Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Ahutubia Katika Hafla ta Utiaji wa Saini Ikulu Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia katika hafla ya Utiaji wa Saini ya Mkataba wa Mgao wa Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia, baada ya utiiji wa saini hiyo pia alihudhuria Mtawala wa Ras Al Rakhaimah Sheikh Saud Bin Saqr Al Qasim na Viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, hafla hiyo imefanyika katika viwanja vya Ikulu Zanzibar.23/10/2018.

MALENGO ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuhakikisha kuwa faida zitakazopatikana kutokana na rasilimali ya mafuta na gesi asilia zinachangia katika ukuaji wa uchumi na zinawanufaisha wananchi wote bila ya kuwatenga na kuwabagua wengine.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameyasema hayo leo katika viwanja vya Ikulu Mjini Zanzibar katika hafla ya Utiaji Saini Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia, hafla iliyofanyika katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na viongozi kutoka Ras al Khaimah.

Katika hafla hiyo ambayo mapema Rais Dk. Shein na mgeni wake Shaikh Saud Bin Saqr Al Qasimi, Mtawala wa Ras Al Khaimah walishuhudia utiaji saini wa Mkataba huo, aliwahimiza wananchi waendelee kushirikiana na kuimarisha umoja na mshikamano ili kuweza kupata mafanikio yanayotarajiwa.

Dk. Shein alisema kuwa suala la utafutaji wa mafuta na gesi asilia ni jambo linalohusu maendeleo ya Zanzibar na kamwe halitakiwi lilete mfarakano katika jamii na badala yake linatakiwa liwaunganishe wananchi.

Aliwataka wananchi kujiepusha na watu wachache ambao wameamua kulitumia jambo hilo kuwa ajenda ya kuwagawa watu jambo ambalo ni kinyume na malengo ya Serikali ya kuzishughulikia rasilimali hizo.

Aidha, Rais Dk. Shein aliendelea kuwahimiza wananchi wa Zanzibar wawe na subira kwa kutambua kwamba suala la utafutaji wa mafuta na gesi asilia ni kazi inayochukua muda mrefu.

Rais Dk. Shein alitoa shukurani kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli kwa kushirikiana nae vyema pamoja na mashirikiano mazuri yaliopo baina ya Serikali zao mbili hatua ambayo imepelekea Mkataba huo umeweza kutiwa saini.

Dk. Shein alisema kuwa Rais Magufuli ametimiza wajibu wake yeye na wasadizi wake kwa manufaa ya ndugu zao wa Zanzibar kwa kuhakikisha kwamba shughuli hiyo inafanikiwa “Nampongeza kwa dhati”, aliongeza Rais Dk. Shein.

Dk. Shein alitoa shukurani kwa Mtawala wa Ras Al Khaimah Shaikh Saud Bin Saqr Al Qasimi pamoja na ujumbe aliofuatana nao kwa kujumuika pamoja katika hafla hiyo huku akitoa shukurani maalum kwa viongozi wa Serikali ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kwa kushirikiana kwa kufanya kazi pamoja kwa lengo la kuimarisha sekta za kiuchumi na kijamii.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wake wanathamini sana jitihada za Serikali ya (UAE) katika kuimarisha maendeleo ya sekta zote muhimu ikiwemo maji,elimu, biashara, usafiri wa anga na maendeleo ya sekta ya mafuta na gesi asilia kwa kuendelea kushirikiana vizuri baina yao ppamoja na wananchi wote kwa jumla.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali zote mbili zina dhamira ya dhati ya kuendeleza suala hilo  ambapo zililazimika kufanya marekebisho ya sheria muhimu na kutunga sheria mpya zilizo bora zaidi, madhubuti na zenye kuzingatia maslahi ya pande zote mbili za Muungano.

Alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kwa hatua alizozichukua ili kuhakikisha kuwa kabla ya kustaafu kwake suala hilo linapatiwa ufunbuzi na kuondoa kero ya muda mrefu.

Rais Dk. Shein alisema kuwa tukio la utiaji saini Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia linathibitisha jinsi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba inavyotekeleza kwa mafanikio Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM, Sera zake na ahadi ambazo ziliahidiwa wakati wa kampeni mwaka 2015.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inajivunia hatua hiyo muhimu kwa maendeleo na utekelezaji wa dhamira ya kuiendeleza sekta ya Mafuta na Gesi Asili hapa Zanzibar “Tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutufikisha hapa hivi sasa tuendelee kuomba dua njema ili Mwenye Mungu atupe Baraka zaidi na aturahisishie utekelezaji wa hatua zinazofuata”.

Alisema kuwa Mkataba huo uliotiwa saini hivi leo unahusisha kitalu cha Pemba-Zanzibar tu ambacho kinajumuisha maeneo yaliyopo nchi kavu na baharini hivyo, viko vitalu ambavyo havimo katika makubaliano hayo yaliosainiwa hivi leo.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kwa kutoa nasaha kwa wananchi waendelee kushirikiana katika  kuimarisha na kuiendeleza sekta ya mafuta na gesi asilia kwani ana imani kwamba matokeo ya juhudi hizo yatakuwa na manufaa na mchango mkubwa katika kuendeleza uchumi wa Zanzibar.

Alisema kuwa kuimarika kwa uchumi ni kunawiri kwa hali na maisha ya watu wa Zanzibar hali ambayo itapelekea kuongezeka kwa Pato la Taifa na Pato la kila mwananchi jambo ambalo litanyanyua hali ya maisha yao ya kila siku.

“Hapana shaka shughuli za kiuchumi na ustawi wa jamii zitaimarika jambo hili faida yake ni mfano wa afya na kiwiliwili yaani afya inapoimarika na kiwiliwili huimarika na hunawiri….hata hivyo bado ni mapema mno kuelezea faida zote zitakazopatikana iwapo tutafanikiwa katika suala hili”,alisema Dk. Shein.

Nae Mtawala wa Ras Al Khaimah Shaikh Saud Bin Saqr Al Qasimi akitoa salamu zake kwa wananchi wa Zanzibar alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa jinsi anavyowapenda watu wa Zanzibar ikiwa ni pamoja na ufuatiliaji wake na watu kwa kufanikisha jambo hilo kwa haraka.

Alitoa shukurani kwa viongozi wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jumla kwa kufanya kazi kwa bidii kwa lengo la kujenga mustakabali na maendeleo ya watu wa Tanzania.
Mtawala huyo wa Ras al Khaimah alitoa pongezi kwa mapokezi makubwa aliyoyapata huku akipongeza juhudi kubwa zilizochukuliwa ndani ya mwaka mmoja katika kuhakikisha jambo hilo linafanikiwa.

“Tuna furaha kubwa katika nafsi zetu tunafungua ukurasa mpya wa maendeleo na mustakabali mpya wa maendeleo na tunaona fahatri kubwa sana kujenga maendeleo na mustakabali wa Zanzibar”,alisema Sheikh Al Qasimi.

Aidha, alisisitiza kuwa Ras al Khaimah pamoja na nchi zote za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) wana uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu kwa nchi za Afrika ya Mashariki ikiwemo Tanzania ambapo kwa Zanzibar wana uhusiano maalum.

Mapema   Katibu Mkuu Wizara yaArdhi, Nyumba, Maji na Nishati Ali Khalil Mirza alisema kuwa Mkataba huo ni wa kwanza wa aina yake katika historia ya Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar na huo ndio wmanzo wa miradi mingi ya Mafuta na Gesi Asilia itakayokuja yenye lengo la kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Alieleza kuwa historia fupi ya zoezi la utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia kwa Tanzania lilianza katika miaka 50 ambapo kwa upande wa Zanzibar Kampuni za British Petroleum (BP) na Shell kwa pamoja zilifanya utafiti huo kwa kuchimba visima vya utafiti kadhaa katika maeneo ya Unguja na Pemba.

Aliongeza kuwa Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji (PSA) ni Mkataba unaoingiwa baina ya Serikali na Kampuni za Kimataifa za Utafutaji, Uchimbaji na Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia ambapo hatua hatua hiyo ya leo ya kusaini Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji wa Mafuta na Gesi Asilia umepita katika hatua zote za kisheria na ni Mkataba halali kwa pande zote mbili.

Alisisitiza kuwa mnamo mwaka 2015, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania liliridhia Sheria ya Mafuta Na.21 ya mwaka 2015 ambayo imeipa Serikali ya Ma;pinduzi ya Zanzbar Mamlaka ya kushughulikia rasilimali za Mafuta na Gesi Asilia wenyewe.

Baada ya hafla hiyo, Rais Dk. Shein akiwa na mgeni wake walikula chakula cha usikua ambacho Dk. Shein alimtayarishia mgeni wake huyo na ujumbe wake.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.