wa siri za Serikali, maadili, Sheria na Kanuni za kazi.
 
98.   Mheshimiwa Spika, katika kuongeza kasi ya mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya VVU katika sehemu za kazi, Ofisi imetoa mafunzo kwa wafanyakazi 50 juu ya kujikinga na maambukizi mapya ya VVU. Katika mafunzo hayo wafanyakazi hao wameazimia kuweka siku maalum kwa ajili ya kuendesha zoezi la kupata ushauri nasaha na kupima afya zao kwa hiari.
 
99.   Mheshimiwa Spika, Ofisi imesimamia kazi ya kufanya matengenezo katika majengo ya Ikulu ya Mkoani. Kazi nyengine zilizofanyika ni pamoja na kupaka rangi katika jengo la Ofisi ya Ofisa Mdhamini, uwekaji wa mtandao mpya wa maji Ofisi Kuu na Ikulu ya Chake Chake ili kupata huduma hiyo kwa urahisi.
 
100.      Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Ofisi ya Ofisa Mdhamini – Pemba imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuwajengea uwezo wafanyakazi sita katika mafunzo ya muda mfupi na mrefu;
(ii)     Kuimarisha uwezo wa Ofisi katika kuratibu Mipango, Sera na Utafiti;
(iii)    Kuimarisha mazingira bora ya kufanyia kazi, stahili na kutoa huduma bora;
(iv)   Kuimarisha uwezo wa utendaji wa Serikali za Mitaa – Pemba; na
(v)     Kuhamasisha wafanyakazi juu ya uwelewa wa masuala mtambuka ikiwemo UKIMWI, Jinsia na Mazingira.
 
101.   Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Ofisa Mdhamini – Pemba iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 645.8 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida.

IDARA YA URATIBU WA TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA

102.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ilitengewa TZS. 701.4 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 1,291.0 milioni ikiwa ni Ruzuku kwa Baraza la Manispaa. Hadi Machi 2013, iliingiziwa TZS. 399.0 milioni sawa na asilimia 56.9 kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 990.0 milioni sawa na asilimia 76.7 ambazo ni Ruzuku ya Baraza la Manispaa.
 
103.   Mheshimiwa Spika, Idara kupitia Tume ya Kurekebisha Sheria, imeanza mchakato wa kuandaa Sheria mpya ya Vileo kufuatia kupitwa na wakati Sheria ya zamani (Cap Na. 163/1928). Kwa kuwa Sheria hiyo inaigusa Jamii, mchakato wake wa kuiandaa uliwashirikisha wadau na wananchi katika maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba. Mswada wa Sheria hiyo unatarajiwa kuwasilishwa katika Baraza la Wawakilishi katika mwaka ujao wa fedha 2013/2014.
 
104.   Mheshimiwa Spika, Idara imeratibu mkutano mmoja wa mashirikiano ya pamoja baina ya Viongozi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Ofisi ya Waziri Mkuu (TAMISEMI) uliofanyika Pemba kuanzia tarehe 12 hadi 14 Desemba, 2012. Lengo la mkutano huo ni kubadilishana mawazo, uzoefu na utaalamu miongoni mwa Viongozi na watendaji wa pande zote mbili katika kuratibu na kusimamia utekelezaji wa majukumu ya Mamlaka ya Serikali za Mikoa na Serikali za Mitaa.
 
105.   Mheshimiwa Spika,  mkutano huo wa mashirikiano uliazimia mambo muhimu yakiwemo kuunda kikosi kazi kwa pande zote mbili kitakachoangalia uwepo wa Sheria ndogo ndogo za Serikali za Mitaa na utekelezaji wake katika usimamizi wa usafi wa mazingira pamoja na ziara za kubadilishana uzoefu. Maazimio hayo ni muhimu kwa maendeleo ya Serikali za Mikoa na Serikali za Mitaa. Hivyo basi, Ofisi yangu imeanza kuyafanyia kazi maazimio hayo hatua kwa hatua ikiwemo ziara ya mafunzo kwa Watendaji na Viongozi wa Serikali za Mitaa katika Jiji la Mwanza ya kujifunza na kubadilishana uzoefu juu ya usafi wa Mji na mazingira.  
 
106.   Mheshimiwa Spika, Idara imetoa mafunzo kuhusu utawala bora katika usimamizi wa majukumu ya Serikali za Mitaa kwa Waheshimiwa Madiwani wa Kamati za Fedha, Sheria na Afya katika Halmashauri tano. Aidha, Idara imefuatilia utekelezaji wa miradi ya Halmashauri zote Unguja na Pemba. Matokeo ya jumla yanaonesha kuwa kiwango cha utekelezaji wa shughuli zilizopangwa kinaridhisha.
 
107.   Mheshimiwa Spika, Idara iliendelea kuwawezesha watumishi wake kuhudhuria mafunzo ya muda mfupi na mrefu. Watumishi watatu walipatiwa mafunzo ya muda mfupi katika fani za Utawala na Uongozi wa Serikali za Mitaa na wawili mafunzo ya muda mrefu katika fani za Utunzaji wa Kumbukumbu na Usimamizi wa Rasilimali Watu.
 
108.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha mazingira bora kazini na utoaji wa huduma;
(ii)     Kujenga uwezo wa watumishi;
(iii)    Kuimarisha uratibu wa Taasisi za Mikoa, Wilaya, Serikali za Mitaa na Wadau wa maendeleo; na
(iv)   Kuimarisha ushirikishwaji wa wananchi katika utawala wa kidemokrasia.
 
109.   Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 643.6  milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 1,200.0 milioni ikiwa ni Ruzuku kwa Baraza la Manispaa.

MAMLAKA ZA SERIKALI ZA MIKOA

110.   Mheshimiwa Spika, Mamlaka za Serikali za Mikoa zimepewa jukumu la kuratibu na kusimamia utekelezaji wa maagizo ya Serikali katika maeneo yao ya utawala. Aidha, iliratibu kwa ufanisi mkubwa shughuli za kupata maoni ya wananchi katika Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia, Mikoa na Wilaya ilisimamia kikamilifu zoezi la Sensa ya Watu na Makaazi ya mwaka 2012 kupitia Kamati za Sensa za Wilaya na Mikoa kwa kushirikiana na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali. Pamoja na hayo, naomba kutoa maelezo kuhusu utekelezaji wa malengo ya Mamlaka za Serikali za Mikoa kwa mwaka 2012/2013 na utekelezaji wa malengo yaliyopangwa kwa mwaka 2013/2014.

MKOA WA MJINI MAGHARIBI

111.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013 Mkoa wa Mjini Magharibi uliidhinishiwa TZS. 1,099.0 milioni kwa kazi za kawaida na hadi kufikia mwezi wa Machi 2013, Mkoa huu umeingiziwa TZS. 709.4 milioni sawa na asilimia 64.5 ya makadirio ya matumizi.
 
112.   Mheshimiwa Spika, hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa wa Mjini Magharibi imeendelea kuwa nzuri ingawa kumejitokeza matukio ya uhalifu ambayo yaliishitua jamii. Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa imekutana katika vikao vyake mbali mbali kupanga mikakati ili kuhakikisha kuwa vitendo hivyo vya uhalifu vinadhibitiwa. Mkoa umeendelea kushajihisha uimarishaji wa ulinzi shirikishi katika Shehia zote za Mkoa. Hata hivyo, mkazo zaidi umewekwa katika Shehia za Kianga, Sharifumsa, Kwaalinatu na Amani. Kutokana na hatua hiyo, matokeo yanaonesha kuwa uhalifu umepunguwa na hasa utumiaji wa madawa ya kulevya katika Shehia hizo.
 
113.   Mheshimiwa Spika, Operesheni maalum ya kuwaondosha wanyama wanaozurura ovyo Mjini pamoja na wafanyabiashara wanaofanya biashara kiholela tena sehemu zisizoruhusiwa katika Masoko imefanyika. Operesheni hii inayosimamiwa na Mkoa kupitia Baraza la Manispaa na Halmashauri ya Wilaya ya Magharibi imeweza kudhibiti uzururaji wa wanyama na zaidi ya wanyama 190 wamekamatwa na kupelekwa katika maeneo maalum yaliyotengwa. Kwa wale wanyama waliogombolewa huwa wanarejeshewa wenyewe kwa masharti maalum yakiwemo wanyama hao kupelekwa nje ya Mji na gharama za upelekaji huo hulipwa na mmiliki wa mnyama husika. Aidha, wanyama wote waliogombolewa huwekwa rangi maalum na pindipo akikamatwa tena hatua za kisheria huchukuliwa dhidi ya mmiliki.
114.   Mheshimiwa Spika, Katika kuimarisha ufanisi na utendaji kazi, Mkoa umefanikiwa kulipa Stahili za wafanyakazi, kununua vifaa vya kutendea kazi, kuanza matengenezo madogo na makubwa ya Ofisi. Aidha, mafunzo ya Sheria Namba 2/2011 ya Usimamizi wa Utumishi wa Umma Zanzibar yametolewa kwa wafanyakazi. Wafanyakazi 13 wamesomeshwa katika ngazi ya Stashahada ya Uzamili, Stashahada na Cheti kwa fani za Uhasibu, Uandishi wa Habari, Utunzaji wa Kumbukumbu, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Rasilimali Watu, Ukatibu Muhtasi na Utawala wa Umma. Mchanganuo wa watendaji waliopatiwa mafunzo unaonekana katika Kiambatanisho Nambari 9.
 
115.   Mheshimiwa Spika, mafunzo juu ya kupambana na UKIMWI na kupiga vita unyanyasaji wa kijinsia yametolewa kwa wafanyakazi 91, Masheha 45, na makundi matatu ya kijamii yakiwemo watu wenye ulemavu, watu wenye kuishi na VVU na makundi yaliyo katika mazingira hatarishi. Kamati za mazingira za Wilaya zimeundwa na kuendesha vikao, ufuatiliaji na uhamasishaji wananchi juu ya uhifadhi wa mazingira, usafishaji wa misingi ya maji machafu pamoja na upandaji wa miti.
 
116.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umeratibu na kusimamia miradi mbali mbali iliyoanzishwa na wananchi. Utekelezaji wa miradi hiyo kwa hatua mbali mbali unaonekana katika Kiambatanisho Nambari 10. Aidha, jumla ya vikundi 51 vya SACCOS na Ushirika vimetembelewa na kupatiwa ushauri wa kuviendeleza vikundi vyao.
 
117.   Mheshimiwa Spika, kazi nyengine zilizotekelezwa na Mkoa ni pamoja na:-
(i)          Kukutana na Wakurugenzi Mipango, Sera na Utafiti wa Wizara 16 za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa azma ya kuimarisha na kusaidia utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika Mkoa;
(ii)        Utatuzi wa migogoro kumi na moja ya ardhi kati ya 34 iliyoripotiwa pamoja na kutoa mafunzo juu ya matumizi bora ya ardhi kwa jamii;
(iii)       Kufuatilia na kutoa mafunzo ya uwekaji wa kumbukumbu katika Shehia 27 kati ya 84;
(iv)      Kufuatilia kesi saba za udhalilishaji wa wanawake na watoto;
(v)        Kusimamia uandikishaji wa watoto 13,321 waliofikia umri wa kuanza darasa la kwanza;
(vi)      Kuhamasisha ukulima wa kilimo cha mpunga ambapo jumla ya ekari 1,912 zimelimwa kati ya ekari 1,800 zilizolengwa awali na ekari 1,042 kati ya ekari 917 za mazao ya chakula na ekari 237 za mboga mboga;
(vii)     Wananchi 63 wamepatiwa misaada ya kijamii na kiuchumi; na
(viii)   Utoaji wa mafunzo juu ya Uibuaji Miradi, Upangaji wa Mipango na Usimamizi wa Fedha kwa Wajumbe wa Kamati za Maendeleo za Shehia 25 na kuwashirikisha Wenyeviti na Makatibu pamoja na washika fedha wa Kamati hizo.
 
118.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mkoa wa Mjini Magharibi unatarajia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha kiwango cha utendaji kwa wafanyakazi wa Mkoa wa Mjini Magharibi na Sekta ziliopo;
(ii)     Kuimarisha hali ya ulinzi na usalama ndani ya Mkoa;
(iii)    Kuhakikisha jamii yenye afya njema; na
(iv)   Kuhakikisha maendeleo endelevu kwa jamii.
 
119.   Mheshimiwa Spika, ili Mkoa wa Mjini Magharibi uweze kutekeleza malengo iliyojipangia kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 1,455.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida.

MKOA WA KUSINI UNGUJA

120.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Mkoa uliidhinishiwa TZS. 1,064.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi mwezi Machi 2013, uliingiziwa TZS. 680.4 milioni sawa na asilimia 63.9 ya fedha zilizoombwa.
 
121.   Mheshimiwa Spika, kwa ujumla hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa imezidi kuimarika. Kamati ya Ulinzi na usalama ilifanya vikao tisa kutathmini hali hiyo ndani ya Mkoa. Aidha, kikao kimoja cha Kamati ya Maendeleo ya Mkoa (RDC) kimefanyika na vikao vitatu kujadili utekelezaji na uratibu wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010.
 
122.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umefanya ukaguzi katika vituo 17 vya mitihani vya Wilaya zote mbili kati ya vituo 29 viliomo katika Mkoa. Aidha, Mkoa uliratibu kikao kimoja kilichojadili mbinu za kukabiliana na utoro maskulini. Mikakati iliobuniwa na kutekelezwa katika Mkoa imesaidia kupunguza tatizo la utoro ambapo katika hatua ya awali wanafunzi 18 wa Skuli ya Charawe wamerejeshwa Skuli na kuendelea tena na masomo.
 
123.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umefuatilia hali ya usambazaji wa maji safi na salama. Miradi ya maji safi na salama ndani ya Mkoa inaendelea vizuri ikiwemo ujenzi wa matangi ya maji yaliopo Machui, Jumbi na Pongwe. Aidha, ulazaji wa mabomba ya maji safi katika Shehia za Chwaka na Miwani umekamilika na huduma imeanza kupatikana.
 
124.   Mheshimiwa Spika, sambamba na hayo, Mkoa umesimamia kikamilifu kilimo cha mpunga ambapo jumla ya ekari 1,444.5 za mpunga katika Wilaya ya Kati na ekari 119.0 katika Wilaya ya Kusini zimechimbwa na kuburugwa. Hatua hii inafanya jumla ya ekari zilizochimbwa, kuburugwa na kupandwa katika Mkoa wa Kusini Unguja kufikia 1,563.5.
 
125.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umeratibu mchakato wa kuwatambua watoto wanaoishi katika mazingira magumu na hatarishi. Katika utambuzi huo jumla ya watoto 35 wametambuliwa na kupatiwa msaada wa sare za skuli, viatu na vifaa vya kusomea. Aidha, katika kuufanya utaratibu huu uwe endelevu, Mkoa umetenga fedha kwa ajili ya kuwasaidia watoto hao.
 
126.   Mheshimiwa Spika, kazi nyengine zilizotekelezwa na Mkoa ni pamoja na:-
(i)          Kuanza ujenzi wa Ofisi ya Wilaya ya Kati hadi kufikia hatua ya kuinua msingi;
(ii)        Kusimamia matengenezo ya vyombo vya usafiri pamoja na ununuzi wa samani na vifaa vya Ofisi;
(iii)       Kuwajengea uwezo wa kiutendaji wafanyakazi wake ambapo wafanyakazi saba wamepatiwa mafunzo ya muda mfupi na mrefu katika fani za Upangaji na Usimamizi wa Miradi, Uhasibu na Udereva; na
(iv)      Kutoa taaluma kwa wafanyakazi wake juu ya namna ya kujikinga na maambukizi mapya ya VVU. Jumla ya wananchi 85 nao waliweza kupatiwa ushauri nasaha na kupima VVU kwa hiari wakati wa Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani.
 
127.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mkoa wa Kusini Unguja umekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)          Kusimamia shughuli za ulinzi na usalama;
(ii)        Kuratibu, kusimamia, kufuatilia na kusaidia utekelezaji wa shughuli za sekta mbali mbali;
(iii)       Kuwajengea uwezo wafanyakazi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na mrefu ili kuongeza ufanisi kazini;
(iv)      Kusimamia na kuzitumia ipasavyo rasilimali watu na vitu katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii;
(v)        Kuendeleza jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Wilaya na matengenezo madogo madogo; na
(vi)      Kuratibu shughuli Mtambuka zikiwemo za UKIMWI, mazingira na masuala ya watu wenye ulemavu.
 
128.   Mheshimiwa Spika, ili Mkoa wa Kusini Unguja uweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 1,147.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

MKOA WA KASKAZINI UNGUJA

129.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Mkoa wa Kaskazini Unguja ulitengewa TZS. 1,083.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi Machi 2013, uliingiziwa TZS. 735.0 milioni sawa na asilimia 67.9 ya makadirio ya matumizi ya kawaida.
 
130.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umeratibu vikao sita vya Kamati ya Ulinzi na Usalama ambavyo vilijadili masuala mbali mbali na kupitia taarifa za hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa. Hali ya usalama katika Mkoa imeendelea kuimarika kufuatia hali ya udhibiti wa vitendo vinavyoashiria uvunjifu wa amani.
 
131.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umeendesha mikutano mitano ya kuhamasisha wananchi juu ya umuhimu wa kushiriki katika utekelezaji wa Miradi ya maendeleo pamoja na kufanya mikutano miwili ya Kamati ya Maendeleo ya Mkoa na mikutano sita ya Kamati za Maendeleo ya Wilaya. Mkoa ulisimamia utekelezaji wa miradi mbali mbali ya wananchi ikiwemo ujenzi wa mabanda matatu ya Skuli ya Matetema, ujenzi wa Skuli ya Kidagoni,  ujenzi wa mabanda mawili ya Skuli ya Pangeni, ujenzi wa ukumbi wa kufanyia mitihani, ujenzi wa maktaba Tumbatu Jongowe na ujenzi wa kituo cha Afya Bumbwini Kiongwe. Aidha, Mkoa ulikuwa na jumla ya migogoro ya ardhi 20 ambayo imeripotiwa. Katika jitihada zake za kutatua migogoro hiyo, minane iliyopo katika maeneo ya Matemwe, Kiwengwa, Pwani Mchangani na Nungwi imetatuliwa, migogoro minne imepelekwa mahakamani kutokana na utata wake. Jumla ya migogoro minane imo katika hatua ya kupatiwa ufumbuzi.
 
132.   Mheshimiwa Spika, wafanyakazi wa Mkoa wameendelea kujengewa uwezo kwa kuwapatia  mafunzo ya muda mrefu na mfupi katika ngazi ya Stashahada ya juu na Shahada ya pili ya Maendeleo Vijijini, Shahada ya kwanza ya Uhasibu, Stashahada ya Ukatibu Muhutasi na Stashahada ya Manunuzi na Ugavi. Aidha, wafanyakazi 21 wamepatiwa mafunzo ya siku mbili juu ya Utawala bora. Jumla ya mikutano 12 imefanyika juu ya uhamasishaji wa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU kwa wafanyakazi na wananchi kwa ujumla.
 
133.   Mheshimiwa Spika, kazi nyengine zilizofanywa na Mkoa ni pamoja na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za mashamba darasa 12, vituo vya kilimo viwili na mabonde ya mpunga sita. Mkoa pia ulifuatilia shughuli za mifugo na uvuvi ambapo vituo sita vya mifugo, wafugaji 75 wa ng’ombe na 53 wa kuku pamoja na Skuli 36 za mafunzo ya mifugo na madiko sita ya uvuvi. Aidha, Skuli 41, vituo 31 vya elimu ya watu wazima, Maktaba mbili pamoja na madarasa 38 mapya vimefuatiliwa sambamba na shughuli nyengine za sekta za afya, mazingira na utalii.
 
134.   Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa jengo jipya la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa umekamilika kwa kiwango cha kuweza kuhamiwa. Aidha, ukarabati wa jengo la Ofisi ya Mkuu wa Wilaya Kaskazini “A” umefanyika.
 
135.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mkoa wa Kaskazini Unguja unakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha hali ya ulinzi na usalama katika Mkoa;
(ii)     Kuimarisha ushiriki wa wananchi katika utawala wa kidemokrasia;
(iii)    Kuongeza uelewa wa wafanyakazi katika masuala mtambuka (UKIMWI na Mazingira);
(iv)   Kuandaa mazingira mazuri katika uendeshaji wa shughuli za Ofisi; na
(v)     Kuwajengea uwezo wafanyakazi.
 
136.   Mheshimiwa Spika, ili Mkoa wa Kaskazini Unguja uweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 1,247.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida.

MKOA WA KUSINI PEMBA

137.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Mkoa uliidhinishiwa jumla ya TZS. 1,741.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida, kati ya hizo TZS. 1,169.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida za Mkoa, TZS. 363.0 milioni Ruzuku kwa Baraza la Mji Chake Chake na TZS. 209.0 milioni kwa ajili ya Ruzuku Baraza la Mji Mkoani. Hadi kufikia mwezi Machi 2013, Mkoa uliingiziwa TZS. 683.3 milioni sawa na asilimia 58.5 ya fedha zilizoidhinishwa kwa kazi za kawaida, TZS. 258.0 milioni sawa na asilimia  71.1 ya Ruzuku kwa Baraza la Mji Chake Chake na TZS. 151.7 milioni sawa na asilimia 72.6 ya Ruzuku kwa Baraza la Mji Mkoani.
 
138.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umefanya vikao vinne vya Kamati ya Ulinzi na Usalama. Aidha, vikao vitatu vya Kamati ya Ukaguzi wa Hesabu na vikao viwili vya Bodi ya Zabuni vimefanyika. Mkoa pia umeratibu utekelezaji wa miradi ya sekta mbali mbali zikiwemo za kilimo, elimu, afya, miundombinu, utawala bora na maendeleo ya vijana.
 
139.   Mheshimiwa Spika, kiwanja kinachokusudiwa kujengwa nyumba ya Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa tayari kimepatikana pamoja na hati miliki ya kiwanja hicho. Mtaalamu wa kutayarisha michoro amepatikana na hatua za ujenzi zinatarajiwa kuanza mara baada ya kukamilisha kazi yake.
 
140.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umesimamia Miradi mbali mbali ya maendeleo ya wananchi katika Wilaya zake zote mbili, maelezo ya kina ya utekelezaji ya miradi hiyo yamewekwa katika Kiambatanisho Nambari 15. Aidha, mfanyakazi mmoja amepatiwa mafunzo ya muda mrefu katika ngazi ya cheti Chuo cha Utumishi wa Umma Unguja. Mkoa pia umetayarisha semina kwa wafanyakazi 76 juu ya Jinsia na namna ya kujikinga na maambukizi mapya ya VVU na UKIMWI.
 
141.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mkoa wa Kusini Pemba unakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha ulinzi na usalama  kwa raia na mali zao;
(ii)     Kuimarisha uratibu, usimamiaji na ufuatiliaji wa kazi za maendeleo ya Mkoa;
(iii)    Kuimarisha kiwango cha taaluma kwa wafanyakazi saba kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu na mfupi;
(iv)   Kuwajengea uwezo wafanyakazi juu ya kujikinga na maambukizi mapya ya VVU na UKIMWI; na
(v)     Kuimarisha mazingira bora ya kazi ili kuleta ufanisi, umakini na uwajibikaji.
 
142.   Mheshimiwa Spika, ili Mkoa wa Kusini Pemba uweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya TZS 1,871.0 milioni kwa matumizi ya kawaida. Kati ya hizo, TZS. 1,290.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya kawaida ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, TZS. 370.0 milioni ni Ruzuku kwa Baraza la Mji Chake Chake na TZS. 211.0 milioni ni Ruzuku kwa Baraza la Mji Mkoani.
 

MKOA WA KASKAZINI PEMBA

143.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Mkoa wa Kaskazini Pemba uliidhinishiwa jumla ya TZS. 1,384.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida, kati ya hizo TZS. 275.0 milioni ni Ruzuku kwa Baraza la Mji Wete. Hadi mwezi Machi 2013, Mkoa uliingiziwa TZS. 709.6 milioni sawa na aslimia 64.0 ya fedha zilizoidhinishwa na TZS. 176.0 milioni sawa na asilimia 64.0 ya fedha za Ruzuku kwa Baraza la Mji Wete.
 
144.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umefanya vikao 15 vya Kamati ya Ulinzi na Usalama ambavyo vimepelekea hali ya usalama na amani katika Mkoa huu kuimarika. Aidha, umeratibu na kusimamia utekelezaji wa Miradi ya maendeleo ya sekta mbali mbali ikiwemo elimu, afya, maji safi, miundombinu ya barabara, kilimo, mifugo, uvuvi, ustawi wa jamii na maendeleo ya wanawake, vijana na watoto. Mkoa pia, umefuatilia utekelezaji wa Miradi ya maendeleo iliyoanzishwa na wananchi ikiwemo ya vituo vya afya vya Bwagamoyo na Kifundi, ujenzi wa madarasa ya Skuli ya Kiuyu Kipangani pamoja na uendelezaji wa ujenzi wa barabara zinazojengwa na Kampuni ya MECCO na H. Young. Barabara hizo ni za Mtambwe, Pandani, Konde, Gando, Kangagani na Likoni.
 
145.   Mheshimiwa Spika, Mkoa umefanya ukarabati mdogo katika Ofisi ya Ofisa Tawala Mkoa kwa kukata vyumba (partition) pamoja na kufanya marekebisho ya mfumo wa umeme na kuvuta laini mpya ya maji na baadhi ya matengenezo ya nyumba za Wakuu wa Wilaya ya Wete na Micheweni. Aidha, katika kuimarisha taaluma ya wafanyakazi kiutendaji, Mkoa umewapatia wafanyakazi saba  mafunzo ya muda mfupi na mrefu katika fani ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, Utunzaji wa kumbukumbu, Uhasibu, Ununuzi na Ugavi, Rasilimali Watu na Sayansi ya Jamii.
 
146.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mkoa wa Kaskazini Pemba unakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha mazingira bora ya kazi na kuona wafanyakazi wanawajibika ipasavyo;
(ii)     Kuimarisha ulinzi na usalama wa raia na mali zao;
(iii)    Kusimamia, kuratibu na kufuatilia  shughuli mbali mbali za kisekta na maendeleo ya Mkoa;
(iv)   Kuwajengea uwezo wa kielimu wafanyakazi saba kwa kuwapatia mafunzo ya muda  mrefu na mfupi; na
(v)     Kuwajengea uwezo wafanyakazi juu ya kujikinga na maambukizi mapya ya VVU na UKIMWI.
 
147.   Mheshimiwa Spika, ili Mkoa wa Kaskazini Pemba uweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya TZS. 1,558.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida. Kati ya hizo TZS. 280.0 milioni kwa ajili ya Ruzuku ya Baraza la Mji Wete.

IDARA YA URATIBU WA IDARA MAALUM ZA SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR

148.   Mheshimiwa Spika, Idara hii ina wajibu wa kusimamia na kuratibu kazi za Idara Maalum za SMZ zikiwemo za kusimamia utekelezaji wa Sera, Sheria na Kanuni za Idara Maalum, kusimamia vikao vya Tume ya Utumishi pamoja na Mahkama ya Rufaa za Idara Maalum za SMZ. Aidha, Idara ina majukumu ya kisera ya kuoanisha miundo ya kiutumishi, maslahi ya maafisa na wapiganaji, kuwajengea uwezo wa kiutendaji na kuratibu masuala ya michezo na utamaduni ndani ya Idara Maalum za SMZ.
 
149.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ilitengewa TZS 200.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi mwezi Machi 2013, Idara ilikuwa tayari imeingiziwa TZS 105.0 milioni sawa na asilimia 52.5 ya fedha zilizoidhinishwa.
 
150.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Uratibu wa Idara Maalum za SMZ imeandaa Miundo ya Utumishi (Scheme of Services) ya Idara Maalum za SMZ ili kuimarisha maslahi na majukumu ya watumishi wa Idara hizo. Miundo hiyo tayari imewasilishwa Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa ajili ya kupata maamuzi. Miundo ya Utumishi ya Idara hizo inatarajiwa kuanza kutumika katika mwaka ujao wa fedha wa 2013/2014.
 
151.   Mheshimiwa Spika, vikao vitatu vya Tume ya Utumishi ya Idara Maalum na Kamati ya Ajira ya Idara Maalum za SMZ vimefanyika kupitia utaratibu wa ajira katika Idara hizo. Sambamba na hilo, Tume ya Utumishi ya Idara Maalum ilizingatia maombi ya kupandishwa vyeo kwa Wapiganaji na Maofisa pamoja na kusikiliza malalamiko kutoka kwa watumishi wa Idara Maalum za SMZ. Aidha, vikao vitatu vya Mahkama ya Rufaa ya Idara Maalum za SMZ vimefanyika ambapo jumla ya rufaa nne zilijadiliwa na kutolewa maamuzi.
 
152.   Mheshimiwa Spika, katika kuwaendeleza watumishi kitaaluma, wafanyakazi wake wawili wamepatiwa mafunzo ya muda mrefu na mfupi katika fani za Mipango ya Maendeleo na Habari na Mawasiliano. Vilevile, Idara imeendelea kuweka mazingira mazuri ya kazi ili kuongeza ufanisi kwa kununua vitendea kazi vikiwemo samani za Ofisi.
 
153.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ya Uratibu wa Idara Maalum za SMZ ina mpango wa kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuweka mazingira mazuri ya kufanya kazi ili Idara iweze kutoa huduma nzuri;
(ii)     Kuimarisha uratibu na ufuatiliaji wa shughuli za Idara Maalum za SMZ Unguja na Pemba;
(iii)    Kuwajengea uwezo wa kiutendaji watumishi wa Idara kwa kuwapeleka mafunzoni ndani na nje ya Zanzibar; na
(iv)   Kuandaa vikao vya rufaa vya Idara Maalum za SMZ.
 
154.   Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Uratibu wa Idara Maalum za SMZ iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 144.8 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida.
 

TUME YA UTUMISHI YA IDARA MAALUM ZA SMZ

155.   Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka ujao wa fedha wa 2013/2014, Tume ya Utumishi ya Idara Maalum za SMZ itakuwa na kasma yake ndogo na hivyo kuiondoa kutoka katika kasma ya Idara ya Uratibu ya Idara Maalum. Hatua hii imechukuliwa ili kuifanya Tume hiyo iweze kusimamia vizuri kazi zake.
 
156.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Tume ya Utumishi ya Idara Maalum inakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha mazingira bora ya Utumishi wa Idara Maalum;
(ii)     Kutoa elimu kwa Maafisa na Wajumbe wa Tume ya Utumishi ya Idara Maalum za SMZ;
(iii)    Kuhakikisha kazi za Tume zinafanyika ipasavyo; na
(iv)   Kufuatilia ajira na maslahi ya Watumishi wa Idara Maalum za SMZ kwa kushirikiana na Tume ya Utumishi Serikalini.
 
157.   Mheshimiwa Spika, ili Tume ya Utumishi ya Idara Maalum za SMZ iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, katika mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 53.2 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

KIKOSI MAALUM CHA KUZUIA MAGENDO (KMKM)

158.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM) kilitengewa TZS 9,660.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 200.0 milioni kwa kazi za maendeleo. Hadi kufikia Machi 2013, Kikosi kiliingiziwa TZS. 6,188.3 milioni sawa na asilimia 64.1 ya bajeti iliyoombwa kwa kazi za kawaida. Kwa upande wa kazi za maendeleo, fedha zilizoingizwa ni TZS. 115.0 milioni sawa na asilimia 57.5 ya fedha za maendeleo.
 
159.   Mheshimiwa Spika, Kikosi cha KMKM kimeendelea kutoa huduma ya chakula kwa Makamanda na Wapiganaji wake katika muda wote wanapokuwa kazini na mafunzoni. Vile vile kimeimarisha nguvu za ulinzi wa doria na kufanikiwa kukamata vyombo 14 na mali walizokuwa wakizitorosha na kuleta nchini kimagendo (Kiambatanisho Nambari 16). Vyombo na mali zinazokamatwa huwa vinakabidhiwa Mamlaka husika kwa hatua zao za kisheria. Aidha, vyombo vyake vikubwa vimefanyiwa matengenezo pamoja na kuvipeleka chelezoni na kufanya ununuzi wa vifaa vya mawasiliano.
 
160.   Mheshimiwa Spika, kitengo cha uzamiaji (Diving Section) nacho kimeimarishwa kwa kukinunulia vifaa pamoja na kuendesha mafunzo maalum ya uzamiaji ili kuweza kukabiliana na majanga. Hivi karibuni, Maofisa wanne wamekwenda Uingereza kwa ajili ya mafunzo zaidi ya uzamiaji kivitendo chini ya mwaliko wa kampuni ya “L&W UK and Indeep Diving and Marine Service” ya nchini humo.
 
161.   Mheshimiwa Spika, Kikosi kimekamilisha malipo ya sare za Maafisa na Wapiganaji wake 500. Matengenezo ya Ofisi ya mipango na kitengo cha manunuzi pamoja na kununua samani za Ofisi navyo vimefanyika.
 
162.   Mheshimiwa Spika, Kikosi kimefanya ukarabati na ujenzi katika majengo mbali mbali ikiwemo Ofisi ya Idara ya Mipango. Kitengo cha Manunuzi, banda jipya la kulala askari katika Kambi ya Msuka, hanga moja la kulala askari katika Kambi mpya ya KMKM Tumbatu ambalo limefikia hatua ya uezekaji pamoja na ujenzi wa mnara wa Bendera katika Kisiwa cha Tumbatu.
 
163.   Mheshimiwa Spika, Hospitali ya KMKM Kibweni imeendelea kutoa huduma za afya kwa Makamanda na Wapiganaji pamoja na wananchi wanaoishi maeneo jirani. Takwimu zinaonesha upo muitiko mkubwa wa wananchi kupatiwa huduma katika hospitali hiyo jambo ambalo limesaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja. Jumla ya wananchi 16,865 wakiwemo Makamanda na Wapiganaji walifika hospitalini hapo na kupatiwa huduma, kati yao wanawake ni 8,645 na wanaume ni 8,220.
 
164.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo kimepanga kutekeleza malengo yafuatayo:
(i)       Kuwapatia chakula bora askari wanapokuwa kazini na mafunzoni;
(ii)     Kuimarisha hali ya ulinzi wa doria;
(iii)    Kuimarisha sehemu ya uzamiaji kikosini;
(iv)   Kuhakikisha kuwa Maofisa na Wapiganaji wanawajibika ipasavyo kwa kupatiwa stahiki zao;
(v)     Kuwapatia sare Maofisa na wapiganaji wote;
(vi)   Kuendeleza kuwapatia elimu ndani na nje ya Kikosi; na
(vii)  Kuendeleza ukarabati wa majengo mbali mbali ya Kikosi Unguja na Pemba.
 
165.   Mheshimiwa Spika, ili Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo kiweze kutekeleza malengo iliojipangia kwa ufanisi, katika mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 9,452.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

JESHI LA KUJENGA UCHUMI (JKU)

166.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013 Kikosi cha JKU kilidhinishiwa TZS. 7,504.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 300.0 milioni kwa miradi ya maendeleo na hadi Machi 2013, Jeshi la Kujenga Uchumi limeingiziwa TZS. 5,196.0 milioni sawa na asilimia 69.2 ya fedha.
 
167.   Mheshimiwa Spika, Jeshi la Kujenga Uchumi limeendelea kujenga mazingira mazuri ya kiutendaji kwa kuwapatia watumishi wake fursa za masomo ya muda mfupi na mrefu. Jumla ya wafanyakazi 10 wanaendelea na masomo katika ngazi za Shahada ya Uzamili, Shahada ya Kwanza, Stashahada na Cheti.
 
168.   Mheshimiwa Spika, Jeshi la Kujenga Uchumi limeendelea kuimarisha mradi wa ufugaji wa kuku na ng’ombe wa maziwa kwa kununua vifaranga 2,000 (1,000 vya nyama na 1,000 vya mayai) pamoja ng’ombe wawili wa maziwa. JKU pia imesimamia kilimo cha mazao ya nafaka na miti ya matunda kwa kulima ekari 130 za mpunga, ekari 10 za mahindi, ekari 5 za mtama, ekari 140 za muhogo, ekari 20 za kunde na ekari 5 za miti ya kudumu.
 
169.   Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha Skuli za Ufundi na Sekondari, Jeshi la Kujenga Uchumi limeanzisha fani tatu za mafunzo ya ufundi ambazo ni ufundi wa ushoni, ufundi bomba na useremala katika Skuli ya Ufundi Chokocho na vifaa kwa ajili ya mafunzo hayo vimenunuliwa. Aidha, ununuzi wa vifaa vya maabara ya Skuli ya Sekondari ya JKU Mtoni vimenunuliwa.
 
170.   Mheshimiwa Spika, Kikosi cha JKU kimeendelea kutoa huduma za afya kwa watumishi wake na wananchi wa maeneo jirani. Katika kipindi cha mwaka 2012/2013 jumla ya wananchi 23,653 wamepatiwa huduma za afya katika vituo mbali mbali vya JKU. Aidha, elimu ya kujikinga na maambukizi mapya ya VVU imetolewa kwa wananchi wa maeneo jirani na watumishi waliopo katika kambi mbali mbali Unguja na Pemba.
 
171.   Mheshimiwa Spika, JKU imeendelea kuweka mazingira mazuri ya kuendeshea mafunzo kwa vijana, jumla ya vijana 400 wa kujitolea wamesajiliwa na wanaendelea kupatiwa mafunzo. Katika kuimarisha michezo Kikosi cha JKU kimenunua vifaa vya michezo mbali mbali pamoja na kugharamia ushiriki wa timu zake katika mashindano ndani na nje ya Zanzibar sambamba na Tamasha la Michezo lililofanyika Zanzibar.
 
172.   Mheshimiwa Spika, kwa ajili ya kuweka mazingira bora ya utendaji kazi kwa askari wake, JKU imenunua samani za Ofisi, jokofu, vitanda na magodoro 300, sare za askari 200 pamoja na kufunga mtambo wa simu.
 
173.   Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha mashirikiano baina ya vikosi vya JKU na JKT, Jeshi la Kujenga Uchumi, limeratibu vikao viwili vya mashirikiano baina ya Viongozi Wakuu wa vikosi hivyo ambapo masuala mbali mbali yanayohusu mafunzo kwa vijana yalijadiliwa pamoja na kubadilishana uzoefu katika nyanja mbali mbali.
 
174.   Mheshimiwa Spika, pamoja na kutekeleza majukumu na malengo yaliopangwa, Jeshi la Kujenga Uchumi kwa kutumia vyanzo vyake vya ndani limefanikiwa kuezeka nyumba ya Mkuu wa Kanda (Zone) Pemba, nyumba ya kuishi askari katika kambi ya Mwambe, kufanya ukarabati wa Ofisi ya JKU Upenja, kufanya ukarabati mkubwa wa mabweni ya kuishi askari wa kambi ya Kama na uanzishaji wa duka la dawa liliopo Makao Makuu.
 
175.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Jeshi la Kujenga Uchumi linakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kutoa mafunzo kwa vijana wanaojiunga na JKU katika nyanja za kilimo, mifugo, ufundi, kazi za amali na ulinzi wa Taifa ili waweze kujitegemea na kuijenga Nchi yao;  
(ii)     Kuwapatia wapiganaji sare na vifaa;
(iii)    Kutoa mafunzo kwa watumishi ili kuongeza ufanisi wa kazi;
(iv)   Kuimarisha mashirikiano na Taasisi mbali mbali ndani na nje ya Zanzibar; na
(v)     Kuimarisha utoaji wa huduma kwa wana JKU na jamii kwa ujumla.
 
176.   Mheshimiwa Spika, ili Jeshi la Kujenga Uchumi liweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 7,457.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 250.0 milioni kwa kazi za maendeleo.

IDARA YA CHUO CHA MAFUNZO (MF)

177.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Chuo cha Mafunzo iliidhinishiwa TZS. 5,890.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 400.0 milioni kwa mradi wa maendeleo. Hadi Machi 2013, Idara iliingiziwa TZS 4,007.0 milioni sawa na asilimia 68.0 ya fedha zilizoidhinishwa kwa kazi za kawaida na TZS. 145 milioni sawa na asilimia 36.3 kwa ajili ya mradi wa maendeleo.
 
178.   Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha makaazi ya wanafunzi wa Vyuo vya Mafunzo, matengenezo ya Chuo cha Kinumoshi yamefanyika. Pia, Idara ya Chuo cha Mafunzo kwa Kanda za Mashamba inayotarajiwa kujengwa Langoni imefanyiwa makisio ya ujenzi na michoro yake imekamilika. Sambamba na hayo, vyoo katika mabweni mawili ya kulala wanafunzi katika Chuo cha Mafunzo Langoni tayari vimeshawekwa. Aidha, upimaji wa mashamba ya Kinumoshi na Ubago umekamilika na gharama za hatimiliki zimeshalipwa. Taratibu za kupatiwa hatimiliki hizo zinaendelea.    
 
179.   Mheshimiwa Spika, katika kuweka mazingira mazuri ya kazi, Idara imenunua gari moja aina ya Toyota Vitara, samani za ukumbi wa mkutano wa Makao Makuu na magodoro 80 kwa matumizi ya wanafunzi. Idara pia imenunua dawa kwa ajili ya matumizi ya wanafunzi na askari. Aidha, Idara imeendelea kuwajengea uwezo watumishi wake kwa kugharamia masomo ya muda mrefu na mfupi kwa watumishi watano wa Idara katika fani za Uhasibu, Katibu muhutasi na Ustawi wa Jamii.
 
180.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014, Idara ya Chuo cha Mafunzo imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha huduma bora za urekebishaji tabia kwa wanafunzi, kuwaendeleza na kuwajengea uwezo wanaporudi katika jamii;
(ii)     Kuhakikisha haki za binadamu zinatolewa kwa wanafunzi na wale walioko rumande kwa mujibu wa Sheria za nchi, kikanda na makubaliano ya Kimataifa;
(iii)    Kuweka mazingira mazuri ya kazi, maendeleo na ustawi wa maafisa na wapiganaji pamoja na usimamizi mzuri wa fedha; na
(iv)   Kuendelea na ujenzi wa Chuo kipya cha Mafunzo Hanyegwa Mchana.
 
181.   Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Chuo cha Mafunzo iweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 6,099.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 300.0 milioni kwa mradi wa maendeleo.

KIKOSI CHA ZIMAMOTO NA UOKOZI ZANZIBAR (KZU)

182.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013, Kikosi cha Zimamoto na Uokozi kiliidhinishiwa TZS. 3,099.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi mwezi  Machi, 2013 Kikosi kimeingiziwa TZS. 2,126.0 milioni sawa na asilimia 68.6 ya makadirio ya matumizi.
 
183.   Mheshimiwa Spika, jitihada zinaendelea za kujenga vituo vya zimamoto katika kila Wilaya. Jumla ya vituo vitatu vimeanzishwa na kutoa huduma. Vituo hivyo ni Mwanakwerekwe Wilaya ya Magharibi Unguja, eneo la Bandarini Unguja na eneo la Bandarini Mkoani Pemba. Kituo cha bandari ya Mkoani kwa sasa kitakuwa kikitoa huduma za zimamoto na uokozi katika Wilaya ya Mkoani na maeneo jirani. Hatua za ujenzi wa Kituo cha Marumbi Wilaya ya Kati zimeanza. Aidha, hatua zitachukuliwa za kupatikana eneo katika Wilaya za Micheweni na Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba pamoja na Wilaya ambazo huduma hizi hazijafika.
 
184.   Mheshimiwa Spika, Idara imewapatia sare Maafisa wake, vyakula kwa askari wanaolala kambini na waliopo mafunzoni na dawa kwa matumizi ya Maafisa na Wapiganaji wa Kikosi. Aidha, wapiganaji na maofisa 77 wamepatiwa mafunzo ndani na nje ya nchi. Mafunzo hayo ni katika fani za Uongozi Mkubwa, Uongozi Mdogo, Uzimaji moto, Matumizi ya Kompyuta, Masjala, Sheria na Fedha.
 
185.   Mheshimiwa Spika, Kikosi kimeendelea kufanya matengenezo ya mara kwa mara ya magari yaliopo pamoja na kununua vipuri na vitendea kazi vikiwemo; “Foam compound”, “Carbon Dioxide”, “Delivery Horse 35 na B.A”. Aidha, Kikosi kimenunua jumla ya gari tatu za kuzimia moto na gari moja ya kuchukulia wagonjwa. Malipo ya asilimia 75 ya gharama za ununuzi wa gari hizo yameshafanywa.
 
186.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Kikosi cha Zimamoto na Uokozi kimelenga  kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kupunguza muda wa kuwahi kufika katika tukio la moto na majanga mengine bila ya kuzidi dakika 15;
(ii)     Kuboresha ujenzi wa vituo na kupatikana vifaa vya kazi vituoni ili kuleta ufanisi wa huduma zinazotolewa;
(iii)    Kuwapa motisha wafanyakazi ili kukuza ufanisi na tija kwa aina ya huduma zinazotolewa nchini;
(iv)   Kuboresha Rasilimali Watu kwa kuwapatia Maafisa na Maaskari elimu za aina mbali mbali;
(v)     Kuendelea kutoa elimu ya tahadhari za moto; na
(vi)   Kuongeza uhusiano na mashirikiano ya namna ya kukabiliana na majanga mbalimbali Kitaifa na Kimataifa.
 
187.   Mheshimiwa Spika, ili Kikosi cha Zimamoto na Uokozi kiweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 3,113.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

KIKOSI CHA VALANTIA ZANZIBAR (KVZ)

188.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Kikosi cha Valantia kilitengewa TZS. 3,784.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 100.0 milioni kwa matumizi ya kazi za maendeleo. Hadi mwezi Machi 2013, Kikosi cha Valantia kimeingiziwa TZS. 2,224.0 milioni sawa na asilimia 58.8 ya fedha zilizoidhinishwa kwa matumizi ya kawaida na TZS. 40.0 milioni sawa na asilimia 40.0 kwa matumizi ya  mradi wa maendeleo.
 
189.   Mheshimiwa Spika, Kikosi cha Valantia kimeendelea kuimarisha nguvu za ulinzi na usalama kwa kuwapatia chakula cha kutosha askari wanaokaa zamu katika kambi zote za Kikosi. Aidha, Kikosi kimeendelea kusimamia masuala ya usafiri ili kuimarisha shughuli za ulinzi na utawala.
 
190.   Mheshimiwa Spika, Kikosi kimeendelea kuwajengea uwezo wa kiutendaji Maafisa na Wapiganaji wake ndani na nje ya Kikosi. Katika kipindi hiki Kikosi kimedhamini mafunzo kwa askari sita katika ngazi ya Stashahada na Shahada. Aidha, dawa kwa ajili huduma za afya kwa askari na raia zimenunuliwa pamoja na ununuzi wa gari mbili aina ya Land Rover.  Kikosi kimekamilisha malipo ya gharama za uungaji wa umeme katika kambi ya Ndugukitu ilioko Pemba. Pia, Kikosi kimenunua sare seti 127 kwa ajili ya matumizi ya maafisa na askari wake.
 
191.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Kikosi cha Valantia kina mpango wa kutekeleza malengo yafuatayo:-
(i)       Kuimarisha nguvu za ulinzi na usalama;
(ii)     Kuwaongezea uwezo wa kiutendaji wapiganaji wa kikosi cha Valantia;
(iii)    Kuandaa mazingira mazuri ya utendaji kazi kwa wapiganaji wa kikosi cha Valantia;
(iv)   Kuendeleza ujenzi pamoja na kuyapatia hatimiliki maeneo ya Kikosi ya Unguja na Pemba; na
(v)     Kuhakikisha wafanyakazi wanawajibika ipasavyo.
 
192.   Mheshimiwa Spika, ili Kikosi cha Valantia kiweze kutekeleza malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2013/214, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS. 3,258.0 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS. 70 milioni kwa matumizi ya mradi wa maendeleo.
 

MIRADI YA MAENDELEO YA OFISI YA RAIS NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI

193.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/13, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ilipanga kutekeleza Miradi minane ya maendeleo na fedha zilizotengwa kwa Miradi hiyo ni TZS. 1,906.0 milioni. Miradi yenyewe ni kama ifuatavyo:-
i)     Mradi wa Uimarishaji Nyumba za Viongozi na Nyumba za Serikali
 
194.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa Uimarishaji Nyumba za Viongozi na Nyumba za Serikali uliidhinishiwa TZS. 400.0 milioni na hadi kufikia Machi 2013, Mradi huu uliingiziwa TZS. 306.9 milioni ambazo ni sawa na asilimia 76.7 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza kazi zifuatazo:-
(i)       Matengenezo ya Ikulu ya Mkoani yapo katika hatua za mwisho kukamilika;
(ii)     Ujenzi wa ghala katika Ikulu Kuu ya Mnazi mmoja nao umekamilika;
(iii)    Ikulu ndogo ya Laibon Dar es Salaam imefanyiwa matengenezo kwa kuwekewa malighafi maalumu ya kuziba paa la zege ili kuzuia kuvuja; na
(iv)   Ikulu ya Dodoma imefanyiwa matengenezo makubwa ya vyoo.
 
195.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mradi wa Uimarishaji Nyumba za Viongozi na Nyumba za Serikali umetengewa TZS. 600.0 milioni na umepanga kutekeleza kazi zifuatazo:-
 
(i)       Kuanza ujenzi wa nyumba za walinzi katika Ikulu ya Laibon  Dar es Salaam;
(ii)     Kufanya ukarabati wa Ikulu ya Chake Chake;
(iii)    Kufanya matengenezo katika Ikulu Kuu ya Mnazi Mmoja yakiwemo kubadilisha madirisha ya zamani;
(iv)   Kujenga ukuta wa nyumba zilizokuwa za Posta katika Ikulu ya Migombani;
(v)     Kujenga ukuta wa kuzuia mmong’onyoko katika Ikulu ya Mkoani;
(vi)   Kujenga ukuta wa Ikulu ndogo Mkokotoni; na
(vii)  Kuendeleza ujenzi wa nyumba ya mapumziko ya Micheweni.
ii)   Mradi wa Kuimarisha Mawasiliano - Ikulu
 
196.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kuimarisha Mawasiliano – Ikulu uliidhinishiwa TZS. 100.0 milioni na hadi kufikia Machi 2013, Mradi huu uliingiziwa TZS. 13.3 milioni ambazo ni sawa na asilimia 13.3 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza kazi zifuatazo:-
(i)    Hatua za awali za ukarabati wa chumba cha kutayarishia vipindi katika Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi zimeanza.
 
197.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mradi wa Kuimarisha Mawasiliano – Ikulu umetengewa TZS. 150 milioni na utatekeleza kazi zifuatazo:-
(i)      Ununuzi wa Gari la matangazo kwa ajili ya huduma za Rais Pemba; na
(ii)    Ununuzi wa vifaa vya matangazo.
iii) Mradi wa Uimarishaji wa Serikali za Mitaa
 
198.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa Uimarishaji wa Serikali za Mitaa uliidhinishiwa TZS. 150.0 milioni na hadi kufikia Machi 2013, Mradi huu uliingiziwa TZS. 46.9 milioni ambazo ni sawa na asilimia 31.3 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza kazi zifuatazo:-
(i)      Utayarishaji wa Mpango Mkakati wa Utekelezaji wa Sera;
(ii)    Utayarishaji wa muongozo na Rasimu ya Sheria ya Serikali za Mitaa;
(iii)   Kufanya mapitio ya vyanzo vya mapato vya Serikali za Mitaa; na
(iv)  Semina za Wadau kujadili utekelezaji wa Sera ya Serikali za Mitaa ikiwemo Semina kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi.
 
199.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mradi wa Uimarishaji wa Serikali za Mitaa umetengewa TZS. 150 milioni na utatekeleza kazi zifuatazo:-
(i)      Kuandaa Kanuni za Sheria ya Serikali za Mitaa;
(ii)    Kufanya tathmini ya mahitaji ya watumishi katika Serikali za Mitaa;
(iii)   Kuhakiki mipaka ya Mamlaka ya Mikoa na Serikali za Mitaa; na
(iv)  Kufanya tathmini na kuandaa mfumo, utaratibu na miongozo ya fedha.
iv)  Mradi wa Kiwanda cha Ushoni (Zanzibar Quality Tailoring LTD)
 
200.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa “Zanzibar Quality Tailoring Ltd” uliidhinishiwa TZS. 256.0 milioni na hadi kufikia Machi 2013, Mradi huu uliingiziwa TZS. 5.8 milioni ambazo ni sawa na asilimia 2.3 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza yafuatayo:-
(i)          Kugharamia shughuli za uendeshaji wa kiwanda zikiwemo ununuzi wa vifaa vidogo vidogo kama mikasi na nyuzi za kushonea.
 
201.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mradi wa Kuimarisha Kiwanda cha Ushoni umetengewa TZS. 350.0 milioni na utatekeleza kazi zifuatazo:-
(i)      Ununuzi wa vifaa pamoja na kutafuta malighafi za uzalishaji; na
(ii)    Kujenga uwezo wa watendaji na kiwanda.
v)    Mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya KMKM
 
202.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya KMKM uliidhinishiwa TZS. 200.0 milioni na hadi kufikia Machi 2013, Mradi huu uliingiziwa TZS. 115.0 milioni ambazo ni sawa na asilimia 57.5 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza yafuatayo:-
 
(i)      Ujenzi umeendelea kwa hatua za kumalizia ambapo kazi zilizofanyika ni upigaji plasta, uwekaji wa dari na ununuzi wa vigae; na
(ii)    Uezekaji wa jengo litakalotumika kwa ajili ya kufulia nguo.
 
203.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014, Mradi wa Ujenzi wa Hospitali ya KMKM utakuwa umekamilika.
vi)  Mradi wa Ujenzi wa Chuo cha Mafunzo
 
204.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ujenzi wa Chuo cha mafunzo uliidhinishiwa TZS. 400.0 milioni na hadi kufikia Machi 2013, Mradi huu uliingiziwa TZS. 145.0 milioni ambazo ni sawa na asilimia 36.3 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza yafuatayo:-
(i)      Malipo ya Mshauri Elekezi na msimamizi wa ujenzi; na
(ii)    Ujenzi wa msingi unaozunguka eneo la Chuo Kipya cha Mafunzo, nguzo za ukuta mkubwa na uzio.
 
205.   Mheshimiwa Spika,  kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mradi wa Ujenzi wa Chuo kipya cha Mafunzo Hanyegwa Mchana umetengewa TZS. 300.0 milioni na utatekeleza kazi zifuatazo:-
(i)       Kujenga ukuta wa urefu wa mita 600 wenye kimo cha mita 1.5;
(ii)     Kujenga msingi jengo la watoto;
(iii)    Kufanya malipo ya Mshauri Elekezi; na
(iv)   Kufanya malipo ya mafuta na matengenezo ya zana
vii)               Mradi wa Ujenzi wa Makao Makuu ya Valantia
 
206.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ujenzi wa Makao Makuu ya Valantia uliidhinishiwa TZS. 100.0 milioni na hadi kufikia Machi 2013, Mradi huu uliingiziwa TZS. 40.0 milioni ambazo ni sawa na asilimia 40.0 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza yafuatayo:-
(i)       Ujenzi wa mesi na ukumbi wa mikutano umefikia hatua ya juu na unasubiri kuezekwa.
207.   Mheshimiwa Spika,  kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mradi wa Ujenzi wa Makao Makuu ya Valantia umetengewa TZS. 70.0 milioni na utatekeleza kazi zifuatazo:-
(i)       Kuanza ukarabati Mkubwa wa nyumba Namba 1900; na
(ii)     Kumaliza Ujenzi wa Ukumbi wa Mikutano.
viii)             Mradi wa Shamba la Mfano la Pamoja - Bambi
 
208.   Mheshimiwa Spika, Mradi wa Shamba la Mfano la Pamoja - Bambi ambao unatekelezwa kwa pamoja baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Misri. Utekelezaji wake haukufanyika kutokana na kutoingiziwa fedha.
 
209.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Mradi wa Shamba la Mfano la  Pamoja - Bambi umetengewa TZS. 250.0 milioni na utatekeleza kazi zifuatazo:-
(i)       Kukamilisha ujenzi wa nyumba moja;
(ii)     Kuendeleza Shamba la Bambi;
(iii)    Kufanya ukarabati wa nyumba ya Wataalamu; na
(iv)   Kujenga ghala jipya la kisasa.

MAMLAKA YA SERIKALI ZA MITAA

210.   Mheshimiwa Spika, Serikali za Mitaa ndio mhimili mkubwa wa utekelezaji wa majukumu ya Serikali katika lengo zima la kuhakikisha yanakuwepo maendeleo endelevu katika nchi yetu. Katika kufanisha azma hiyo, Serikali kupitia Mpango wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa imedhamiria kuziwezesha Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoa huduma bora kwa wananchi. Hata hivyo, jukumu hilo haliwezi kutekelezeka iwapo Serikali hizi hazitokuwa na wataalamu, pia hazitaweza kuongeza mapato na kuwa na nidhamu katika matumizi. Hivyo, mkazo uliwekwa katika kuimarisha mfumo wa ukusanyaji mapato. Kwa mfano, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Baraza la Manispaa limeendesha zoezi la kutathmini viwango vya leseni na thamani za nyumba ili kuwa na takwimu sahihi za walipa kodi (tax payers).
 
211.   Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hiyo, Serikali itaimarisha usimamizi wa mapato na matumizi katika Serikali za Mitaa. Hivyo, Taasisi hizo zinawajibu wa kuhakikisha kuwa Sheria, Kanuni na Taratibu za Fedha zinazingatiwa. Aidha, Ofisi yangu itahakikisha Serikali za Mitaa zinaongeza uwazi katika mapato na matumizi ili kuwawezesha wananchi kushiriki katika kupanga, kufuatilia na kutathmini Mipango na utekelezaji kulingana na vipaumbele vyao.
 
212.   Mheshimiwa Spika, Serikali imeendeleza juhudi za kuimarisha usafi katika Manisapaa ya Zanzibar. Katika kufanikisha hilo, Baraza la Manispaa limefanya malipo kwa Taasisi saba za kijamii na Polisi Jamii ambazo imeingia nazo mkataba wa kutoa huduma za kufanya usafi katika maeneo ya masoko, barabara, misingi ya maji machafu na maji ya mvua kwa kutumia utaratibu wa ‘Out Sourcing’. Utaratibu huu shirikishi umesaidia sana kuimarisha huduma za uzoaji taka katika maeneo mbali mbali ya Manispaa.
 
213.   Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina ya utekelezaji wa malengo ya Serikali za Mitaa kwa mwaka wa fedha 2012/2013, ukusanyaji wa mapato na malengo yatakayotekelezwa kwa mwaka wa fedha 2013/2014 yameainishwa katika kitabu cha “Majadweli ya Utekelezaji wa Malengo ya Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha 2012/2013 na Malengo ya Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2013/2014

JUMLA YA MAPATO NA MATUMIZI YA OFISI YA RAIS NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI

214.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ilipangiwa kukusanya jumla ya TZS. 66.5 milioni. Kati ya fedha hizo, TZS. 25.5 milioni zilipangwa kukusanywa na Kikosi cha Jeshi la Kujenga Uchumi, hadi kufikia Machi 2013, JKU ilikusanya TZS. 8.0 milioni sawa na asilimia 31.4. Chuo cha Mafunzo, kilipangiwa kukusanya TZS. 41.0 milioni, hadi Machi 2013, ilikusanya TZS 10.0 milioni sawa na asilimia 24.4.
 
215.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ilikadiriwa kutumia jumla ya TZS. 48,560.1 milioni. Kati ya hizo, TZS. 44,516.1 milioni kwa kazi za kawaida, TZS. 1,906.0 milioni kwa kazi za maendeleo na TZS. 2,138.0 milioni kwa ajili ya Ruzuku za Baraza la Manispaa na Mabaraza ya Miji ya Mkoani, Chake Chake na Wete. Hadi kufikia Machi 2013, Ofisi ilikuwa imeshaingiziwa TZS. 28,741.9 milioni sawa na asilimia 64.6 kwa kazi za kawaida, TZS. 672.9 milioni sawa na asilimia 35.3 kwa kazi za maendeleo na TZS. 1,575.7 milioni sawa na asilimia 73.7 kwa ajili ya Ruzuku (Kiambatanisho Nambari 11, 12 na 13).
 
216.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi inatarajia kukusanya jumla ya TZS. 121.3 milioni, kati ya fedha hizo, TZS. 25 milioni  zitakusanywa na Kikosi cha Jeshi la Kujenga Uchumi, TZS. 41 milioni zitakusanywa na Chuo cha Mafunzo, TZS. 15.8 milioni zitakusanywa na Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo, TZS. 10 milioni zitakusanywa na Kikosi cha Zimamoto na Uokozi na TZS. 7 milioni zitakusanywa na Kikosi cha Valantia. Fedha zitakazokusanywa na Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho ni 22.5 milioni.
 
217.   Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi iweze kutekeleza majukumu na malengo yake ya mwaka wa fedha 2013/2014, naomba sasa Baraza lako Tukufu liidhinishe jumla ya TZS. 49,819.9 milioni. Kati ya hizo, fedha za matumizi ya kazi za kawaida ni TZS. 45,888.9 milioni sawa na asilimia 92.1, TZS. 1,870.0 milioni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo sawa na asilimi 3.8 na TZS. 2,061.0 milioni sawa na asilimia 4.1 kwa ajili ya Ruzuku kwa Baraza la Manispaa na Mabaraza ya Miji ya Chake Chake, Mkoani na Wete (Kiambatanisho Nambari 11, 12 na 13).

HITIMISHO

218.   Mheshimiwa Spika, kwa mara nyengine tena nachukua fursa hii kuwashukuru wote Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa mashirikiano yenu makubwa mnayoendelea kutupatia wakati wote. Kama nilivyosema mwanzoni, mafanikio ya utekelezaji wa majukumu na malengo ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi yamewezekana kutokana na ushirikiano wenu. Shukurani zangu za pekee ziende kwa Viongozi na Wafanyakazi wote wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambao wamekuwa wakinipa msaada mkubwa katika kutekeleza majukumu ya kila siku ya Ofisi hii.
 
219.   Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa naomba nitumie fursa hii tena kuwashukuru washirika wetu wote wa maendeleo ambao wametuunga mkono wakati wote wa kutekeleza majukumu ya Ofisi yetu. Shukurani hizi ziwaendee washirika wetu wote wa maendeleo nikitarajia kuwa wataendelea na moyo huo huo. Sio rahisi kuwataja wote lakini nitaje wachache ambao ni Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China, Serikali ya Jamhuri ya Watu wa Korea, India, Mashirika ya Kimataifa yakiwemo Benki ya Dunia (WB), Shirika la Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) na Shirika la Uhamiaji la Kimataifa (OIM).
 
220.   Mheshimiwa Spika, napenda nitoe tena shukurani zangu za dhati kwako binafsi na kwa Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza lako Tukufu kwa kunisikiliza.
 
221.   Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
 
(Dkt. Mwinyihaji Makame)
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
Zanzibar

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.