Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                               26.08.2017
---
UONGOZI wa Mkoa wa Kusini Pemba kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi umepongezwa kwa kuyabainisha na kuyarejesha Serikalini mashamba ya Serikali na kuagizwa kwa wale wote ambao bado wanayaficha mashamba hayo ni bora wayarejeshe wenyewe vyenginevyo wakibainika wawachukulie hatua kali za kisheria.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  aliongeza kuwa hatua hizo kali za kisheria zichukuliwe bila ya kujali wadhifa wa mtu, cheo alichonacho ama umaarufu wake.

Agizo hilo limetolewa leo na Dk. Shein huko katika ukumbi wa Makonyo, Jimbo la Wawi, Wilaya ya Chake Chake Mkoa wa Kusini Pemba wakati akitoa majumuisho ya ziara yake kwa Mkoa huo aliyoifanya kuanzia Agosti 24 mwaka huu.

Aidha, Dk. Shein aliuagiza uongozi wa Mkoa huo pamoja na Wilaya zake kusimamia vizuri ukusanyaji mapato na kushirikiana na wafanyabiashara katika kuwashajiisha ili walipe kodi na kuongeza mapato ya Serikali.

Aliwataka viongozi hao kutojiingiza katika kuwasaidia kukwepa kodi wala kuwakingia kifua kwa makosa yao wanayoyafanya katika kukwepa kulipa kodi huku akiwataka kuwashajiisha wafanyabiashara watoe risiti wanapouza bidhaa zao na kuwaelimisha wananchi wapewe risiti wanaponunua bidhaa.

Pia, Dk. Shein ameiagiza Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo kufanya mkutano maalum na Wakuu wa Mikoa na Wilaya zote za Unguja na Pemba kwa ajili ya kupanga na kupeana majukumu ya utekelezaji wa mpango wa Utalii kwa Wote huku akiuagiza uongozi wa Mkoa kushirikiana na Wizara hiyo kulishughulikia eneo la  historia la Mkamandume.

Kwa upande wa wajibu wa Chama Cha Mapinduzi, Dk. Shein ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa chama hicho kwa upande wa Zanzibar aliwataka wanaCCM kuendeleza umoja na mshikamano uliopo na kuepuka mivutano miongoni mwao na kama ipo waachane nayo kwani haina tija.

Aliwataka wanaCCM kuandaa utaratibu mzuri wa kusimamia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa CCM ya mwaka 2015-2020 sambamba na kuyatumia Matawi ya CCM kwa ajili ya kukiimarisha chama hicho na kujiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliuagiza uongozi wa Mkoa na Wilaya zake zote mbili kushirikiana na Maafisa Ukaguzi wa Elimu katika maskuli na iwapo watawabaini walimu watoro kazini na wale wanaofanya siasa skuli wamuarifu Waziri wa Eloimu na Mafunzo ya Amali ili awachukulie hatua kwa mjibu wa sheria ya Utumishi wa Umma namba 2 ya mwaka 2011.

Aidha, katika kuhakikisha kuwa majengo ya skuli yanakuwa na ubora unaotakiwa na kuweza kutumika kwa muda mrefu alitaka Wizara hiyo ya Elimu kuhakikisha majengo ya madarasa yanayojengwa yanakuwa na mazingira bora na yenye viwango.

Pia, alitoa agizo kwa uongozi wa Mkoa kuwa soko jipya linalojengwa katika eneo la Tibirinzi kuanzia jana (25.8.2017) liitwe soko la Tibirinzi badala ya soko la Katar na kuutaka uongozi huo kulisimamia suala hilo kwa nguvu zake zote bila ya kugombana na watu.

Dk. Shein alitoa wito kwa Mabaraza ya Miji ya Mkoa huo, kusimamia vizuri usafi wa Miji pamoja na mipango miji na kutaka kuendelea kuwachukulia hatua waatu wanaojenga karibu sana na barabara.

Alisisitiza kuwa Mkoa ni lazima uwe na mpango wa muda mrefu wa kulishughulikia tatizo la nafasi ya maegesho ya gari linaloendelea kujitokeza katika mji wa Chake Chake.

 Aliwataka viongozi wote wa Mkoa huo kwenda kubainisha halafu watafute mbinu ya kuiondosha hali ya wizi wa karafuu na ni vyema wakalifuatilia suala hilo ili kuujua ukweli huku akiahidi kuwa Serikali inatekeleza ahadi yake ya kumpa mkulima asilimi 80 ya bei ya soko.

Kwa kukinga ajali za barabarani zinazotokea mara kwa mara kisiwani Pemba pia, Dk. Shein alieleza kupata taarifa ya kuwepo vijana katika eneo la Chake Chake wenye kuiga nyendo za kundi la ‘T-One hasa nyakati za usiku na kuutaka Mkoa kushirikiana na Jeshi la Polisi kuwachukulia hatua wasiozingatia sheria za barabarani.

Dk. Shein. Alieleza kufurahishwa kwake na upatikanaji wa maji katika Mkoa wa Kusini Pemba ambao umefikia asilimia 83.

Dk. Shein pia, aliwapongeza wanafunzi wa kike kwa kufanya vizuri katika masomo yao na kueleza haja ya kufanywa utafiti ili kuweza kujua ni kwa nini watoto wa kiume wamekwua wakiachwa nyuma.

Katika maelezo yake Dk. Shein alieleza kutoridhishwa na kuona kuwa hakuna Mkoa hata mmoja uliotoa taarifa juu ya maendeleo ya skuli 19 za  Sekondari za Wilaya na kueleza kuwa atakuwa anafuatilia matokeo ya skuli hizo ambazo zimejengwa kwa gharama kubwa na Serikali.

Sambamba na hayo, aliupongeza uongozi wa Mkoa huo kwa kuimarisha ulizni na usalama katika kuhakikisha wananchi wanaendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii katika hali ya amani na utulivu na kuutaka uendelee kusimamia amani, umoja na mshikamano na kutoa huduma kwa wananchi bila ya ubaguzi kwani wote ni wamoja.

Aliitaka Mikoa yote ya Pemba iendeleze juhudi za kushajihisha ufugaji wa samaki katika Mikoa na maeneo mbali mbali yanayoweza kuendeleza shughuli hizo.

Dk. Shein apia, aliwataka viongozi wote wakiwemo wa Mawaziri, Wabunge, Wawakilishi, Wakuu wa Mikoa,  Makatibu Wakuu, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wilaya, Maafisa Wadhamini, viongozi wa Serikali, chama cha CCM, Masheha, Makamanda.

Dk. Shein amemaliza ziara yake katika Mikoa yote ya Unguja na Pemba iliyoanza tarehe 12 Agosti mwaka huu huko katika Mkoa wa Kaskanini Unguja ikiwa na lengo la kuangalia utekelezaji wa miradi ya maendeleo chini ya utekelezaji wa Ilani ya  Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2015-2020 pamoja na uimarishaji wa Matawi na Maskani za CCM hapa nchini.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.