Waziri
wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe akiwasilisha
bajeti ya Wizara hiyo Bungeni jijini Dodoma ambapo imetengewa kiasi cha sh.
bilioni zaidi ya 40.1 kwa mwaka huu wa fedha 2020/2021.
Na Eleuteri Mangi,
WHUSM-Dodoma
Ni miaka minne tangu Sheria
ya Huduma za Habari Namba 12 ya Mwaka 2016 imepitishwa nchini na Bunge mnamo Novemba
5, 2016 na kusainiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John
Pombe Magufuli Novemba 16 mwaka huo huo.
Miongoni mwa matakwa
ya sheria hiyo ambayo yameainishwa kuisimamia na kuiboresha tasnia ya habari na
kuifanya kuwa taaluma kamili ili iheshimike kama taaluma nyingine ni hatua kuingiza
kipengele cha kiwango cha elimu, hatua itakayowasidia kuongeza weledi katika
utendaji kazi wanataaluma hao.
Kifungu cha 67(b) cha
Sheria ya Huduma za Habari Namba 12 ya Mwaka 2016 kikisomwa kwa pamoja na
Kanuni ya 17(20(a) ya Kanuni za Sheria ya Huduma za Habari, 2017 vinawataka
wanahabari wote kujiendeleza na kuwa na sifa ya kitaaluma ya angalau Stashahada
(Diploma) ndani ya kipindi cha miaka mitano baada ya kuanza kwa Sheria hiyo
iliyoanza kutumika rasmi nchini Desemba 31, 2016.
Akiwasilisha Bungeni Hotuba
ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha kwa Mwaka 2020/2021 Waziri
wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe amesema kuwa
kipindi cha miaka mitano cha mpito kinakwisha mwezi Desemba 2021 ni vema
wanataaluma hao wajiendeleze wapate sifa za kitaaluma kwa kiwango
kilichoainishwa kisheria ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa
sheria hiyo.
“Natumia nafasi hii
kuwapongeza wengi walioitikia wito na ambao kwa sasa wanajiendeleza au
wameshamaliza masomo yao, natoa wito kwa waandishi wa habari nchini ambao bado
hawajajiendeleza kielimu kukidhi matakwa ya sheria wafanye hivyo ili waweze
kuendelea na kazi ya uandishi wa habari baada ya muda huu wa mpito kuisha” alisisitiza
Dkt. Mwakyembe.
Hakika imebaki miezi
20 kwa wanataaluma ambao bado hawajaanza kujiendeleza kielimu, sasa ni muda
muafaka kufanya hivyo ili kupata sifa za kuwa mwanataaluma kamili wa habari.
Sheria ya Huduma za
Habari imekuja wakati muafaka ambapo imekuwa ni hatua muhimu kwa tasnia ya
habari kwa kuihamisha taaluma ya hiyo kutoka fani ambayo mtu yeyote anaweza
kujinasibu nayo hadi kuwa taaluma kamili yenye sifa mahsusi, maadili
yanayojulikana pamoja na vyombo vya kusaidia kusimamia utekelezaji wake ikiwemo
Bodi ya Ithibati na Baraza Huru la Vyombo vya Habari.
Idara ya Habari
(MAELEZO), inasimamia na kuratibu shughuli za Serikali upande wa habari. Katika
kutekeleza majukumu yake, Idara hiyo imegawanyika katika sehemu tatu ambazo ni
Sehemu ya Ukusanyaji na Usambazaji wa Habari, Usajili wa Magazeti na
Mawasiliano Serikalini ambapo kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari Namba 12
ya Mwaka 2016 kifungu cha 4 (1) Mkurugenzi wa Idara ya Habari ndiye msimamizi
mkuu wa Idara hiyo.
Mkurugenzi Msaidizi
wa Idara hiyo, sehemu ya Usajili wa Magazeti, Patrick Kipangula amebainisha kuwa utekelezaji wa sheria hiyo
unaenda vizuri hatua inayoonesha kuwa kuna mwitikio mkubwa wa waandishi wa
habari kujiendeleza kielimu.
Aidha, amesema kuwa
sehemu hiyo ya Idara ndiyo yenye mamlaka ya kutoa vitambulisho vya waandishi wa
habari (Press Card) ambapo kuanzia mwezi Januari hadi Aprili 2020 vitambulisho
vya wanahabari 638 vimetolewa na kati yao takribani asilimia 80 ya vitambulisho
hivyo vya waaandishi wana sifa na wana kiwango cha elimu kinachotakiwa kwa
mujibu wa sheria yaani Stashahada katika tasnia ya habari.
Aidha, Taasisi ya
Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika (MISA-TAN) ikiwa mdau muhimu wa tasnia ya
habari nchini ambayo miongoni mwa malengo yake makuu ni kukuza, kuboresha na
kuleta utofauti wa utendaji kazi wa vyombo vya habari vikiongozwa na weledi
katika utendaji kazi wao kwa kuzingatia taaluma ya habari ikiwemo kiwango cha
elimu.
Akizungumzia hotuba
ya Waziri mwenye dhamana ya habari aliyoitoa Bungeni jijini Dodoma hivi
karibuni, Mwenyekiti wa MISA-TAN nchini Salome Kitomari amesema kuwa tangu
sheria hiyo imepitishwa na kufanya kazi nchini, taasisi hiyo imekuwa ikitoa
mafunzo na kuwasisitiza waandishi wa habari kujiendeleza kielimu ambapo kwa
upande wao wamekuwa wakitoa mafunzo mbalimbali kuhusu sheria zinazosimamia
taaluma hiyo.
“Wapo ambao walitusikia
na kufuata matakwa hayo ya kisheria na sasa wamemaliza vyuo vikuu na wengine wamemaliza
diploma, lakini kuna ambao wapo katika hatua mbalimbali ikiwemo kumalizia masomo
yao katika vyuo walivyojiunga kusoma” alisema Kitomari.
Aidha, Mwenyekiti huyo
ametoa wito kwa waandishi wa habari nchini kutimiza takwa hilo la kisheria kwani
imeshakuwa sheria tayari na haina mbadala, hivyo lazima kila mwandishi wa
habari ambaye atapenda kufanya kazi hiyo awe na elimu angalau kiwango cha
Stashahada katika tasnia ya habari.
Zaidi ya hayo,
amesema kuwa muda ulioainishwa kwa maana ya muda wa mpito uliotolewa kisheria unakaribia
kuisha kwani muda huo ulishatolewa tangu Desemba 31, 2016 na ukomo wake ni Desemba
31, 2021.
“Napenda kuwaambia
waandishi wa habari wenzangu, kama kweli unaipenda kazi yako ya uandishi wa
habari, nenda darasani ukasome ule wakati wa ujanja ujanja na kufanya mambo
mbalimbali yaende umekwisha, sasa hivi ni wakati wa kuhakikisha una cheti chako
kwa sababu itafikia wakati kama huna cheti hata ‘Press Card’ hutapata”
amesisitiza Kitomari.
Kwa upande wa usajili
wa wanachama wa MISA-TAN, Mwenyekiti huyo amesema kuwa taasisi hiyo ina wanachama
wa zamani ambao wamekuwa wakihimiza kila mara kujiendeleza kielimu na ikitokea
kunapata na kupokea wanachama wapya ambao bado wanaendelea na masomo
wanawasisitiza kumalizia masomo yao ili waweze kuwa na sifa stahiki zilizoainishwa
kisheria.
Kwa mujibu wa Kanuni
ya 17 inayofafanua Sheria ya Huduma za Habari Na. 12 ya 2016 imebainisha kuwa mtu
mwenye sifa ya kupata ithibati ya kuwa mwandishi wa habari ni pamoja na
wahariri wa habari, waandishi wa habari, watangazaji, waandishi wa habari wa
kujitegemea, wapiga picha, watayarishaji wa habari na watangazaji wa redio na runinga
wanaofanya kazi katika vyumba vya habari, watu waliofanya kazi ya kutukuka
katika tasnia ya habari pamoja na mtu mwenye shahada yoyote ambaye lazima awe
na stashahada ya tasnia ya habari.
No comments:
Post a Comment