Habari za Punde

Hotuba ya maoni ya kamati ya kusimamia ofisi za viongozi wakuu


HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA KUSIMAMIA OFISI ZA VIONGOZI WAKUU WA KITAIFA KUHUSIANA NA BAJETI YA OFISI YA MAKAMO WA KWANZA WA RAIS KWA MWAKA 2015/2016.
Mhe. Spika,
Nianze kwa kutanguliza jina la Mwenyezi Mungu Mtukufu, ambae kwake tunamtegemea na kumuomba msamaha wa makosa yetu makubwa na madogo. Pia tunamshukuru kwa kuweza kutukutanisha hapa tukiwa wazima na wenye Afya njema, katika kuwatumikia wananchi wetu waliotuchagua kwa mapenzi makubwa.
Mhe. Spika,
Pili naomba pia kukushuru wewe mwenyewe binafsi kwa kuweza kuliongoza Baraza lako tukufu hili la Wananchi wa Zanzibar, kwa kipindi chote cha uhai wa Baraza hili la nane kwa umahiri mkubwa na kwa kushirikiana na wasaidizi wako bila ya matatizo yoyote bila ya kuonyesha upendeleo kwa upande wowote.
 Pia nachukua nafasi nyingine ya kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema yake ya mvua aliyotupa nchini mwetu, ambayo bila ya kutuneemesha neema hii, maisha yetu hayataweza kuendelea. Aidha, kwa kuwa mvua zinazoendelea kunyesha zimeleta maafa kwa baadhi ya wananchi wetu, nachukua nafasi hii kuwapa pole wale wote ambao wameathirika na mvua hizo na nawaomba sana waendelee kuwa na subira na kuchukua hatua madhubuti ya kuepuka madhara makubwa ya mvua hizo, lakini waendelee kuiamini Serikali yao kwani imeonesha mashirikiano makubwa na kuwasaidia katika maafa haya na mengine yanayotokea katika nchi yetu.
Mhe Spika, pia katika hili tunaendelea tena kuwapongeza viongozi wetu wote wakuu wa Nchi kwa kuonysha moyo wa kuwafariji wananchi wetu waliopatwa na maafa ya mafuriko ya Mvua kubwa ya Masika iliyonyesha hivi karibuni, kwa kweli tuliwaona viongozi wetu hawa walitoka maofisini mwao na kuwemo mitaani kuwafariji watu wetu hawa kwa niaba yao tunawashukuru na tunawaomba waendelee na moyo huo huo wa kuwa karibu na jamii kwa hali na mali.

Mhe. Spika,
Kwa heshima kubwa kamati yangu tunampongeza sana Mhe Makamo wa Kwanza wa Rais, kwa kuendelea kuiongoza Afisi yake ya Makamo wa Kwanza wa Rais kwa umahiri mkubwa na pia kuendelea kumshauri vizuri Mhe Rais wa Zanzibar katika kuiongoza nchi yetu sote tunaamini mafanikio yote tunayoyapata ya maendeleo hapa Zanzibar basi ni mashauriano ya pamoja baina ya Mhe Rais wetu wa Zanzibar, Makamo wa kwanza wa Rais na Makamo wapili wa Rais, kwa kukaa pamoja na kuangalia mustakbal wa nchi yetu katika kuwaletea maendeleo hapa Zanzibar, tunawaomba viongozi wetu waendelee kukaa pamoja kwa kushauriana na tumuombe Mwenyeenzi Mungu awajaalie waendelee kuelewana kwani wakielewana wao ndipo Nchi yetu itakapopata Baraka na neema ili wananchi wetu wafaidike na matunda ya Nchi yetu.
Mhe Spika,
Pia kamati yangu inampongeza sana Mhe Waziri wa Nchi Afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, kwa kuweza kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa kwa kumsaidia Makamo wa kwanza wa Rais katika shughuli zake, Mhe Spika, Waziri huyu ni mwanamke shupavu asiyeyumba wala kuterereka katika kutekeleza majukumu yake, na ndio maana ameweza kubeba sifa ndani na nje ya nchi yetu, kamati yangu katika kipindi chote cha miaka mitano imeweza kupata mshirikiano makubwa kutoka kwa Waziri huyu, kwani pia hakusita kutaka msaada wetu pale alipokua akikwazwa na utekelezaji wa shughuli zake na bila kusita kamati yangu iliweza kutoa msaada mkubwa ili kufanikisha majukumu yake , ndio maana leo tunajivunia alau kuweza kupata eneo la kujenga nyumba za kurekebishia tabia za vijana wetu walioathirika na madawa ya kulevya( Rehabilitation Centre) huko kidimni Mkoa wa Kusini Unguja, hayo ni baadhi tu kati ya mafanikio hayo.
Mhe Spika, kwa kuwa Mhe Waziri yeye ni (Hajat) na katika hotuba yake ametuombea Dua sote turudi tena hapa Barazani ili kuliendeleza gurudumu hili tuliloliacha basi Mweneenzi Mungu aikubali dua yake ili tuweze kuwa pamoja mwakani kuja kuisimamia Bajet yake hii. Amin.
Mhe Spika, pia kamati yangu inaungana na Waziri kutoa mkono wa pole kwa Familia ya aliyekua mjumbe mwenzetu Marehem Salmin Awaadh Salmin. Sote basi tumumbe Mwenyenzi Mungu aiweke roho ya mwenzetu  peponi Amin.
Mhe Spika,
Kamati yangu inatoa shukrani zetu za dhati kwa Katibu Mkuu wa Afisi hii kamati yangu pamoja na kuisimamia Afisi hii lakini imeweza kuchota mengi kutoka kwa Katibu Mkuu huyu Senior katika SMZ,  Naibu Katibu wake ,Wakurugenzi, Makamishna pamoja na watendaji wote wa Afisi hii ya Makamo wa Kwanza.
Nichukue tena nafasi hii kuwapongeza Wajumbe wote wa Baraza hili la Nane la Wawakilishi, lililoanza uhai wake Novemba 2010, kwa Mashirikiano na kufanya kazi kwa pamoja baina ya Wajumbe hawa, bila ya kujali tofauti zao za kisiasa kwa kweli kumenipa faraja sana na kujiamini kwa kusimama tena leo hii katika kikao cha mwisho cha Bajeti ya Ofisi hii ya Makamo wa Kwanza wa Rais. Niendelee kuwaomba Wajumbe kudumisha mapenzi na mashirikiano ya pamoja katika kujenga nchi yetu hii ya Zanzibar, ambayo ni utegemezi wake, ni nguvu za pamoja za watu wake, ambao ndio sisi na wananchi wa Majimbo yetu yote.
Mhe Spika,
Baada ya shukrani nyingi kwa watu mbali mbali tulioshirikiana nao sasa naomba niingie katika kuichangia Hotuba ya Mhe Waziri afisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, kama hivi ifuatavyo;-
Mhe Spika,
Kwa kweli kwa niaba ya kamati tumpe pole sana Mhe Waziri, kwani majukumu yote aliyopewa kuyasimamia katika Afisi yake ni masuala magumu ambayo yanachangamoto nyingi kwani karibu yote wao hawana uwezo wa kuyashulikia moja kwa moja isipokua inabidi yashughulikiwe na taasisi nyingine chini ya isimamizi wenu inawezekana wakati mwingine hamuridhiki na uharaka au kwa kasi mnayoitarajia lakini mnabakia kusikitika, au kusononeka lakini pamoja na hayo tunawapomngeza kwa kuwasimamia kwa karibu na kutoa ushauri pale inapobidi ili kuhakikisha kwamba ufumbuzi unapatikana.
Mhe Spika,
Kamati yangu inaipongeza Idara ya Uratibu ya shughuli za Makamo wa Kwanza wa Rais kwa kuweza kuratibu shughuli zake zote za kitaifa pamoja na zile zinahusu masuala ya nje ya nchi ya Makamo wa kwanza , lakini bado kamati yangu inaungana na Mhe Waziri kwa idara hii kuendelea kukabiliana na changamoto wa ukosefu nyumba za makaazi kwa Makamo wa Kwanza wa Rais hapa Unguja, bado tunakodi nyumba ya mtu binafsi, vil;e vile Pemba tunakodi na Dar-es- Salaam ndio kabisaaa  anafikia Hoteli, Mhe Spika, Kamati yangu kwa kweli hairidhiki kabisa na hali hii kwani huyu ni kiongozi mkubwa katika Nchi yetu, lakini pia inaigharimu Serikali kutumia pesa nyingi sana kulipia majengo hayo pesa ambazo zingeliweza kuwahudumia wananchi wetu kwa shughuli zao mbali mbali za kijamii na kimaendeleo. Kwa hiyo tunaiomba Serikali katika muhula ujao kupitia Tume ya Mipango tunaitaka Serikali kuhakikisha inampatia Makamo wa Kwanza wa Rais Makaazi ya kudumu Unguja, Pemba na Dar-es Salaam, ili awe na utulivu lakini vile vile kuokoa pesa za wananchi.
Mhe Spika,
Jukumu jingine ambalo Afisi hii ya Makamo wa Kwanza ni usimamizi wa Mazingira, kama nilivyoeleza hapo mwanzo miongoni mwa changamoto zilipo katika eneo hili la uharibifu wa Mazingira kwa kweli hali yetu sio nzuri katika usimamizi wa jambo hili, kwani ukizingatia nchi yetu ni visiwa lakini bado uelewa wa wananchi wengi katika uhifadhi wa Mazingira hapa Zanzibar ni mdogo sana kwani ukiangalia kuanzia katika miradi mikubwa mingi hapa Zanzibar huwa haifanyiwi tathmini ya kimazingira kabla ya kuanzisha miradi hiyo jambo ambalo hasa katika fukwe zote za Zanzibar kuna uharibifu mkubwa wa Mazingira na wakati mwingine sisi viongozi ndio tunaowakingia vifua watu hao bila ya kujua kuwa tunaliangamiza taifa letu, na waswahili wanamsemo wao kua hili gogo tulilokalia ndio tunalolikata yaani.( VISIWA VYA UNGUJA NA PEMBA) hali hii kwa kweli inasikitisha sana kwani athari kubwa tumeanza kuziona, leo hii tusije kushangaa siku moja tiamka Kisiwa cha Kisiwa Panza kikiwa kimezama chote kwa maji ya Bahari.(Mwenyenzi Mungu atuepushie mbali)
Mhe Spika,
Leo hii wananchi wengi hasa katika kisiwa cha Pemba wameingia katika umaskini mkubwa waliokua hawakuutarajia katika maisha yetu kwani yale maeneo waliyokua wakilima mpunga na mazao mengine tangu enzi za mababu zetu hivi sasa yamevamiwa na maji ya Bahari na hawawezi tena kuyatumia kwa ajili ya Kilimo, jambo ambalo walikua kilimo wakikitegemea kwa chakula, kusomesha watoto wao, pamoja na mahitaji mengine, hii yote inatokana na uharibifu wa mazingira hasa kwenye maeneo ya fukwe unayofanywa na katika maeneo mengine. Kwa hiyo nitoe wito kwa sisi sote tuungane katika kupiga vita uharibifu wa mazingira.
Mhe Spika,
Kutokana na kuokoa muda nimetoa mfano mmoja tu katika uharibifu wa mazingira ambapo eneo hili ndilo linaloongoza katika kuwatia umasikini watu wengi kwa hiyo nawaachia wajumbe wengine ili waongelee maeneo mengine ya yenye uharibifu wa Mazingira.
Mhe Spika,
Pamoja na hayo lakini kamati yangu tunatoa pongezi kwa Serikali kwa kusikia kilio chetu cha muda mrefu kwenye eneo hili kwa kuleta Sheria itakayoanzisha taasisi maalum itakayosimamia masuala ya mazingira tunaamini ikiweza kusimamia vizuri Basi athari hiyo haitoweza kuendelea kua mbaya zaidi na kutoa miongozo ya kudhibiti Pale palipokwisha kuharibika.
Mhe Spika,
Kamati yangu inaipongeza Serikali kupitia Idara ya watu wenye Ulemavu kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuratibu masuala yote yanayohusu watu wenye ulemavu na pia kuweza kukamilisha Data base ya kuwatambua watu wote wenye ulemavu kwani hii itasaidia kuwatambua ili kuweza kurahisisha upatakanaji wa mahitaji muhimu kwa wakati ya watu hao, lakini pia nitoe pongezi maalum kwa mkurugenzi wa Idara hii kwa kazi kubwa anayoifanya katika kupigania haki za watu wenye ulemavu, kwa hiyo tunawaomba waendelee na utendaji wao bora , kwa hiyo natoa wito kwa Mkurugenzi wa Idara hii kuanza mikakati ya kutafuta Wawakilishi na Wabunge wao wenyewe watakaokuja kuwawakilisha katika chombo hiki cha Baraza la Wawakilihi na Bunge ili kuja kutetea fursa, maslahi na huduma bora kwa kundi lao ndani ya vyombo vya kutunga Sheria baada ya Katiba mpya kupitishwa. Pia tunawapongeza kwa kuanzisha mfuko wa watu wenye ulemavu mfuko ambao utaweza kusaidia shughuli zao mbali mbali za kujiongezea kipato na kuwaletea maendeleo.
Mhe Spika,
Kama nilivyoeleza hapo mwanzo Waziri amekabidhiwa mambo mazito mingoni mwao ni mapambano dhidi ya maradhi thakili yanayoangamiza wananchi wetu, yaani maradhi ya ukimwi, tunampongeza Mkurugenzi wa Tume ya Ukimwi kwa kazi kubwa ya kueleimisha jamii katika mapambano dhidi ya maradhi ya Ukimwi, lakini kamati yangu inasikitika sana pale inaposikia kua washirika wa Maendeleo wameanza kupunguza misaada yao katika mapambano dhidi ya Maradhi ya Ukimwi.
Kwa hiyo kamati yangu inaitaka Serikali pamoja na kuongeza fungu katika mapambano dhidi ya maradhi ya ukimwi lakini bado fungu hilo ni dogo halitoshi kwa kulingana na gonjwa lenyewe, pia kamati yangu inawapongeza viongozi wa ZAPHA + Kwa jitihada zao za kujikusanya na kuweza kutoa misaada mbali mbali kwa wale waliopata maambukizi ya maradhi hayo pia na kwa wale ambao tayari wameathirika, kwani bila ya jitihada zao basi hali ingelikua mbaya zaidi. Kutokana na elimu wanayoendelea kuitoa kwa jamii basi hata hali ya unyanyapaa imepungua kwa kiasi kikubwa ingawa bado kuna mnaeneo mengine unyanyapaa bado upo, kwa hiyo bado jitihada ya kuwafikia watu katika maeneo hasa ya vijijini iendelee na kwa hiyo iko haja kwa Serikali kuandaa utaratibu wa kuisaidia fungu la fedha ZAPHA+ hasa baada ya hao wahisani kupunguza kwa kiasi kikubwa misaada kwa masuala ya Ukimwi.
Mhe. Spika,
Kamati yangu imeendelea kujadili na kutafakari kwa kina bajeti za Wizara tatu inazozisimamia, ikiwa ni pamoja na Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais.
Kamati yetu imepokea bajeti kwa Wizara zote hizo katika mfumo mpya wa Programu, ambao unaitwa Program Based Budget (PBB). Mfumo huu kama ulivyokwisha elezwa na Mhe. Waziri na kama Wajumbe wako walivyopata mafunzo yake kupitia Semina ya tarehe 14 -15 Mwezi huu, unatofautiana sana na ule tuliouzoea wa Line Budget, ambao Wajumbe walikuwa wanajadili kifungu kwa kifungu, lakini sasa wanalazimika kujadili Progamu kubwa na ndogo.
Mhe. Spika,
Pamoja na kutolewa semina kwa Wajumbe wote tarehe 14 -15/05/2015, na pamoja na ukweli kuwa mabadiliko haya yalianza kuelezwa na Wajumbe kupata maelezo yake takriban miaka miwili nyuma, utakubaliana na mimi kuwa, kabla ya Kamati zetu kupitia bajeti za Wizara husika, ama kabla ya Kamati ya Wenyeviti kupitia bajeti kuu ya Serikali, ilipaswa kwanza Wajumbe wote wawe na uelewa mpana zaidi na hasa kwa namna ulivyowasilishwa katika vitabu vya bajeti.
Kwa hiyo kamati yangu inaenedelea kuitaka Serikali kwa kushirikiana na Afisi yetu ya Baraza la Wawakilishi mara tu baada ya Uchaguzi Mkuu kutoa mafunzo upya kwa Wajumbe wako wa Baraza hili tukufu la Wawakilishi ili kuweza kuisimamia Bajeti hii tunayoipitisha hapa Barazani.
Mhe. Spika,
Kamati yangu ilifanya uchambuzi wa bajeti ya Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, pamoja na kukosa elimu ya matendo kabla ya bajeti hiyo na imelazimika kujifunza haraka sana wakati huo huo wa upitishaji wa bajeti. Katika kuipitia bajeti hiyo, Kamati yangu itaizungumza Ofisi hii katika maeneo matatu makuu kama ifuatavyo:
OFISI YA MAKAMO WA KWANZA WA RAIS ZANZIBA
Mhe Spika,
Bado Ofisi hii inaendelea na makusanyo ya mapato yake kupitia Idara ya Mazingira, ambayo inategemea kupata mapato hayo kupitia ada ya hifadhi ya mazingira ambayo kwa mwaka jana ilikadiriwa kukusanywa Tsh. 10,500,000, na ilipofikia Machi 2015, Idara ilifanikiwa kukusanya Tsh. 8,700,000, sawa na asilimia 83 ya makadirio. Sasa Idara hii kwa mwaka huu wa 2015/2016 imekadiriwa kukusanya Tsh. 23,100,000, kwa nyongeza ya Tsh. 12,600,000, ambayo ni sawa na asilimia 220 ya makadirio ya mwaka uliopita, fedha ambayo kwa namna ambavyo haikuweza kukusanywa kamili kwa miaka iliyopita ambapo Idara hii kwa mfano mwaka 2012/2013 ilikadiriwa kukusanya Tsh. 8,130,000 na ulipotimia mwaka iliweza kukusanya Tsh. 7,618,000 sawa na asilimia 94 ya makadirio. Ni wazi kuwa, kwa mwaka huu pamoja na ukweli kuwa Idara na Wizara kwa ujumla wanategemea kupata mafanikio makubwa baada ya kusainiwa kwa Sheria mpya ya Mazingira, bado kuna changamoto kubwa ya kupatikana makusanyo kamili ya yaliyokadiriwa.

Mhe. Spika,
Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais kupitia Idara ya Mazingira, imekisia kukusanya Tsh. 11,612,000 kupitia chanzo kipya cha ada ya ukaguzi wa mazingira. Chanzo hiki kimeelezwa kwa Kamati kuwa kinatokana na Sheria mpya ya usimamizi wa Mazingira ambayo itaipa Idara ya Mazingira ruhusa kamili ya kukagua miradi ya mazingira na hivyo taasisi zinazohusika na ukaguzi wa mazingira kupitia miradi yao mbali mbali, watatakiwa kufanyiwa ukaguzi huo. Chanzo hiki kinaifanya Ofisi hii kuwa na dhima ya makusanyo ya Tsh. 34,712,000.
Hata hivyo, Kamati haina pingamizi na chanzo hicho wala kima kilichokisiwa kukusanywa, kwani kula uhondo kwataka matendo na asiye na matendo hula uvundo. Hivyo, hatupendi kuona fedha hizo zilizokadiriwa zinashindwa kukusanywa, mbali na kuelezwa kwenye vitabu hivyi vya bajeti. Ni lazima Idara ya Mazingira kwa muongozo wa Ofisi hii ya Makamo wa Kwanza wa Rais, ikajifanya juhudi kubwa katika kukusanya fedha hizo, ili mwaka ujao iweze kupatiwa kima cha juu zaidi katika makusanyo yake. Kamati yangu inaamini kua ikiwa Mamlaka hii ya usimamizi wa itafanya kazi yake ipasavyo basi watakusanya zaidi ya kiwango hicho kilichowekwa kwani kuna adhabu nyingi kwa wale watakao kiuka sheria na kukiuka sheria ya Mazingira jambo ambalo limekua ni utamaduni wa wazanzibari pamoja na wawekezaji kukiuka kwa makusudi taratibu za uhifadhi wa mazingira.
Mhe. Spika,
Ofisi hii sasa inatambuliwa matumizi yake kupitia fungu kuu la B01, ambapo jumla ya fedha zinazohitajika kwa matumizi ya kazi za kawaida ni Tsh. Bil, 2,923,400,000 na fedha zinazohitajika kwa matumizi ya maendeleo ni Tsh. 450,000,000. Fedha hizo zinatarajiwa kutumika kwa program kuu tatu na program ndogo sita kama ifuatavyo:
Programu Kuu ya Usimamizi wa Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi, yenye program ndogo mbili ambazo ni Usimamizi wa Mazingira na Usimamizi wa Mabadiliko ya Tabianchi.
Programu Kuu ya Pili ni Usimamizi wa Masuala ya Watu wenye Ulemavu ambayo ina program ndogo moja ya Usimamizi wa Masuala ya Watu wenye Ulemavu, na
Program Kuu ya Tatu ni Mipango na Utawala yenye program ndogo tatu ambazo ni Uongozi na Utawala, Mipango, Sera na Utafiti na Uratibu wa masuala ya Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, Pemba.
Mhe. Spika,
Program Kuu zote hizi zimeelezwa huduma zake zinazotarajiwa kutolewa pamoja na viashiria vya mafanikio yanayotarajiwa kufikiwa kwa mwaka wa 2015/2016. Aidha, kwa program ndogo ya Usimamizi wa Mazingira inatarajiwa kutumia Tsh. 174,076,000 ambapo Tsh. 161,376,000 zinatarajiwa kutumika kwa kuendeleza mazingira endelevu kwa jamii na Tsh. 12,700,000 zitatumika kwa kukuza uelewa wa kimazingira kwa jaimii.
Mhe. Spika,
Jumla ya Tsh. 155,460,000 zinahitajika kwa matumizi ya Tsh. 73,060,000 zinazotarajiwa kutumiwa kwa ujumuishwaji wa watu wenye ulemavu, Tsh. 2,400,000 zinahitaji kwa kukuza uelewa wa jamii juu ya masuala ya watu wenye ulemavu, huku Tsh. 80,000,000 zikihitajika kwa uwezeshaji wa watu wenye ulemavu.
Mhe. Spika,
Kamati yetu pia iliridhika kwa Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais kuidhinishiwa Tsh. 2,593,864,000 kwa Tsh. 2,051,997,000 kutumika kwa kuimarisha ufanisi wa utendaji kazi na uongozi, kusaidia jamii katika kazi za maendeleo na kuongeza uelewa wa jamii juu ya masuala yanyaosimamiwa na Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais.

Mhe. Spika,
Kamati imeelezwa na kuridhika kuwa Tsh. 53,744,000 zitumike kwa kuimarisha mfumo wa upatikanaji wa taarifa na kuzisambaza kwa wadau, Tsh. 17,527,000 zitumike kwa kuratibu masuala mtambuka yanayosimamiwa na Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, huku utayarishaji wa sera na mipango ya maendeleo utumie Tsh. 22,448,000.
Mhe. Spika,
Program ndogo ya uratibu wa masuala ya Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, Pemba unahitaji fedha za kutosha, hali iliyoifanya Kamati yangu kuridhishwa na kuidhinishwa matumizi ya Tsh. 448,148,000 ambapo jumla ya Tsh. 426,480,000 zitumike kwa kuimarisha ufanisi wa utendaji kazi na uongozi na Tsh. 21,668,000 zitumike kwa kuratibu, kufuatilia na kukuza mashirikiano kwa masuala ya Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, kisiwani Pemba.
Mhe. Spika,
Jumla ya Tsh. 450,000,000 zimekadiriwa na Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais kwa miradi ya maendeleo chini ya program ya Usimamizi wa Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi, ambapo program hii kubwa chini ya program ndogo ya Usimamizi wa Mabadiliko ya Tabianchi inakusudiwa kuratibu na kusimamia masuala ya mabadiliko ya tabianchi ambapo kazi kuu ni kutayarisha nyenzo na mipango ya usimamizi, kuratibu mikutano ya ya usimamizi, kujenga uwezo wa wadau na kukuza uelewa juu ya athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuzisaidia jamii katika kukabiliana na athari za mabadiliko hayo.
Mhe. Spika,
Fedha hizo za maendeleo zinazoombwa zitasimamiwa na Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais chini ya Idara ya Mazingira , Wizara ya Kilimo na Maliasili kupitia Idara ya Misitu na Maliasili zisizorejesheka, kwa mfano kuna Tsh. 37,000,000 zimekadiriwa kutumiwa kwa kuimarisha mazingira wezeshi kwa kuongeza matumizi mbadala ya misitu Zanzibar. Aidha, utekelezaji wa program ndogo hii ya Usimamizi wa Mabadiliko ya Tabianchi utafanywa kwa mashirikiano na Wizara ya Fedha kupitia Idara ya Fedha za Nje, Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati kupitia Idara ya Nishati na Madini na Jumuiya ya CODECOZ na kuratibiwa na Idara ya Mipango, Sera na Utafiti.
Mhe. Spika,
Fedha zote hizo Tsh. 450,000,000 zinakadiriwa kupatikana kutoka kwa Washirika wa Maendeleo ambao ni UNDP huku fedha hizo ama zikiwa ni ruzuku ya nje na fedha za ndani. Aidha, pamoja na ukweli kuwa, katika vitabu vya bajeti vilivyowasilishwa kwa Kamati, Serikali haikuonekana kuchangia fedha yoyote, imeelezwa na Mhe. Waziri kupitia ripoti yake kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatarajiwa kuchangia Tsh. 174,076,000 kwa ajili ya utekelezaji wa program hii.  Kwa hiyo katika eneo hili kamati yangu inaomba ufafanuzi mpaka kufikia sasa jee iyo fedha kwa upande wa Serikali jee zimeshaingizwa?
TUME YA KITAIFA YA KURATIBU NA UDHIBITI WA DAWA ZA KULEVYA ZANZIBAR
Mhe. Spika,
Tume ya Kitaifa ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya Zanzibar inakadiriwa kutumia Tsh. 166,091,000 kwa ajili ya mishahara, Tsh. 134,680,000 kwa matumizi ya maposho na Tsh. 166,329,000 zitatumika kwa matumizi ya uendeshaji wa Ofisi, na hivyo kwa pamoja fedha zinazoombwa ili ziidhinishwe na Baraza hili ni Tsh. 467,100,000. Fedha zote hizo zimeombwa chini ya program kuu mbili, Programu ya Dawa za Kulevya yenye program ndogo mbili ya Udhibiti wa usafirishaji na usambazaji wa dawa za kulevya na program ndogo ya Kinga ya Msingi ya Mahitaji ya Dawa za Kulevya. Na program kuu ya pili ni Utawala na Uendeshaji wa Tume ya Dawa za Kulevya ambayo program yake ndogo ni hiyo hiyo ya Utawala na Uendeshaji wa Tume ya Dawa za Kulevya.
Mhe. Spika,
Bado tukumbuke kuwa, Zanzibar imeendelea kuwa sehemu hatarishi ya Uingizaji na Usambazaji wa dawa za kulevya. Vijana wetu wanaendelea kuathirika na matumizi haya ya dawa za kulevya hali inayolipelekea Taifa hili kukosa nguvu kazi na kurudi nyuma kimaendeleo. Hivyo, ili kukabiliana na tatizo sugu la dawa za kulevya, Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais kupitia Tume hii imeweka program ndogo ya kudhibiti usafirishaji na usambazaji wa dawa za kulevya Zanzibar, ambapo jumla ya Tsh. 30,908,000 zinahitajika kwa kudhibiti uingizaji na usafirishaji wa dawa za kulevya na Tsh. 26,906,000 zinahitajika kwa kuzuia usambazaji wa dawa za kulevya.
Mhe. Spika,
Pamoja na kima hicho kilichotengwa kwa shughuli hizo za udhibiti na usambazaji wa dawa za kulevya, ilivyokuwa malalamiko makubwa ya wananchi dhidi ya matumizi ya madawa ya kulevya yanalegwa katika uingizwaji na usambazaji wa dawa hizo kwa watumiaji mbali mbali na kwa kuzingatia ukweli kuwa Serikali hufanikiwa zaidi kuwashughulikia watumiaji kuliko waletaji na wauzaji wa dawa hizo, fedha zilizotengwa katika kutekeleza porgramu ndogo hii ni chache sana na inaonesha bado Serikali kwa ujumla inahitajika iwe makini sana na jukumu hili zito ambalo ndio chanzo cha kuenea matumizi ya madawa ya kulevya Zanzibar.
Mhe. Spika,
Jumla ya Tsh. 376,036,000 zinahitajika kwa program ya Utawala na Uendeshaji wa Tume ya Dawa za Kulevya kwa kujenga uwezo wa wafanyakazi katika uratibu wa mapambano ya Dawa za Kulevya ambapo jumla ya Tsh. 304,690,000 zinahitajika na kwa ajili ya Uratibu wa Shughuli Tume ya Dawa za Kulevya Pemba, fedha zinazohitajika ni Tsh. 71,346,000. Aidha, kwa ujumla utekelezaji wa program ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya unaoratibiwa na Tume ya Kitaifa ya Kuratibu na Udhibiti wa Dawa za Kulevya unakadiriwa kutumia Tsh. 91,064,000/-.
TUME YA UKIMWI ZANZIBAR
Mhe. Spika,
Kwa mwaka wa fedha 2015/2016, Tume ya Ukimwi inahitaji kupatiwa Tsh. Bil. 1,703,600,000, ambazo fedha zitakazotumika kwa kazi za kawaida ni Tsh. Mil. 721,200,000 na fedha za maendeleo ni Tsh. Mil 982,400,000. Fedha hizo zinatarajiwa kutumika chini ya program kuu mbili, program ya Kuratibu Muitiko wa Taifa wa Ukimwi ina program ndogo mbili ya Mawasiliano na utetezi wa masuala ya Ukimwi na Uratibu wa muitiko wa Taifa wa Ukimwi, na program kuu ya pili ni Utawala na Uendeshaji wa Tume ya Ukimwi ambayo program yake ndogo ni Utumishi na Uendeshaji wa Tume ya Ukimwi.
Mhe. Spika,
Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais kupitia Tume ya Ukimwi, imeahidi mbele ya Kamati kuwa, kwa kutekeleza program zote mbili na program ndogo zilizomo, itakapofika June 30 ya mwaka 2016, itakuwa imeshatekeleza mambo yafuatayo:
·       Imezifikia Shehia 20 kwa maonesho.
·       Imefanya program 150 za jamii kwa makundi maalum.
·       Imewafikia watu 1400 wa makundi maalum.
·       Imechapisha na kusambaza vipeperushi, vijarida 5000 kwa walengwa.
·       Imetoa vipindi 36 vya redio na TV.
·       Imehamasisha mikoa mitano kwa kuitaka kuchukua hatua za kupunguza mazingira hatarishi ya Ukimwi.
·       Imetoa mikutano 16 ya kuziratibu taasisi zinazotekeleza shughuli za utetezi na uhamasishaji wa masuala ya ukimwi.
·       Imezijengea uwezo taasisi 30 zinazojishughulisha na masuala ya Ukimwi, na
·       Imetoa asilimia 100 ya fedha kwa utekelezaji wa program za maisha na afya ya uzazi kwa vijana nje ya Skuli.
Mhe. Spika,
Inatarajiwa sana kwa Serikali sikivu kuwa mbali na kusema maneno na kuacha wananchi wake watende matendo. Serikali sikivu siku zote hutenda matendo na kuwaacha wananchi wake na watu wengine kusema maneno. Hii ni kwa sababu, tendo hukidhi haja maridhawa kuliko neno. Na haja ikishughulikiwa kwa matendo hupatikana upesi, lakini ikishughulikiwa kwa maneno, huchelewa kama sadaka.
Mhe. Spika,
Kwa muda mrefu Serikali yetu husema maneno ikiwa ni pamoja na haja ya kuleta mabadiliko ya mfumo wa bajeti katika kipaumbele cha program za kila Taasisi zake, na kuwaacha wananchi wake waje waipime na kuzipima taasisi hizo katika utekelezaji wa program hizo na viashiria vyake, leo tunaisifu kwa kutendo matendo ya waliyouyasema muda mrefu wa nyuma. Hata hivyo, hatua hii bado haijakidhi shida ya maneno ya wananchi na dhiki kubwa inayoipa taasisi zake, nayo ni kupatiwa na kuingiziwa fedha kamili za matumizi kama vile yalivyokadiriwa na Baraza hili katika mikutano mbali mbali ya bajeti.
Mhe. Spika,
Serikali yetu pamoja na ahadi nyingi za mfumo huu mpya wa bajeti, iwapo tutashindwa kukushanya kama tulivyopanga na ikiwa itaacha kufanya matendo ya kuziingiza fedha inazoahidi leo na katika kikao hiki cha bajeti kwa Wizara na taasisi zake, itaendelea zaidi kutoa mzigo mzito kwa Taasisi hizo na hatimae kwa wananchi.
Mhe Spika, kwa upande wa mambo ya kiujula naomba kuishauri Serikali kuangalia matatizo yanayowakabili hasa wananchi katika kisiwa cha Pemba kwa kuvamiwa na maji ya Bahari kwenye maeneo yao ya kilimo ambayo wanayategemea kwa kuendeshea maisha yao, kwa hiyo uvamizi huo umewaacha wananchi hao katika umasikini mkubwa kwani hawana njia nyingine yeyote ya kuendeshea maisha yao, kwa hiyo ni lazima Serikali kuandaa mradi maalum kwa kuyahami maeneo hayo ambayo kila siku yanaongezeka bila ya kuweka utaratibu basi umasikini utakua unaongezeka siku hadi siku na baadae utakua ni mzigo mkubwa kwa Serikali yetu.
Mhe. Spika,
Mwisho kabisa wa hotuba yangu hii fupi, naomba nitoe shukurani zangu za dhati kwako wewe na Waheshimiwa Wajumbe wote, bila ya kuwasahau Wajumbe wa Kamati yangu na Makatibu Kamati. Aidha, naomba ruhusa yako niendelee kuwatambua kama ifuatavyo:
1.    Mhe Hamza Hassan Juma                    Mwenyekiti
2.  Mhe. Saleh Nassor Juma                      Makamo Mwenyekiti
3.  Mhe. Ali Mzee Ali                                 Mjumbe
4.  Mhe. Ashura Sharif Ali                           Mjumbe
5.  Mhe.Shadya Mohammed Suleiman        Mjumbe
6.  Mhe. Makame Mshimba Mbarouk          Mjumbe
7.  Mhe. Subeit Khamis Faki                         Mjumbe
8.  Ndg.Rahma Kombo Mgeni                     Katibu Kamati
9.  Ndg.Othman  Ali Haji                            Katibu Kamati
Mhe. Spika,
Naendelea kumshukuru Mhe. Waziri, Ofisi ya Makamo wa Kwanza wa Rais, Katibu Mkuu wa Ofisi hii na watendaji wake wote kwa mashirikiano mema waliyoipatia Kamati kwa muda wote wa uhai wa Kamati yetu.
Mhe. Spika,
Kama sitakosea kutoa nasaha zangu kwa Katibu Mkuu na watendaji wake, huku nikijua kuwa sisi viongozi wa siasa huongoza Taasisi hizi kwa muda na wao ni waajiriwa wa kudumu, niendelee kuwaeleza kuwa, wao ndio roho ya Ofisi hii ya Makamo wa Kwanza wa Rais. Kutekeleza kwao kwa majukumu yao kwa kuzingatia Katiba na Sheria ni matarajio makubwa sana ya wananchi wa nchi hii. Aidha, wao ni wataalamu na ni wajuzi wa mambo mbali mbali, lakini wenye dhamana ya kuwaletea maendeleo na kuimarisha ustawi wa wananchi wa Zanzibar kupitia Ofisi yao hii.
Mhe. Spika,
Tunaendelea kuwanasihi watendaji hawa waendelee kutekeleza majukumu yao kwa uadilifu mkubwa. Dhamana hii waliyonayo ni mzigo mzito mbele ya Muumbaji wao. Kutekeleza kwao kwa majukumu yao, kusishawishike na tamaa ya mali, kwani mioyo mingi haitoshwi na mali. Walakini, kwa kweli fikira ya mali isiyo kadiri, ni mzigo usiochukulika.
Mhe. Spika,
Sasa niwaombe Waheshimiwa Wajumbe watumie vipawa vyao na uwezo wao mkubwa katika kuijadili bajeti ya Ofisi hii. Watumie elimu na uzoefu wao walioupata katika miaka yote mitano ya uhai wao na uhai wa Baraza hili la Nane, huku wakijua kuwa, zaidi ya nusu ya hasara za wanaadamu hutokea kwa sababu wenyewe hawataki kutumia vipawa vyote walivyopewa. Tusipotumia vipawa na elimu tuliyopewa katika kujadili na kuchambua bajeti kama hii, ambapo ndio moja kati ya majukumu manne makuu yaliyoelezwa na kifungu cha 88 cha Katiba ya Zanzibar, tutawanyima sana wananchi wetu waliotutuma kuwawakilisha katika chombo hiki, haki yao ya uwakilishi bora. Kwahiyo, tuijadili kwa busara na upeo wa elimu na juhudi zetu kwa kutoa michango kwa lengo la kuiboresha.
Mhe. Spika,
Naomba kuwasilisha.

............................
Hamza Hassan Juma,
Mwenyekiti,
Kamati ya Kusimamia Afisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.