Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Samia Suluhu Hassan akifunga Jukwaa la Nishati Tanzania katika Ukumbi wa Varde Zanzibar leo March 11,2020.
HOTUBA YA MHESHIMIWA SAMIA SULUHU HASSAN,
MAKAMU WA RAIS WA JAMUHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, WAKATI WA UFUNGAJI
WA JUKWAA LA NISHATI TANZANIA, KATIKA UKUMBI WA HOTEL VARDE - ZANZIBAR
TAREHE 11 MACHI, 2020
Mheshimiwa Simai
Mohammed Said, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Zanzibar ambaye anamwakilisha
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Zanzibar;
Mheshimiwa Dk. Medard
Kalemani, Waziri wa Nishati – Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Salama
Aboud Talib, Waziri wa Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati, Zanzibar;
Mheshimiwa Hassan
Khatib Hassan, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharib Unguja;
Mheshimiwa Jeroen
Verheul, Balozi wa Uholanzi nchini Tanzania;
Mwenyekiti wa Jukwaa
la Nishati ambaye pia ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Karume ya Sayansi na Teknolojia;
Waheshimiwa Wabunge
na Wawakilishi;
Waheshimiwa Mabalozi
wa Nchi mbalimbali mliopo;
Makatibu Wakuu na Naibu
Makatibu Wakuu wa Wizara mbalimbali za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na
Serikali ya Jamuhuri ya Muungano ya Tanzania;
Waheshimiwa Mabalozi
Wadogo mliopo Zanzibar;
Wawakilishi wa
Mashirika ya Kimataifa;
Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam;
Mkuu wa Taasisi ya
Teknolojia ya Dar es Salaam;
Wawakilishi wa Vyuo
Vikuu na Taasisi za Utafiti wa Masuala ya Teknolojia vya Uholanzi;
Wakuu wa Taasisi za
Umma na Maafisa Wengine wa Serikali;
Wawakilishi wa
Makampuni ya Nishati ya Sekta Binafsi na Mashirika yasiyo ya Kiserikali;
Washiriki wa
maonyesho;
Waandishi wa Habari;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Habari za Asubuhi (Mchana),
Kwanza kabisa, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa
kutujaalia afya njema na kuweza kujumuika katika tukio hili muhimu. Pili, napenda kumshukuru Mheshimiwa Riziki
Pembe Juma, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali - Zanzibar, kwa kunipa heshima ya kuwa mfungaji wa Mkutano wa Tatu wa Kimataifa
kuhusu Jukwaa la Nishati Tanzania, ambao umefanyika kwa siku tatu hapa
Zanzibar. Aidha, nimejulishwa kwamba mkutano wenu ulitanguliwa na maonesho ya
nishati na nishati mbadala kutoka Taasisi za Elimu ya Juu, Mashirika ya Umma,
Makampuni ya Nishati na Mashirika yasiyo ya Kiserikali yanayojishughulisha na
upatikanaji na usambazaji wa nishati mbali mbali.
Nina taarifa pia kwamba katika siku mlizokuwa hapa, zimewasilishwa mada
mbalimbali kuhusu masuala yahusuyo Nishati na washiriki wamepata nafasi ya
kubadilishana ujuzi na uzoefu kuhusu maendeleo ya nishati ulimwenguni. Nakupongezeni
sana kwa kuandaa maonesho na vile vile, kuwasilisha mada zenye mawanda mapana kuhusu
nishati ambazo bila shaka washiriki wamenufaika si tu na elimu kupitia mada hizo,
lakini pia kuona vitu na mambo mbalimbali yahusuyo nishati kwa ujumla. Hongereni sana Taasisi ya Karume ya Sayansi na
Teknolojia ambayo ndiyo Mwenyekiti wa Mkutano huu, kwa kushirikiana na Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam, kwa uratibu na mpangilio
mzuri wa uendeshaji wa mkutano huu mkubwa wenye maslahi makubwa kwa wananchi na
Taifa letu.
Washiriki na Wageni
Waalikwa;
Madhumuni ya Mkutano
huu pamoja na mambo mengine, ni kujadili upatikanaji wa nishati hususan nishati
endelevu itakayowezesha ujenzi wa uchumi wa viwanda katika nchi yetu. Nimefurahishwa
na Kaulimbiu ya Mkutano huu inayosema “ENERGY TRANSITION IN SUB SAHARAN AFRICA,
ADVANCES IN EDUCATION, INNOVATION AND RESEARCH FOR A NEW GENERATION OF ENERGY
PROFESSIONALS”.
Kaulimbiu
hii ni mahsusi kabisa na imekuja wakati ambapo nchi yetu inaweka mkazo mkubwa
katika elimu hususan masomo ya sayansi na ufundi, uvumbuzi na utafiti. Nafahamu wataalamu wameijadili kwa kina kaulimbiu
hii lakini niseme tu kuwa utekelezaji wake utahitaji utashi wa kisiasa, mipango
madhubuti na mikakati ya dhati ambayo itawianishwa na mipango ya Serikali ili
kuharakisha upatikanaji wa matokeo tunayoyatarajia.
Serikali
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
zimeweka mikakati mbalimbali ya kuwezesha kupatikana kwa nishati safi, yenye
gharama nafuu na ya uhakika, katika maeneo yote ya nchi yetu. Nishati hii itachochea kwa kiasi kikubwa
uanzishwaji na uendelezaji wa viwanda nchini na kuiwezesha nchi yetu kufikia
Malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa ya kuwa nchi ya uchumi wa kipato cha kati
ifikapo mwaka 2025. Kwa dhati kabisa
nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe
Magufuli kwa kuanzisha na kusimamia miradi mikubwa ya Nishati endelevu ambayo
haijawahi kutekelezwa tangu nchi yetu ipate uhuru. Miradi hiyo itakapomalizika
itazalisha umeme utakaoifanya Tanzania kujitegemea katika nishati na hata kuwa
na ziada ya kuuza kwa nchi za jirani.
Ndugu Washiriki wa Kongamano,
Tunapoliangalia suala la upatikanaji wa nishaji endelevu, hatuna budi kulinasibisha na Mabadiliko ya Tabianchi. Serikali zetu zinatambua umuhimu wa matumizi ya nishati endelevu siyo tu kutokana na unafuu wa gharama kwa wananchi, lakini pia ni nishati rafiki kwa mazingira. Suala la uharibifu wa mazingira hususan katika nchi za kusini mwa jangwa la Sahara kwa kiasi kikubwa linachangiwa na ukataji wa misitu kwa ajili ya kupata nishati. Tafiti zinaonesha kwamba ukataji misitu kwa ajili ya kuchoma mkaa ni chanzo kikubwa cha uharibifu wa mazingira na ekolojia ya nchi yetu. Ripoti ya Benki ya Dunia ya Hali ya Mazingira Tanzania ya mwaka 2017 imeonesha kuwa Tanzania ni moja kati ya nchi zenye kiwango kikubwa cha ukataji wa miti duniani. Inakisiwa kuwa kiasi cha hekta 483,859 za miti zimekatwa katika kipindi cha 2002 hadi 2013, hii ni wastani wa hecta 48,389 kwa mwaka.
Kutokana na ukweli
huo, ndiyo maana Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (2015 – 2020)
inaielekeza Serikali kutoa kipaumbele katika nishati za makaa ya mawe, maji (hydro), gesi asilia na nishati jadidifu
(renewable energy) inayojumuisha jua
na upepo.
Katika kuitekeleza
Ilani, leo hii, miradi mikubwa ya nishati inayotekelezwa katika nchi yetu
inalenga vyanzo endelevu nilivyovitaja hapo juu. Hivyo basi, ni jukumu lenu
kama wasomi na wataalam kuisadia Serikali kufanya tafiti zitakazowezesha
upatikanaji wa nishati endelevu kwa kutumia vyanzo visivyoharibu mazingira
yetu.
Hivyo,
kwa kuwa Mkutano huu utatoka na maazimio mahsusi, rai yangu kwenu ni kujiwekea muda
(timeframe) wenye uhalisia
utakaowezesha kujipima na kupata matokeo halisi ya utekelezaji wa maazimio hayo,
kwa kutumia vigezo vinavyopimika. Ni
vyema mkaepuka kujiwekea malengo makubwa na yasiyotekelezeka au kujiwekea
malengo madogo ambayo utekelezaji wake hautakuwa na tija kwa Taifa letu.
Serikali
zetu mbili yaani, Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar zinayasubiri kwa hamu maazimio ya Mkutano huu ili kuona
namna bora ya kusukuma utetekelezaji wake
kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vizazi vijavyo.
Ndugu Washiriki, Wageni Waalikwa,
Mabibi na Mabwana,
Nimefurahi
kuona kwamba walengwa wakubwa katika Mkutano huu ni wasomi na wataalam wetu
kutoka Vyuo Vikuu na Taasisi za elimu ya juu, ambavyo ndivyo vinavyoandaa wataalamu
wanaohusika na masuala haya ya tafiti na uvumbuzi wa teknolojia mbalimbali
zihusuzo nishati. Nafahamu zipo
changamoto za uhaba wa fedha katika kuendeleza masuala ya tafiti, ila pamoja na
changamoto hiyo bado kazi kubwa inafanyika.
Nitumie fursa hii kupongeza kazi
kubwa inayofanywa na Vyuo Vikuu na Taasisi za Elimu ya Juu hapa nchini katika
upande wa nishati. Aidha, nitoe pongezi na shukurani za dhati kwa
Vyuo Vikuu vya nchini Uholanzi kwa utayari wao wa kushirikiana na vyuo na
taasisi zetu katika kuvijengea uwezo wa kufanya tafiti zinazohusu nishati
mbadala. Ni imani yangu kuwa ushirikiano
huu utakuwa na manufaa makubwa kwa taifa letu.
Rai
yangu ni kwa Jukwaa la Nishati Tanzania kuhakikisha kuwa linaratibu vyema na
kwa ufanisi kati Taasisi za Serikali, Taasisi za Kitaaluma, Mashirika ya
Kimataifa na Wadau wa Sekta ya Nishati ili kazi zao kwa pamoja zifanikishe malengo
tuliyojiwekea kitaifa.
Ndugu Washiriki, Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Nimalizie
hotuba yangu kwa kuwapongeza watu wote ambao kwa namna moja ama nyingine wameshiriki
katika hatua mbalimbali za kuandaa maonesho pamoja na Mkutano huu. Aidha, kwa niaba ya Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Watanzania, napenda kuishukuru Serikali ya Uholanzi na
Umoja wa Vyuo Vikuu vya Uholanzi kwa kutoa msaada wa fedha za kujenga mahusiano
na ushirikiano baina ya Vyuo Vikuu vya Nchi zetu katika utaalamu na tafiti zinazohusu
nishati. Ni matumaini yangu kuwa ushirikiano huu utaendelezwa.
Sambamba
na hilo, naviagiza Vyuo Vikuu vyetu na Tasisi za Elimu ya Juu zilizoko katika
Jukwaa la Nishati Tanzania kutumia taaluma zenu ili kuhakikisha kuwa matokeo ya
tafiti mnazofanya yanatumiwa na kuleta tija kwa jamii ya Watanzania hasa walioko
vijijini, ili waweze kufaidika na matumizi ya nishati safi na ya gharama nafuu.
Kazi
hiyo ya Vichwa na Mikono yenu itakayofanikiwa
kufikisha nishati mbadala vijijini,
itasaidia sana kuacha kukata miti hovyo, na hivyo, kuachana na uharibifu
wa mazingira na kurejeleza ekolojia ya nchi yetu.
Washiriki wa Mkutano, Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Baada ya kusema hayo sasa naomba kutamka
rasmi kuwa MKUTANO WA TATU WA KIMATAIFA
KUHUSU JUKWAA LA NISHATI TANZANIA umefungwa rasmi. Nawatakia safari njema ya kurejea majumbani
kwenu na kwa wale waliotenga muda wao vizuri niwatakie utalii mwema katika
fukwe nzuri na tulivu hapa Zanzibar.
MUNGU
AIBARIKI NCHIN YETU
MUNGU
AIBARIKI NCHI YA UHOLANZI
MUNGU
ABARIKI USHIRIKIANO WETU
ASANTENI
SANA KWA KUNISIKILIZA.
No comments:
Post a Comment