Habari za Punde

PROF.MKENDA; TAMASHA LA URITHI FESTIVAL KUFANYIKA PAMOJA NA JAMAFEST MWAKA HUU


Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Jamafest Tanzania Bibi.Joyce Fissoo akitoa ufafanuzi wa kuwepo kwa takribani programu kumi na moja za Kiutamaduni  katika Tamasha la JAMAFEST katika kikao cha ushirikiano wa Wizara ya Maliasili na Utalii katika kuandaa Tamasha la Urithi Festival kilichofanyika leo Jijini Arusha.

Na Anitha Jonas – WHUSM 22/07/2019 Arusha.
Tamasha la Urithi Festival kwa mwaka huu kufanyika pamoja na Tamasha la Utamaduni la Jumuiya ya Afrika (JAMAFEST) jijini Dar es Salaam.

Kauli hiyo imetolewa leo Jijini Arusha na Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii Prof. Adolf Mkenda alipokuwa akifanya kikao cha pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Bibi.Susan Mlawi kuzungumza namna ya Wizara hizo zitakavyoweza kuungana kuandaa Tamasha la Urithi kama ilivyokuwa imeagizwa na Waziri Mkuu.

"Kwa mwaka huu itakuwa vyema kuyaunganisha matamasha haya mawili kwani yote yana lengo moja la kutangaza Utalii wa Kiutamaduni, na tarehe za uendeshwaji wa matamasha hayo zipo sawa" Prof.Mkenda.

Akiendelea kuzungumza katika kikao hicho Prof.Mkenda alisema kwa sasa sekta ya utalii inataka kuongeza wigo zaidi na kutangaza utalii kwa Kiutamaduni ikiwemo Vyakula vya Asili,Ngoma,Mila na Desturi za Makabila mbalimbali, lengo ikiwa ni kuonyesha ulimwengu utajiri wa Utamaduni uliyopo Tanzania,kama nchi za wenzetu wa India na China wanavyofanya.

Halikadhalika kwa upande wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Bibi.Susan Mlawi alimshukuru Katibu Mkuu huyo kwa kuridhia matamasha hayo kuunganishwa kwani lengo ni moja la kutangaza sekta ya Utalii wa Utamaduni wa Taifa.

Pamoja na hayo Bibi.Mlawi aliendelea kufafanua kuwa Tamasha la JAMAFEST  huandaliwa na kila baada ya miaka miwili na kwa mwaka huu Tanzania ndiyo mwenyeji na wizara ya Habari Utamaduni Sanaa na Michezo ndiyo mwenye jukumu la kuandaa tamasha hilo kwa sasa kama wizara yenye dhamana ya Utamaduni.

"Tamasha hili la JAMAFEST ni kubwa na tunatarajia kuwa na washiriki zaidi ya elfu moja kutoka nchi za wanachama wa Jumuiya, katika tamasha hili kutakuwa na matukio mbalimbali ambayo yataongeza chachu kwa Sanaa za Ufundi,Maigizo ya Jukwaani,ziara ya kutembelea vivutio vya Utalii,ambapo kila nchi wanachama itateua mtu mmoja wa kwenda kutembelea vivutio hivyo," alisema  Bibi.Mlawi.

Halikadhalika tamasha hilo linauwezo wa kutengeneza jukwa zuri ambalo litatangaza filamu za kiutalii za taifa kupitia shindano la Serengeti Film Festival ambalo nalo litafanyika wakati huo.

Naye mjumbe wa Kamati ya Maandalizi ya Urithi Festival Prof.Martin Mhando alisema kuunganishwa kwa matamasha haya mawili kutusaidia zaidi kutangaza utalii wa Utamaduni na pamoja na kukuza uchumi wa nchi kwa sekta ya utalii itapata fursa ya kunadi bidhaa za Kiutamaduni ikiwemo vinyago na michoro mbalimbali.

Halikadhali naye Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Jamafest Tanzania Bibi.Joyce Fissoo alisema tamasha hilo litakuwa na mambo mbalimbali ikiwemo maonyesho ya vyakula vya asili kutoka nchi wanachama,Sanaa za Ufundi,Mashindano ya Michezo ya Jadi na Maonyesho ya Mavazi ya Kiutamaduni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.