Habari za Punde

Je Unaijua historia ya chai?













Na Ali Shaaban Juma
Chai  ni  kinywaji maarufu duniani ambapo katika baadhi ya mataifa zao hilo ni moja kati ya mazao ya biashara yanayoingiza fedha za kigeni kwa mataifa hayo.

Kihistoria, Chai ni moja kati ya vinjwaji vikongwe kabisa duniani. Wanahistoria wengi wankubaliana kuwa kinywaji hicho asili yake ni China ambako inasadikiwa kuwa kinywaji hicho kilianza kunywewa kiasi miaka 5,000 iliyopita.

Kumbukumbu hizo za kihistoria zinaeleza kuwa miaka Elfu tano iliyopita, mtawala mmoja wa China aliona majani yaliyodondoka katika chungu cha maji ya moto aliyoteleka. Mtawala huyo alionja maji hayo na ladha yake aliipenda na pia alipata uchangamfu fulani kutokana na kinywaji hicho. Hali hiyo ilitokea kwa bahati tu ambapo mtawala huyo aliendelea kunywa kinywaji hicho kwa kuchemsha majani ya mmea huo katika maji. Kuanzia hapo chai ikaanza kupata umaarufu huko China na kuwa ni kinywaji cha kawaida miongoni mwa watu wa enzi hizo.

Nadharia nyengine inaeleza kuwa kabla  ya hapo, miaka 800 baada ya kuzaliwa Nabii Issa tayari mtawala mmoja wa Kibuda aliandika historia ya matumizi ya chai. Mtawala huyo alieleza kuwa kinywaji hicho kinasaidia utulivu na usikivu katika mahubiri ya dini ya Kibuda.

Kwa upande mwengine, Wamishonari wa Kibuda huko nchini Japan enzi hizo walitumia chai kuwa ni kinywaji cha lazima katika mahubiri na ibada zao. Baadae Chai ilifika nchini India ambako pia waumini wa Kibuda walitumia kinywaji hicho wakati wa usiku wanaposimulia hadithi za Buda.

Baada ya chai kupata umaarufu huko nchini Japan, Wajapani wa enzi hizo walianzisha utamaduni wa karamu maalum ya chai iliyoitwa “Cha-no-yu” maneno ambayo tafsiri yake ni “maji ya moto kwa chai”.

Utamaduni huo ulizoeleka haraka miongoni mwa Wajapani ambapo kulitengenezwa vibaku maalum vya kutilia chai hiyo ambapo ili kuonesha heshima anayekunywa chai hiyo hutakiwa kukaa kitako na mtindo maalum.

Mwandishi wa habari na mwanahistoria mwenye asili ya Ugiriki na Ireland aitwae Lafcadio Hearn ambae ni mmoja kati ya watu wachache kutoka nje ya Japan kupata uraia wa taifa hilo enzi hizo aliandika kwa urefu kuhusiana na utamaduni huo wa Wajapan wa kunywa chai.

Biashara kati ya bara Ulaya na China na Japan ilianza katika karne ya 13 ambapo Wazungu kutoka Ulaya waliokwenda huko China na Japan kufanyabiashara walianza kupata taarifa ya kuwepo kinywaji hicho. Pole pole wafanyabiashara hao kutoka Ulaya walianza kunywa chai na kuzoea kinywaji hicho. Ingawa katika hatua hiyo chai ilikuwa bado kujulikana barani Ulaya, lakini tayari taarifa ya kuwepo mmea huo unaochemshwa na kunywea na watu ilianza kufika barani Ulaya.

Katika kipindi hicho, hakuna mfanyabiashara aliyebainisha ni vipi chai inalimwa au inapikwa huku kukiwa na maelezo tofauti kuhusu jinsi chai inavyopikwa. Kuna wale walodhani kuwa Chai ilipikwa kwa kuchemsha maji yaliyotiwa chumvi ambapo wengine walidhani kuwa kinywaji hicho kilipikwa kwa kuchemshwa maji yanayochanganywa na asali au mimea mengineyo.

Dhana hiyo ya upishi wa chai iliondoka barani Ulaya hapo mwaka 1560 pale Wamishonari wa Ureno walipoanzisha njia ya biashara kati ya China na bara Ulaya kwa kupitia Ureno na Uholanzi. Wamishonari hao walikuwa ndio watu wa mwanzo kuingiza chai barani Ulaya. Kutokana na gharama kubwa za kusafirisha chai kutoka China hadi Uholanzi enzi hizo, Chai ilikuwa ni kinywaji cha matajiri na hivyo moja kwa moja kuongeza umaarufu wa kinywaji hicho barani Ulaya hasa miongoni mwa matajiri wa Uholanzi.
Kutokana na kwamba bado chai ilikuwa ni kinywaji kipya barani Ulaya, kulikuwa na mabishano miongoni mwa madaktari, wasomi na hata waliouza dawa za kienyeji kuhusu usalama wa kinywaji hicho kwa binaadamu. Baadhi ya watu hao walitilia shaka usalama wa kinywaji hicho cheusi na kichungu. Marumbano hayo yalidumu kwa miaka kadhaa
Kutokana na kuongezeka kwa vyombo vya usafiri kiwango cha chai iliyoingizwa barani Ulaya kutoka China kiliongezeka katika miaka 1600 na hivyo kufanya kinywaji hicho kupungua bei na kuongezeka wanywaji. Baadhi ya wanyaji chai wakati huo walianza kugundua kuwa kinywaji hicho kilikuwa kikichangamsha kinyume na dhana potofu iliyokuwepo kuwa kinywaji hicho si kizuri kiafya.
Baada ya chai kuanza kupata umaarufu huko Ureno na Uholanzi, katika mwaka 1652 kinywaji hicho kilianza kuuzwa sokoni mjini London nchini Uingereza pamoja na kahawa na Kakao. Hadi kufikia mwaka 1700, Uingereza ilikuwa ikiingiza nchini humo wastani wa Ratili 240,000 za chai kutoka China. Chai ilizidi kupata umaarufu nchini Uingereza ambapo watu wa taifa hilo walikifanya kinywaji hicho kuwa rasmi wakati wa asubuhi na usiku. Ni katika kipindi hicho ambapo utamaduni wa kualika watu katika chai rasmi ya usiku ulipoanza nchini Uingereza.
Kampuni kubwa ya biashara ya Uingereza enzi hizo iitwayo “East India Trading Company” ilikuwa ndio muingizaji mkuu wa Chai nchini Uingereza kwa vile kampuni hiyo ilikuwa ikifanya misafara ya baharini kati ya Uingereza na India. Kuongezeka kwa mahitaji ya chai barani ulaya kusababisha kuwepo kwa ushirika wa kibiashara wa zao hilo kati ya Ureno, Uingereza, India na China. Kwa wakati huo, China na India walikuwa ni wazalishaji wa chai na Uingereza na Ureno walikuwa ni wanunuzi na wasafirishaji wa zao hilo kwenda barani Ulaya.
Hata hivyo kutokana na tama ya kipato kati ya washirika hao wa biashara, kulizuka sitofahamu na ndipo kampuni ya Uingereza ya East India Trading Company ilipohodhi njia ya biashara ya mwambao wa pwani ya India na kuwafukuza Wadachi na Wafaransa.
Waingereza hao badala ya kununua na kusafirisha chai, waliwalazimisha wakulima wa India kulima Mirungi waliyopeleka huko China ambako walibadilisha majani hayo kwa chai.
Biashara hiyo ya mirungi ndiyo iliyosababisha kuzuka kwa vita vya mirungi, “Opium War” katika miaka ya 1800 na kusababisha kuporomoka kwa himaya ya biashara ya chai ya  Waingereza katika bara la Asia.
Mwanzo mwa karne ya 19, chai ilisababisha mabadiliko makubwa ya kijamii barani Ulaya na Marekani. Katika mwaka 1864, mwanamke mmoja aliyemiliki duka la mikate aliweka meza za kunyea chai mbele ya duka lake na kuwabembeleza wale walonunua mikate kukaa katika viti hivyo  na kunywa chai pamoja na mikate walonunua.
Duka hilo lilipata umaarufu mkubwa ambapo pia baadhi ya watu walikutana hapo na kubadilishana mawazo. Kwa vile chai sio kilevi, mwanamke huyo hakupata kikwazo cha kuendesha biashara hiyo ambapo si muda mrefu baadae katika maeneo mengine huko nchini Uingereza mikahawa kadhaa ya chai ilianzishwa na kupata umaarufu.
Biashara ya watumwa ilifanyika kati ya bara la Amerika na Afrika ilichangia kuenea kwa zao hilo hasa katika visiwa vya Caribbean, Afrika na Marekani ambako mashamba makubwa yalianzishwa kwa kutumia vibarua watumwa. Kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya chai duniani, makampuni kadhaa makubwa yaliyouza bidhaa hiyo duniani yalianzishwa barani ulaya mwanzoni mwa karne ya 19.
Viwanda vya kusafiru na kushindika chai vilijengwa barani Ulaya ambapo zao hilo lililimwa kama mali ghafi barani Afrika na Asia na kusafirishwa nje na makampuni makubwa ya Ulaya. Baadhi ya makampuni makubwa ya Ulaya yanayouza chai duniani ni pamoja na Brooke Bond, PG Tips, Lipton na Limtex.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.