Habari za Punde

Kamati ya Kudumu ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa Watembelea Ofisi ya Rais Zanzibar.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa Mhe. Panya Ali Abdallah, akizungumza na Watengaji wa Ofisi ya Rais walipofika kutembelea Ofisi hiyo kupata Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi..  

Na.Abdi Shamna Ikulu Zanzibar.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Baraza la Wawakilishi Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa Zanzibar Mhe. Panya Ali Abdalla amesema hatua ya Serikali kufanya sherehe za Mapinduzi kisiwani Pemba mwaka huu, inaakisi uwiano sawa uliopo kati ya wananchi wa visiwa vya Unguja na Pemba.

Mwenyekiti huyo amesema hayo leo wakati Kamati hiyo ilipokutana na Uongozi wa Wizara ya Nchi (OR) na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Ikulu mjini hapa, kupitia taarifa ya utekelezaji wa shughuli mbali mbali za Wizara kwa kipindi cha Julai hadi Disemba, 2018.

Amesema sherehe hizo zilizoambatana na uzinduzi wa miradi ya maendeleo, zimepanua wigo wa upatikanaji wa huduma kwa wananchi wa Pemba pamoja na wafanyabiashara kupata fursa muhimu ya kuendesha shughuli zao.

Alisema ni jambo la faraja kwa wananchi wa kisiwa hicho kufikiwa na matukio matatu makubwa na muhimu katika kipindi cha mwaka 2018/19, ikiwemo Kongamano la Diaspora, Siku ya Chakula Duniani pamoja na sherehe za Mapinduzi.

Aliwapongeza wana Diaspora kwa kushiriki kikamilifu katika mipango ya maendeleo ya nchi, hatua inayolenga kusaidia ukuaji wa kiuchumi pamoja na upatikanaji wa huduma za  kijamii, ikiwemo afya.

Alisema upatikanaji wa vifaa vya tiba, ikiwemo vile vinavyotumiwa na watu wenye ulemavu, unaunga mkono juhudi za serikali katika uimarishaji wa afya ya jamii nchini.

Aidha, aliipongeza Wizara hiyo kw ajuhudi kubwa zilizochukuliwa kuzifanyia matengenezo Ikulu za Chake chake na Micheweni, ikizingatiwa ugeni mkubwa uliomfikia Rais katika sherehe za Mapinduzi. 

Nae, Mjumbe wa Kamati hiyo, Ali Suleiman Ali, alipongeza juhudi zinazochukuliwa na kitengo cha Habari, Ofisi ya Rais katika utoaji wa taarifa kuhusiana na miradi mbali mbali inayoendeshwa hapa nchini.

Mjumbe huyo alishauri  juhudi zaidi zifanyike ili kupanua wigo wa utoaji wa taarifa, hususan pale panapokuwepo uzinduzi wa miradi mikubwa ya kitaifa.

"Ushauri wangu panapokuwa na uzinduzi wa miradi mbali mbali  mikubwa, uzinduzi wake ufanyike rasmi na vyombo vya habari viwepo ili kumsaidia Mheshimiwa Rais katika utekelezaji wa Ilani", alisema.

Alisema hali ilivyo hivi sasa, taarifa za matukio mengi zimekuwa hazivuki mipaka ya Visiwa vya Zanzibar na Pemba.

Aidha, Mjumbe wa Kamati hiyo Mussa Ali Mussa aliiomba Wizara hiyo kuchukuwa hatua za dharura kuufanyia ukarabati ukuta wa Ikulu ya Mkoani, unaokabiliwa na mmong'onyoko, ili kuunusuru na mvua zijazo.

Vile vile aliomba Wizara hiyo kuimarisha huduma za usafiri kwa wafanya kazi wa Wizara hiyo kisiwani Pemba ,kulifanyia matengenezo jengo la GSO na kupatiwa vifaa vya kisasa wafanyakazi wake.

Mapema, Waziri wa Wizara ya Nchi (OR) na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Issa Haji Ussi, alisema katika kipindi hicho, Wizara imefanikiwa kupata fedha kutoka Serikali kwa asilimia 94, hivyo kuwezesha kutekeleza vyema majukumu yaliopangwa.

Alizitaja  miongoni mwa kazi zilizotekelezwa kwa ufanisi na Idara za Wizara hiyo  kuwa ni pamoja na ahadi za Rais, utoaji wa taarifa, mafunzo, ujenzi wa majengo, kuimarisha usalama wa serikali, ukaguzi, mikutano na Diaspora,  pamoja na uimarishaji wa huduma za maktaba.

Kazi nyingine zilizotekelezwa katika kipindi hicho ni pamoja na uimarishaji wa maendeleo ya michezo, uhusiano wa kimatifa, ukarabati wa nyumba za viongozi, ukaguzi wa majengo na nyenginezo.  

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.