Habari za Punde

Naibu Waziri wa Afya Zanzibar atembelea Kambi ya Maafa Zanzibar

 Naibu Waziri wa Afya Harusi Said Suleiman akisalimiana na wawakilishi wa mashirika ya WHO na UNICEF alipowasili katika kambi ya maafa kuona mazingira ya Kambi hiyo iliyopo Skuli ya Sekondari ya Mwanakwerekwe C nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
 Naibu Waziri wa Afya Harusi Saidi Suleiman akiongozwa na Afisa Msaidizi wa kambi ya maafa Makame Khatib Makame kutembelea kambi hiyo iliopo  Skuli ya Mwanakwerekwe C.
 Mwakilishi wa WHO Zanzibar Dkt. Ghirmany Andemichael akiangalia dawa za Shirika la Msalaba mwekundu  alipofika  Ofisi yao waliofungua kutoa huduma katika kambi hiyo.  
 Afisa kutoka Shirika la WHO Zanzibar Michael Habtu akichunguza maji yanayotumika katika kambi ya maafa kujua ubora wake.

 Naibu Waziri wa Afya Harusi Said Suleiman akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji Kamisheni ya kukabiliana na maafa Zanzibar Ali Juma Hamad vidonge vya waterguard na maji ya ORS kwa ajili  kambi ya maafa, wa kwanza (kushoto) Naibu Katibu Mkuu Wizara ya  Afya Halima Maulid Salum.

Naibu Waziri wa Afya Harusi Said Suleiman akizungumza na baadhi ya wananchi waliohifadhi katika kambi ya maafa Mwanakwerekwe C.
Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar.

Na Ramadhan Ali-Maelezo Zanzibar

Maafisa wanaoshughulikia wananchi waliohifadhiwa katika kambi ya maafa Mwanakwerekwe C wameshauriwa kutoa elimu ya Afya kwa wananchi hao ili kuwaepusha na maradhi ya mlipuko ikiwemo kipindupindu.

Naibu Waziri wa Afya Bi. Harusi Said Suleiman ametoa ushauri huo alipoitembelea kambi ya maafa kuona mazingira  na matatizo yanayowakabili katika kambi hiyo akiambatana na wawakilishi wa Mashirika ya WHO na UNICEF waliopo Zanzibar.

Amesema  kambi inakusanya watu wengi wenye desturi na taratibu za maisha tofauti hivyo suala la kutoa elimu ya Afya itakayosaidia maambukizi ya maradhi ni kitu muhimu .
Amewata wananchi hao  kufuata taratibu na maelekezo ya maafisa wa kambi hiyo ikiwemo  kunywa maji yaliyotiwa dawa na kukosha mikono baada ya kutoka chooni na kabla ya kula ili wawe walimu wazuri watakaporejea kwenye makaazi yao.

Afisa Msaidizi wa Kambi ya maafa Makame Khatib Makame amemueleza Naibu Waziri wa Afya kwamba hivi sasa kambi inawatu 420 wakiwemo wanawake 240.

Amesema huduma zote muhimu zinatolewa ndani ya kambi hiyo na wameanzisha utaratibu wa kuwapeleka  na kuwarejesha watoto wanaosomo katika skuli zao.

Wananchi wanaohifadhiwa katika kambi ya maafa wameiomba Serikali kuweka utaratibu wa kuwasaidia watakaporejea katika makaazi yao kwa vile wamepoteza vifaa vingi vya matumizi baada ya nyumba zao kujaa maji.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.