Habari za Punde

Rais Dk Shein akutana na Balozi wa Nambia nchini

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi DK.Ali Mohamed Shein akisalimiana na mgeni wake Balozi wa Namibia katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe,Theresia Samaria Balozi wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.]30/05/2017.

 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi DK.Ali Mohamed Shein akizungumza na mgeni wake  Balozi wa Namibia katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe,Theresia Samaria Balozi wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.]30/05/2017.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi DK.Ali Mohamed Shein akifuatana na  mgeni wake  Balozi wa Namibia katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe,Theresia Samaria Balozi baada ya mazungumzo yao wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.]30/05/2017.


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                               30.05.2017
---
RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa ipo haja kwa Zanzibar kushirikiana na Namibia katika kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo biashara na uvuvi hatua ambayo itaimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati ya Tanzania na nchi hiyo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa  Namibia  katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Bi Theresia Samaria.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Samaria kuwa Zanzibar na Namibia  zina mambo mengi ya kushirikiana kwa pamoja ambayo yanaweza kuleta mafanikio makubwa kwa pande zote mbili.

Dk. Shein alieleza kuwa  uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Namibia ni njia moja wapo kubwa itakayopelekea kuimarika zaidi kwa mahusiano na mashirikiano hayo hasa katika sekta za maendeleo ikiwemo biashara na uvuvi.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa kutokana na nchi hiyo kupiga hatua kubwa katika sekta ya uvuvi, itakuwa ni muwafaka zaidi hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar imezungukwa na bahari ya Hindi na hivi sasa imejiwekea mikakati mikubwa katika kuimarisha sekta hiyo hasa katika uvuvi wa bahari kuu.

Aliongeza kuwa, kwa upande wa sekta ya biashara pande hizo mbili zinaweza kuimarisha na kuendeleza sekta hiyo hasa ikizingatiwa kuwa nchi zote hizo zimepakana na Bahari ya Hindi hivyo ni rahisi zikatumia usafiri wa majini.

Dk. Shein alieleza kuwa katika kuhakikisha Zanzibar inaimarika katika sekta ya biashara ikiwa ni pamoja na usafiri na usafirishaji imo katika mikakati ya kujenga bandari yake mpya ya Mpigaduri ambayo itasaidia zaidi kuimarisha sekta hiyo kwani itakuwa kubwa na itaweza kutoa huduma bora zaidi kuliko bandari iliyopo hivi sasa.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tayari imenunua meli yake mpya ya MV Mapinduzi II ambayo kwa mashirikiano ya pamoja baada ya Serikali kulifanyia kazi suala hilo inaweza kufanya safari kati ya Zanzibar na Namibia hatua ambayo itaimarisha sekta ya biasahara na hata sekta ya utalii.

Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya mashirikiano ya sekta hizo mbili muhimu, nchi hizo zinaweza kuimarisha ushirikiano katika sekta ya elimu, afya pamoja na kuanzisha ziara za kutembeleana kati ya viongozi, wataalamu pamoja na watendaji wa pande mbili hizo ili kukuza uhusiano, kupanua wigo wa kitaalamu na kimaendeleo kwa manufaa ya pande zote mbili.

Nae Balozi wa Namibia katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bi Theresia Samaria alimueleza Dk. Shein kuwa Namibia itaendelea na dhamira yake ya kuimarisha zaidi uhusiano wa kidugu uliopo kati yake na Tanzania ikiwemo Zanzibar ambao umejengwa kabla na baada ya uhuru wa nchi hiyo wa mwaka 1990.

Balozi Samaria alitumia fursa hiyo kufikisha salamu za Rais wa nchi yake Rais Hage Geingob kwa Dk. Shein ambapo alisisitiza kuwa nchi hiyo itaendeleza ushirikiano wake na kukuza uhusiano wa kihistoria na Zanzibar.

Katika maelezo yake Balozi Samaria alimueleza Dk. Shein, kuwa ni vyema nchi za bara la Afrika zikashirikiana katika sekta  za maendeleo kwani anaona fahari iwapo nchi yake itakuza ushirikiano na Zanzibar hasa katika sekta ya biashara.

Alieleza kuwa kwa upande wake ameona kuna faida nyingi zinaweza kupatikana katika sekta ya biashara iwapo mashirikiano yatakuwepo hasa ikizingatiwa kuwa Zanzibar imekuwa ikizalisha mazao mbali mbali  ambayo kwa nchi yake yanahitajika kwa kiwango kikubwa .

Aidha, Balozi Samaria alieleza kuwa mashirikiano katika sekta ya uvuvi pamoja na biashara  kati ya nchi yake na Zanzibar yanaweza kupata mafanikio hasa ikizingatiwa kuwa nchi yake imepiga hatua kubwa katika kupambana na uhalifu baharini.

Aliongeza kuwa nchi hizo zinaweza kushirikiana katika sekta kadhaa za maendeleo hasa ikizingatiwa Namibia imelingana  na Zanzibar kutokana na kupitiwa wa Bahari ya Hindi kwa upande wake wa Mashariki na kupelekea shughuli za uvuvi kuimarika zaidi.

Balozi Samaria alieleza kuwa utekelezaji wa Sera ya Diplomasia ya Uchumi kutaimarisha hatua za kukuza uhusiano  na ushirikiano katika sekta za maendeleo kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar na Namibia.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.