NA HAJI NASSOR, PEMBA
MJASIRIAMALI wa mboga mboga na
matunda ya biashara, Mkubwa Ali Mkubwa mkaazi wa Vitongoji wilaya ya Chakechake
kisiwani Pemba, amesema anawashangaa vijana wanaopanga foleni kusubiri ajira ya
serikali, na kukipa mgongo kilimo.
Alisema
huu sio wakati tena kwa vijana kupanga foleni kwenye ngazi za maofisi ya
serikali, kwa kusubiri ajira zisizotosha, na badala yake wakijpanga vyema
kwenye kilimo wanaweza kupata mafanikio ya haraka.
Akizungumza
na mwandishi wa habari hizi shambani kwakwe Makaani Shehia ya Vitongoji wilaya
ya Chakechake, alisema hakuna serikali inayowatosheleza wananchi wake kiajira,
hivyo ni vyema kwa vijana wakajikusanya ili kuendesha kilimo.
Mjasiriamali
huyo, alisema kwenye kilimo sifa yake kubwa hakuna kusubiri mwisho wa mawezi
matumizi yake, bali ni wakati wowote, baada mazao kupevuka, jambo ambalo ndio
njia rahisi ya kupungaza ukali wa maisha.
“Mimi
hata leo ukiniambia niache kilimo niendele serikali, wala sikukilizi maana sasa
ndimu, tungule, vitango, vitunguu maji, mchicha na migomba ndio utajiri wangumkubwa”,alifafanua.
Mjasiriamali
huyo anaemilika shamba la mchanganyiko wa mboga mboga mbali mbali , lenye ekari
zaidi ya mbili na nusu, alieleza kuwa, kwa msimu mmoja wa uvunaji hujipatia
wastani kati ya shilingi milioni mbili (2,000,000), na kwa msimu wa mwaka huu
malengo yake yamepata mtikisiko kutokana na soko kuanza kupwaya.
Alieleza
kuwa kwa sasa ndimu zenye thamani ya zaidi ya shilingi 600,000, vitango vyenye
thamani ya shilingi 200,000, tungule zenye thamani ya shilingi 800,000 na gunia
mbili na nusu za vitunguu maji anavyotarajia kuvuna, soko lake anamashaka nalo.
“Unajua
kila msimu wa uvunaji kipindi kama hichi, huwa tayari wateja wameanza
kujitokeza hadi kufuata bidhaa huku kwenye shamba, lakini kwa msimu huu mambo
sio mazuri na hasara iko njiani kunifika’’,alieleza.
Katika
hatua nyengine mjasiriamali huyo ameziomba taasisi zenye kutoa mikopo kwa
wafanyabiashara kuacha kuweka riba, kwani kufanya hivyo huwakosesha wengine
haki hiyo.
Hafife
Juma Hamad aliejiriwa na mjasiriamali huyo kwa shughuli mbali mbali, amesema
maisha yake yamebadilika kiasi, hasa kwa vile hana wasiwasi wa kusaidia familia
yake kifedha.
“Hukaa
wee, lakini kisha hulipwa kati ya shilingi 150,000 hadi shilingi 200,000 ambapo
malipo hayo hutegemea na mavuno yalivyo, ambpo kwangu mimi hii ni
faraja’’,alifafanua.
Muajiriwa
mwengine kwenye shamba hilo Saada Ali Mkubwa, alisema mjasiriamali huyo, kwake
amekuwa mkombozi kutokana na kumsaidia kupata ajira kwenye sekta ya kilimo.
“Mimi
hapa nipo kiajira, lakini pia najifunza jinsi ya kilimo cha kisasa kupitia
mjasiriamali huyu, lakini soko ndio tatizo maana mboga mboga zisiponunuliwa na
sisi hata kipato chetu hushuka’’,alifafanua.
Aidha
waajiriwa hao wamesema malengo yao ya baadae sio kubakia hapo, bali na wao ni
kuanzisha mboga mboga kama hizo, kwa vile wamekuwa pia wakipata ujuzi wa namna
bora ya kilimo cha mboga mboga.
Sheha
wa shehia ya Vitongoji Ayoub Suleiman Salim, amemtaka mjasiriamali huyo,
kujiunga na vikundi vya saccos, ambavyo hutoa fedha bila ya riba.
“Kama
anaona mabenki na taasisi nyengine zinazotoa mikopo yenye riba, basi ajiunge na
vikundi vya kuweka hisa, wapo wengi waliochukua mikopo mpaka shilingi 800,000
hadi shilingi milioni moja na sasa wako vizuri”,alifafanua.
Mjasiriamali
huyo alieacha kazi ya ujenzi wa nyumba na kujiingiza kwenye kilimo cha mboga
mboga, alianza na mtaji wa shilingi 500,000 na kwa sasa ameshachimba kisima na
kwa mwaka wa kwanza alipata mvuno ya shilingi 600,000 mvuno wa pili shilingi
milioni mbili, na mvuno wa tatu alipata shilingi 1,000,000 na kwa sasa
anategemea kuvuna mazao yenye thanani ya shilingi 1,000,000 ingawa inategemeana
na soko.
No comments:
Post a Comment