Habari za Punde

CCM Zanzibar Yaipongeza SMZ Kwa Kuongeza Wastaafu Pencheni.

Na Is-haka Omar, Zanzibar. 
CHAMA Cha Mapinduzi Zanzibar kwa moyo mkunjufu kinapongeza na kuisifu kitendo kilichofanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar  kwa  kuongeza pencheni kwa Wastaafu waliomaliza utumishi wao wakipokea mshahara  wa  kima cha chini serikalini.

Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC wa Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Bi. Waride Bakari Jabu amesema ongezeko  la shilingi 50,000 ni sawa na asilimia 125 lililofanywa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, linajibu masuala mengi ya msingi ya kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Akielezea kufarajika kwake na kiwango hicho cha pencheni kilichoongezwa kwa wastaafu, Katibu huyo wa Kamati Maalum ya NEC Zanzibar amesema suala la kuongeza shilingi 50,000  hadi kufikia shilingi 90,000  kinatakiwa kupongezwa na wananchi.

Amesema kitendo hicho kilikofikiwa na Serikali (SMZ) cha kuamua kuwaongezea wastaafu wake pensheni kinalenga sio tu kuwasaidia wastaafu hao kupambana na hali ngumu ya maisha, bali pia kwa kiasi kikubwa kitaleta uwiyano wa karibu na nyongeza ya mishahara ya wafanyakazi wa Serikali liyofanyika hivi karibuni.

Ameeleza kuwa CCM pia  inaipongeza  serikali ya awamu ya saba kwa imeimarisha maslahi ya watumishi wa umma katika kuongeza viwango vya mishahara ya kima cha chini kutoka shilingi 150,000 hadi shilingi 300,000 ambalo ni ongezeko la asilimia 100,  pamoja na kutekeleza mpango wa utoaji wa pencheni jamii kwa wazee wote waliofikisha miaka 70 bila ya kujali kazi aliyokuwa akiifanya.

Hata hivyo, Bi. Waride ameiomba Serikali kupitia Wizara yenye Mamlaka ya Fedha kufanya kila linalowezekana kuhakikisha wastaafu waliokuwa na nyadhifa serikalini wanapatiwa pensheni kulingana na nyadhifa walizokuwa nazo hapo kabla.

Aidha amesema  CCM inaridhishwa na kasi ya Dkt. Shein katika Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Mwaka 2015/2020,  hivyo tunawasihi  wananchi na viongozi wa Serikali kufuata nyayo hizo kwa kumsadia kiongozi huyo ili Taifa lizidi kuimarika kiuchumi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.