Habari za Punde

Serikali Yakabidhi Pikipiki 32 Kwa Maafisa Elimu Kata Katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi.

Mkuu wa Wilaya ya Moshi,Kippi Warioba akizungumza wakati wa hafla fupi ya kukabidhi pikipiki 32 kwa Maafisa Elimu kata waliopo katika wilaya ya Moshi.
Baadhi ya Mafisa Elimu Kata katika Halmashauri ya wilaya ya Moshi wakifuatilia hotuba iliyokuwa ikitolewa na Mkuu wa wilaya ya Moshi ,katika hafla fupi ya kukabidhi pikipiki kwa ajili ya kusaidia katika Sekta ya Elimu.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Moshi ,Michael Kilawila akiungumza wakati wa hafla hiyo iliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri hiyo.
Baadhi ya Maafisa Elimu kata waiwa katika hafla hiyo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Moshi,Tatu Kikwete akizungumza katika hafla hiyo.
Kaimu Afisa Elimu Halmashauri ya wilaya ya Moshi,Abdalah Komesha akisoma taarifa kuhusu makabidhiano ya pikipiki hizo ambazo zimetolewa kwa Maafisa Elimu kata hao.
Baadhi ya Maafisa Elimu kata wakiwa katika hafla hiyo.
Mwakilishi wa Mkuu wa Kikosi cha Usalama Brabarani mkoa wa Kilimanjaro,Meja Hilda Mlay akitoa elimu ya usalama barabarani kwa Maafisa Elimu kata ambao wamekabidhiwa pikipiki kwa ajili ya kurahisisha kazi zao.
Mkaguzi wa Magari wa Polisi ,Francis Arthur akitoa elimu namna ya kutumia pikipiki kwa watendaji hao.
Mkuu wa Wilaya ya Moshi,Kippi Warioba akikabidhi funguo ya  pikipiki kwa mmoja wa Maafisa Elimu kata wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya pikipiki hizo ambazo zitasaidia katika kukuza Elimu kupitia mradi wa KKK.kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Moshi,Michael Kilawila na mwisho ni Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo,Tatu Kikwete. 
Maafisa Elimu kata wakiwa wamevalia kofia ngumu ,tayari kuanza safari mara baada ya kukabidhiwa pikipiki kwa ajili ya kurahisisha utendaji kazi wao.
Sehemu ya pikipiki zilizokabidhiwa kwa Maafisa Elimu kata ,katika Halmashauri ya wilaya ya Moshi.

Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii,Kanda ya Kaskazini.
MKUU wa Wilaya ya Moshi, Kippi Warioba amesema hatarajii kupokea taarifa ya ajali, wala mwaliko wa kwenda hospitalini kumjulia hali, ofisa wa serikali aliyelazwa wodini au chini ya uangalizi maalumu (ICU) kutokana na ajali iliyosababishwa na ‘munkari’ wa kukimbiza pikipiki za umma, zaidi ya spidi 150.
Warioba aliyaeleza hayo juzi, wakati akizungumza na Waratibu wa Elimu Kata 32 waliokabidhiwa pikipiki aina ya Honda TVS, kwa ajili ya kutekeleza Mpango wa Kukuza Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu unaotambuliwa kama KKK.
“Na kwa kweli nitasikitika sana, kualikwa kumtembelea mmoja wa maofisa wetu akiwa ameumia ama amepoteza maisha, tunawahitaji kweli kweli, jamii imewekeza kwenu, serikali imewekeza kwenu mpaka mkafikia hapo mlipo kwa uwezo mlionao,
“Kada hii ya watumishi haifanyi mambo ya kihuni barabarani, na wala sitaki kusikia mara umekamatwa umebeba mkaa au umeazima pikipiki inatumika na watu wasiohusika, sijaona hata mmoja mwenye umri wa kwenda kuchezea maisha yake. Wako ambao wakiendesha wakisikia muungurumo anaamsha hisia, anaona kama ana paa, wako ambao wakiendesha na kupigwa upepo wanahisi uhuru zaidi, na ndio maana hatizami anakwenda spidi 50 hadi 150.”
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, Tatu Kikwete akitoa ufafanuzi kuhusu matumizi ya vyombo hivyo, alisema pikipiki hizo kwa kuwa ni mali ya serikali zipo taratibu lazima zifuatwe katika uendeshaji na ndio maana amaemua kumwita Mwakilishi wa Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani mkoa wa Kilimanjaro (RTO, Meja Hilda Mlay na Mkaguzi wa magari, Francis Arthur na maofisa wa Bima.
Kaimu Ofisa Elimu ya Msingi, Abdalah Komesha alisema halmashauri hiyo yenye jumla ya shule za msingi 274, imepokea pikipiki hizo zilizotolewa kupitia mradi wa Lanes kwa ajili ya kufanya ufuatiliaji wa utendaji kazi katika shule zilizopo katika kila kata.
“Hizi pikipiki ni lazima zitumike ndani ya kata husika na kama ni nje ya kata, iwe kwa kibali maalumu kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji, lakini pia itatakiwa kutumika siku za kazi tu na kama ni nje ya utaratibu ni lazima kuwe na kibali na wala hazitakiwi kutumika kubeba mizigo mizito na abiria,”alisema Komesha
Ili kuepukana na ajali hizo kwa watumishi wa umma, Meja Mlay kutoka Ofisi ya RTO Kilimanjaro, aliwataka waratibu hao wa elimu wa kata kuomba kibali kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Moshi, Tatu Kikwete kujiunga na darasa maalumu la mafunzo ya usalama barabarani yanayotolewa na kikosi hicho.
Julai 2 mwaka huu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Seleman Jaffo na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako, walikabidhi pikipiki 2,894 kwa ajili ya waratibu wa elimu katika kata za nchi nzima kwa ajili ya kuboresha sekta hiyo.
Mwisho

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.