Habari za Punde

Nchi za Afrika Mashariki Zashauriwa Kuutafakari Mkataba wa EPA


Na.Grace Semfuko-MAELEZO
Nchi za kiafrika zimeshauriwa kutafakari kwa mapana zaidi kabla ya kuingia kwenye mkataba wa Mpango wa Ushirikiano wa Kiuchumi (EPA) baina ya Jumuiya za nchi mbalimbali za Afrika na Nchi za Ulaya Jumuiya za Ulaya ili kuepuka kujitokeza  mikanganyo ya mipango ya uendeshaji wao ya uchumi,  ambapo kila nchi ina vipaumbele vyake.

Hayo yamebainishwa Jijini Dar Es Salaam leo na Mtaalamu wa Uchumi, Profesa Daktari Helmut Asche wa Chuo Kikuu cha Leipzig, nchini Ujerumani, Profesa Asche amekuwa mshauri bingwa wa masuala ya uchumi mara kadhaa kwa nchi mbalimbali za Afrika.

Akiongea na waandishi wa Habari katika Ukumbi wa Mikutano wa  Kimataifa wa Julius Nyerere, alisema baadhi ya nchi za Afrika hadi sasa hazijasaini mkataba wa EPA kwa kusita na yaliyomo kwenye mkataba kwa kuwa  yanakosa manufaa kwa nchi zao. Hata hivyo baadhi ya nchi za Afrika zimekwishasaini Mkataba huo huku zingine zikiendelea kuutafakari.

Kwa upande wa Tanzania, bado haijasaini mkataba huo ingawaje wasomi na Wataalamu wa mambo ya uchumi tayari wameonyesha kutoukubali mkataba huo.

“Ni muhimu kwa Nchi za Afrika kuangalia manufaa wanayoweza kuyapata katika mkataba huo, wasikimbilie kuusaini kwani kila nchi ya Afrika ni bora kuutathmini mkataba huo ili kuepuka migongano baina ya vipaumbele vyao” alisema Profesa Asche.

Akifafanua, Profesa Asche alisema anatambua sekta binafsi ya Tanzania inavyotegemewa kuinua uchumi wa Taifa kama ilivyo kwa sekta binafsi kwenye mataifa ya Ulay, lakini ili kila mmoja anufaike kwa upande wake ana mchakato wa utekelezaji kwa vipaumbele vyake,

“Tanzania kwa mfano, inahitaji Viwanda, na hivyo viwanda vinahitaji malighafi na kipaumbele kitakuwa  kuuza  nchini na ziada nchi za nje, na si vinginevyo.”

Asche aliongeza kuwa kabla ya nchi yoyote kuusaini Mkataba wa EPA ni muhimu kuangalia utashi wake wa kisiasa na vipaumbele vyake  ikilinganisha na utashi wa malengo ya nchi yaliyomo ndani ya Mkataba huo.

Rais Dkt John Pombe Magufuli mwaka 2017 alihoji kuhusu Mkataba wa EPA na kusema ni chimbuko la ukoloni mamboleo.

Kadhalika Wabunge wa Chama Tawala na upinzani ndani wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamekuwa wakihoji manufaa yanayokusudiwa ndani ya mkataba wa EPA bna kuonesha hofu yao.

Kwa Upande wa Tanzania Mkataba huo wa mpango wa ushirikiano wa kiuchumi baina ya Jumuiya ya Nchi za Ulaya na Afrika EPA umekuwepo tangia mwaka 2007, na Oktoba 2014 Jumuiya ya Afrika Mashariki EAC na ile ya Ulaya EU walikamilisha majadiliano baina yao na walitarajia kufunga mkataba wa makubaliano mwezi Julai 2016.

Hata hivyo mwaka 2017 Wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki wengi wao katika vikao mbalimbali waliukataa mkataba huo wakiashiria kuweza kukwamisha dhamira ya mikakati kadhaa ukiwemo wa kuinua viwanda Afrika Mashariki.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.