Na Mwandishi Wetu
Serikali imetenga kiasi
cha shilingi bilioni kumi kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za askari polisi kote
nchini, ikiwa ni kukabiliana na changamoto ya makaazi ya askari na uchakavu wa
vituo vya polisi ili kuwawezesha askari hao kutekeleza majukumu yao kwa
ufanisi.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi
Hamad Masauni alipotembelea kijiji cha Makongoro wilaya ya Bunda mkoani Mara
kuona changamoto wanazokutana nazo askari polisi katika kutekeleza majukumu yao
ya ulinzi na usalama.
Alisema wizara iko
katika mpango maalumu wa kuboresha makazi ya askari polisi nchini huku akitoa
wito na nafasi kwa wadau wa maendeleo pia kujitokeza na kuunga mkono juhudi za
Rais Dk.John Magufuli kuboresha makazi
ya askari polisi
“Katika kukabiliana na
changamoto ya askari nchi nzima tayari tushaanza kujenga makazi ya askari wetu
tukianza na nyumba za polisi Kusini Pemba na tutaendelea na ujenzi huo wa
nyumba 400 katika mikoa mingine nchini na kutokana na hali niliyoiona hapa
Bunda basi tutatoa kipaumbele hapa”Alisema Naibu Waziri Masauni
Akizungumza wakati wa
ziara hiyo Mkuu wa Wilaya ya Bunda, Lydia Bupilipili, ametoa rai kwa wananchi
kuhakikisha wanashirikiana na serikali katika ujenzi wa makazi ya askari polisi
wilayani humo huku Mwenyekiti wa Kijiji hicho Mussa Masilu aliongeza kuwa nyumba hizo ni chakavu na zinashusha
hadhi ya Askari Polisi
Hadi sasa serikali
imeshaanza taratibu za awali ikiwemo tathmini ya ujenzi wa nyumba hizo mia nne
za askari polisi nchini ambapo mikoa mbalimbali itanufaika na ujenzi huo utakaotekelezwa kwa awamu tofauti
ukienda sambamba na ujenzi na ukarabati wa vituo vya polisi.
No comments:
Post a Comment