Habari za Punde

Tuwekeze kwenye teknolojia na vifaa ya vya kisasa - Dk Mwinyi

10 Oktoba, 2023

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyashauri Mashirika ya umma ya utangazaji Kusini mwa bara la Afrika kuendelea kuwekeza kwenye teknolojia ya hali ya juu kwa kuongeza vitendea kazi vya kisasa vinavyoendana na maendeleo na mabadiliko ya sayansi na teknolojia ya dunia.

Dk. Mwinyi ameyasema hayo alipofungua mkutano mkuu wa 30 wa vyombo vya utangazaji vya umma vya nchi za Kusini mwa bara la Afrika SABA, hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndenge, mkoa wa Mjini Magharibi.

Rais Dk. Mwinyi alisema Mashirika hayo hayana budi kubuni, kusimamia na kutekeleza mikakati madhubuti inayopimika ili kwenda sambamba na mabadiliko yanayojitokeza.

Alisema Afrika inashuhudia namna ya vyombo vya utangazaji vikiwemo vyombo vya umma vya utangazaji vilivyo umuhimu kwa kutoa taarifa zinazochangia maendeleo ya kiuchumi, kijamii, kisiasa, kiutamaduni na kujenga amani, utulivu, usalama na utengamano wa Afrika.

Alisema Tanzania na nchi nyengine wanachama wa SABA na bara zima la Afrika imekubaliana kuhakikisha vyombo vya utangazaji vya umma kuwa vyanzo vya uhakika vya mapato ili kuhimili changamoto za kifedha na hivyo kutimiza ipasavyo dhana ya kukuza, kulinda na kutangaza utamaduni wa Mwafrika. 

Akizungumzia kuhusu mkutano huo, Rais Dk. Mwinyi aliwasihi washiriki kujadili hoja zitakazosaidia kuweka mbele maslahi ya watu na nafasi ya Bara la Afrika katika kuandaa na kutangaza habari zinazolenga kuleta maendeleo ya kiuchumi, kisiasa, kiutamadumi na utengamano wa kijamii pamoja na kusimamia mijadala yenye mawanda mapana kwa Maslahi ya bara la Afrika na kujenga taswira njema ya bara hilo kwa yale wanayoyatangaza ndani na   nje ya Afrika.

Pia Rais Dk. Mwinyi aliwataka washiriki wa mkutano huo kutembelea na kujionea uzuri wa visiwa vya Zanzibar kwa kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo nchini ikiwemo Mji Mkongwe ambao ni mmoja wa urithi wa dunia, Mlima Kilimanjaro, Hifadhi za Taifa za Serengeti, Ngorongoro, Manyara

Hata hivyo aliwasihi SABA kuendelea kubuni na kutumia teknolojia ya kisasa ya TEHAMA, kushirikiana na kubadilishana ujuzi na uzoefu wa huduma za utangazaji kwa umma kwa manufaa ya wanufaika wa huduma hizo

Alizungumza kwenye mkutano huo Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhandisi Kundo Andrea Mathew alisema sekta ya Habari na mawasiliano na tehama ni kielelezo muhimu cha matumisi sahihi ya TEHAMA, aidha alieleza mashirika ya Umma yana jukumu la kuangalia vyanzo vya kukuza maudhui sambamba na kuyataka mashirika hayo kuendelea kubadili mifumo ya zamani (analogue) na kuja ya kidijitali ili kukuza kulinda na kuenzi maudhui ya asili kwa kutumia teknolojia ya kisasa.

Naye, Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto, Riziki Pembe Juma kwa niaba ya Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Tabia Maulid Mwita, alieleza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na wadau wa bahari ili kuendeleza sekta hiyo inayokwenda sambamba na maendeleo ya sayansi na teknolojia.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Utangaji la TBC, Ayoub Rioba Chacha alisema mbali na mambo muhimu yanayojadiliwa na mkutano huo pia ni chachu ya mabadiliko, kujifunza na kubadilishana uzoefu baina ya mashirika ya nchi wa washiriki wa mkutano huo na kwa kutumia teknolojia wamefanikiwa kusafirisha habari kimataifa.

Mkurugenzi wa Shirika la Utamgazaji Zanzibar, Ramadhan Bukini alieleza mkutano huo ni muhimu kwa shirika hilo ambapo kwasasa liko kwenye mabadiliko makubwa ya kiutendahi hasa maboresho ya usikivu wa redio na televisheni kuendana na teknolojia ya kisasa mbali na kutoa huduma bora kwa wananchi pia Shirika hilo limeanza kujiendesha kibiashara kwa lengo la kujipatia mapato.

Wakati dunia inashughulikia wimbi la mapinduzi ya nne ya viwanda inayochagizwa na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano, mkutano huo wa siku tatu umepanga kujadili masuala ya TEHAMA katika ukuaji wa uchumi wa kidijitaji kwa mataifa ya Afrika.

Huu ni mkutano wa tatu kufanyika Tanzania ambapo wa kwanza ulifanyika Dar es Salaam, wapili Arusha na huu wa Zanzibar.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.