Na Maulid Yussuf WEMA
Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar imesema itaendelea kutoa elimu kwa waokaribia kustaafu Ili kujiweka vizuri katika maisha yao ya uraiyani.
AKizungumza katika hafla ya kuwaaga wastaafu waliomaliza muda wao wa utumishi Serikalini, huko katika Ukumbi wa Idara ya Elimu Mbadala na watu wazima Rahaleo, Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo Amali bwana Ali Khamis Juma amesema hali hiyo itaweza kumsaidia mstaafu kujiweka katika hali ya utayari kwenye maisha yake.
Amesema Serekali ilikuja na maamuzi hayo baada ya kuona wengi wa wanaostaafu hujisahau kuwa ipo siku watamaliza muda wa utumishi wao wa kazi, ambapo huwapelekea kupata matatizo mengi yakiwemo maradhi ya kudumu wakati wakiwa uraiyani.
Aidha amewataka wastaafu hao kwenda kujituma na sio kupumzika kwa kuwafundisha vijana kazi na nidhamu kwa ujumla ili kuendelea kuokoa vijana walipo mitaani.
Nae Mkurugezi Idara ya Elimu Mbadala na Watu Wazima bi Mashavu Ahmada Fakih amesema kuwa ingawa watumishi wanastaafu lakini bado Taifa linawahitaji, hivyo amewaomba kuendelea kulitumikia Taifa wanapokuwa uraiyani ili kuleta maendeleo nchini.
Bi Mashavu alitumia muda huo kwa kuwawasifu wastaafu hao kwa kusema kuwa wamefanya kazi kwa uzalendo na Utumishi mkubwa katika kutafuta maendeleo ya nchi na Taifa lao.
Amewasisitiza watumishi wanao endelea na kazi kufuata nyao za watumishi waliomaliza muda wao kutokana na juhudi kubwa walizokuwa nazo wakati wakiwa kazini.
Akitoa shukurani kwa niaba ya wastaafu wenziwe bwana Issa Suleiman Saleh, wameushukuru uongozi kwa maandalizi waliyowataarishia na kusema kuwa wapo tayari kutoa ushauri wao wa kiutendaji wa kazi kadri watakapohitajika ili kuleta maendeleo nchini.
Jumla ya wastaafu kumi wameangwa kutoka vitengo tofauti vya Idara ya Elimu Mbadala na Watu Wazima ikiwemo Forodhani, Rahaleo, Kituo cha Elimu mbadala Chimbuni na Mwanakwerekwe.
No comments:
Post a Comment