Na
Abdulla Ali na Rahma Khamis - Maelezo
Wananchi
wana haki ya kuwauliza Wawakilishi wao kuhusiana na Fedha wanazozipatiwa kutoka
Serikalini kwa ajili ya maendeleo ya Majimbo yao.
Hayo
ameyaeleza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais Zanzibar Mhe.
Mohamed Aboud Mohamed wakati akijibu swali la mwakilishi wa nafasi za wanawake Mhe.
Shadya Mohammed Suleiman katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani nje
kidogo ya Mji wa Zanzibar alipotaka kujua hatua zinazochukuliwa na Serikali kwa
wale wote walioshindwa kuwasilisha ripoti zao za fedha za majimbo yao.
Amesema
Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wanatakiwa kuwasilisha kwa wakati ripoti za
matumizi ya fedha za Majimbo yao wanazopatiwa na Serikali ili kuimarisha
maendeleo ya wananchi wao.
Aidha
amekiri kuwa hadi sasa Majimbo mengi bado hayajafanya marejesho ya matumizi ya
fedha za mfuko wa Mwaka wa fedha 2013/2014.
“Hata
hivyo napenda kutoa pongezi zangu za dhati kwa waheshimiwa wawakilishi wa
majimbo 3 ambayo ni Mtoni, Donge na Chambani pamoja na Kamati zao kwa kufanya
marejesho kwa Mwaka 2013/2014 kwa wakati”, ameeleza Waziri Mohamed.
Amesema
kuwa Serikali kupitia Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais inawataka waheshimiwa
kutekeleza matakwa ya Sheria ili lengo lililokusudiwa kufikiwa kwa nia ya
kuwaletea maendeleo wananchi katika maeneo yao.
Vilevile
Waziri huyo amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ina nia njema kwa
wananchi wake na ndio maana wawakilishi wao wa majimbo wanapewa kipaombele cha
kupatiwa fedha za Mfuko wa Jimbo ili ziwasaidie katika matatizo yao
madogomadogo lakini kwa masikitiko makubwa wawakilishi hao wanashindwa
kuwasilisha ripoti zao za fedha hizo jambo linalopelekea kurejesha nyuma
maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla.
Hata
hivyo amefahamisha kuwa serikali imejiwekea kuleta maendeleo katika majimbo
yake yote bila ya kuangalia kuwa majimbo hayo yanaongozwa na vyama pinzani au chama
tawala.
No comments:
Post a Comment