Habari za Punde

Waziri Mhe.Bashungwa Ameipongeza DSTV Kwa Kujali Maudhui ya Kitanzania Katika Kukuza Sanaa.

 

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe.Innocent Bashungwa ametoa pongezi kwa  Kampuni ya DSTV Tanzania kwa kuwa mstari wa mbele  kusaidia Tasnia ya Filamu nchini kupitia Chaneli zao

Waziri Bashungwa amesema hayo alipokutana na  Viongozi wa DSTV leo Julai 5, 2021 Jijini Dar es Salaam ikiwa ni ziara ya kuendeleza  mahusiano kati ya Wizara na Kampuni hiyo

“Mimi nawapongeza  DSTV kwa kuwa  mstari wa mbele katika kukuza sanaa yetu ukizingatia mmeweka Chaneli ya Maisha Magic Bongo kwaajili ya filamu na tamthiliya za kitanzania tu hii ina manufaa sana kwa wasanii wetu kama dada yangu Lamata hapa kaweza kujiajiri na kuwaajiri Watanzania wenzie wengi kama waandishi wa miswada, wapiga picha na wasanii kwa ujumla hii yote ni kutokana na DSTV kutoa mwanya kwa wasanii wetu kuonyesha kazi zao" amesema Mhe.Bashungwa.

Mhe.Bashungwa ameongeza kuwa Kampuni hiyo imesaidia  kukuza  lugha ya Kiswahili  katika Bara  la Afrika na Dunia.

Hata hivyo Waziri Bashungwa  ameiagiza COSOTA kufanya msako mkali kwa wezi wa kazi za wasanii nchini hasa wasambazaji wa Cable TV mikoani ambao hujiunga kiholela na kusambaza kwa wateja ambao hawaingizii mapato Kampuni na Serikali.

‘Swala hili la wezi (Pirates) wa maudhui na kazi za wasanii  naagiza COSOTA na BASATA kusimamia kisawa sawa na  kuwachukulia sheria haraka iwezekanavyo na nasikia kesi mnazo na wanajulikana na ushahidi mnao sasa naomba niwaagize mkalifanyie kazi hili maana hawa ndiyo wanao dhorotesha tasnia na wasanii kwa ujumla hata mapato serikali inakosa maana wanatumia njia zisizo sahihi”amesisitiza Mhe.Bashungwa.

Katika kikao hicho Mkurugenzi mtendaji wa DSTV  Jacqueline Woiso amemshukuru Waziri Bashungwa kwa kutembelea ofisi hizo ambapo  amemuomba  kusaidia kutatua changamoto za Chaneli za bure za kitanzania kwakuwa ni kikwazo kikubwa kwao kupata wateja, Na Mhe. Bashungwa ameahidi kutatua changamoto hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.