Habari za Punde

Dk Shein : lazima tuwe na mpango maalum kuzifanyia matengenezo barabara zinapoharibika

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                                                   26 Agosti , 2015
---
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano pamoja na Mfuko wa Barabara wametakiwa kuhakikisha kuwa wanakuwa na mpango maalum wa kuzifanyia matengenezo barabara nchini ili barabara hizo ziweze kudumu kwa muda mrefu.

Akizungumza mara baada ya kuzindua rasmi barabara za Wete-Gando na Wete Konde jana Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alisema kumekuwa na ulegevu katika kuzifanyia matengenezo barabara na matokeo yake ni barabara hizo huachwa hadi kufikia hali ya kuharibika kabisa.

Katika hafla hiyo iliyofanyika huko katika kijiji cha Ukunjwi, wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba, Dk. Shein alibainisha kuwa azma ya serikali ni kuhakikisha kuwa kisiwa cha Pemba sasa kinaunganishwa kwa barabara kila upande kama ilivyo kwa kisiwa cha Unguja hivyo serikali imo mbioni kutekeleza mradi wa ujenzi wa barabara ya Ole hadi Kengeja (35 km) ambayo ilibuniwa na Rais wa Kwanza wa Zanzibar Mzee Abeid Amani Karume.

Alieleza pamoja na barabara hiyo, serikali inaifanyia marekebisho makubwa barabara ya Ole hadi Konde ambayo ni ya kiwango cha lami kuimarisha uwezo wake na pia barabara ya zamani kutoka Chake-Chake hadi Wete (22.1 km) ujenzi wake utaanza hivi karibuni kupitia fedha za mkopo wa Benki ya Kiarabu  ya Maendeleo ya Uchumi ya Afrika (BADEA) na Mfuko wa Maendeleo wa Saudi Arabia(Saud Fund).

Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi kuzitunza barabara hizo kwa kuepuka vitendo vinavyopelekea kuharibu barabara ikiwemo uchimbaji wa mchanga na mawe maeneo ya barabara pamoja na kutoondoa alama za barabarani yakiwemo mabango mbalimbali yanayoelekeza watumiaji wa barabara hizo.
Kuhusu kukamilika kwa ujenzi wa barabara za Wete- Gando na Wete- Konde 

Dk. Shein aliwapa changamoto wananchi kwa kuwataka kuzitumia barabara hizo kujiimarisha kiuchumi kwa kupanua shughuli zao za uzalishaji mali ikiwemo kilimo cha matunda na mbogamboga.


Aidha aliwakumbusha kuwa kwa kukamilika barabara hizo maana yake ni kuvifungua vijiji hivyo kwa watu kutoka nje hivyo wajiandae kuwapokea wageni na kuwakumbusha kuendeleza utamaduni na sifa ya ukarimu za wananchi wa Unguja na Pemba.

Aliwatahadharisha wananchi dhidi ya kukaidi amri ya serikali ya kutojenga katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya upanuzi wa barabara yaani hifadhi ya barabara kwa kuwa kufanya hivyo ni kinyume na sheria.

Aliagiza Wizara ya Miundombinu kuwataka wananchi wanaokaidi amri hiyo kuvunja majengo yao wao wenyewe vinginevyo Wizara ichukue hatua za kuyavunja majengo hayo.

Aidha aliwataka kuacha na vitendo vya kulala barabarani  nyakati za usiku kwa kuwa kufanya hivyo kunahatarisha maisha yao kwani barabara hizo hutumika kwa vyombo vya usafiri wakati wote.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuushukuru uongozi wa Ufalme wa Saudi Arabia pamoja na Uongozi wa BADEA kwa kuendelea kuiunga mkono jitihada za 
Serikali na wananchi wa Zanzibar za kujiletea maendeleo.

Katika maelezo yake kumkaribisha Mgeni, Naibu Waziri wa Miundombinu na Mawasiliano Issa Haji Ussi (Gavu) alieleza kuwa Wizara yake inakusudia kuweka taa za kuongozea  magari katika makutano ya barabara ya Gando, Chake-Chake na Kizimbani.

Aidha aliongeza kuwa Wizara hiyo imeweka viguzo maalum za kuonesha mipaka ya barabara na kutoa wito kwa wananchi kuheshimu maeneo hayo yaliyotengwa.

Kuhusu fidia Naibu Waziri huyo alikiri kuwa bado wizara yake haijakamilisha ulipaji wa fidia kwa baadhi ya wananchi walioathriwa na ujenzi wa barabara ya Wete – Gando na kwamba fidia hiyo italipwa.    

Kwa upande wake Katibu Mkuu Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Dk. Juma Akil alieleza kuwa barabara hizo zenye urefu wa kilomita 30.2 ni utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya ujenzi wa barabara tatu za mkoa Kaskazini Pemba zenye urefu wa kilomita 52.2. 

Alifafanua kuwa Awamu ya Pili itakuwa ni ujenzi wa barabara ya Wete- Chake-Chake ambao ujenzi wake unaanza mara moja baada ya kukamilika ujenzi wa Awamu ya Kwanza.

Dk. Akil alifafanua kuwa ujenzi wa barabara hizo ambao uliofanywa na Kampuni ya Mwananchi Engineering and Contractors Limited (MECCO) ya Tanzania umegharimu jumla ya shilingi bilioni 36 badala ya shilingi bilioni 23.7 zilizopangwa awali kutokana na sababu mbalimbali.

Alizitaja baadhi ya sababu hizo kuwa ni ucheleweshaji wa malipo ya fidia kwa wananchi na kuchelewa malipo ya hati mbalimbali za madai ya malipo za mkandarasi kutoka pande zote zinazogharamia mradi huo.

Alibainisha kuwa mchango wa serikali katika mradi huo ni kulipa fidia wananchi ya nyumba, vipando na uhamishaji wa huduma za jamii ikiwemo mabomba ya maji, umeme na simu na kulipa asilimia 28.6 ya kila hati ya malipo ya mkandarasi.
                                        

Postal Address: 2422 Tel.:0776 613 015 Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.