Habari za Punde

Mhe. Bashungwa- vyama vya michezo tumieni Taifa CUP kuwapata wachezaji wa bora wa Taifa.

 

Wanamichezo wanaoshiriki Kombe la Taifa Cup wakiwa katika maandamano ya Ufunguzi wa Michuano hiyo iliozinduliwa jana katika uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam.

Na John Mapepele.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Innocent l. Bashungwa ametoa wito kwa vyama vya kitaifa vya michezo, kutumia mashindano ya Taifa CUP 2021 kuchagua vipaji vya wachezaji na kuviendeleza ili kupata vipaji vitakavyounda timu za Taifa za michezo mbalimbali kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini.

Mhe. Bashungwa ameyasema hayo, leo Desemba 10,2021 wakati alipokuwa akifungua mashindano ya Taifa CUP 2021 kwenye Uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam.

Amesema azma ya Serikali ni kuhakikisha kuwa wananchi wa Tanzania, wanashiriki kikamilifu katika shughuli za michezo kwa kuwa michezo inatoa mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi hususan kwenye maeneo ya uchumi, siasa na jamii.

“Kimsingi michezo ni ajira, amani, mshikamano, afya na furaha. Kutokana na umuhimu huu wa sekta ya michezo, Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo imeamua kwa dhati kabisa, kwa kusaidiana na Vyama vya Michezo chini ya Baraza la Michezo la Taifa, kuanzisha shindano la Taifa Cup ambalo lilikuwa halipo kwa miaka kadhaa”. Amefafanua Mhe. Bashungwa.

Amesema, mashindano ya Taifa Cup 2021 yameshirikisha michezo michezo mitatu ambayo ni soka, netiboli na riadha pamoja na michezo ya jadi.

Ameongeza kuwa amefarijika kuona wananchi wa pande mbili za Muungano wameendelea kuunganishwa   na mashindano haya na wanashirikiana vyema, kupitia sekta  ya michezo, ambapo amesisitiza kuwa ana amini kuwa katika mashindano haya, kutakuwa ushindani mkubwa katika michezo yote mitatu, na aliyejiandaa vema ndie atakaye kuwa mshindi.

Kupitia hotuba yake amemshukuru Mhe. Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa dhamira yake ya dhati ya kutaka kuona sekta ya michezo, pamoja na sekta za Utamaduni na Sanaa, zinapiga hatua kubwa kwa manufaa ya Watanzania.

Amepongeza kamati ya maandalizi ya mashindano haya na viongozi wa mikoa yote iliyoleta timu zao kwenye mashindano haya, bila kujali changamoto mbalimbali katika kuandaa ikiwa ni pamoja na maandalizi ya timu, na kuzisafirisha mpaka hapa Dar es Salaam

Ametoa rai kwa wanamichezo wanaoshiriki mashindano hayoambao bado hawajachanja, kwenda kuchanja ili kujikinga na ugonjwa wa Uviko 19 na amewakumbusha watanzania wote kuchukuwa hatua za kujikinga na maambukizi ya virusi vya korona, kwa kuwa ugonjwa huo bado upo ambapo amesisitiza kuwa ni wajibu wa kila mwananchi kunachukua hatua madhubuti, kadiri ya maelekezo ya wataalamu wetu wa afya.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.