Habari za Punde

Khamis Ali Makame: mjasiriamali aliewakomboa wenzake

 MJASIRIAMALI anatengeneza bidhaa zinazotokana na vyuma, ikiwa ni pamoja na milango, majiko na madirisha, Khamis Ali Makame alieaajiri vijana watatu wenye ulemavu eneo la Wawi wilaya ya Chake Chake Pemba, (Picha na Zainab Atupae, Pemba).
 Mojawapo ya kazi ya vijana hawa ambayo tayari imeshakamilika
VIJANA watatu wenye ulemavu wa viungo ambao wameajiriwa na mjasiriamali wa kutengeneza bidhaa zinazotokana na vyuma Khamis Ali Makame, wakishauriana jambo kalba ya kuanza kazi hiyo, kwenye afisi yao iliopo Wawi Chake Chake Pemba, (picha na Zainab Atupae, Pemba).

 Amewaajiri wenye ulemvu watatu, apunguza foleni ya ajira serikalini
Na mwandishi wetu- PEMBA

Khamis Ali Makame ni mjasiri amali wa uchomaji vyuma  katika kijiji cha Wawi , aliyefanikiwa kupata mafanikiyo yake  kwa kazi hiyo.

Aliezaliwa katika kijiji cha Mchangani  Vitongoji Chake Chake, na sasa ana umri 30,  na alipata elimu yake ya msingi skuli ya Vitongoji, na kumaliza darasa la saba  na hakuendelea tena.

“Kiukweli kusoma sikuwa na ari .….. kwani nimemaliza darasa la saba  ila tokea zamani ilikuwa napenda  niwe na kazi hii ya uchomaji vyuma  na niliamini ikosiku nitapata”, alisema mjasiri amali huyo.

Wahenga walisha nena kuwa “jitihada wajada” yaani anaetafuta hakosi na ikosiku utapata, usemi huu umemnufaisha vyema kijana Khamis.

 “Hakuna kazi rahisi, maana hata hii yangu sio nyepesi, maana wakati napewa ujuzi na kaka yangu, niliona ugumu wake’’,aliniambia huku akikata chuma.


Huku kijasho chemba mba kikimtiriri kwenye paji lake la uso, na ili kufanikisha kazi yake, utaalamu na nguvu kidogo ni jambo la lazima.

Ofisi hiyo  inatengenezwa vitu tofati ikiwa ni pamoja na kutengeza milango ya mageti, madirisha ya mageti, majiko ya  vyuma na  misheki ya kutolea moto.

 Kijana huyo mchakarikaji wa maisha, alinihadithia kuwa, alianza kuvisarifu vyuma kwa kuchukuliwa na kaka yake kazini, tokea mwaka 2005, akiwa miongoni mwa wanafunzi sita.

“Namini kila aliye kwenda pale alikuwa na hamu ya kutaka kupata ule ujuzi, na kuhakisha baadae anajiajiri mwenyewe.

Kadri siku zilivyokuwa zikisonga mbele, na yeye kuendelea kujichotea ujuzi kwa kaka yake, alianza kuona nuru ya maisha yake yakimsogolea.

Miaka 10 baade, baada ya kujiweza kimaisha, akiamini sasa hakuna chuma kinachomshinda kukikata apendavyo kama papai, alianza taraibu kuondoka.

“Unajua mwandishi, nilipofika miaka 10 ya kumfuata kaka kuusaka ujuzi wa kubena vyuma, nilijiona kama sasa naweza kujitegemea’’,alidakiza kwa furaha.

Suali: ni mwaka gani umeweza kujipatia  ofisi yako maalumu na kuweza kuwaajiri  watu wako.

Mwaka jana, kijana Khamis sasa rasmi alikata shauri na kuamua kutafuta sehemu yake, ili kujiendeleza na sasa akitaka kuyasahau machungu ya miaka 10.

“Unajua maisha ni safari yenye changamoto, sasa usipojitambua unaweza kukata tamaa mapema, mimi leo nnafuraha ya kua na ofisi yangu binafi bila ya kutegemea mtu”,alisema.

Oktoba 12 mwaka 2013 alipata kiwanja chake eneo la Wawi  wilaya ya Chake Chake mita chache kabla ya kukifikia kiwanda cha mafuta ya makonyo, ambapo ndipo alipoangusha nanga ya maisha.

“Kila penye nia pana njia, Mungu alinipa uwezo wa kupata sehemu yangu  ya kujiendeleza  na kuwatafuta watu ambao nilikuwa na nia  nao ya kuwajiri katika ofisi  yangu’’,alifafanu.

Mjasiriamali huyo, wakati akiwa kwenye mafunzo ya kuchoma na kukata vyuma, alijiwekea malengo ya kuwajiri watu wenye ulemavu, akiamini kwamba ndio kundi lililokosa uwangalizi.

 “Husikia kwenye vyombo vya habari, kwamba wenzetu wenye ulemavu, wanakosa ajira hata kama watakuwa na sifa, ndio maana mimi nimeamua kuwaleta hapa kusaka nao maisha”,alieleza.

Roho ya mjasiriamali huyo, kwa sasa imetulia tuli, kama maji mtungini, maana ameshajiekeza kwenye ofisi yake na amewaajiri vijana watatu kuendelea kuvitesa vyuma.

Vijana hao ambao nao ni wataalamu wa kukifanya chuma kama karatasi, alianza nao kusaka ujuzi, miaka 10 iliopita na baada ya yeye kujiona anajiweza ndio akawatupia jicho.

Wafanya kazi wanaokula mzigo kwenye ofisi hiyo ambao wanaulemavu, ni kijana Said Ali Saadun, Salum Bakar pamoja na Rashid Salum.

Kwa pamoja wenyewe walisema hawaamini kwamba kijana Khamis, amewachukua kwenye ofisi hiyo na kuendelea na kazi ya kuvichekecha vyuma .

“ Sisi hapa twashukuru sana, maana tupo tunaganga njaa na mwenzetu, maana tulikuwa tumeshakwama kimaisha, hivyo fursa aliotupa Khamis twashukuru’’,walieleza kwa furaha.

Mjasiriamali huyo kwa kushirikiana na wapiganaji wake, wakiwa wanajikita kwenye kutengeneza bidhaa zote za vyuma, kama milango ya mageti, anafurahia kazi wanazozifanya.

“Sisi ambao tunajidanganya kwamba hatuna ulemavu, hatuna huruma na wenye walemavu, hatutaki kuwasaidia kisha tukadai    hawezi kufanya kazi”, alisema kwa uchungu.

Katika kufanikisha kazi zao, alisema amewashawapangia bei kila  bidhaa, ili wanapofika wateja, wawe na kauli moja.

Kwa sasa kwenye ofisi hiyo ya mjasiriamali Khamis Makame Ali, mlango mmoja wa geti  hupatikana kati ya shilling 200,000 hadi shilingi 250,000 wakati na dirisha  moja kutegemeana na ukubwa na aina, huanzia shilingi  80,000.

Jiko la kawaida kwa mjasiriamali huyo huuza kati ya shilingi 10,000 na mchoteo wa mkaa (mshebeki) hupatikana kwa shilingi 2,000.

“Unajua kila penye mafanikio,  elewa na changamoto  hazichezi mbali, maana wateja kwanza ndio kilio chetu’’,alieleza.

Bei ni ndogo ukilinganisha na gharama inayotumika katika kutengeza bidhaa, na hata hutokezea siku nyengie kukosa mteja hata mmoja.

Kijana Khamis alianza na mtaji wa shilingi laki 800,000 kwa kujinunulia malighafi ambapo kwa sasa anabidhaa ambazo kama akiziuza anaweza kujipatia shilingi laki 400,000 hadi laki 500,000.

Hata hivyo, aliahidi kuendelea kujitengenezea njia ya maisha na anaamini iko siku atafikia malengo yake kwenye kazi hiyo.

Haridhishwi hata kidogo kuona vijana wenye nguvu na maarifa wakiishia vijiweni, kwa vile zipo kazi za kujishughulisha na kujipatia walau shilingi ya chakula.

Kijana huyo kwa kauli yake, alisema anashangaa kuona wapo watu na taasisi za umma wakiendelea kuwatenga watu wenye ulemavu, na kuwajengea dhana kwamba hawawezi.

Ameishauri Serikali na viongozi wengine kuwapa kipaumbele watu wa kundi hilo, ili kuona wanapata mitaji kupitia ofisi yake..                              

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.