Habari za Punde

Dk Shein aipongeza Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati kwa kutekeleza vyema miradi ya maji

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                  26 Agosti , 2015

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amezindua mradi mkubwa wa Maji na Usafi wa Mazingira Zanzibar na kusifu jitihada za Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati kwa namna inavyotekeleza miradi ya kuwapatia wananchi maji safi na salama.

Alieleza kuwa jitihada za wizara hiyo zimewezesha Zanzibar kuzalisha lita milioni 163 za maji ikiwa ni asilimia 76 ya mahitaji yake ambayo hadi Disemba mwaka jana yalikuwa ni lita 214,580,240 hivyo kuwa na upungufu wa asilimia 24.

Dk. Shein aliwaambia mamia ya wananchi na wageni waliohudhuria uzinduzi wa mradi huo uliofanyika jana katika kijiji cha Taif, Wilaya ya Wete, mkoa wa Kaskazini Pemba kuwa lengo la mradi huo ni kuimarisha upatikanaji wa huduma za maji na kuimarisha usafi wa mazingira  mijini na vijijini zikiwemo skuli.

Utekelezaji wa Mradi huo alibainisha kuwa ni miongoni mwa hatua za utekelezaji wa ahadi zake kwa wananchi alizozitoa wakati akiomba ridhaa yao kuongoza Zanzibar katika uchaguzi wa mwaka 2010 kupitia mipango mbalimbali ya maendeleo.

Aliitaja mipango hiyo kuwa ni pamoja na Dira ya Maendeleo 2020, MKUZA II na Ilani ya Uchaguzi 2010-2015 ambazo zote zimetilia mkazo suala upatikanaji wa maji safi na salama kwa waanchi katika maeneo wanayoishi. 

Dk. Shein alisema ni jambo la kujivunia kuona kuwa huduma za maji safi na salama zinazidi kuimarika hivyo kutekeleza kwa vitendo malengo ya Mapinduzi ya mwaka 1964.

Mradi huo Maji na Usafi wa Mazingira Zanzibar  unajumuisha pia Ujenzi wa Miundombinu ya Kuimarisha na Kuendeleza huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira katika miji mitatu ya Pemba(Chake-Chake, Mkoani na Wete).


Aliitaka wizara hiyo pamoja na Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kujidhatiti zaidi katika kutekeleza miradi ya maji na kutoa wito kwa wananchi kufuatilia kwa karibu taarifa kuhusu huduma za maji ambazo hutolewa mara kwa mara katika televisheni na redio.

Sambamba na wito huo, aliwataka wananchi 
kuhakikisha kuwa wanatunza miundombinu ya maji na vyazo vya maji na kuwatanabahisha kuwa miradi hiyo inagharimu fedha nyingi hivyo ni rasilimali muhimu kutunzwa na kuhifadhiwa kwa manufaa ya taifa.

Aliwaeleza wananchi hao kuwa mradi huo ambao umegharimu jumla ya shilingi bilioni 67.73 kuwa sehemu kubwa ya fedha hizo ni mkopo ambao unapaswa kurejeshwa hivyo ni wajibu wao kuutunza mradi huo na kuwakumbusha kuwa wanaorejesha mkopo ni serikali na wananchi wenyewe.

Alibainisha kuwa wakati huu ambapo uchumi unaruhusu kukopa, Serikali haitasita kufanya hivyo ili kuhakikisha kuwa inafikia azma na malengo ya Mapinduzi ya kumpatia kila mwananchi popote alipo huduma ya maji safi na salama.

Dk. Shein aliwashukuru washirika wa maendeleo na taasisi nyingine pamoja na watu binafsi kwa mchango wao mkubwa katika kusaidia miradi ya maji   nchini na kueleza matumaini yake kuwa washirika hayo wataendelea kuziunga mkono juhudi za Serikali na wananchi wa Zanzibar.

Akitoa maelezo ya kitaalamu ya maradi huo, Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati Ali Khalil Mirza alieleza kuwa mradi wa Maji na Usafi wa Mazingira Zanzibar ambao ulitekelezwa kwa pamoja kati ya Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB),Shirika la Makazi la Umoja wa Mataifa (UN-Habitat) na Serikali ulihusisha maeneo makuu manne.

Aliyataja maeneo hayo kuwa ni Kuijengea uwezo Mamlaka ya Maji ili kuiwezesha kutoa huduma bora, ujenzi wa miundombinu ya kusambaza huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira vijijini Unguja na Pemba, Ujenzi wa Miundombinu ya Kuimarisha na Kuendeleza huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira katika miji mitatu ya Pemba na Kuimarisha na Kuvitunza vyanzo vya Maji Unguja na Pemba.

Kuhusu gharama za mradi alieleza kuwa umegharimu jumla ya shilingi bilioni 67.73 ambapo shilingi bilioni 50.85 ni mkopo toka benki ya AfDB na benki hiyo ilitoa fedha nyingine shilingi bilioni 6.10    zilikuwa ni msaada. UN-Habitat ilitoa msaada wa shilingi bilioni 2.50 

Kwa upande wake Serikali ilitumia shilingi bilioni 8.28 kwa ajili ya kulipa fidia mali na mazao ya wananchi yaliyathirika na ujenzi wa maradi pamoja na kupeleka umeme katika vituo vya maji.

Alifafanua kuwa kukamilika kwa Ujenzi wa Miundombinu ya Kuimarisha na Kuendeleza huduma ya Maji na Usafi wa Mazingira katika miji mitatu ya Pemba (Chake-Chake,Mkoani na Wete) tayari kumewezesha wananchi 70,852 kupata huduma hiyo. 

Alibainisha kuwa sehemu hiyo ya mradi ilihushisha uchimbaji wa visima 18 pamoja na ujenzi wa vituo na kufunga pampu,kuchimba misingi na kulaza mabomba kilomita 83.5 na ujenzi wa matangi 6 ya ardhini na ya minara yenye uwezo wa kuhifadhi lita 7,600,000 kwa pamoja.

Alieleza matangi mawili yamejengwa Taifu -eneo ulipozinduliwa mradi na Mtemani katika wilaya ya Wete, Machomane Chake-Chake na Uweleni Mkoani.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) Bwana Sabas Marandu mbali ya kueleza kuridhishwa kwake na ushirikiano ambao Benki yake imeupata kutoka serikalini na ZAWA wakati wote wa utekelezaji wa mradi huo alimhakikishia Mheshimiwa Rais kuwa fedha za mradi huo zimetumika kama ilivyopangwa.

Dk. Shein yuko kisiwani Pemba kwa ziara siku nne kuanzia jana kukagua shughuli za maendeleo ikiwemo kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi mbali mbali katika sekta za elimu, maji, barabara na mazingira.

                                        
Postal Address: 2422 Tel.:0776 613 015 Fax: 024 2231822 


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.