Habari za Punde

Tanzania na Burundi Zatakiwa Kuregeza Msimamo Ndani ya EAC

Mwenyekiti wa shirikisho la waajiri la jumuiya ya Afrika Mashariki(EAEO),Rosemary Ssenabulya akizungumza na waandishi wa habari jijini Arusha hivikaribuni kuhusu mafanikio na changamoto za shirikisho hilo,kushoto kwake ni katibu wa shirikisho hilo,Agrey Mlinuka na kulia kwake ni mkurugenzi mtendaji wa shirikisho la waajiri nchini Kenya,Jacqueline Mugo(Habari picha na Pamela Mollel wa jamiiblog)

Tanzania  na Burundi zimeombwa kulegeza misimamo yao kwa kuondoa gharama za vibali vya kufanya kazi kwa raia wa nchi zinazounda jumuia ya Afrika Mashariki (EAC) kama zilivyofanya nchi za Rwanda, Uganda na Kenya ambazo nazo ni wanachama wa jumuiya hiyo.

Akizungumza jijini Arusha hivikaribuni Katibu wa Chama cha Waajiri Afrika Mashariki (EAEO), Aggrey Mlinuka alisema kuwa hadi sasa nchi za Tanzania na Burundi ndizo nchi pekee zilizobakia katika kutoza gharama za vibali vya wageni hasa raia wa Jumuia ya Afrika Mashariki.

Mlimuka alisema kuwa mbali na nchi hizo kuondoa utaratibu huo pia amependekeza kwamba utaratibu wa utoaji vibali hivyo usichukua muda mrefu kama ilivyo sasa kwa nchi za Tanzania na Burundi na kushauri muda wa kuchukua vibali hivyo haustahili kuzidi siku 30.

Katibu huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha waajiri Tanzania (ATE) alisema kuwa  chama chao kiliwasilisha mapendekezo hayo mbele ya  Katibu Mkuu wa Jumuia ya Afrika Mashariki, Dk. Richard Sezibera ambaye anamaliza muda wake April 20 mwaka huu.

“EAEO na Sezzibera tumefanya kazi kubwa kuhakikisha jumuiya inasonga mbele kwa kasi kubwa mbali na changamoto zilizopo katika nchi moja moja, lakini tuna uhakika tutazitatua kwa manufaa na maslahi ya wana jumuiya wote,” alisema Mlinuka.

Alisema kuwa Katibu Mkuu mpya Liberata Mfumukeko kutoka kutoka Burundi anatakiwa kuendeleza pale ambapo Dk Sezzibera anapoishia ambapo ni kuhakikisha kwamba unakuwepo utatu wa ajira katika jumuiya ya Afrika Mashariki.

Mbali na hilo pia amemtaka katibu mkuu huyo mpya kuhakikisha protokali ya soko la pamoja kipengele cha pili cha jumuia ya Afrika Mashariki kinatekelezeka ikiwa ni pamoja na kuondoa vikwazo vya wananchi kuingiliana kutoka sehemu moja kwenda nyingine kibiashara pamoja na kutafuta ajira ndani ya nchi wanachama.

Awali Mwenyekiti wa chama cha waajiri Kenya(FKE) Jacqueline Mugo alisema kuwa nchi wanachama hazipaswi kuwa na uoga katika yale ambayo yanaonekana kuwa na manufaa na uhai wa Jumuia ya Afrika Mashariki yakiwemo masuala ya ajira na mengineyo. 

Mkutano wa siku moja ulikutanisha vyama vyote vya waajiri wa nchi zinazounda jumuia ya Afrika Mashariki vikiwa na malengo ya kuhakikisha wananchi wa jumuiya hiyo wanapata ajira popote pale wanapokwenda ndani ya jumuiya ya Afrika Mashariki.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.