Habari za Punde

Kutoka baraza la Wawakilishi: Kifafa cha mimba ni miongoni mwa mambo matano yanayosababisha vifo


Na Abdulla Ali na Rahma Khamis - Maelezo

Kifafa cha Mimba ni miongoni mwa mambo matano makuu yanayosababisha vifo vya moja kwa moja vya akina mama wajawazito Nchini.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mhe. Mahamoud Thabit Kombo wakati akijibu swali la mwakilishi wa nafasi za wanawake Mhe. Shadya Mohammed Suleiman katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani nje kidogo ya Mji wa Zanzibar aliyetaka kujua ni vipi wizara ya afya Zanzibar imejipanga kukabiliana na tatizo la vifo vya akina mama wajawazito vinavyotokea wakati wa kujifungua.

Amesema kuwa miongoni mwa mambo yanayosababisha vifo vya moja kwa moja vya akina mama ni pamoja na Kutokwa na damu nyingi kabla au baada ya kujifungua (Haemorrage), Shindikizo la damu wakati wa ujauzito (Hypertensive Disorder During Pregnancy), Uzazi kanadamizi (Obstructed Labour), Maambukizo kwenye mfumo mzima wa damu (Sepsis) ambavyo hupelekea kuharibika au utoaji wa mimba usio salama unaopelekea unaopelekea maambukizi kwenye mfumo mzima wa damu (Septic Abortion).

Amefahamisha kuwa Serikali kupitia Wizara yake imekuwa ikiwashajihisha sana akina mama kuanza kwenda vituo vya afya mapema kwa ajili ya kupima ujauzito ambapo mama mjamzito anatakiwa kuhudhuria kituo cha afya kila baada ya wiki 2 hadi Mwezi 1.

Ametanabahisha kuwa iwapo akina mama watakwenda vituo vya afya mapema itawapelekea kuvifahamu viashiario hatari kwa wakati ambavyo vitaweza kushughulikiwa na kutafutiwa ufumbuzi kwa muda muwafaka kama miongozo ya huduma ya dharura kwa akina mama na watoto wachanga inavyoeleza.

Hata hivyo Naibu huyo amewataka akina mama wajawazito kuhudhuria vituo vya afya mapema na kwa mpangilio maalum unaoshauriwa na wataalamu wa afya kwani kutasaidia kupunguza matatizo ya vifo kwa akina mama hao wakati na baada ya kujifungua.

Sambamba na hayo amesema Wizara yake inajitahidi kuongeza wafanyakazi katika vituo vya afya mbalimbali vilivyopo Nchini hususan Vijijini kwa mujibu wa hali ya kiuchumi itakavyoruhusu. 

 

IMETOLEWA NA HABARI MAELEZO- ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.