Mhesmiwa Spika;
Kwanza kabisa naomba nitumie nafasi hii
adhim kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehma, Muumba wa Mbingu na Ardhi
pamoja na vilivyomo ndani yake, kwa kutupa neema ya uhai na uzima katika
kutekeleza majukumu yetu ya kila siku kwa hali ya amani na utulivu.
Aidha,
napenda kuchukuwa nafasi hii kukushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii ya
kuwasilisha muhtasari wa Ripoti ya Kamati yetu ya Sheria, Utawala Bora na Idara
Maalum, Ripoti ambayo inawasilisha shughuli zetu zote ambazo tumezitekeleza kwa
kipindi kilichopita.
Mheshimiwa Spika;
Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum imeundwa kwa mujibu wa Kifungu
cha 85 cha Katiba ya Zanzibar, 1984 na Kanuni ya 106(1) ya Kanuni za Baraza la
Wawakilishi – Zanzibar, Toleo la 2016 na
kuainishwa majukumu yake chini ya Jadweli la Kwanza la Kanuni hizo la mwaka
2016.
Mheshimiwa Spika;
Napenda
kuchukua nafasi hii muhimu kwa kuwashukuru Wajumbe wa Kamati hii kwa
mashirikiano yao makubwa ambayo yameiwezesha kamati yetu kufanya kazi zake kwa
ufanisi na uzoefu mkubwa. Wajumbe wenyewe ni hawa wafuatao:-
1.
Mhe. Machano Othman
Said - Mwenyekiti
2.
Mhe. Mwantatu Mbarak
Khamis - Makamo M/kiti
3.
Mhe. Wanu Hafidh
Ameir - Mjumbe
4.
Mhe. Nadir Abdullatif
Yussuf - Mjumbe
5.
Mhe. Saada Ramadhan
Mwendwa - Mjumbe
6.
Mhe. Mohammed Said
Mohammed - Mjumbe
7.
Mhe. Ali Khamis Bakar - Mjumbe
8.
Ndg. Rahma Kombo
Mgeni - Katibu
9.
Ndg. Ali Alawy
Ali - Katibu.
Mheshimiwa Spika;
Katika utaratibu uliowekwa katika utekelezaji
wa kazi za Kamati kwa muda wote uliopita, Kamati yetu ilipanga kufuatilia utekelezaji
wa malengo na majukumu ya Wizara zifuatazo:-
i.
Wizara ya Nchi (OR)
Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
ii.
Wizara ya Nchi (OR)
Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ
Mheshimiwa Spika;
Kamati ilifanya
kazi zake kwa muda wa wiki sita (06) ambapo kwa upande wa Unguja ilitumia wiki
nne (04) na Pemba wiki mbili (02). Muda huo ulikuwa mdogo sana kwa namna ya wizara
hizi zilivyo na ukubwa wa Idara na Taasisi zake.
Mheshimiwa Spika;
Hata hivyo, Kamati inawapongeza sana na
kuwashukuru viongozi wa Wizara hizo wakiongozwa na Mawaziri wao, Naibu waziri,
Makatibu Wakuu, Manaibu makatibu wakuu, Makamishna, Wukurugenzi, Maafisa
Wadhamini Pemba na watumishi wao wote kwa ushirikiano wao mkubwa waliotuonesha
katika kufanikisha majukumu yetu, licha ya kuwepo kwa changamoto mbali mbali
zinazowakabili na kufanyakazi katika mazingira magumu na yenye upungufu wa
nyenzo lakini wameweza kutekeleza majukumu yao ya kazi kadri hali ilivyokuwa
inaruhusu.
Mheshimiwa Spika;
Naomba sasa uniruhusu nieleze kwa ufupi kabisa
baadhi ya mambo yaliyojitokeza katika kazi za Kamati kwa Wizara kama
ifuatavyo:-
WIZARA YA NCHI (OR) KATIBA, SHERIA, UTUMISHI WA
UMMA NA UTAWALA BORA:
Mheshimiwa Spika;
Wizara ya Nchi
(OR) Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora inazo Idara na Taasisi
mbali mbali ambazo zinafanya kazi kwa mujibu wa malengo yaliyopangwa chini ya
Wizara hii. Hivyo, katika kukamilisha majukumu ya Kamati yetu tulifanikiwa
kuzitembelea Idara na Taasisi kadhaa ambazo zimeunda Wizara hii na kujionea
shughuli zao mbali mbali ambazo zimekabiliwa na changamoto kubwa kutokana
upungufu wa vitendea kazi na udogo wa ukomo wa Bajeti.
Mheshimiwa Spika;
Kamati
inaipongeza sana Wizara ya Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora
pamoja na Serikali kwa juhudi zake za kuanzisha mahkama ya watoto Mahonda, ambayo
imefunguliwa hivi karibuni na Mhe. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dkt Ali Mohammed Shein, hivyo mahkama hiyo inatarajiwa kupunguza
idadi ya kesi za udhalilishaji na ukatili dhidi ya watoto kwani vitendo hivyo
vimeshamiri sana katika Mkoa huu wa Kaskazini Unguja. Ni matumaini yetu kuwa
uanzishwaji wake utasaidia sana katika uendeshaji wa kesi zote zinazohusu
watoto na kurahisisha upatikanaji wa haki za mtoto katika Mahkama zote za
watoto ikiwemo Vuga na Chake-Chake kisiwani Pemba.
Mheshimiwa Spika;
Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum katika ziara zake imebaini
kuwepo kwa changamoto kubwa ya vyombo vya usafiri katika Idara na Taasisi mbali
mbali zilizochini ya wizara hii, jambo ambalo linarudisha nyuma juhudi zao
katika utekelezaji wa majukumu yao. Aidha, changamoto hii inaikabili zaidi
Idara ya Nyaraka na Kumbu kumbu za Taifa, ambapo hadi sasa wana gari moja tu na
kutokana na uhaba huo wameona wanunue vespa moja, wakati Tume ya Utumishi
Serikalini hawana hata gari moja la kuwasaidia, hivyo huenda katika majukumu
yao ya kazi kwa kutumia usafiri wa Daladala jambo ambalo ni kikwazo kikubwa
katika utekelezaji wa majukumu yao.
Mheshimiwa Spika;
Afisi ya Afisa
Mdhamin Pemba inajitahidi sana katika kusimamia na kutekeleza majukumu yao na
kuhakikisha wameenda sambamba na malengo ya wizara na Serikali kwa ujumla.
Aidha, Kamati imebaini kuwepo kwa
baadhi ya Idara kutoingiziwa fedha za matumizi moja kwa moja isipokua fedha
hizo huingizwa katika kurugenzi zao kuu ziliopo Unguja kitu ambacho
kinasababisha Ofisi kuu Pemba kutumia fedha zake kwa ajili ya kuendeshea Idara
hizo. Aidha, kutokuwepo kwa baadhi ya TaasisiS Pemba ikiwemo ikiwemo Ofisi
ya Mwanasheria Mkuu, Tume ya Kurekebisha Sheria,
Tume ya Utumishi Serikalini na Ofisi ya Serikali Mtandao
(E- Government) kunasababisha kuzorota kwa kazi za Taasisi hizo muhimu za
Serikali.
Mheshimiwa
Spika;
Kamati inaagiza kuchukuliwa hatua zinazofaa suala la kutoingizwa
fedha za matumizi moja kwa moja katika baadhi ya idara zilizopo Pemba na kufanyiwa
haraka uwepo wa Taasisi zilizokosekana
kisiwani Pemba ili kuondoa changamoto zinazojitokeza kwa kukosekana ofisi hizo.
Mheshimiwa
Spika;
Lengo la Serikali ni kuona kwamba Idara na Taasisi zake
zinafanikiwa katika utekelezaji wa majukumu yao na zinaleta ufanisi katika
kuleta maendeleo kwa Nchi yetu. Aidha, Kamati
imegundua kuwepo kwa changamoto kubwa ya vitendea kazi kwa upande wa Mahkama
zote zilizopo Unguja na Pemba jambo ambapo kwa kiasi kikubwa linachangia
kurundikana na kuchelewa kwa uendeshaji
wa kesi katika Mahkama zetu. Vile vile, tatizo hili linaonekana kuwa kubwa
zaidi katika Taasisi ya ZAECA, CAG na Idara ya Nyaraka. Taasisi ambazo
zinajukumu zito la kulinda na kusimamia rasili mali za Serikali ili zisipotee
kwa watu wabadhirifu na watu wasiokuwa na imani na maendeleo ya Nchi yetu.
Mheshimiwa Spika;
Kamati inasisitiza tena kwa mara nyengine na kuishauri
Serikali kwamba juhudi za makusudi zifanyike za kupatiwa vitendea kazi ili kuhakikisha
malengo ya Taasisi hizi yanafikiwa kwa mujibu wa taratibu walizopangiwa.
Mheshimiwa Spika;
Katika
kukabiliana na changamoto hii kwa upande wa Chuo cha Utawala wa Umma, Zanzibar,
Kamati inashauri katika bajeti inayokuja Chuo kizingatie mahitaji ya watu wenye
ulemavu kwa kuwapatia vifaa vya kisasa vya kujifunzia na kuboresha miundombinu
ya majengo ili iweze kuwa rafiki kwao.
Vile
vile kamati inaagiza chuo kuajiri wakalimani ambao watasaidia wanafunzi wenye
ulemavu wa uziwi kupata nafasi ya kujifunza kwa uhakika na urahisi zaidi
tofauti na ilivyo sasa kutokana na uhaba wa vitendea kazi na wataalamu. Kamati
pia inakitaka Chuo hiki kujiimarisha tawi la Pemba kwani hivi sasa yupo
mtumishi mmoja tu wa kudumu.
Mheshimiwa Spika;
Kamati
imesikitishwa sana juu ya maendeleo ya baadhi ya Taasisi zetu ambazo
zinatuongoza na kulinda haki za raia wa Nchi hii, huku tukiamini kwamba baadhi
ya Taasisi hizo ni mihimili mikuu katika kuchunga na kulinda haki za wananchi.
Ni dhahiri kuwa mazingira mazuri na salama kwa watendaji wa Taasisi hizo ndio
yatakayo leta tija kwa maendeleo ya Nchi.
Mheshimiwa Spika;
Kuwepo kwa uchakavu
na ubovu wa majengo ya Mahkama kwa Unguja na Pemba kunarudisha nyuma nguvu na
ari ya utendaji katika mazingira yao ya kazi. Kamati
ilifanya ziara katika Mahkama ya Mfenesini na Mwanakwerekwe na kuona hali ya majengo
yake hayafai kabisa, hayana nafasi, lakini hadi leo bado Mahkama ya Mfenesini wana
choo kimoja ambacho wanatumia Mahakimu, Makarani, mahabusu na wananchi
wanaokuja katika kufatilia kesi zao; hali hii pia ipo katika Mahkama ya
Mwanakwerekwe.
Mheshimiwa
Spika;
Kwa upande wa Mahkama ya Wete nayo hairidhishi katika mazingira
yake ya kazi kwani jengo lake ni bovu na halina nafasi ya kutosha pamoja na
miundombinu mibovu ya maji. Mahkama hii inakabiliwa na ukosefu wa vitendea kazi
kama vile makabati ya kuhifadhia majalada, ukosefu wa kompyuta ambapo ofisi
nzima ipo kompyuta moja tu, lakini hata meza na viti vimechakaa kiasi ambacho havifai
kwa matumizi ya Mahkama.
Mheshimiwa
Spika;
Kamati
imebaini kuwepo kwa ongezeko kubwa la kesi za ubakaji na udhalilishaji na jamii
kutokua na uelewa wa kutosha juu ya kesi hizo, lawama kubwa ya ikiwahusisha
Mahkama na Muendesha Mashtaka wa Serikali na Jeshi la Polisi.
Mheshimiwa Spika;
Kamati inaagiza
kufanyiwa kazi suala zima la kesi za udhalilishaji katika jamii kwani limekua
ni changamoto kubwa inayoikabili jamii na hata kukosekana imani kwa chombo cha
mahkama na jamii. Adiha, Kamati inasisitiza kuwepo kwa mashirikiano mazuri
wakati wa uendeshaji wa kesi za udhalilishaji kwa Jeshi la Polisi, DPP na
Mahkama kwa kuhakikisha wamesimamia vyema upatikanaji wa ushahidi ambao utawatia
hatiani watendaji wa kesi hizi bila kujali utafutaji wa suluhu unaopelekwa
kutoka jamii ya waathirika. Pia, ni vyema Serikali kuziangalia na kuzifanyia
marekebisho sheria ili adhabu ya wabakaji iwe kubwa kuliko ilivyo sasa.
Mheshimiwa Spika;
Vile vile, Kamati
inaagiza ofisi ya Mufti kuimarisha mashirikiano yake na ofisi ya DPP katika kuangalia
kesi za Walimu wa Madrasa ili kuweza kujua na kupata taarifa juu ya kesi hizo.
Kamati inaishauri ofisi ya Mufti itoe maagizo ya barua kwa Maimamu wote Unguja
na Pemba ili watoe elimu ndani ya Miskiti yao kwa lengo la kuisaidia jamii juu
ya kuepuka na janga la vitendo vya ngono za jinsia moja.
Mheshimiwa Spika;
Kamati inaziagiza Idara na Taasisi ambazo
bahazijafungua Ofisi zao Kisiwani Pemba zifanye hivyo katika mwaka huu wa
fedha.
Mheshimiwa Spika;
Kamati yetu
inahisi kuwa pamoja na juhudi za Serikali kusimamia utekelezaji wa majukumu ya
watumishi wake, bado kuna changamoto ya wataalamu katika Idara na Taasisi mbali
mbali za Serikali kitu ambacho kinaleta ukakasi katika ufanikishaji wa malengo
ya maendeleo.
Mheshimiwa Spika;
Kutokana na
changamoto hii Kamati inaishauri wizara kwa kushirikiana na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kuwasomesha watumishi wake katika ngazi mbali mbali za kielimu
pamoja na kuajiri watu ambao ni wazalendo na wenye sifa za kutosha katika
maeneo husika.
Mheshimiwa Spika;
Kamati yetu imebaini kuwa lipo tatizo la
upatikanaji wa ajira pamoja na tatizo sugu na la muda mrefu la wafanyakazi
waliofikia umri wa kustaafu kutokufanya hivyo. Kamati inashauri kwamba Serikali
iweke wazi Kada ambazo zitaruhusiwa kuongezewa muda wa kazi wafanyakazi wake
waliofikia umri wa kustaafu badala ya kuangalia umaarufu wa mfanyakazi wa
sehemu husika. Hatua hii itasaidia kutoa ajira kwa vijana wapya ili nao watoe
mchango wao katika ujenzi wa maendeleo ya Nchi yao.
WIZARA YA NCHI (OR) TAWALA ZA MIKOA, SERIKALI ZA
MITAA NA IDARA MAALUM ZA SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR
Mheshimiwa Spika;
Wizara ya Nchi
Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ
inaundwa na kusimamiwa ni Idara na Taasisi mbali mbali zilizogawika maeneo
makuu manne katika kutimiza majukumu yake pamoja na Ofisi ya Afisa Mdhamini
Pemba. Aidha, Kamati inaipongeza sana Serikali kwa kuweza kuwapatia fungu lao
la bajeti kwa asilimia kubwa katika Taasisi na Idara zake zote tofauti na miaka
ya nyuma. Kamati imebaini kwa Taasisi zote za wizara hii imepatiwa bajeti kwa
zaidi ya asilimia 95%.
Mheshimiwa Spika;
Kamati inaunga mkono mpango wa Serikali wa
kuleta mfumo mpya wa Ugatuzi wa Madaraka Mikoani ambao utatumika kuendeshea
Taasisi hizi. Hivyo, katika kukabiliana na changamoto ambazo zitakuja kuwa ni
kikwazo cha majukumu yao, Kamati inaagiza Serikali za Mitaa kuwapa elimu
watendaji wake wakiwemo masheha, madiwani na wafanyakazi wa kawaida kulingana
na mabadiliko ya sheria na mazingira halisi ya utekelezaji wa sheria hizo
katika mfumo wa Ugatuzi.
Mheshimiwa Spika;
Kamati
imegundua katika baadhi ya Mabaraza ya Miji pamoja na Halmashauri zake kuwepo
kwa tatizo la ukusanyaji wa Mapato pamoja na usiamamiaji mbovu uliopo kwa
wafanyabiashara na wamiliki wa mahoteli. Hali hii imejitokeza kwa upande wa
Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini A na B kwa Unguja na Baraza la Mji Wete na
Mkoani kwa Pemba. Kamati inaagiza Serikali za Mitaa kuhakikisha kuwa wamefikia
malengo waliyojipangia na wamesimamia vyema ukusanyaji wa mapato katika vyanzo
vyao mbali mbali na kuhakikisha hakuna mianya ya uvujaji wa mapato hayo ya
Serikali.
Mheshimiwa Spika;
Katika uanzishawaji
wa mfumo wa Madaraka kwa Wananchi (Ugatuzi) ni vyema Taasisi zitakazo husika na
Mfumo huu kupewa elimu ya kutosha juu utoaji wa huduma kwa wanajamii badala ya
kujikita katika uzalishaji wa mali pekee kama inavyoeleweka kwa baadhi ya
Halmashauri na Mabaraza. Vile vile, Kamati inashauri Serikali za Mitaa
kusimamia vyema utoaji wa huduma za kijamii na kuhakikisha kila mmoja
zimemfikia na kwa kiwango chenye ubora kutokana na mapato wanayokusanya kupitia
vyanzo vyao vya mapato.
Mheshimiwa Spika;
Katika ziara ya Baraza la Mji Chake-Chake,
Wete na Mkoani, Kamati imeona wamekabiliwa na tatizo kubwa la uhaba wa
wataalamu kama wahandisi, maafisa mipango na maafisa wa manunuzi na ugavi.
Kamati inashuri kwa Mabaraza haya na yale yenye matatizo sawa na haya
kuhakikisha wameajiri wataalamu wa fani mbali mbali ambao wanahitaji ili kusaidia
kuleta ufanisi wa majukumu yao.
Mheshimiwa Spika;
Kamati imebaini
kuwepo kwa baadhi ya Masheha ambao uwezo wao wa kazi umepunguwa kutokana na
ugonjwa au umri mkubwa, hivyo Kamati inaagiza wizara kufanya mabadiliko ya
Masheha ambao uwezo wao wa kazi umepungua kutokana na ugonjwa, umri mkubwa au
kukosa uadilifu katika utekelezaji wa majukumu yao.
Aidha,
Kamati inaona ni vyema kuchukuliwa hatua za haraka kwa Askari Jamii ambao
watabainika vitendo vyao haviendani na maadili ya uaskari au wanatumia vibaya
majukumu waliyopewa kwa mujibu wa taratibu walizowekewa na kusababisha kuitia
Serikali doa kwa wananchi au wageni wanaoingia Nchini, hususan maeneo ya Mji
Mkongwe ambako ni kioo cha Nchi yetu.
Mheshimiwa Spika;
Kamati ya
Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum ilifanya ziara ya kutembelea vikosi vyote
vitano (5) vya SMZ kwa upande wa Unguja na Pemba na kujionea shughuli zao mbali
mbali za kizalendo na kuleta maendeleo ndani ya Nchi.
Aidha,
Kamati inapongeza sana juhudi zinazofanywa na wapiganaji wetu wa vikosi hivi
kwa kazi ngumu na nzito wanazozifanya za kulinda usalama na kuhakikisha wanadumisha
uwepo wa amani na utulivu katika Nchi yetu.
Mheshimiwa Spika;
Sambamba na
hayo, Kamati katika ziara yake hiyo imeweza kubaini changamoto mbali mbali
zinazorudisha nyuma maendeleo ya Idara hizi kama vile:- Kuwepo kwa maslahi
madogo ya wapiganaji, kuwepo kwa majengo na vitendea kazi ambavyo havikidhi
haja ya askari wetu, ukosefu wa sare (uniform) za askari pamoja na kuwepo kwa
ukosefu wa Hatimiliki na zaidi kwa upande wa Kambi za Pemba.
Mheshimiwa Spika;
Tatizo la
ukosefu wa mahanga ya askari vituoni ni changamoto kubwa katika kufanikisha
majukumu ya vikosi vyetu kwa unguja na Pemba, kwani vipo baadhi ya vikosi
ambavyo havina kabisa makaazi ya askari wake na wanalazimika kutumia majengo
yao ya ofisi kama mahanga ya kulala kwa muda wa usiku. Hali hii imejitokeza
zaidi katika Kikosi cha Zimamoto na Uokozi Mwanakwerekwe, Wete na Uwanja wa
Ndege wa Chake-Chake Kisiwani Pemba.
Mheshimiwa Spika;
Kamati inaishauri Serikali katika kutafuta
majengo yanayostahiki ya ofisi na makaazi mazuri, uniform za askari wake pamoja
na mambo mengine, basi isiwaachie vikosi peke yake katika kupambana na
changamoto hizi na badala yake wajiwekee utaratibu maalum wa kusaidia ujenzi wa
mahanga ya askari kupitia miradi ya maendeleo kama ilivyo kwa Taasisi nyengine
za Serikali.
Mheshimiwa Spika;
Kamati inaishauri
Serikali kuangalia umuhimu wa kuanzisha kiwanda ambacho kitashughulika na
utengenezaji wa Sare na viatu vya askari wetu ili kuepusha gharama kubwa
inayotumika kwa kuagizia nje ya Nchi.
Mheshimiwa Spika;
Aidha, Kamati inashuri
Serikali kuandaa Mfuko wa Bima ya Afya kwa wafanyakazi wote wa Idara Maalum
katika kuwajengea mazingira mazuri ya utendaji wao, kwani baadhi ya askari wa vikosi
hivyo hujitolea maisha yao moja kwa moja katika kuokoa maisha ya watu, hivyo
nao wafikiriwe kwa kuangaliwa maisha yao wakati watapofikwa na matatizo ya kiafya.
Hata hivyo, Kamati inaiomba Serikali kuanzisha mfuko wa Hifadhi ya jamii kwa
upande wa vikosi vya SMZ kwa kuangalia utaratibu unaotumika wa vikosi vya
ulinzi na usalama vya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili nao
wapate kujifariji wakati wanapofikia muda wa kustaafu.
Mheshimiwa Spika;
Kamati inaagiza Wizara kufuatilia maeneo yote
ya Kambi za Idara Maalum na kusimamia upatikanaji wa Hatimiliki za maeneo hayo
hususan kwa upande wa vituo vya JKU Pemba kama vile Msaani, Chokocho na Ngezi
pamoja na kituo cha KMKM Sengenya - Mtambwe, Kojani, Tundauwa, nk. Vile vile, kwa
kuwa Serikali imeamua kurudisha tena utaratibu wa kuwapeleka vijana wa kujenga
Taifa katika vituo vya JKU, Kamati inaishauri Serikali kuwapatia vifaa na vijana
wa kutosha katika Jeshi la Kujenga Uchumi ili kuweza kuzalisha kwa kiwango
kizuri.
Mheshimiwa Spika;
Baadhi ya kambi
za vikosi vya SMZ vimekosa huduma ya Afya kama vile Chuo cha Mafunzo Kengeja,
JKU Chokocho na Chuo cha Mafunzo Tungamaa na kufuatilia maeneo ya mbali na makaazi
yao jambo ambalo ni kikwazo kwa wapiganaji wetu waliovituoni. Kamati inaona ipo
haja ya kuwa na vituo vya Afya katika kambi zote za Unguja na Pemba ambazo pia,
vituo hivyo hutumiwa na Wananchi jirani wanaoishi karibu na Kambi hizo. Aidha,
Kamati inaitaka Serikali ifanye juhudi zake zote ili Kambi ya KMKM Sengenya
ipatiwe Rada mpya kutokana na kuharibika kwa muda mrefu kwa Rada iliyokuwepo
awali.
Mheshimiwa Spika;
Tatizo la kutoshirikishwa kwa maafisa wa
vikosi vya Pemba katika uandaaji wa Bajeti za Idara zao pamoja na tatizo la
kutokuwa na sub-vote kwa upande wa vikosi vilivyopo Pemba, imekuwa ni
changamoto kubwa katika kufanikisha miradi yao na hivyo kushindwa kufikia
malengo yaliyokusudiwa. Aidha, Kamati inaiagiza Wizara ya Nchi (OR) Tawala za
Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ kuhakikisha wanasimamia vikosi
vyote vya zoni ya Pemba kupatiwa Voti zao wenyewe na kuachana na mfumo wa
kufikiriwa matumizi kwa kutengewa kiasi kidogo cha fedha ambazo hazisaidii chochote
katika kutatua matatizo yao pamoja na kuendesha kazi za vikosi. Pia ni vyema
kwa maafisa wa vikosi hivyo zone ya Pemba washirikishwe wakati wa uwandaaji wa
Bajeti ya vikosi vyao.
HITIMISHO
Katika
kutimiza wajibu na majukumu yake Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara
Maalum, imeitumia vyema Kanuni ya 106 (1) ya mwaka 2016 na kutoa ushauri na
maelekezo ambayo matumaini yetu ni kuleta ufanisi katika ukamilishaji wa
majukumu ya kila siku kwa Serikali, kupitia Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais
Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa pamoja na Wizara ya Nchi
Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maaalumu za SMZ.
Aidha,
Kamati inashauri kwamba wakati Kamati inapofanya ziara zake za kikazi basi
awepo Waziri au Katibu Mkuu wa Wizara husika ili kujua matatizo yanayokabili Idara
na Taasisi zao.
Kamati
inawashukuru sana Mheshimiwa Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Katibu wa
Baraza la Wawakilishi Zanzibar pamoja na watendaji wengine wote wa Afisi ya
Baraza la Wawakilishi waliochangia kwa njia moja ama nyengine katika
kufanikisha majukumu ya utekelezaji wa kazi za Kamati hii.
Mheshimiwa Spika; NAOMBA KUTO HOJA
Ahsante;
(Mhe. Machano
Othman Said)
Mwenyekiti,
Kamati ya
Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum
Baraza la
Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment