STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 16.10.2017
KIKUNDI cha Taarab cha Taifa kimekonga nyoyo za hadhira
iliyohudhuria katika hafla ya Chakula maalum cha usiku kilichoandaliwa na Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa ajili ya wageni
kutoka Serikali ya Oman ambao walikuwepo nchini kwa ziara maalum ya kuimarisha
uhusiano na ushirikiano.
Hafla hiyo ambayo mgeni
rasmi alikuwa Rais Dk. Shein, ilifanyika hapo jana katika ukumbi wa zamani wa
Baraza la Wawakilishi, Kikwajuni mjini Zanzibar ambapo Makamo wa Pili wa Rais
Balozi Seif Ali Idd na Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein nao
walihudhuria.
Viongozi mbali mbali wa
Serikali ya Oman pamoja Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walihudhuria ambapo
kwa upande wa Serikali ya Oman Waziri wa Mafuta na Gesi wa nchi hiyo Dk.
Mohammed bin Hemed Al Ruhmi aliongoza ujumbe wa Oman.
Taarab hiyo ilienda
sambamba na chakula hicho maalum cha usiku kilichoandaliwa na Rais kwa ajili ya
wageni hao na kuweza kutoa burudani murua ambayo iliweza kuwafurahisha wageni
pamoja na wenyeji wa hafla hiyo.
Waimbaji wa kikundi
hicho cha Taifa cha taarab waliimba nyimbo mbali mbali za taarab zikiwemo zile
za asili ambazo hadi hivi leo bado zinaendelea kupendwa kutokana na muziki na
ala zake sambamba na ujumbe uliomo kwenye nyimbo hizo.
Waimbaji mahiri kutoka
katika kikundi hicho waliweza kutoa burudani safi ya nyimbo zao akiwemo Sabina
Bint Hassan aliyoimba nyimbo isemayo ‘Kama yalivyonipata’ nyimbo iliyotungwa na
Mzee Haji na kutiwa sauti na Abass Machano.
Professa Mohammed Ilyas
naye hakuwa nyuma katika kutoa burudani kwenye usiku huo maalum kwa kuimba
nyimbo isemayo ’Nipepee’, ambapo naye Saada Nassor aliimba wimbo uitwao ‘Kibali’, wimbo
uliotungwa na Chimbeni Kheir na kutiwa sauti na yeye mwenye Chimbeni Kheir
ambaye hivi sasa ni Mshauri wa Rais katika masuala ya utamaduni, utalii na
michezo.
Makame Faki na nyimbo
yake ‘Tumependana wenyewe’ nyimbo iliyotungwa na Nasma Khamis na kutiwa sauti na
yeye mwenyewe Makame Faki almaarufu Sauti ya Zege, nayo iliweza kukonga nyoyo
za hadhira hiyo iliyofika katika hafla hiyo sambamba na nyimbo ‘Nnae’
iliyoimbwa na Idd Suwed.
Makofi, hoihoi, nderemo na
vigeregere vilisikika katika ukumbi huo pale wageni kutoka Serikali ya Oman
walipoomba wimbo wa ‘Kama yalivyonipata’ uimbwe tena na bila ya ajizi Sabiha
Bint Hassan na kikundi chake hicho cha Taifa uliirejea nyimbo hiyo.
Akitoa neno la shukurani
katika hafla hiyo kwa niaba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Waziri wa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Issa Haji Gavu alisisitiza kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendeleza uhusiano kati yake na Serikali ya Oman kwa
mafanikio ya pande zote mbili.
Waziri Gavu aliongeza
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa upande wake itaendeleza uhusiano, ushirikiano pamoja na
umoja uliopo kati yake na Oman huku akipongeza juhudi zinazochukuliwa kwa kila
upande katika kuhakikisha malengo hayo yanafikiwa.
Aidha, Waziri Gavu alieleza
kuwa kuwepo kwa uhusiano na kukuza ushirikiano uliopo ni mbegu ya kuimarisha
umoja na mshikamano kati ya Oman na Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment