Habari za Punde

Dk Shein akutana na makamo wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Korea Kusini (Koica)

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Makamo wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Korea Kusini "KOICA GLOBAL" Bw.Kwon  Taemyon akiwa na ujumbe wake walipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo pamoja na mwenyeji wa Ujumbe huo Waziri wa Kilimo,Maliasili,Mifugo na Uvuvi Mhe,Hamad Rashid Mohamed(hayupo pichani),[Picha na Ikulu.]
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia)  akizungumza na  Makamo wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Korea Kusini "KOICA GLOBAL" Bw.Kwon  Taemyon akiwa na ujumbe wake walipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo pamoja na mwenyeji wa Ujumbe huo Waziri wa Kilimo,Maliasili,Mifugo na Uvuvi Mhe,Hamad Rashid Mohamed(hayupo pichani),[Picha na Ikulu.]
 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (katikati)  akizungumza na  Makamo wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Korea Kusini "KOICA GLOBAL" Bw.Kwon  Taemyon (wa pili kushoto) akiwa na ujumbe wake walipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo pamoja na mwenyeji wa Ujumbe huo Waziri wa Kilimo,Maliasili,Mifugo na Uvuvi Mhe,Hamad Rashid Mohamed(wa pili kulia) akiwepo Katibu Mkuu Kiongozi Dkt.Abdulhamid Yahya Mzee(kulia),[Picha na Ikulu.]

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia)  akiagana na   Makamo wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Korea Kusini "KOICA GLOBAL" Bw.Kwon  Taemyon baada ya mazungumzo yao yaliyofanyika ukumbi wa  Ikulu Mjini Zanzibar leo (katikati) Waziri wa Kilimo,Maliasili,Mifugo na Uvuvi Mhe,Hamad Rashid Mohamed,[Picha na Ikulu.] 


 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                        14.4.2016
---
JAMHURI ya Korea Kusini imeahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo kwa kutambua juhudi kubwa zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwaletea maendeleo endelevu wananchi wake.

Akizungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Makamo wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Korea ya Kusini (KOICA), Bwana Kwon Taemyon aliyasema hayo leo huko Ikulu Mjini Zanzibar akiwa ameambatana na ujumbe wake kutoka Shirika hilo.

Katika mazungumzo hayo viongozi hao walitumia fursa hiyo kuzungumza na kutilia mkazo juu ya ushirikiano wa muda mrefu uliopo kati ya Korea ya Kusini na Tanzania ikiwemo Zanzibar na viongozi wote hao kwa pamoja waliahidi kuuimarisha uhusiano na ushirikiano huo.


Bwana Taemyon alimueleza Dk. Shein kuwa Jamhuri ya Korea inathamini uhusiano na ushirikiano uliopo kati yake na Zanzibar na itaendelea kuiunga mkono katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo miradi ya kilimo, ufugaji, uvuvi, mifugo pamoja na sekta nyenginezo iliyopo sambamba na kuanzisha miradi mengine mipya hapa Zanzibar.

Makamo huyo wa Rais wa Shirika hilo la Maendeleo la (KOICA), alisema kuwa miongoni mwa nchi katika bara la Afrika ambazo nchi hiyo imeziwekea kipaumbele katika kuimarisha miradi ya maendeleo na kuanzisha miradi mengine mipya ni Tanzania ambapo na Zanzibar nayo itafaidika kwa kiasi kikubwa katika kipaumbele hicho.

Aidha, katika mazungumzo hayo Makamu huyo wa Rais wa (KOICA) alimueleza Dk. Shein azma ya Shirika hilo la kusaidia mradi mkubwa wa ufugaji wa samaki ambao utawasaidia kwa kiasi kikubwa wananchi ikiwa ni pamoja na kutoa elimu pamoja na kusaidia nyenzo nyengine muhimu za ufugaji huo  hatua ambayo itaongeza soko la ajira sambamba na kipato kwa wananchi na Taifa kwa jumla.

Kiongozi huyo alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Serikali ya nchi yake pamoja na wananchi wa nchi hiyo wako Tayari kuisaidia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na watu wake.

Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa upande wake alitoa shukurani na pongezi kwa Serikali ya Korea ya Kusini kwa mashirikiano makubwa sambamba na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi yake mbali mbali ya maendeleo.

Dk. Shein alisema kuwa pande mbili hizo zina historia kubwa katika mashirikiano na uhusiano wake hatua ambayo imeweza kusaidia na kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo kilimo, ufugaji wa wanyama, uvuvi, mazingira na ufugaji wa samaki, elimu pamoja na sekta nyenginezo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliipongeza Jamhuri ya Korea kwa kusaida miradi kadhaa ukiwemo mradi mkubwa wa kilimo cha umwagiliaji maji na kuimarisha eneo la hekta 2,105 za miundombinu ya umwagiliaji maji katika mabonde ya Cheju, Kilombero na Chaani kwa Unguja na Mlemele na Makwararani kwa Pemba,  hatua itakayosaidia katika kupambana na umasikini na kukuza uchumi hapa nchini.

Aidha, Dk. Shein alieleza juhudi za makusudi zinazochukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kuimarisha kilimo cha umwagiliaji maji ambacho mafanikio yake yatasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuharakisha ukuaji uchumi wa Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein hakuchelea kumueleza Makamo huyo wa Rais wa (KOICA) azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha uvuvi wa bahari kuu ambapo juhudi maalum zimekuwa zikichukuliwa katika kutafuta wawekezaji na tayari wapo walioonesha nia ya kuekeza huku akipongeza azma ya (KOICA) ya kuanzisha mradi mkubwa wa ufugaji samaki hapa Zanzibar.

Sambamba na hilo Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo azma ya  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuaanzisha viwanda vya uvuvi hatua ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuinua kipato cha wananchi pamoja na kukuza pato la taifa.

Dk. Shein alilipongeza Shirika hilo katika juhudi zake za kuunga mkono  kilimo hicho cha umwagiliaji maji hapa Zanzibar ambapo lengo kubwa la Serikali ni kuhakikisha kiwango cha uagiziaji wa mchele kutoka nje ya nchi kinapungua kwa kuzalisha nusu ya mchele unaoagiziwa kutoka nje kuazia mwaka 2018 hadi 2019.

Ujumbe huo wa Makamu wa Rais wa Shirika la Maendeleo la Korea Kusini (KOICA) uliofika Ikulu kufanya mazungumzo na Rais pia, uliongozana na Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mhe. Hamad Rashid Mohammed pamoja na viongozi wa Wizara hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.