MUHTASARI WA HOTUBA YA
MWENYEKITI WA KAMATI YA KATIBA, SHERIA NA UTAWALA YA BARAZA LA WAWAKILISHI,
KUHUSU MAKADIRIO YA BAJETI YA WIZARA YA KATIBA NA SHERIA MWAKA 2015/2016
Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii
kumshukuru Mwenyezi Mungu mtukufu kwa kutujaalia afya njema na kutuwezesha
kukutana hapa kwa ajili ya kutekeleza wajibu wa kulijenga taifa letu. Aidha
napenda kuchukua nafasi hii pia kukushukuru wewe Mheshimiwa Spika kwa kunipa
nafasi hii adhimu ya kutoa maoni ya Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala kuhusu
makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka wa
fedha 2015/2016.
Mheshimiwa Spika,
Nitumie nafasi hii pia
kumshukuru Waziri wa Katiba na Sheria, Mheshimiwa Abubakar Khamis Bakar, Katibu
Mkuu ndugu Asaa Ahamad Rashid na Naibu Katibu Mkuu wake Ndugu Mdungi Makame
Mdungi na watendaji wote wa Wizara ya Katiba na Sheria ambao kwa kipindi chote
cha miaka miwili na nusu tumefanya nao kazi kwa mashirikiano makubwa. Naomba
nikiri kuwa Wizara hii ni miongoni mwa Wizara ambazo zimefanikiwa sana katika
utendaji wake kutokana na kupokea na kufanyiakazi kwa vitendo ushauri unaotolewa
na kamati. Nidhamu hii ya utendaji ndiyo leo inanifanya kwa niaba ya Kamati,
kuwapongeza watendaji wa Wizara hii, na kuwataka waendelee kudumisha mashirikiano
baina yetu na wao.
Mheshimiwa Spika,
Kazi
yetu ya kupitia Bajeti ya Wizara hii isingekamilika bila ya mashirikiano ya
hali ya juu ya wajumbe wote wa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ambao
walifanya kazi hii kwa kujitolea. Kazi kubwa imefanywa na Kamati hii chini ya
uongozi wa Mwenyekiti wetu mahiri, Mheshimiwa Ussi Jecha Simai ambaye hivi
sasa anapata nafuu kutokana na mitihani
wa maradhi, na tunamuomba Mwenyezimungu ampe afya njema na uzima ili arudi tena
na kuungana na sisi katika kuwatumikia wananchi wetu.
Mheshimiwa Spika,
Naomba
nitumie muda huu mchache, kuwatambuwa Wajumbe wote wa Kamati ya Katiba, Sheria
na Utawala huku nikithamini mchango wao mkubwa uliofanikisha Kamati hii
kuwasilisha muhutasari huu wa hotuba. Naomba niwataje kama ifuatavyo:-
1.
Mhe. Ussi Jecha Simai
Mwenyekiti
2.
Mhe. Abdalla Juma Abdalla
Makamo Mwenyekiti
3.
Mhe. Wanu Hafidh Ameir
Mjumbe
4.
Mhe. Nassor Salim Ali
Mjumbe
5.
Mhe. Bikame Yussuf Hamad
Mjumbe
7.
Mhe. Suleiman Hemed Khamis
Mjumbe
Mheshimiwa
Spika,
Katika
kipindi chote cha miaka miwili na nusu ya uhai wa kamati hii, shughuli zake
zimekuwa zikiratibiwa na Makatibu wetu wa Kamati, ambao nawashukuru kwa
kushirikiana nasi kwa kipindi chote hicho, pamoja na shukurani hizo naomba
niwataje kama ifuatavyo:-
1.
Ndg. Aziza Wazir Kheir Katibu
2.
Ndg. Khamis Hamadi Haji
Katibu
Mheshimiwa Spika,
Kwa niaba ya wajumbe wa kamati tunawashuru sana.
Mheshimiwa Spika, Wizara
ya Katiba na Sheria ndiyo sehemu ya kielelezo cha utawala wa sheria katika
nchi, kukosekana kwa Wizara hii kunapelekea utaratibu mbovu wa utekelezaji wa
sheria za nchi. Wizara hii ndiyo inayoratibu uendeshaji wa moja ya mihimili
mitatu ya dola ambao ni Mahakama, kutokana na jambo hilo ndiyo maana
nikatangulia kusema kuwa Wizara hii ni sehemu ya kielelezo cha utawala wa nchi
kutokana na umuhimu wake huu.
Mheshimwia Spika,
Katika
bajeti ya mwaka huu inayotumia mfumo wa programu, Wizara ya Katiba na Sheria,
imepangiwa programu kuu mbili katika fungu la Wizara, ambazo ni programu ya
Usajili na Usimamizi wa Masuala ya Dini yenye programu ndogo nne, na programu
ya Mipango na Uendeshaji wa Sekta ya sheria yenye programu ndogo tatu.
Mheshimiwa Spika,
Katika
programu kuu ya kwanza, kamati imepitia programu zake ndogo nne, ambapo
programu ndogo ya kwanza ya Usajili wa Matukio ya kijamii inayosimamiwa na
Ofisi ya Mrajis wa Vizazi na Vifo, imewekewa lengo kuu ambalo ni kuimarisha
mfumo wa usajili wa matukio. Katika kufikia lengo hilo ofisi ya Vizazi na Vifo
imepangiwa kutumia Shilingi 421,
191,000. Kamati yetu imetazama changamoto za Ofisi hii na kuona kuwa kiwango hicho
cha fedha ni kidogo kuweza kufikia malengo hayo kwa ufanisi, na kwa kuwa keki
yetu haitoshelezi kamati yetu inaomba Serikali kuhakikisha kuwa hicho kidogo
kilichokasimiwa kwa Ofisi hii basi kipatikane ili Ofisi hii ya Mrajisi wa
Vizazi na Vifo iweze kufikia sehemu ya lengo na shabaha zilizomo katika
programu iliyopangiwa.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yetu inachukuwa nafasi hii kutambuwa na kuipongeza Ofisi hii kwa kujitahidi
kutanuwa wigo wa usajili kwa maeneo yote nchini. Takribani kila Wilaya sasa
imeshawekwa Afisi za Usajili wa Vizazi na Vifo na kurahisisha upatikanaji wa
huduma hiyo kwa wananchi.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
imeelezwa kuwa katika bajeti ya mwaka huu wa fedha 2015/2016, Wizara ya Katiba
na sheria imetayarisha Mpango kazi wa utekelezaji wa Mkakati wa Mabadiliko ya
Sheria (Zanzibar Legal Sector Reforms) ambapo pamoja na mpango kazi, miradi
sita imeambatanishwa na Mkakati huo. Moja ya mradi huo ni Mradi wa kuimarisha
Usajili wa Vizazi, Vifo, ndoa, talaka na kuasili mtoto. Kamati yetu inapongeza
hatua hiyo kubwa iliyofikiwa, hofu yetu kubwa katika utekelezaji wake ni ile
ile ya upatikanaji wa fedha za kutosha katika kuendesha Mradi huo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yangu inaiomba Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais, Ikulu na Utawala Bora kupitia Tume
ya Mipango, ambayo miradi hiyo itapelekwa kwake kwa hatua zaidi, kukaa na
Wizara ya Katiba na Sheria na kuona ni namna gani miradi hiyo itaingizwa katika
mipango ya Serikali ili kupatiwa fedha na hatimaye iweze kutoa matokeo
yanayokusudiwa kwa wananchi.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
imepitia programu ndogo ya pili, ya usajili wa Biashara na Mali, ambayo katika
bajeti ya mwaka huu 2015/2016, imetengewa shilingi 1,290,605,000, chini ya
Wakala wa Usajili wa Biashara na Mali. Katika kufikia lengo kuu la kuimarisha
mfumo wa usajili wa biashara na mali, kamati inashauri Serikali kuitumia Ofisi
ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Mali, kuweka mfumo mmoja wa usajili wa
Kampuni, jumuiya na nyaraka kwa njia ya dijitali.
Mheshimiwa Spika,
Mfumo
mmoja wa usajili wa Kampuni na jumuiya nyengine kwa njia ya dijitali ni muhimu
katika kuimarisha ukusanyaji kodi na uwekaji wa takwimu kwa usahihi. Kamati
imeona kuwa kampuni zinazosajiliwa nchini taarifa zake za usajili zinawekwa na
Wakala wa Usajili wa Bishara na Mali, kampuni hizo hizo zinafanya biashara na
kutakiwa kulipa kodi ambapo baadhi ya Kampuni hizo zinapopeleka marejesho
katika taasisi za kodi, huwa hazipeleki baadhi ya taarifa muhimu kwa nia ya
kukwepa kodi au kupunguza viwango vya matozo na kuikosesha mapato Serikali.
Mheshimiwa Spika,
Sote
tunakumbuka kuwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, ametutaka wajumbe wa Baraza hili
kumsaidia kutambua vyanzo vya mapato na yeye atavishughulikia. Katika kutambua
huko kamati yangu inaona kuwa uwepo wa mfumo mmoja wa usajili wa Kampuni kwa
njia ya dijitali ni chanzo muhimu cha mapato na kitasaidia kuongeza mapato ya
Serikali.
Mheshimiwa Spika,
Katika
mfumo huo taarifa za Kampuni zote zitawekwa katika mfumo wa dijitali na Wakala
wa Usajili wa Biashara na Mali, ambapo taasisi nyengine za kodi kama TRA na ZRB
zitaweza kupata taarifa hizo kwa usahihi kutoka kwa Wakala wa Usajili wa
Biashara na Mali na kuweza kuzitoza kodi taasisi hizo kwa usahihi. Kamati yangu
inaomba Serikali kuisaidia mipango ya kuanzishwa kwa mfumo huo ambao wataalamu
wameshafanya ‘study’ kwa awamu ya
kwanza, na hivi sasa umekwama utekelezaji wake katika hatua zilizobakia
kutokana ukosefu wa fedha.
Mheshimiwa Spika,
Baadhi
ya nchi za hapa hapa Afrika, zimefanikiwa katika kuimarisha mapato yake ya
ndani kupitia mfumo huu wa usajili wa Kampuni na Jumuiya nyengine kwa mfumo
mmoja wa dijitali, mfano mzuri wa nchi hizo ni jirani zetu Rwanda, ambapo wao
wameanza kupata mafanikio katika mfumo huu. Kamati imeona kuwa katika bajeti ya
mwaka huu 2015/2016, kuna Mradi wa Mageuzi ya Mfumo wa Usajili wa Biashara
umetengewa shilingi bilioni moja, kamati inasisitiza sana fedha hizo zipatikane
ili mfumo huo uanzishwe.
Mheshimiwa Spika,
Katika
programu ndogo ya Usimamizi wa Hakimiliki, imewekewa lengo la kuimarisha
Usimami wa upatikanaji wa haki za wasanii na wabunifu. Kamati yangu inaipongeza
Ofisi ya Hakimiliki na Mkurugenzi wake kwa kazi kubwa anayofanya ya kusimamia
haki za wasanii na wabunifu licha ya uchanga wake na changamoto kadhaa
zinazokabili Ofisi yake.
Mheshimiwa Spika,
Programu
hii ndogo ya Usimamizi wa Hakimiliki imetengewa shilingi 240,000,000, ambazo
hizo zimekusudiwa kuleta matokeo yaliyolengwa kwa Ofisi hii. Kamati yangu
imekuwa ikitafakari kwa kiasi gani fedha hizo zitaweza kutatuwa changamoto za
Ofisi, mbali ya kufikia malengo yaliyokusudiwa. Kamati imetembelea Ofisi hii na
imebaini kuwa kuna baadhi ya vitendea kazi muhimu vinakosekana kama vile
usafiri. Kama tunavyojua kazi za Ofisi hii siyo za Ofisini tu, pia inahitajika
kufatilia ukusanyaji wa mirahaba katika vyombo mbali mbali vya habari na
mahoteli. Kamati inashauri Serikali kuiongezea bajeti Ofisi hii ili iweze
kutatua changamoto hizo na kufikia malengo yake.
Mheshimwa Spika,
Ofisi
ya Msajili wa Hakimiliki ina upungufu wa wataalamu mbali mbali hasa katika fani
ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, tokea mwaka 2012 Ofisi hii imekuwa
ikiomba kupatiwa wataalamu hao na wengine katika fani mbali mbali, lakini hadi
hivi sasa bado Tume ya Utumishi Serikali haijafanikisha kupatakana kwa nafasi
hizo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
inaitanabahisha Serikali kuwa isitegemee mfumo huu wa bajeti wa PBB ulete
matokeo wanayokusudia kwa haraka bila ya kwanza kuziwezesha taasisi
zinazosimamia progamu hizo, kwa kuzipatia nyenzo na wataalamu wa kufanikisha
mipango hiyo. Tunaitaka Tume ya Utumishi ya Serikali kuwapatia wataalamu hao
ili lengo lililowekwa katika Programu hii ndogo ya Usimamizi wa Hakimiliki
liweze kufanikiwa.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
imebaini changamoto nyengine ya usimamizi wa hakimiliki kwa vyombo vya sheria
hasa baadhi ya mahakama zetu ambazo wanapopelekwa watuhumiwa wanaonyonya haki
za wasanii sheria hazifatwi ipasavyo. Kamati yangu inataarifa ya kesi ambayo
inamuhusisha mtu mmoja aliyetumia kinyume na sheria hakimiliki na mtu huyo
kutakiwa kulipa na akakataa. Jambo la kusataajabisha, wakati mtu huyo
anapelekwa mahakamani akajisifu kuwa atatumia uwezo wake wa kifedha kuachiwa,
na kweli kesi ilipofika mahakamani mtu huyo aliachiwa kwa sababu zinazotia
shaka.
Mheshimiwa Spika,
Mambo
haya ndiyo tunayoyapigia kelele kila siku katika Baraza hili ya vyombo vyetu
vya kusimamia haki vifuate sheria, haiwezekani mtu anapelekwa mahakamani
anajisifu kutumia uwezo wake wa kifedha na kuachiwa na huku ameshadhulumu haki
ya mtu. Kamati inaomba Wizara kulichunguza suala hili kwa kumchukuliwa hatua za
kinidhamnu Hakimu aliyehusika na kadhia hii ya aibu kwa mujibu wa sheria.
Aidha, tunaiomba Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi ilifuatilie suala
hili kwa kuwasiliana na Taasisi ya Hakimiliki, na hatua stahiki zichukuliwe ili
kukomesha mambo haya yasijitokeze tena na kuvunja moyo juhudi za wasanii na
Ofisi zetu zinazosimamia haki zao.
Mheshimiwa Spika,
Programu
ndogo ya Usimamizi wa Masuala ya Dini imewekwa chini ya Kamisheni ya Wakf na
Mali ya Amana na Ofisi ya Mufti ambapo Kamisheni ya Wakf imekasimiwa shilingi
587,800,000 na Ofisi ya Muft imetengewa shilingi 357,612,000. Kiasi hicho cha
fedha ni kidogo kwa taasisi hizo zenye majukumu makubwa yanayogusa jamii moja
kwa moja. Kamati yangu inashauri kuwa katika kuhakikisha kuwa Taasisi hizo
mbili angalau ziweze kufanya majukumu yake ya kawaida basi zipatiwe fedha hizo
kwa wakati na kama zilivyokasimiwa.
Mheshimiwa Spika,
Kamisheni
ya Wakf, imekuwa ikikusanya fedha kutoka katika ada za huduma mbali mbali
wanazotoa kama vile mirathi, hata hivyo, fedha hizo hivi sasa zimepunguzwa
kiwango chake na hicho kilichobaki
kinakusanywa na ZRB. Hatua hiyo imedhoofisha Kamisheni ya Wakf, ambayo imekuwa
ikizitumia fedha hizo kutatua baadhi ya changamoto za kiofisi kama vile
kufatilia mali za Wakf, mirathi zakka na sadaka. Shughuli hizo zote zinaweza
kuzorota ufuatialiji wake iwapo fedha hizo zitaendelea kuingizwa katika mfumo
wa Serikali kupitia ZRB.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yangu inaiomba sana Wizara ya Fedha, kufikiria upya makusanyo ya fedha za
Mirathi kuzibakisha kwa Kamisheni ya Wakf ili ziendelee kusaidia uendeshaji wa
shughuli zao muhimu ambazo zinakwama kutoka na uingizwaji mdogo wa fedha za
matumizi mengineyo.
Mheshimwa Spika,
Hivi
karibuni kumekuwa na mizozo mingi inayohusu mali za wakf na mirathi na
kupelekea hata mahakama zichukuwe hatu kali zidi ya wahusika ambao mara nyingi
wamekuwa ni wana ndugu wa familia. Mnamo mwezi Febuari, mwaka 2015 kumeripotiwa
katika vyombo vya habari hapa nchini, ikiwemo ZBC, kuhusu uamuzi wa Mahakama
kuwafunga gerezani kwa muda wa wiki mbili wanafamilia wa familia moja maarufu
nchini, kwa kupinga maamuzi ya mahakama kutoka na kesi ya Wakf iliyohusu
wanandugu wa familia hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Uwepo
wa Kamisheni ya Wakf ulitegemewa matukio kama hayo yasiwepo au yasijitokeze
katika hali kama hiyo, kwa vile Kamisheni inajukumu la kusimamia na kutoa elimu
ya kutosha kwa jamii kuhusu namna ya usimamizi wa mali za wakf na mirathi na
kuweka dawati maalumu la ushauri wa kitaalamu kwa familia zinazokinzana ili
kabla ya familia hizo kufikisha mashauri yao mahakamani ziweze kwanza kupata
ushauri kutoka kamisheni ya Wakf na ikishindikana ndiyo hatua nyengine zifuate.
Kwa kufanya hivyo, mheshimiwa Spika, tutaweza kupunguza migogoro ya familia
kuhusu mali za mirathi na wakf na kupunguza utitiri wa kesi katika mahakama
zetu.
Mheshimiwa Spika,
Katika
kufikia lengo la programu hii ndogo ya usimamizi wa masuala ya dini, Ofisi ya
Mufti inajukumu kubwa la kuhakikisha kuwa jamii inaepukana na vitendo viovu na
mpromoko wa maadili. Kamati yangu inashauri Ofisi ya Mufti kutambuwa jukumu
lake na kusaidia kubainisha mambo mbali mbali katika jamii yanayosababisha
mporomoko wa maadili kwa kushirikiana na miskiti na madrasa kuyakemea kwa nguvu
zote na kuyaondoa.
Mheshimiwa Spika,
Aidha
tunaitaka Serikali kushirikiana na Ofisi ya Mufti katika kuchukuwa hatua dhidi
ya vitendo viovu vinavyochangia mporomoko wa maadili ya jamii yetu katika
jamii. Sote tunatambuwa kuwa jamii yetu imejengeka katika maadili mazuri ya
heshima na ustaarabu wa hali ya juu. Haitawezekana kuacha mporomoko wa maadili
uendelee katika jamii kama vile hakuna mshughulikiaji, Ofisi ya Mufti ilibebe
jukumu hili kwa nguvu zote na wananchi watowe ushirikiano na Ofisi ya Muft
katika kupiga vita vitendo vyote vinavyopelekea mporoko wa maadili katika jamii
bila ya kuona haya waka muhali.
Mheshimiwa Spika,
Katika
programu kuu ya pili ya Mipango na Uendeshaji wa Sekta ya Sheria jumla ya
shilingi bilioni tatu, milioni kumi na mbili na tisini na mbili elf,
(3,012,092,000) zimepangwa kwa uendeshaji wa programu ndogo za Uongozi na uendeshaji wa Sekta ya sheria, Mipango, Sera
na Utafiti na Uendeshaji wa Wizara Pemba. Kamati haina tatizo na Programu hii,
isipokuwa tunasisitiza kuwa maslahi ya wafanyakazi wa Mahakama hasa kwa
Mahakimu wa Mahakama za mwanzo yatazamwe upya. Kamati yangu inashauri Serikali
kuharakisha sera ya malipo ili mahakimu wa mahakama za mwanzo nao wapatiwe
nyongeza stahiki.
Mheshimiwa Spika,
Jengo
jipya la Wizara ya Katiba na Sheria, liliopo Mazizini limekamilika na
tunaipongeza Serikali kwa hatua ile kubwa ya kimaendeleo. Katika kukamilisha
ujenzi ule bado kuna changamoto ndogo ndogo ambazo Mheshimiwa Waziri amezieleza
na sisi kamati tunaisisitiza zitatuliwe hata kwa kubana vifungu ili jengo lile
lihamiwe.
Mheshimiwa Spika,
Katika
fungu G 02, la Mahakama Kuu, kuna programu kuu mbili, ya kwanza ni Usimamizi wa
Upatikanaji wa haki ambayo ina progamu ndogo moja ya usimamizi wa upatikanaji
wa haki. Progamu ya pili ni ya usimamizi wa shughuli za uendeshaji na utawala
wa Mahakama ambayo ina programu ndogo za uendeshaji na utawala wa Mahakama
Unguja na Uendeshaji wa shughuli za Mahakama Pemba.
Mheshimiwa Spika,
Programu
zote hizo zimepangiwa jumla ya shilingi bilioni tano, milioni mia moja na arobaini
na tatu na laki moja, (5,143,100,000). Kamati yangu imetazama vizuri programu
ndogo ya pili ya kusimamia shughuli za Mahakama Pemba, ambayo imepangiwa
shilingi bilioni moja, milioni mia tano
na tisini na nne, laki tano na kumi na tisa elfu, (1,594,519,000) ambapo kamati imeona kuwa kiasi hiki cha
fedha hakitawezesha kukamilisha hatua ya ukarabati wa jengo la Mahakama Kuu,
Chake Chake ambapo kwa mwaka huu wa fedha ilihitajika kiasi cha kutosha cha
fedha ili kuwezesha kukamilika kwake. Kamati inataka kujuwa ni kiasi gani
katika fedha hizi zilizotengwa kitaweza kufanikisha kukamilisha ukarabati wa
jengo la mahakama ya Chake Chake.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yangu imeshapiga kelele sana tokea bajeti ya mwaka jana 2014/2015 kuwa jengo la
Mahakama ya chake chake Pemba lipo katika hali mbaya, wanaofanyaka kazi pale ni
banaadamu wenzetu, wanastahiki kufanyakazi zao katika mazingira salama na sivyo
Kama lilivyo hivi sasa.
Mheshimiwa Spiaka,
Kamati
yangu ilitegemea sana katika bajeti ya mwaka huu Serikali ingeona umuhimu wa
kuweka fedha za kutosha ili ukarabati wa jengo lile ukamilike. Kamati
haijaridhika na kasma hii ndogo katika programu ndogo ya kusimamia shughuli za
Mahakama Pemba, tunaitaka Serikali kubana vifungu vya matumizi mengine na
kusaidia kupatikana fedha ya kutosha ili ukarabati wa Mahakama Pemba ukamilike.
Mheshimwa Spika,
Katika
fungu G 03, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu Zanzibar, kuna progaramu kuu mbili ambazo
zimetengewa jumla ya shilingi bilioni moja, milioni kumi na laki mbili
(1,010,200,000). Kamati yangu imebaini changamoto kadhaa zinazokabili Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu ambazo zinaweza kuathiri utekelezaji wa programu hizo kwa
kiwango hicho cha fedha kilichowekwa. Moja wa changamoto hizo ni uhaba wa fedha
na kutoingizwa kwa fedha kwa mujibu wa maombi wa ‘cash flow’ iliyopelekwa
Wizara ya Fedha. Kamati yangu bado inasisitiza kuwa Serikali izingatie sana
umuhimu wa taasisi zinazosimamia haki, hasa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ambayo
inasimamia kesi zote za madai za Serikali. Kamati inatanabahisha kuwa shughuli
za Ofisi hii zinapokwama athari yake ni kubwa kwani Serikali inaposhindwa kesi
italazimika kulipa gharama kubwa za kesi hizo.
Mheshimiwa Spika,
Changamoto
nyengine kubwa ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ni
kutopata ushirikiano wa kutosha kwa baadhi ya taasisi za Serikali ambazo
zimeshitakiwa Mahakamani. Ofisi ya mwanasheria Mkuu imekuwa ikifanya
mawasiliano na taasisi hizo kuwatanabahisha juu ya athari za kutotoa
ushirikiano ambazo hupelekea Serikali kushindwa kesi na kulipa fedha nyingi
kama fidia.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yangu inaitaka Serikali kutoka toleo kwa taasisi zote za Serikali kuhakisha
kuwa kila taasisi ambayo ina kesi inayosimamiwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali
kuwapeleka maafisa wa Sheria wa Taasisi hizo kuripoti kila inapohitajika kwa
mwanasheria Mkuu na kuhakikisha kuwa ushauri unaotolewa na Mwanasheria Mkuu
unafanyiwa kazi na maafisa hao kwa kushirikiana na wakuu wa taasisi hizo.
Mheshimiwa Spika,
Aidha,
tunaitaka Serikali kutumia vyema sheria namba 3 ya mwaka 2010, sheria ya
Mwenendo wa Mashitaka ya au Dhidi ya Serikali, katika kifungu cha 7 cha sheria
hiyo, kumuwajibisha Afisa yoyote wa umma ambaye kwa uzembe wake atasabisha
Serikali ishindwe Kesi mahakamani, ikiwemo kutotoa ushirikiano kwa Mwanasheria
Mkuu, na kumtaka Afisa huyo kulipa fidia ambayo Serikali itatakiwa ilipe kwa
mujibu wa sheria hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Katika
fungu G 04, Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka nayo imepangiwa programu Kuu mbili
za Uendeshaji na Usimamizi wa kesi za jinai na Mipango na Uendeshaji ambazo
kila moja ikiwa na programu ndogo mbili, jumla yake ni shilingi bilioni moja ,
milioni mia sita na ishirini na saba na laki moja (1,627,100,000).
Mheshimiwa Spika,
Programu
zinazosimamiwa na Ofisi hii ni kubwa na kiwango cha fedha kinachoingiziwa
hakilingani na ukubwa wa Progamu hizo, Ofisi hii inalazimika kufanya kazi zake
kwa vile ni wajibu wake lakini kamati tumeona kuwa inafanya kazi hizo katika
hali ngumu.
Mheshimiwa Spika,
Uendeshaji
wa mashitika unataka ufanisi na ufanisi unatokana na matayarisho kwa waendesha
mashitaka, kuimarishwa kwa maslahi yao ili kuwajenga nguvu na morali kwa kazi
ngumu ya kupambana na wahalifu, hivyo, kamati bado inarejesha kilio kwa
Serikali kuwatazama vizuri kimaslahi wanasheria wa DPP ambao tunawetegemea sana
kutuondolewa wezi, majambazi, wabakaji, matapeli n.k katika jamii, kwa
kuthibitisha mashitaka yao mahakamani na kufungwa gerezani.
Mheshimiwa Spika,
Tujiulize
iwapo kama waendesha mashitaka hao, kama hawatafanya kazi hiyo kwa ufanisi,
jamii yetu itakalika? Tusisahau kuwa kwa sababu hiyo tu, Waendesha mashitaka
wengi wenye uwezo mkubwa katika Ofisi ya DPP, wameshaacha kazi na kutafuta
shughuli nyengine za kufanya. Kamati yangu bado inasisitiza tena kuwa Serikai
ione umuhimu wa vijana wetu hawa kuwaongezea maslahi yao ili tusiendelee
kuwapoteza.
Mheshimiwa Spika,
Mashitaka
hayathibitiki mahakamani bila ya ushahidi, na ushahidi katika dunia ya leo siyo
ule wa kuona kwa macho na kusikia, matendo mengi ya jinai yanayofanywa na
wahalifu kama vile udhalilishaji na mauwaji, hufanyika kwa namna ambayo siyo
macho wala masikio yanaweza kushuhudia, isipokuwa kwa vyombo maalumu ambavyo
hutumika kushuhudia matokea ya jinai hizo, mfano wa vyombo hivyo ni mashine ya
vinasaba ya DNA.
Mheshimiwa Spika,
Kwa
mara nyengine, kamati yangu inarejesha kilio chetu kwa Serikali kuhakikisha
kuwa mashine ya DNA inapatikana ili Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka iweze
kuthibitisha makosa hayo mahakama kwa
njia za kitaalamu na kupatikana hatia kwa wahalifu. Sote tunafahamu hali
ya vitendo vya udhalilishaji ilivyo nchini kwetu na namna tunavyokerwa na hali
hiyo, kama ni hivyo basi, kamati yangu inaikumbusha Serikali kuwa kama
ilivyofanya kwenye mkakati wa ununuzi wa meli mpya ambayo karibuni itawasilia
nchini na mkakati kama huo ufanyike ili mashine ya DNA ipatikane, hilo
linawezekana tukitimiza wajibu wetu.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yangu pia inataka maelezo kutoka kwa Waziri, vipi bajeti ya DPP imezingatia
upatikanaji wa jengo la kudumu kwa Afisi ya DPP kisiwani Pemba, pamoja na hatua
za kumalizia ujenzi wa nyumba za waendesha mashitaka Mkokotoni. Kamati inataka
kujuwa ni vipi Wizara kwa kushirikana na wizara ya Fedha, itasaidia kupatakana
fedha kwa ajili ya kukamisha ujenzi wa nyumba hizo ili ule mpango wa kuendesha
mashitaka kiraia uweze kuenea katika Wilaya zote za Unguja na Pemba.
Mheshimiwa Spika,
Tume
ya kurekebisha Sheria, imepangiwa jumla ya shilingi milioni mia tano na
ishirini na saba (527, 000,000) kwa ajili ya kuendesha programu kuu mbili za
Mapitio ya Sheria na Utawala na Uendeshaji. Mafanikio makubwa yamepatikana
tokea kuimarishwa kwa Tume ya Kurekebisha Sheria chini ya Mwenyekiti wake Jaji
Mshibe Ali Bakari na Katibu wake ndugu Asma Jidawi. Kamati inawapongeza sana
pamoja na watendaji wao wote na tunataka waendeleze juhudi za kuisaidia
Serikali kuwa na sheria nzuri zinazotekelezeka.
Mheshimiwa Spika,
Nitumie
fursa hii kuzitaka taasisi za serikali ambazo zinafanya mapitio ya Sheria zao
kwa nia ya kufanya marekebisho kushirikiana na Tume kwani wao ndiyo wenye
jukumu la kisera na utaalamu kufanyakazi hiyo. Aidha, kamati inaipongeza Tume
ya Kurekebisha Sheria kwa kurejea kuwa mwanachama hai katika Umoja wa Tume za
Kurekebisha Sheria za Afrika Mashariki na Kati (ALRAESA) na kufanikiwa kujiunga
na Umoja wa Tume za Kurekebisha Sheria
za nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola (CALRAs) pamoja na kuanzisha ushirikiano
na taasisi mbali mbali za kimataifa zenye jukumu sawa na Tume. Kamati yangu
inaishauri Tume kutumia vyema fursa hizo katika ngazi ya kimataifa ili iweze
kupata utaalamu na uzoefu katika kukabiliana na changamoto za maboresho ya
sheria.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
yangu ina mengi ya kueleza katika Wizara hii ambayo, lazima nikiri tena kuwa
imekuwa ikipokea na kutekeleza kwa vitendo ushauri wa Kamati lakini kutokana na
muda naomba nimalizie kwa kukushukuru na kuwashukuru wajumbe wako kwa utulivu
wao wakati wote wa kuwasilisha muhtasari wa maoni haya ya kamati ya Katiba,
Sheria na Utawala. Nawaomba wajumbe tushirikiane katika kuichangia kwa kutoa
ushauri, maelekezo na hatimaye kuipitisha ili Mheshimiwa Waziri apate
kutekeleza programu alizopangiwa katika bajeti hii.
Mheshimiwa Spika,
baada ya hayo machache nakushukuru na naunga mkono hoja.
Ahsante
……………………
Abdalla Juma Abdalla
Makamo Mwenyekiti,
Kamati ya Katiba, Sheria na
Utawala,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment