HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA KUSIMAMIA OFISI ZA VIONGOZI WAKUU WA KITAIFA
KUHUSIANA NA MAKADIRIO YA MAPATO NA
MATUMIZI YA WIZARA YA NCHI, OFISI YA RAIS NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI
KWA MWAKA WA FEDHA 2016/2017.
Mheshimiwa
Spika,
Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi
Mungu mwingi wa utukufu, kwa kutujaalia uzima na Afya njema tukaweza kukutana
tena katika Baraza hili la Tisa kwa ajili ya kuendelea kuwatumikia wananchi
wetu, aidha kukushukuru na kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika kwa kuchaguliwa
kwako kuliongoza Baraza hili tukufu, ni imani yangu kwamba utaliongoza Baraza
hili kwa uadilifu wa hali ya juu na kuimarisha Demokrasia katika chombo hiki
muhimu cha wananchi.
Mheshimiwa Spika,
Napenda kuchukua nafasi hii
kuwapongeza wawakilishi wote waliomo katika Baraza lako Tukufu kwa kuchaguliwa
kwao kuja kuwawakilisha wananchi, ni wazi kwamba wananchi wamejenga imani kubwa
kwetu, nasi ahadi yetu kwao ni kwamba tutawatumikia kwa dhati kama ambavyo
walivyotuamini kutuleta katika chombo hichi kwa lengo la kutetea maslahi yao.
Mheshimiwa Spika,
Sina budi pia kumshukuru Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na watendaji wake wote
wakiongozwa na Katibu Mkuu kwa mashirikiano waliyotupatia wakati wa kupitia
makadirio ya Bajeti ya Wizara hii lakini pia nawashukuru Wajumbe wa Kamati yetu
kwa umoja wao na kazi nzuri waliyoifanya kiasi cha kunirahisishia kazi yangu ya
kuongoza kikao kuwa nyepesi zaidi, kwa hakika ni wajumbe mahiri, ambapo licha
ya upya wao katika Baraza hili na hususan katika Kamati hii wameweza kuijadili
ipasavyo na kuhoji mambo mbali mbali kwa lengo la kuhakikisha kwamba fedha wanazoidhinisha
zinatumiwa kwa matumizi yaliokusudiwa.
Mheshimiwa Spika,
Kwa heshima ya hali ya juu napenda
kuwatambua Wajumbe hao kwa majina kama hivi ifuatavyo:-
1. Mheshimiwa
Omar Seif Abeid Mwenyekiti
2. Mheshimiwa
Panya Ali Abdalla M/Mwenyekiti
3. Mheshimiwa
Amina Iddi Mabrouk
Mjumbe
4. Mheshimiwa
Hussein Ibrahim Makungu
Mjumbe
5. Mheshimiwa
Mohammed Said Mohammed Mjumbe
6. Mheshimiwa
Mussa Ali Mussa Mjumbe
7. Mheshimiwa
Mtumwa Suleiman Said Mjumbe
8. Mheshimiwa
Simai Mohammed Said Mjumbe
Aidha kamati yetu inafanyakazi na
makatibu wawili ambao kwa kiasi kikubwa wamekuwa wakitusaidia sana katika
kutekeleza majukumu yetu, makatibu hao ni:-
1.
Ndg Maryam Rashid Ali Katibu
2.
Ndg Othman Ali Haji Katibu
Mheshimiwa Spika,
Ikumbukwe kwamba miongoni mwa
majukumu ya msingi ya Kamati yetu ni kuchambua mapendekezo ya Serikali kuhusu
makadirio ya Wizara husika ya mapato na matumizi ya kila mwaka, hivyo katika
kutekeleza jukumu hilo lililoelezwa katika kanuni ya 114(e) kamati yangu ilikaa
na kujiadili na hatimae kupitisha Makadirio ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi mnamo tarehe 10/05/2016 na leo hii kwa ruhusa yako na kwa
niaba ya Kamati nawasilisha maoni ya Kamati kuhusiana na Bajeti hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Baada ya utangulizi huo mfupi sasa
naomba nitekeleze jukumu nililopewa na Kamati la kuwasilisha maoni ya Kamati
yetu hapa mbele ya Baraza lako tukufu moja kwa moja.
KUHUSU MFUMO WA BAJETI WA PBB
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kuanzia mwaka wa fedha 2015/2016 imeanzisha mfumo wa bajeti unaozingatia
programu yaani Program Based Budget (PBB) ambapo kwa bajeti hii itakuwa ni
kipindi cha pili kutekelezwa, licha ya kuwa ilishaanza kutekelezwa kwa mwaka wa
fedha uliopita bado mfumo huu unabakia kuwa mpya kwa Wajumbe wako ukizingatia
kwamba asilimia kubwa ya Wajumbe wa Baraza hili ni wapya hivyo mfumo huu wa PBB
imekuwa ni changamoto kwao kuweza kuufahamu kwa ghafla na kupelekea ugumu
kidogo kuweza kumudu kufanya uchanganuzi wa vitabu vya Bajeti vilivyoletwa
katika kamati zako, sambamba na hilo Wajumbe hawakupatiwa mafunzo ya kutosha,
lakini hata hivyo wamejitahidi kadiri ya uwezo wao kuweza kuchambua bajeti hiyo
kwa msaada wa makatibu wetu ambao kwa kweli tunawashukuru sana.
Mheshimiwa Spika,
Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi kwa mwaka wa fedha
2016/2017 ina mafungu (vote) mawili ambayo ni A01 na A02 na imepanga kutekeleza
Program kuu tano zenye Programu ndogo 14 ambazo kwa ujumla Fedha iliyoombwa kwa
Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ni TZS. 6,490,200,000 (Bilioni
sita, Mia nne tisiini milioni na laki mbili).
Fungu A01 Ofisi ya Rais Ikulu ina
jumla ya Programu kuu tatu na programu ndogo tisa, Programu kuu ni kama zifuatazo:-
1. Programu
ya kusimamia Shughuli za Mheshimiwa Rais na kuimarisha Mawasiliano Ikulu.
2. Programu
ya Ushirikiano wa kikanda, kimataifa na uratibu wa Wazanzibari wanaoishi nchi
za Nje (Diaspora).
3. Programu
ya Utawala na Uendeshaji wa Ofisi ya Rais Ikulu.
Program
ndogo ni hizi zifuatazo:-
I.
Programu ndogo ya uratibu wa shughuli za Mheshimiwa
Rais
II.
Programu ndogo ya kuimarisha mawasiliano baina ya
Mheshimiwa Rais na Wananchi
III.
Programu ndogo ya kuiwakilisha Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika mikutano ya kikanda na kimataifa
IV.
Programu ndogo ya uratibu wa Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar katika masuala ya Diaspora
V.
Program ndogo ya uratibu na usimamizi wa shughuli
za Ofisi ya Rais Ikulu
VI.
Program ndogo ya uratibu wa shughuli za Mipango,
Sera na utafiti za ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
VII.
Program ndogo
ya Kuratibu na kusimamia shughuli za uratibu na usimamizi wa shughuli za
Ofisi ya Rais Ikulu na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Pemba
VIII.
Programu ndogo ya usimamizi wa usalama wa watumishi
wa Umma
IX.
Programu ndogo ya ufuatiliaji na tathmini ya Sera
na Maamuzi ya Serikali
PROGRAMU YA KUSIMAMIA SHUGHULI ZA MHESHIMIWA RAIS NA KUIMARISHA MAWASILIANO
IKULU.
Mheshimiwa Spika,
Programu hii ina Jukumu la
kusimamia shughuli za Mheshimiwa Rais pamoja na kuimarisha Mawasiliano,
programu hii ina programu ndogo mbili ambazo ni programu ndogo ya uratibu wa
shughuli za Mheshimiwa Rais ambayo imetengewa shilingi 2,667,003,000 (Bilioni
mbili,mia sita sitini na saba Milioni, na elfu tatu) na shughuli zinazotarajiwa
kutekelezwa ni pamoja na kufuatilia ahadi na maagizo ya Mheshimiwa Rais,
kuratibu ziara za ndani na za nje za Mheshimiwa Rais, kutoa viburudishaji kwa
wageni wa Mheshimiwa Rais, kuchapisha hotuba na mambo mengine ya Mheshimiwa
Rais, na kutoa zawadi kwa wageni wa Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Spika,
Programu ndogo ya pili ni ya kuimarisha
mawasiliano baina ya Mheshimiwa Rais na Wananchi ambayo imepangiwa shilingi 200,351,000
(Milioni mia mbili, laki tatu na hamsini na moja elfu) na shughuli
zinazotarajiwa kutekelezwa kwa fedha hizo ni pamoja na kutayarisha, kuchapisha
na kusambaza Kalenda za Ofisi ya Rais, kutayarisha, kuchapisha na kusambaza
Jarida la Ikulu, vipeperushi na machapisho mengine, kuimarisha tovuti ya Idara ya
Mawasiliano, Kwa ujumla programu kuu ya kusimamia shughuli za Mheshimiwa Rais
imepangiwa kutumia shilingi 2,867,353,000 (Bilioni mbili, mia nane sitini na
saba Milioni, laki tatu hamsini na tatu elfu).
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu imeridhika na makadirio
yaliopangwa katika programu hii na ilipendekeza mambo mbali mbali ambayo
yatakapozingatiwa yataboresha kwa kiasi kikubwa kumtangaza Rais wetu na
kumfanya awe karibu zaidi na wananchi wake waliopo hapa nchini lakini pia hata
wanaoishi nchi za nje, Kwanza Kamati yangu katika kuona mawasiliano yanaimarika
baina ya Rais wetu na wanachi ni vyema Idara ya Mawasiliano, mbali na kusambaza
majarida na kalenda, imtangaze Rais kwa kutumia mfumo wa kisasa wa teknolojia
na Mawasiliano kwa kutumia njia zinazoendana na dunia ya leo (New Media) kama
vile facebook, twitter, youtube mfano clips muhimu za Rais, shorts clips za sekunde 30 hadi sekunde 45 kwa
ajili ya whatsApp, ili watu waone
shughuli anazozifanya Mheshimiwa Rais, pamoja na kutambulika katika
ulimwengu mzima na kwa jinsia zote na rika zote.
Mheshimiwa Spika,
Aidha Kamati yetu inashauri kwamba
Mheshimiwa Rais angelikuwa na utaratibu wa kuwaalika na kukaa pamoja na
wawekezaji, wafanyabiashara na wadau mbali mbali wa maendeleo kwa lengo
kuzungumza na badilishana nao mawazo lakini pia kuwashukuru wale ambao wamekuwa
wakiisaidia nchi yetu kwa njia moja au nyengine, Jambo hili linaweza kuongeza
hamasa kwa wafanyabiashara na wawekezaji kuwekeza zaidi katika sekta mbali
mbali. Aidha pale ambapo kunatokezea mgeni mashuhuri ambae atastahiki kupewa
zawadi basi zawadi atakayopewa iwe ni zawadi yenye asili na iliyotengenezwa kwa
ubunifu na iambatanishwe pamoja na historia ya mtengenezaji, ili kuhakikisha
kuwa Mgeni anapopewa zawadi hiyo basi anapata kujua historia ya Zanzibar ambayo
wanaweza kuweka kumbukumbu katika makumbusho yao lakini pia itaitangaza nchi
katika masuala ya utalii.
PROGRAMU YA USHIRIKIANO WA KIKANDA, KIMATAIFA NA URATIBU WA WAZANZIBARI
WANAOISHI NCHI ZA NJE.
Mheshimiwa Spika,
Programu hii ina lengo la kuiwezesha
Zanzibar kushiriki katika mikutano ya kikanda na kimataifa, na kuwashirikisha
ipasavyo Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi katika maendeleo ya kiuchumi na
kijamii ya nchi yao. Programu hii ina programu ndogo mbili ambazo ni programu
ndogo ya kuiwakilisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika mikutano ya
kikanda na kimataifa ambayo imepangiwa kutekelezwa kwa shilingi 264,673,000 (Mia
mbili sitini na nne Milioini, laki sita na sabini na tatu elfu) ambapo miongoni
mwa shughuli zitakazofanywa ni pamoja na kuimarisha ushiriki wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar katika mikutano ya kikanda, kuendesha vikao vya ndani vya
kisekta kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kushiriki katika mikutano ya mashauriano
ili kupata msimamo mmoja wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
kushiriki katika mikutano ya kikanda nje na ndani ya nchi na kutoa elimu kwa
jamii juu ya umuhimu wa mtengamano wa Jumuiya za kikanda.
Mheshimiwa Spika,
Programu ndogo ya pili ni ya
uratibu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika masuala ya Diaspora, ambayo
imepangwa kutekelezwa kwa shilingi 239,847,000 (Mia mbili thelathini na tisa
milioni, laki nane na arobaini na saba elfu) na shughuli zilizopangwa kutekelezwa ni pamoja
na kushiriki katika mkutano wa mashauriano
wa Diaspora na Idara inayoshughulikia
masuala ya Diaspora Dar es Salaam, kutoa elimu kwa jamii juu ya dhana ya
Diaspora na umuhimu wake,kushiriki mkutano wa wadau wa Maendeleo kujadili
ajenda za Diaspora, kuandaa kongamano la Watanzania wanaoishi nchi za nje na
kusimamia shughuli za kila siku za Idara ya Ushirikiano wa kimataifa na uratibu
wa Diaspora. Kwa ujumla Programu ya Ushirikiano wa Kikanda, Kimataifa na
Uratibu wa Wazanzibari wanaoishi Nchi za Nje imekadiriwa kutekelezwa kwa
shilingi 504,520,000 (Milioni mia tano na nne, laki tano na ishirini elfu).
Mheshimiwa Spika,
Katika kuona azma ya kuwepo kwa
idara ya uratibu wa wazanzibari wanaoishi nchi za nje inazaa matunda, kamati
yangu inashauri kwamba wafanyakazi wote wanaokwenda ziara nchi za nje au
kushiriki mikutano nchi za nje wawasilishe ripoti za ziara au safari hizo kwa
ujumla wake Serikalini ili ripoti hizo zifanyiwe kazi ili kuleta mafanikio kwa taifa
letu, sambamba na hilo safari hizo ziweze kuleta tija ya kuibua miradi mbali
mbali kutoka kwa wahisani lakini pia, wanapokwenda huko waitangaze vyema nchi
yetu ili wawekezaji wavutike kuja kuwekeza katika sekta mbali mbali.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu katika suala zima la
safari za nje wanazokwenda mawaziri na watendaji mbali mbali wa Serikali
inataka kusisitiza juu ya ripoti hizo wanazoziwasilisha Mawaziri husika katika Baraza la Mawaziri ziambatane
na ripoti za utekelezaji wake ili tuone tija ya kweli inapatikana kwa nchi
yetu, aidha kamati ilitaka kujua juu ya
ziara za Viongozi wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanaposafiri kwenda
safari za nje na kushauri kwamba wakati viongozi hao wanaposafiri ni vyema
wakajitayarisha na kuzingatia faida pamoja na fursa watakazozipata ziinufaishe
na Zanzibar.
Mheshimiwa Spika,
Aidha kamati iliishauri Serikali
kuwa na mashirikiano ya karibu na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
hasa katika Wizara ambazo hazihusiani na Muungano lakini zenye sura ya
Kimuungano kwa mfano Afya, Elimu, Utalii nk. Kamati pia ilihoji juu ya uhusiano
uliopo baina Comoro na Zanzibar hususan katika suala la Kampuni inayoitwa hairu
ambayo ni kampuni ya uvuvi iliyokuwa ije kuwekeza Zanzibar katika masuala ya
uhifadhi wa Samaki ambapo Kamati ilipatiwa taarifa kwamba mipango inaendelea
katika kufanikisha mradi huo.
PROGRAMU YA UTAWALA NA UENDESHAJI WA OFISI YA RAIS IKULU.
Mheshimiwa Spika,
Programu hii ina malengo ya
kuimarisha shughuli za mipango, kuandaa na kuchambua sera na utafiti pamoja na
kuimarisha uwezo wa kiutendaji na uratibu wa shughuli za Ofisi ya Rais Ikulu,
program hii ina program ndogo tano,ambazo ni program ndogo ya uratibu na
usimamizi wa shughuli za Ofisi ya Rais Ikulu, ambayo imepangiwa kutekelezwa kwa
shilingi 1,126,326000 (Bilioni moja, mia moja ishirini na sita milioni, laki
tatu na ishirini na sita elfu) ambazo zinakadiriwa kutumika katika shughuli za kusimamia uendeshaji wa Ofisi ya Rais Ikulu
kwa kulipa mishahara, kununua vifaa vya usafiri, kuboresha na kukarabati
vitendea kazi, ofisi na Majengo, kutoa huduma za kiutawala, kutoa mafunzo kwa
waajiriwa wapya 12 na nyenginezo kama zinavyoonekana katika kitabu cha
makadirio ya Mapato na Matumizi ya cha mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Spika,
Katika program ndogo hii Kamati
yangu inashauri kwamba ili jengo la Ikulu ya Mnazi Mmoja liweze kuwa na haiba
na mvuto zaidi kwa shughuli za Mheshimiwa Rais, ni vyema lifanyiwe ubunifu
katika sehemu yake ya nyuma iliyo mkabala na bahari kwa kujengwa jet ambayo
itaingia katika eneo la ufukwe wa bahari uliopo na kusanifiwa katika mtindo wa
utamamduni wetu ambao sehemu hiyo ataitumia Rais anapokuwa na wageni wake
mashuhuri ili kupata utulivu katika hewa nzuri ya upepo wa bahari ya hindi na
kuwafanya wageni wavutike kuja kuwekeza
Zanzibar.
Mheshimiwa Spika,
Program ndogo ya pili ni ya
uratibu wa shughuli za Mipango, Sera na utafiti za ofisi ya Rais na Mwenyekiti
wa Baraza la Mapinduzi ambayo imekadiriwa kutekelezwa kwa TZS 300,778,000 (Milioni
mia tatu, laki saba na sabini na nane elfu) zitakazotumika kwa kulipa mishahara
kwa wafanyakazi na stahiki nyengine, kutoa mafunzo ya muda mrefu,kusimamia na
kuhuisha tovuti ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kufanya
tathmini hali ya Tehama katika Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, kuandaa na kuratibu vikao vya matayarisho ya hotuba ya Bajeti nk.
Mheshimiwa Spika,
Program ndogo ya tatu ni ya
Kuratibu na kusimamia shughuli za uratibu na usimamizi wa shughuli za Ofisi ya
Rais Ikulu na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Pemba, program hii imekadiriwa
kutumia TZS 663,113,000 (milioni nia sita sitini na tatu, laki moja na kumi na tatu
elfu) ambazo zinatarajiwa kutumika kwa kutoa na kuratibu huduma za utawala,
kulinda, kuhifadhi na kutoa huduma kwa Ikulu na nyumba za Serikali zilizoko
Pemba, kulipa mishahara na stahiki kwa wafanyakazi wa Pemba, kutoa huduma za
usafiri, zana na matengenezo yake, kukarabati majengo ya Ofisi na ununuzi wa
thamani za Ofisi.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu kupitia Programu ndogo
ya uratibu na usimamizi wa ofisi ya Rais Ikulu na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Pemba inashauri kwamba jengo la Ikulu ya Chake Chake kufanyiwa
ukarabati mkubwa kwani haifanani na hadhi ya kuwa nyumba ya kukaa kiongozi
mkubwa wa nchi kwani hali yake hairidhishi. vile vile Kamati inapendekeza kuondoshwa
kwa maofisa wa Serikali ikiwa ni pamoja na maofisa wa Mahakama wanaokaa katika nyumba
iliopo katika eneo la Ikulu, ili nyumba
hiyo iweze kufanyiwa ukarabati. Sambamba na hilo Kamati yangu ilitaka kujua juu
ya matengenezo ya nyumba ya Ikulu ya Mkokotoni ambayo nayo inahitaji kujengewa
uzio kwa ajili ya kuzuia uingiaji ovyo wa watu katika eneo hilo. Aidha Kamati inashauri kwamba Wizara hii ikae
pamoja na Waziri anaehusika na vikosi ili kukarabati sehemu ambayo askari wa
KMKM wanakaa wakati wanapofanya kazi zao za ulinzi, ili iendane na eneo hilo la
Ikulu.
Mheshimiwa Spika,
Programu ndogo ya nne ni ya
usimamizi wa usalama wa watumishi wa Umma ambayo imekadiriwa kutumia TZS
40,000,000 (Milioni arobaini) ambazo fedha hizo zinatarajiwa kutumika katika
usalama wa mali na majengo ya Serikali kwa Unguja na Pemba, kufanya ukaguzi wa
kiusalama wa muda mfupi na endelevu kwa wafanyakazi, kuendesha mafunzo na
semina kwa watumishi. Kamati inashauri kwamba ili wafanyakazi wafanyekazi
katika mazingira yalio salama zaidi ni vyema ukaguzi wa kiusalama wa majengo
ukafanyika mara kwa mara kwani kuna taasisi na idara mbali mbali ambazo
wanafanya kazi katika majengo ambayo sio salama na hivyo kuhatarisha usalama wa
wafanyakazi.
Mheshimiwa Spika,
Kwa ujumla wake Programu kuu ya Programu
ya Utawala na Uendeshaji wa Ofisi ya Rais Ikulu imekadiriwa kutumia TZS 2,126,326,000,
(Bilioni mbili mia moja ishirini na sita milioni laki tatu na ishirini na sita
elfu) ambazo kamati yangu inaona bado ni fedha chache kutengwa kwa Ofisi kubwa
kama hii, hususan ukizingatia uchakavu wa nyumba za Ikulu zinazohitaji
kufanyiwa ukarabati ili ziweze kuendana na hadhi ya Rais wetu
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu pia imepitia Fungu
A02 Ofisi ya Baraza la Mapinduzi, ambalo ni fungu linalojitegemea na kusimamiwa
na Naibu Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi, Fungu hili lina program kuu mbili
na program ndogo tano, program kuu ni:-
1. Programu
ya usimamizi wa Majukumu ya kikatiba na kisheria ya Baraza la Mapinduzi
2. Programu
ya Utumishi na Utawala wa Ofisi ya Baraza la Mapinduzi,
Kwa upande wa program ndogo ni:-
I.
Programu ndogo ya Uratibu na Usimamia shughuli za
Baraza la Mapinduzi na kamati zake
II.
Programu ndogo ya tathmini ya uwajibikaji na
utendaji kazi wa Taasisi za Umma
III.
Programu ndogo ya kukuza ufanisi wa kitengo cha
Teknologia ya Habari na Mawasiliano
IV.
Program ndogo ya utumishi na uendeshaji wa Ofisi ya
Baraza la Mapinduzi
V.
Program ndogo ya pili ni uimarishaji uwezo wa Ofisi
katika kusimamia Sera, Sheria na Utumishi wa Umma
PROGRAMU YA USIMAMIZI WA MAJUKUMU YA KIKATIBA NA KISHERIA YA BARAZA LA
MAPINDUZI NA KAMATI YA MAKATIBU WAKUU
Mheshimiwa Spika,
Programu ya usimamizi wa Majukumu
ya kikatiba na kisheria ya Baraza la Mapinduzi na Kamati ya Makatibu Wakuu
ambayo kwa ina lengo la kutayarisha na kusimamia vikao vya Baraza la Mapinduzi
na Kamati ya Makatibu Wakuu, programu hii ina Programu ndogo tatu, programu
ndogo ya kwanza ni ya kuratibu na kusimamia shughuli za Baraza la Mapinduzi na
kamati zake ambayo imekadiriwa kutekelezwa kwa TZS 109,200,000 (Milioni mia
moja naTisa na laki mbili) ambazo zitatumika katika kutayarisha vikao 12 vya
BLM na Kamati zake, kutayarisha vikao 12 vya Kamati za Baraza la Mapinduzi
kutayarisha vikao 8 vya dharura vya BLM na 8 vya kamati ya Makatibu Wakuu wa
SMZ, kutoa mafunzo ya kujenga uwezo kwa Viongozi wa kisiasa na Sekretarieti ya
Baraza la Mapinduzi.
Mheshimiwa Spika,
Program ndogo ya pili ni ya
tathmini ya uwajibikaji na utendaji kazi wa Taasisi za Umma, ambayo imekadiriwa
kutekelezwa kwa TZS 35,360,000 (Milioni thelathini na tano laki tatu na sitini
elfu) ambazo zitatumika katika shughuli za kutayarisha mikutano miwili ya
tathmini ya utendaji kazi kati ya Mheshimiwa Rais na Viongozi wa Wizara za SMZ,
kusaidia shughuli za kijamii na masuala mtambuka kupitia Mawaziri wasio na
Wizara maalum.
Mheshimiwa Spika,
Program ndogo ya tatu ni ya kukuza
ufanisi wa kitengo cha Teknologia ya Habari na Mawasiliano ambayo nayo imepangiwa
kutekelezwa kwa TZS 31,930,000 (Milioni thelathini na Moja, laki tisa na
thelathini elfu) katika kutekeleza shughuli za kusimamia huduma za mkonga wa
Taifa wa Mawasiliano katika Ofisi, Kwa ujumla Programu kuu ya usimamizi wa
Majukumu ya kikatiba na kisheria ya Baraza la Mapinduzi na Kamati ya Makatibu
Wakuu kwa mwaka wa fedha 2016/2017 imekadiriwa kutumia 176,490,000 (Milioni Mia
moja sabini na sita laki nne na tisiini elfu).
PROGRAMU YA UTUMISHI NA UTAWALA WA OFISI YA BARAZA LA MAPINDUZI
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu pia katika Fungu A02
ilipitia Programu kuu ya Utumishi na Utawala wa Ofisi ya Baraza la Mapinduzi
yenye lengo la kuimarisha mazingira ya kazi, mahusiano ya umma na kuwaongezea
ujuzi wafanyakazi wa Ofisi, Program hii ina program ndogo mbili ambazo ni
program ndogo ya utumishi na uendeshaji wa Ofisi ya Baraza la Mapinduzi na
program ndogo ya uimarishaji uwezo wa Ofisi katika kusimamia Sera , sheria na
Utumishi wa Umma, Programu ndogo ya utumishi na uendeshaji imepangiwa
kutekelezwa kwa TZS 1,179,210,000 (Bilioni moja, mia moja sabini na tisa
Milioni, laki mbili na elfu kumi) ambazo zimepangwa kutekelezwa katika shughuli
mbali mbali, ikiwa ni pamoja na kuboresha miundombinu ya Ofisi, majengo pamoja
na mazingira yake, kuiwakilisha Ofisi katika mikutano, warsha pamoja na
makongamano ya ndani na nje ya nchi, na kurahisisha ufanisi wa shughuli za kiofisi.
Mheshimiwa Spika,
Program ndogo ya pili ni uimarishaji uwezo wa
Ofisi katika kusimamia Sera, Sheria za Utumishi wa Umma, program hii imepangwa
kutekelezwa katika mwaka huu wa fedha kwa TZS 136,300,000 (Mia moja thelathini
na sita milioni na laki tatu) ambazo zimepangwa kutumika katika kuendesha
shughuli za uanzishaji wa Maktaba ya Baraza la Mapinduzi, uimarishaji wa
kitengo cha uhifadhi wa kumbukumbu za Baraza la Mapinduzi, kutayarisha ripoti
ya mwaka ya hali ya utumishi wa umma pamoja na ukusanyaji na ufuatiliaji wa
Sera,Sheria na Miongozo ya Baraza la Mapinduzi. Kwa ujumla wake Programu kuu ya
Utumishi na Utawala wa Ofisi ya Baraza la Mapinduzi katika mwaka wa fedha
2016/2017 imekadiriwa kutumia TZS 1,315,510,000 (Bilioni moja,mia tatu kumi na
tano Milioni, laki tano na elfu kumi).
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu baada ya kuzipitia
Programu zote nilizozitaja hapo kabla imeona fedha hizo ni kidogo kutengwa kwa
ofisi kubwa kama hii ambayo ndio muhimili wa Serikali yetu, ambayo bado ina changamoto nyingi zinazohitaji
kufanyiwa kazi zikiwemo zile za ubovu na uchakavu wa majengo ya nyumba za
Ikulu, uhaba wa vitendea kazi, uhaba wa usafiri kwa ajili ya Idara mbali mbali.
Hivyo Kamati inashauri kwamba hali itakaporuhusa katika Bajeti ya mwaka ujao
2017/2018 watengewe fedha ambazo zitaweza angalau kupunguza changamoto
zinazoikabili Wizara hii muhimu hasa ile ya kukarabati nyumba za ikulu ikiwemo
nyumba ya Kupumzikia ya Mkokotoni ambayo inahitaji kujengewa uzio na ile ya Chake
Chake ambayo iko katika hali isiyoridhisha.
Mheshimiwa Spika,
Mwisho napenda kukushukuru tena
kwa kunipa nafasi ya kuwasilisha maoni ya Kamati yangu kwa niaba ya Kamati
pamoja na kuwashukuru Wajumbe wa Baraza lako Tukufu kwa kunisikiliza, sasa niwaombe
Wajumbe wa Baraza lako waijadili na hatimae waiunge mkono
bajeti hii ili wamuwezeshe Waziri kufanikisha na kutekeleza yale waliojipangia
katika mwaka huu wa Fedha.
Mheshimiwa Spika,
Kwa niaba yangu na kwa niaba ya
Kamati ya kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa kitaifa naunga mkono hoja na
naomba kuwasilisha.
Mhe. Omar Seif Abeid,
Mwenyekiti,
Kamati ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment