Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                             2.07.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa nia na malengo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya elimu ni makubwa hivyo kujitokeza kwa wanannchi na taasisi mbali mbali kuiunga mkono sekta hiyo ili izidi kuimarika ni jambo la faraja.

Dk. Shein aliyasema hayo wakati wa mazungumzo kati yake na viongozi na Masheikh wa Jumuiya ya Khoja Shia Ithna-asheir wakiongoza na Rais wa Jumuiya hiyo Mohammed Raza waliofika Ikulu mjini Zanzibar kumkabizi Rais msaada wa madawadi yaliotolewa na uongozi huo pamoja na familia ya Rais wa Jumuiya hiyo kwa ajili ya wanafunzi wa Zanzibar.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini na imekuwa ikichukua juhudi za makusudi katika kuhakikisha sekta ya elimu inaimarika na ndio maana Rais wa Kwanza wa Zanzibar mara baada ya ukombozi alitangaza elimu bure.

Dk. Shein alisema kuwa katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati Zanzibar ina historia kubwa ya elimu ya dini na dunia kwani ndio nchi iliyokuwa ya mwanzo kuwa na elimu ya dini mnamo miaka 1890 na elimu ya dunia kuanzia mwaka 1905 kwa kuanzisha skuli licha ya kuwa elimu hiyo ya dunia waliipata watu wachache.

“Tumefarajika sana, tunajiona hatupo peke yetu tupo na wenzetu katika kulitafutia ufumbuzi suala hili, madawati ni muhimu kwa ajili ya wanafunzi wetu.....ipo siku Zanzibar itakuwa haina shida ya madawati” alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alieleza kufarajika kwake na mwanzo mzuri uliooneshwa na Jumuiya hiyo pamoja na familia ya Mohamed Raza kwa kutoa mchango wa madawati hayo ambayo yatasaidia katika kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini kwa kuwasaidia wanafunzi kupata vikalio vya uhakika maskulini.

Mapema Rais wa Jumuiya ya Khoja Shia Ithna-asheir Zanzibar, Mohammed Raza alimueleza Dk. Shein kuwa Jumuiya yake imetoa msaada wa madawati 50 na mtoto wake Hassan Mohammed Raza ametoa madawati 50 yenye thamani ya Tsh. milioni 12 kwa ajili ya wanafunzi wa skuli za Zanzibar huku akiahdi kuwa misaada hiyo itakuwa endelevu.

Katika maelezo yake Raza alisema kuwa msaada huo una lengo la kuunga mkono azma ya Dk. Shein ya kuhakikisha suala la upatikanaji wa madawati linapatiwa ufumbuzi hapa nchini hali ambayo ilimpelekea Rais kuunda Kamati ya Kitaifa ya watu 12 ikiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Makunduchi Haroun Ali Suleiman.

Rais huyo wa Jumuiya ya Khoja Shia Ithna-asheir ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Uzini alisema kuwa Jumuiya yake itaendelea kutoa misaada katika sekta zote za maendeleo ikiwemo elimu, afya na nyenginezo huku akiahidi kuwa atahakikisha kwa kushirikiana na Waziri wa Elimu anachukua juhudi kusafiri hadi nje ya Zanzibar kwa ajili ya kulipatia ufumbuzi suala hilo.

Nao Masheikh kutoka Jumuiya hiyo wakiongozwa na  Sheikh Maulana Dhishan Haidar walitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Dk. Shein kwa uongozi wake mahiri sambamba na juhudi zake za kuendelea kusimamia amani na utulivu hapa Zanzibar.

Viongozi hao walieleza azma yao ya kuendelea kuiunga mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na kuendelea kumuunga mkono Rais Dk. Shein katika kuimarisha sekta mbali mbali hapa nchini.

“Zanzibar imeweza kupata maendeleo...watu wake wanapendana....amani na utulivu umeimarika kwa kiasi kikubwa haya yote yanatokana na uongozi bora wa Dk. Shein”,alisema Maulana Haidar.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alitoa pongezi na shukurani kwa Jumuiya na Familia ya Mohammed Raza kwa kutoa msaada huo wa madawati ambayo yatawasaidia wanafunzi wa hapa Zanzibar katika kuweza kujipatia elimu bora kwa ufanisi zaidi.

Waziri Pembe alisema kuwa Wizara kwa upande wake inatoa shukurani kubwa na inathamini mchango huo na kueleza kuwa kwa vile Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina nia nzuri juu ya jambo hilo anamatumaini makubwa kuwa mafanikio yatapatikana.

Waziri huyo wa Elimu alitumia fursa hiyo kupongeza juhudi zinazochukuliwa na Dk. Shein katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya elimu na kuwaomba wananchi na taasisi nyengine kuendelea kutoa michango yao ya vifaa hivyo kwa ajili ya wanafunzi wa Zanzibar.

Hivi karibuni Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliwasilisha rasimu ya uchangiaji na upatikanaji wa madawati maskulini ili kuweza kupunguza upatikanaji wa madawati katika skuli za Zanzibar katika Baraza la Wawakilishi.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.