RAIS
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein
akizungumza na Uongozi wa Benki ya CRDB ukiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya
Wakurugenzi wa CRDB Ndg. Ally Hussein Laay ( kulia kwa Rais) na Mkurugenzi
Mtendaji wa Benk ya CRDB Ndg.Abdulmajid Mussa Nsekela, walipofika Ikulu Jijini
Zanzibar kwa mazungumzo na kumtambulisha Mkurugenzi Mtendaji mpya wa benki
hiyo, hafla hiyo imefanyika leo 13-2-2020.Ikulu Zanzibar
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja kwa
Benki ya CRDB kuendelea kutoa huduma zake kwa pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili
wananchi wote wafaidike na matunda ya benki
hiyo.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo, Ikulu Jijini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi
Mtendaji mpya wa Benki ya CRDB Abdulmajid Mussa Nsekela aliyefika Ikulu kwa
ajili ya kujitambulisha akiwa amefuatana na uongozi wa Benki hiyo ulioongozwa
na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi Ally Hussein Laay.
Katika maelezo yake
Rais Dk. Shein aliipongeza Benki hiyo kwa kuendelea kutoa huduma zake hapa
Zanzibar sambamba na mikakati na malengo yake iliyoyaweka katika kutoa huduma
kwa wananchi pamoja na kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Rais Dk. Shein alisisitiza
haja kwa Benki hiyo kuongeza matawi yake hapa Zanzibar pamoja na kuipongeza
azma yake ya kushirikiana na Serikali katika kuendeleza na kuimarisha miradi
mbali mbali ya maendeleo.
Pia, Rais Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Benki hiyo kwa mipango waliyoipanga ya
kuhakikisha Benki hiyo inaleta tija kwa nchi na wananchi wake huku akieleza
matarajio yake makubwa katika uongozi wa Mkurugenzi huyo mpya wa Benki hiyo ya
CRDB.
Alisisitiza kuwa iwapo
Benki hiyo itaendelea kufanya kazi zake
kwa ufanisi zaidi Benki nyengine hapa nchini zitaweza kupanua wigo kutoka Benki
hiyo hatua ambayo itapelekea kufuatwa ile dhana ya uzalendo kwani wananchi,
Makampuni na hata Serikali wataitumia benki hiyo ikiwemo kukopa fedha badala ya
kwenda kukopa kwenye benki za nje ya nchi.
Aidha, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Benki ni taasisi ya kiuchumi hivyo, kuongezeka kwa benki hapa
Zanzibar ambapo hivi sasa zipo Benki 13 kutaendelea kuongeza ushindani wa
kibiashara sambamba na kukuza uchumi wa Zanzibar ambao umekuwa ukiimarika kila
uchao.
Katika maelezo yake
Rais Dk. Shein alieleza uzoefu alionao wa Benki hiyo kutokana na shughuli zake
inazozifanya kwa muda mrefu hapa nchini ikiwa ni pamoja na kuunga mkono sekta
mbali mbali za maendeleo ikiwemo kilimo, afya, viwanda, biashara, miundombinu
ya barabara, wajasiriamali na mambo mengineyo.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein aliuhakikishia uongozi wa Benki hiyo ya CRDB kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Benki hiyo.
Nae Mkurugenzi
Mtendaji mpya wa Benki ya CRDB Abdulmajid Mussa Nsekela alimueleza Rais Dk.
Shein kuwa atahakikisha anatekeleza vyema majukumu yake ili benki hiyo iendelee
kupata mafanikio zaidi.
Alieleza jinsi Benki
hiyo inavyofanya kazi zake hapa Zanzibar pamoja na Tanzania Bara na kueleza
azma ya Benki ya CRDB ya kuunga mkono miradi mbali mbali ya maendeleo hapa
Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Aliongeza kuwa Benki
hiyo inayomilikiwa na Serikali imekwua ikipata mafanikio makubwa katika utoaji
wake wa huduma hali ambayo ilitokana na hatua iliyochukuliwa ya kwenda kwa
wananchi.
Alieleza kuwa kwa
upande wa Zanzibar Benki hiyo ina matawi mawili hapa Zanzibar ambapo tawi moja
liko Unguja na jengine liko Pemba na ina wafanyakazi 42 hapa Zanzibar na wateja
wapatao 30,062 ikiwa na Mawakala kwa ujumla 145 (128 kwa Unguja na 17 Pemba)
sambamba na kutoa huduma za kifedha katika uwanja wa ndege wa Abeid Amani
Karume.
Pamoja na hayo, Mkurugenzi
huyo alieleza azma ya Benki hiyo ya kufungua tawi lake jipya hapa Zanzibar huku
akionesha maeneo ambayo Benki yake imedhamiria kushirikiana na Zanzibar
yakiwemo miundombinu, kilimo, utalii na ukusanyaji mapato.
Mkurugenzi huyo pia,
alitumia fursa hiyo kumueleza Rais Dk. Shein jinsi Benki ya CRDB ilivyodhamiria
kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika miradi ya kimkakati
kwa lengo la kuendelea kuimarisha uchumi wa Zanzibar.
Mwenyekiti wa Bodi ya
Wakurugenzi Ally Hussein Laay kwa upande wake alisema kuwa Benki hiyo
inayofuata misingi ya Utawala Bora imekuwa na mikakati na Sera madhubuti katika
kuhakikisha inabadilishana madaraka huku akieleza namna Benki hiyo
inavyochangia uchumi wa Tanzania.
Aidha, alieleza
mafanikio makubwa yaliopatikana tokea kuanza kazi kwa Mkurugenzi Mtendaji mpya
Abdulmajib Mussa Nsekela ambaye amechukua nafasi ya aliyekuwa Mkurugenzi
Mtendaji wa Benki hiyo Charles Kimei ambaye amestaafu.
Mapema Waziri wa Fedha
na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa
akiutambulisha uongozi huo kwa Rais Dk. Shein alieleza jinsi Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar inavyoshirikiana na Benki hiyo ya CRDB katika mambo mbali
mbali.
Pamoja na kuchangia
maendeleo ya kiuchumi na kijamii ya nchi, Benki ya CRDB imeendelea kutumia
mfumo wake imara wa kibiashara ili kutekeleza mkakati wa kuimarisha biashara na
uendeshaji wa shughuli zake za kibenki.
Hivi karibuni Benki
hiyo imepata tuzo ya Mfuko wa Kimataifa wa Mazingira ambapo ikidhihirisha
utekelezaji wa falsafa yake, imekuwa ikiendelea na dhamira ya kutoa huduma bora
zaidi kwa wateja pamoja na bidhaa za kifedha za kisasa kwa wateja binafsi na
wakubwa kwa kutumia mifumo imara ya tehama na mtandao wake mpana wa huduma.
Azma na dira ya benki
hiyo wakati wote imelenga katika kukidhi mahitaji ya wateja huku ikitumia uwezo
wa teknolojia kutoa pato zuri kwa wanahisa pamoja na kujali jamii na jumuiya
inayowazunguka ikiwa na kauli mbiu yake isemayo “Benki inayomsikiliza mteja”.
Benki ya CRDB ni
taasisi ya kibenki nchini Tanzania iliyo na thamani kubwa ya rasilimali, mikopo
na amana za wateja ikiwa na lengo la kujipanua katika ukanda wa Afrika
Mashariki ambapo mnamo Julai 29, mwaka 2017 Benki hiyo ilizindua Tawi lake
jipya kisiwani Pemba.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment