Mwenyekiti wa Bodi
ya Benki ya Taifa ya Biashara-NBC Dk. Mussa Assad amesema lengo la kuanzishwa
kwa huduma za benki ya kiislamu katika benki hiyo ni kukidhi mahitaji ya wateja
wao ambayo kwao ni ibada.
Dk. Assad ameeleza
hayo jana wakati akizungumza kwenye hafla ya futari ambayo iliandaliwa na benki
hiyo kwa wateja wao wa Zanzibar.
Mgeni Rasmi katika
hafla hiyo iliyofanyika kwenye hoteli ya Zanzibar Beach Resort mjini Unguja
alikuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed
Shein.
Wengine
waliohudhuria ni pamoja na Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Iddi, Spika
wa Baraza la Wawakilishi Pandu Ameir Kificho, Kadhi Mkuu wa Zanzibar, Mufti
Mkuu wa Zanzibar pamoja na viongozi wengine.
“Tumefungua huduma
za benki ya kiislamu kwa kusikiliza mahitaji ya wateja wetu. Tunafahamu kuwa
huduma hii ni ibadi kwa wateja wetu waumini wa dini ya kiislamu”alisema Dk.
Assad na kusisitiza kuwa daima benki hiyo imekuwa sikivu kwa wateja wake.
Aliongeza kuwa muda
si mrefu benki hiyo itaanzisha huduma nyingine mpya ambazo lengo lake kuu ni
kukidhi mahitaji mbalimbali ya wateja wake.
“tunaelewa wateja
wetu mna mahitaji mbalimbali na ninawaomba msisite kutueleza shida zenu na sisi
tutawasikiliza na kuzuitafutia ufumbuzi ” alieleza.
Awali akizungumza
katika hafla hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Bi. Mizinga Melu alisema
kuwa kuwepo kwa benki hiyo humu nchini hakutakuwa na maana kama benki haitaweza
kuwasaidia wateja wake kukidhi mahitaji yao.
Amesema kwa
kutambua hilo ndio maana pamoja na kuanzisha huduma za benki ya kiislamu
imeongeza pia huduma kwa wateja wanaotaka kufanya safari za Hija.
“miaka mitatu
iliyopita tulianzisha huduma za benki ya kiislamu na mwitikio umekuwa mkubwa
pasi na matarajio yetu na hivyo tumefurahi kwa kuwa tumeweza kukidhi mahitaji
ya wateja wetu kwani hiyo ndio azma yetu” alisema Bi Melu.
Aliongeza kuwa
mpango wa benki yake sasa ni kuongeza huduma zaidi ili wateja waweze kupata
kila huduma ya kifedha wanazohitaji.
Mkurugenzi Mtendaji
huyo aliwaeleza wageni waalikwa na viongozi walihudhuria hafla hiyo kuwa benki
yake inaunga mkono jitihada za Serikali za kuwatelea wananchi maendeleo.
Aliwashukuru wateja
wa benki hiyo Zanzibar kwa ushirikiano wao na kueleza kuwa madhudhurio mazuri
katika hafla hiyo ni kielelezo cha ushirikiano thabiti kati ya benki na wateja
wake.
Wakati
huo huo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi ameupongeza uongozi wa Benki ya Taifa ya Biashara wa kuandaa futari
na kuwakutanisha wateja wa benki hiyo.
Akitoa shukrani
hizo kwa niaba ya Rais, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Maghribi Abdalla Mwinyi amesema
kitendo cha benki hiyo kuwakutanisha wateja wake katika hafla kama hiyo ni cha
kiungwana na kinazidisha upendo baina ya benki na wateja.
“Kitendo chenu cha
kutufutarisha kwa vyakula vya kila aina vyenye ladha asili ya visiwa vyetu
imemvutia kila aliyefika hapa akiwemo Mheshimiwa Rais na viongozi
wengine”alieleza Mkuu huyo wa Mkoa na kusisitiza kuwa huo ni ukarimu mkubwa wa
kushukuriwa.
No comments:
Post a Comment