Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Mhe.Dkt. Khalid Salum Mohammed akiwasilisha Hutuba ya Mapato na Matumizi ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi katika Mkutano wa Kumi wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Chukwani Zanzibar.Kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019.
YALIYOMO
I.
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, natanguliza shukran kwa Mola wetu
muumba na muweza kwa kutujaalia sote uhai, uzima na neema nyengine
zilizotuwezesha kukutana tena alasiri hii ili kutimiza wajibu wetu muhimu kwa
jamii tunayoitumikia na kuiongoza. Wajibu huu unatokana na matakwa ya Kifungu
cha 106 cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 (kama ilivyorekebishwa) na Kifungu
cha 41(3) cha Sheria ya Fedha za Umma namba 12 ya mwaka 2016.
2.
Mheshimiwa Spika, vifungu hivyo vinamtaka Waziri
anayehusika na Fedha, kabla ya kumalizika mwaka wa Fedha, kutayarisha na
kuyawasilisha Baraza la Wawakilishi Makadirio ya Bajeti ya mwaka unaofuata. Kwa
kuwa mwaka wa Fedha wa 2017/18 unakaribia kumalizika, Mapendekezo haya ya
makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa 2018/19 yanawasilishwa ili
kutimiza matakwa hayo ya Kikatiba na Sheria.
3.
Mheshimiwa Spika, kwa sababu hiyo, na kwa heshima
kubwa, sasa naomba kutoa hoja kwamba Baraza lako tukufu likae kama Kamati
Maalum ya kujadili Mapendekezo ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka 2018/19.
4.
Mheshimiwa Spika, jamii inayorudi nyuma kwa maendeleo
yake ya kiuchumi, au yenye migogoro miongoni mwake, au baina yake na Serikali
inayoingoza, au iliyokata tamaa kwa maisha yake ya baadae ni chachu kwa
kukosekana amani ya kudumu na maendeleo ya kweli. Wakati tukielekea kukamilisha
mwaka mwengine wa fedha na wa utekelezaji wa Ilani yetu ya Uchaguzi ya mwaka
2015, nchi yetu imeendelea kupata mafanikio makubwa ya kiuchumi na kijamii; imeshuhudia
utulivu mkubwa na mashirikiano ya wananchi na Serikali yao; na imeendelea
kuleta matumaini mapya ya maisha bora zaidi kwa wananchi wake.
5.
Mheshimiwa Spika, kama ilivyo kwa nchi yoyote,
mafanikio hayo kwa kiasi kikubwa yanatokana na Serikali iliopo madarakani na imani
ya watu wa nchi kwa Serikali hiyo. Kwa hivyo mafanikio tunayoyaona kwetu hayana
budi kunasibishwa na kiongozi wetu, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi. Naomba basi nitumie fursa hii kumpongeza sana Mhe. Dkt. Ali Mohamed
Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kwa mwaka
mwengine wa uongozi thabiti, wenye hekima na subira na wa mfano. Bado
tunamuombea maisha marefu na uongozi wenye uadilifu kwa kipindi chake chote cha
kutuongoza.
6.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameendelea
kufaidika na ushauri na usaidizi wa karibu wa Makamo wake wa Pili, Mheshimiwa
Balozi Seif Ali Iddi. Nasi sote tulio katika dhamana mbalimbali pia
tumefarijika sana na uongozi na maelekezo ya mara kwa mara ya Mheshimiwa Makamo
wa Pili wa Rais. Nachukua fursa hii kutambua mchango mkubwa wa jasho na fikra
zake katika mafanikio tunayoendelea kuyapata na kumpongeza kwa dhati kwa
uongozi wake usioyumba.
7.
Mheshimiwa Spika, kwangu mimi binafsi bado naendelea
kupata heshima kubwa kwa imani ya Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kunipa heshima
ya kutumikia dhamana hii adhimu ya Waziri wa Fedha na Mipango kwa nchi yetu.
Kwangu mimi hii ni heshima kubwa sana na nitaendelea kuithamini, kuishukuru na
kuitumikia kwa uwezo wangu wote.
8.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa pili mfululizo
tunasoma mapendekezo ya Bajeti Kuu ya Taifa wakati Wizara zote zikiwa
zimeshawasilisha mapendekezo ya Bajeti zake. Kwa mara nyengine tena
tumeshuhudia mijadala ya kina katika Baraza hili kwa mapendekezo ya Bajeti
kutoka Wizara za Serikali. Ni dhahiri kuwa kama taasisi, Baraza la Wawakilishi
chini ya uongozi wako Mheshimiwa Spika limezidi kuimarika.
9.
Mheshimiwa Spika, nakupongeza sana wewe, Naibu wako Mheshimiwa
Mgeni Hassan Juma na Wenyeviti wa Baraza, Mhe. Shehe Hamad Mattar na Mhe.
Mwanaasha Khamis Juma, kwa uimara na uweledi mkubwa mnaotumia katika kuliongoza
Baraza hili. Kupitia uongozi wenu, Baraza hili tukufu na nguzo muhimu kwa
mustakabali wa Zanzibar linaweza kutimiza wajibu wake wa Kikatiba wa kuisimamia
Serikali kwa niaba ya Wananchi wote wa Pemba na Unguja.
10.
Mheshimiwa Spika, nawapongeza pia Waheshimiwa Wajumbe
wote wa Baraza lako tukufu kwa umahiri na kujitolea kwao katika kuwakilisha
Wananchi wa majimbo na, kwa ujumla wao, wananchi wote wa Zanzibar. Sisi tuliopo
katika dhamana za Serikali tunathamini sana mchango mkubwa unaotolewa na
Wajumbe wako katika kuimarisha utendaji wa Serikali na katika kukuza demokrasia
na uwajibikaji nchini.
11.
Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo ya utangulizi
na pongezi, naomba nianze kwa kupitia kwa mukhtasari hali ya uchumi wetu na
utekelezaji wa Bajeti kwa miezi tisa ya awali kwa mwaka unaoendelea wa fedha wa
2017/18.
II. HALI YA UCHUMI NA MAENDELEO
12.
Mheshimiwa Spika, maelezo ya kina ya mwenendo wa
uchumi na matokeo yake katika maendeleo yetu niliyatoa leo asubuhi wakati
nilipowasilisha mapitio ya Hali ya Uchumi kwa mwaka 2017 na utekelezaji wa
Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2017/18.
13.
Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza asubuhi, uchumi
wetu umeendelea kuonesha mwenendo mzuri. Sikusudii kurejea maelezo yote
niliyoyatoa asubuhi ya leo lakini niruhusu nigusie tena mambo muhimu ya uchumi
wetu kwa mwaka uliopita, 2017, kama ifuatavyo:
i.
Pato letu halisi la Taifa limeongezeka kwa asilimia 7.5
mwaka jana ikilinganishwa na mwaka 2016 ambapo Uchumi ulikuwa kwa asilimia 6.8.
Kasi hii ya ukuaji ni kubwa zaidi kuliko takriban nchi zote za ukanda wa Afrika
ya Mashariki na ni ukuaji mkubwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita;
ii.
Kujitokeza kiwango
cha Mfumko wa Bei cha asilimia 5.6 ambacho ni kidogo zaidi katika miaka minne
iliyopita;
iii.
Kufanikiwa kupata mzao mkubwa zaidi wa Karafuu wa Tani
8,543.9 ambazo hazijawahi kufikiwa tokea mwaka 1996/97 ambapo Tani 11,368.3 za
Karafuu zilipatikana;
iv.
Kuimarika kwa uzalishaji wa mazao ya chakula kutoka Tani
227,256 mwaka 2016 hadi Tani 304,800 mwaka 2017, sawa na ongezeko la asilimia
34.1; na
v.
Kuendelea kuimarika kwa Sekta ya Utalii ambapo Idadi ya
watalii waliotembelea Zanzibar imeongezeka kwa asilimia 15.2 kutoka watalii
376,242 wa mwaka 2016 hadi 433,474 mwaka 2017.
14.
Mheshimiwa Spika, mwenendo wetu huu wa uchumi
unapaswa kuendelezwa na kuimarishwa zaidi kwani ni chachu muhimu ya maendeleo
yetu. Tayari tunashuhudia kuimarika kwa mapato yetu ya ndani, kama
nitakavyoeleza baadae, kutokana na kuimarika kwa uchumi. Mafanikio haya ni
matokeo ya hali njema ya amani na utulivu inayovutia uwekezaji na shughuli za
biashara, Sera nzuri zilizopo, na uongozi thabiti na wa uadilifu wa Mheshimiwa Dkt.
Ali Mohamed Shein.
III. MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA
BAJETI KWA KIPINDI CHA MIEZI TISA (JULAI 2017– MACHI 2018):
a.
Makadirio ya Mapato
15.
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2017/18 Serikali ilikadiria kukusanya
jumla ya TZS 1,087.4 bilioni ikijumuisha, mapato kutokana na vyanzo vya ndani
jumla ya TZS 675.8 bilioni sawa na asilimia 21.8 ya Pato la Taifa. Kati ya
fedha hizo, jumla ya TZS 627.0 bilioni zilipangwa zitokane na makusanyo ya
vyanzo vya kodi. Kitaasisi, asilimia 55.4 ya mapato hayo yalitarajiwa kukusanywa
na Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB), sawa TZS 347.3 bilioni.
16.
Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ilikadiriwa
kukusanya TZS 258.7 bilioni sawa na asilimia 41.3 ya mapato yote ya kodi na TZS
21 bilioni, sawa na asilimia 3.3 ya mapato ya kodi, zilipangwa kukusanywa na
Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali kutokana na Kodi ya Mapato kwa wafanyakazi wa
SMT waliopo Zanzibar. Aidha, jumla ya TZS 48.8 bilioni zilitarajiwa kukusanywa
kutoka vyanzo mbalimbali visivyo vya kodi.
17.
Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa Misaada kutoka nje, kwa
mwaka 2017/18 ilikadiriwa kupokea Ruzuku ya TZS 82.2 bilioni na Mikopo ya TZS
298.3 bilioni. Hivyo, jumla ya fedha zote zilizotarajiwa kutoka nje ni TZS
380.5 bilioni.
18.
Mheshimiwa Spika, ili kuziba nakisi iliyojitokeza ya
Bajeti, Baraza lako tukufu liliidhinishia Serikali kukopa jumla ya TZS 30.0
bilioni kutoka soko la ndani ili kukidhi upungufu huo wa Bajeti.
b.
Makadirio ya Matumizi
19.
Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2017/18 Serikali ilikadiria kutumia
kiasi hicho cha TZS 1,087.4 bilioni kugharamia Bajeti yake. Jumla ya TZS 590.7
bilioni ziliidhinishwa kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS 496.6 bilioni kwa
matumizi ya kazi za maendeleo. Aidha, kati ya fedha hizo za maendeleo, TZS
116.1 bilioni ni kutokana na mapato ya ndani na TZS 380.5 bilioni kutokana na
mapato kutoka nje.
c.
Utekelezaji Halisi
20.
Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi cha miezi tisa (Julai hadi Machi 2018),
ukusanyaji wa mapato umekuwa wa kuridhisha. Kwa ujumla, Serikali imemudu
kukusanya jumla ya TZS 677.6 bilioni. Kati ya kiasi hicho, TZS 506.6 bilioni,
sawa na asilimia 74.7 ya mapato yote ni mapato ya ndani, TZS 151.0 bilioni,
sawa na asilimia 22.3 ya mapato yote ni mapato kutoka nje na TZS 20.0 bilioni
ni mikopo ya ndani, sawa na asilimia 3 ya mapato yote.
21.
Mheshimiwa Spika, Makusanyo halisi ya TZS 506.6 bilioni ni sawa na asilimia
98 ya makadirio ya kipindi hicho kati ya TZS 515.1 bilioni. Katika kipindi kama
hicho kwa mwaka uliopita (2016/2017), mapato ya ndani yalifikia jumla ya TZS
389.8 bilioni. Utendaji huu unamaanisha ukuaji wa mapato kwa TZS 116.8 bilioni
sawa na ongezeko la asilimia 30.
22.
Mheshimiwa Spika, Kati ya mapato ya ndani, mapato ya Kodi ni TZS 465.2
bilioni, sawa na asilimia 97 ya lengo la kukusanya TZS 478.5 bilioni. Mapato
yasiyo ya kodi ni TZS 41.4 bilioni. Matokeo haya yanaashiria utendaji mzuri
zaidi katika ukusanyaji wa mapato yasiyokuwa ya kodi kupitia Wizara zetu. Makusanyo
hayo ni sawa na asilimia 113 ya makadirio ya TZS 36.6 bilioni. Aidha, mapato hayo yamekuwa kwa
asilimia 75 ikilinganishwa na ukusanyaji wa TZS 23.7 bilioni kwa miezi tisa ya awali
ya mwaka uliopita.
d. Ukusanyaji
wa Mapato Kitaasisi
23.
Mheshimiwa Spika, Kwa kipindi cha mapitio, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
ilikusanya jumla ya TZS 190.5 bilioni sawa na asilimia 99 ya makadirio ya TZS 193.2
bilioni. Kwa kiwango hicho cha utendaji, makusanyo ya TRA yameongezeka kwa asilimia
25 ikilinganishwa na ukusanyaji wa kipindi kama hicho kwa mwaka 2016/2017
ambapo jumla ya TZS 152.5 bilioni zilikusanywa.
24.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB), makusanyo
halisi yamefikia TZS 258.9 bilioni sawa na asilimia 96 ya makadirio ya TZS 269.5
bilioni. Hata hivyo, ikilinganishwa na TZS 197.5 bilioni zilizokusanywa katika
kipindi kama hicho kwa mwaka wa fedha 2016/17, ZRB imeonesha ukuaji mkubwa
zaidi wa mapato wa asilimia 31.1.
25.
Mheshimiwa Spika, Makusanyo ya Kodi ya Mapato kutoka kwa wafanyakazi wa SMT
waliopo Zanzibar yalifikia TZS 15.75 bilioni sawa na asilimia 100 ya makadirio
ya kipindi hicho. Kwa mikopo katika soko la ndani, Serikali imekopa jumla ya
TZS 20.0 bilioni kupitia Hati Fungani, sawa na asilimia 66.7 ya makadirio ya
mwaka ya kukopa TZS 30.0 bilioni.
e.
Mapato ya Nje
26.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi hiki cha mapitio
(Julai – Machi 2018), Serikali imepokea, kutoka kwa nchi wahisani na Mashirika
ya fedha ya Kimataifa, jumla ya TZS 151.0 bilioni ambazo takriban ni asilimia
40 ya makadirio ya mwaka. Kati ya kiasi hicho, Ruzuku ni TZS 34.1 bilioni na
Mikopo ni TZS 116.9 bilioni. Aidha, jumla ya TZS 3.2 bilioni zilipatikana
kutokana na Misaada ya Kibajeti (General Budget Support – GBS) na TZS 2.6
bilioni kutokana na Misamaha ya Madeni (MDRI). Fedha zote zilizopatikana
kutokana na Misaada ya nje zimetumika kwa shughuli za utekelezaji wa Mpango wa
Maendeleo badala ya matumizi ya kawaida ya uendeshaji wa Serikali.
IV.
UTEKELEZAJI
WA HATUA ZA KUIMARISHA MAPATO KWA MWAKA WA FEDHA 2017/18.
27.
Mheshimiwa Spika, kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka
2017, Baraza lako liliidhinisha marekebisho katika Sheria mbalimbali kwa lengo
la kuimarisha ukusanyaji na usimamizi wa Mapato ya Serikali. Mukhtasari wa
utekelezaji wa hatua hizo ni kama ifuatavyo:
i.
Sheria
ya Mafunzo ya Amali (Vocational Training Act)
28.
Mheshimiwa Spika, Marekebisho ya kufungu cha 27 (4)
cha Sheria ya Mafunzo ya Amali (Vocational Training Act No.8 ya 2006)
yamefanywa kwa kutoa tafsiri ya “Gross Monthly Emolument” ambayo mwajiriwa hatakatwa
gharama za mafunzo pamoja na mavazi (uniforms) anazopatiwa na mwajiri wake kwa
mwezi tofauti na ilivyokuwa hapo awali. Kama ilivyotarajiwa, hatua hii haikuwa
na athari yoyote katika ukusanyaji wa mapato bali imesaidia kuleta usawa katika
mfumo wa kodi.
ii.
Sheria
ya Ajira (Employment Act.)
29.
Mheshimiwa Spika, Marekebisho yamefanywa kwenye
Kifungu cha 100 (2) cha Sheria ya Ajira (Employment Act No.11 of 2005) kwa
kuelekeza kuwa malipo yote ya mishahara kufanywa kupitia akaunti za benki za waajiriwa.
Waajiri wengi tayari wameanza kulipa mishahara ya wafanyakazi wao kupitia benki.
Hadi kufikia Machi 2018 jumla ya TZS 2.46 bilioni zimekusanywa kutokana na Kodi
zitokanazo na mshahara, sawa na asilimia 410 ya makadirio kwa mwaka.
iii.
Kanuni
za Ada ya Biashara (Trade Levy Regulations):
30.
Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeacha kutoza Ada ya
Biashara (Trade Levy) kwa uingizaji wa pembejeo za viwandani na malighafi. Tunaamini
kuwa utekelezaji wa hatua hii umeleta faraja kwa wazalishaji viwandani na utasaidia
kuimarisha uendelezaji wa viwanda nchini.
iv.
Kutungwa
kwa Sheria ya Ushuru wa Bidhaa
31.
Mheshimiwa Spika, Kama ilivoahidi, Serikali imetunga
Sheria hiyo ya Ushuru wa Bidhaa na utekelezaji wake umeanza rasmi mwezi wa Agosti
mwaka 2017. Jumla ya TZS 1.2 bilioni zimekusanywa kutokana na hatua hii katika
miezi tisa.
v.
Kufutwa
kwa Sheria ya Ushuru wa Stempu Nam. 6 Ya 1996 na Kutungwa Sheria ya Ushuru wa
Stempu
32.
Mheshimiwa Spika, Sheria mpya ya Ushuru wa Stempu
imetungwa na kuanza kutumika rasmi mwezi wa Julai 2017. Sheria hiyo imechukua
nafasi ya Sheria ya Ushuru wa Stempu namba 6 ya mwaka 1996 ambayo imefutwa. Jumla
ya TZS 0.96 bilioni zimekusanywa sawa na asilimia 240 ya makadirio ya bajeti ya
TZS 0.4 bilioni;
vi.
Kutoza VAT Kwenye Huduma za Fedha
33.
Mheshimiwa Spika, Utekelezaji wa hatua hii umeanza
rasmi mwezi wa Julai 2017. Jumla ya TZS 1.6 bilioni zimekusanywa sawa na
asilimia 45 ya makadirio ya mwaka ya TZS 3.5 bilioni.
vii.
Usajili wa Namba Binafsi za Magari
(Private Number Registration)
34.
Mheshimiwa Spika, Utekelezaji wa hatua hii umeanza
rasmi Desemba 2017 baada ya kusainiwa kwa Kanuni. Lengo la hatua hiyo
linaelekea kufikiwa kwani kwa miezi tisa hiyo hakuna mwananchi yoyote
aliyejitokeza kwa ajili ya usajili huo.
a.
MATUMIZI:
i. Jumla ya Matumizi
35.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha miezi tisa
(Julai - Machi 2018), kupitia Kamati ya Ukomo wa Matumizi, jumla ya TZS 695.0
bilioni zilikadiriwa kutumika. Kati ya matumizi hayo, TZS 461.6 bilioni ni kwa
kazi za kawaida na TZS 233.4 bilioni ni kwa kazi za maendeleo. Hadi kufikia
Machi 2018, matumizi halisi yalifikia TZS 681.6 bilioni sawa na asilimia 98 ya
makadirio ya kipindi hicho. Kati ya matumizi hayo TZS 457.1 bilioni zilitumika
kwa kazi za kawaida na TZS 224.5 bilioni kwa kazi za maendeleo.
ii. Matumizi ya kazi za
kawaida
36.
Mheshimiwa Spika, Matumizi ya kazi za kawaida kwa
kipindi cha mapitio yalifikia jumla ya TZS 457.1 bilioni. Kiwango hicho cha
matumizi kinaashiria kuongezeka kwa matumizi ya kawaida kwa asilimia 34.9
ikilinganishwa na matumizi ya kipindi kama hicho mwaka 2016/2017 ambapo jumla ya
TZS 338.8 bilioni zilitumika. Kati ya matumizi hayo, matumizi ya mishahara
yalifikia TZS 209.7 bilioni sawa na asilimia 100 ya makadirio ya kipindi hicho.
Matumizi hayo ya mishahara ni sawa na asilimia 30.2 ya matumizi yote ya kipindi
hicho na sawa na asilimia 45.8 ya matumizi yote ya kazi za kawaida. Aidha, kwa
ujumla, Matumizi ya kazi za Kawaida yanamaanisha ukuaji wa asilimia 40.3
ikilinganishwa na TZS 149.5 bilioni zilizotumika kipindi kama hicho kwa mwaka
wa fedha 2016/2017.
37.
Mheshimiwa Spika, Mwenendo mzuri wa uwezo wetu wa
kuhudumia Bajeti umejionesha pia katika matumizi ya kuendeshea Serikali (Other
Charges). Matumizi haya yameongezeka kwa asilimia 23.8 kutoka TZS 66.5 bilioni
zilizotumika katika miezi tisa ya awali ya mwaka 2016/17 hadi TZS 82.3 bilioni kwa
miezi tisa ya mwaka huu. Aidha, ikilinganishwa na makadirio ya TZS 84.1 bilioni
kwa kipindi hicho, kiwango hicho cha matumizi kinamaanisha kuwa Serikali
imemudu kutoa Shilingi 98 kati ya kila Shilingi mia moja zilizopangwa kwa ajili
ya uendeshaji wa kazi za kawaida. Haya ni mafanikio makubwa na ya kupongezwa na
kupigiwa mfano.
38.
Mheshimiwa Spika, taswira hiyo hiyo ya kuongezeka uwezo
wa kuhudumia mambo yetu imejitokeza katika utoaji wa Ruzuku kwa Taasisi zetu.
Ikilinganishwa na mwaka uliopita, fedha zilizotolewa na Serikali kwa mwaka huu
ni asilimia 68.7 zaidi. Kwa ujumla, TZS 71.2 bilioni zilitolewa sawa na
asilimia 88 ya makadirio ya TZS 80.9 bilioni ya kipindi hichi. Katika kipindi
kama hicho mwaka jana kiasi kilichotolewa kama Ruzku kwa Taasisi zetu kilifikia
TZS 42.2 bilioni tu.
39.
Mheshimiwa Spika, eneo jengine muhimu katika matumizi
ya kawaida ni matumizi kwa ajili ya huduma za Mfuko Mkuu wa Serikali. Matumizi
hayo ni kwa ajili ya kulipia viinua mgongo, pencheni, ulipaji wa Mishahara kwa
Viongozi Wakuu na waliotajwa katika Katiba, riba za mikopo ya ndani, malipo ya
Wazabuni pamoja na matumizi maalum ya Serikali yanapojitokeza. Kwa miezi tisa
ya awali ilikadiriwa kuwa tungetumia TZS 88.2 bilioni kwa huduma hizo kutoka
TZS 80.6 bilioni zilizotumika katika kipindi kama hicho mwaka uliopita. Hata
hivyo, matumizi halisi yalifikia TZS 93.9 bilioni sawa na asilimia 106 ya
makadirio yakimaanisha pia ukuaji wa asilimia 16.5.
iii. Matumizi ya kazi za
Maendeleo
40.
Mheshimiwa Spika, Katika kipindi cha mapitio, Kamati
ya Ukomo wa Matumizi ilikadiria kuwa matumizi kwa kazi za maendeleo yangefikia
TZS 233.4 bilioni. Matumizi halisi yamefikia TZS 224.5 bilioni sawa na asilimia
96 ya lengo. Matumizi kutokana na fedha zetu za ndani yameongezeka kwa asilimia
86 baada ya kufikia TZS 73.5 bilioni kutoka TZS 39.5 bilioni zilizotumika
katika kipindi kama hicho mwaka 2016/17. Hata hivyo, makadirio kutokana na
fedha za ndani yalikuwa kutumia TZS 82.4 bilioni, hivyo utendaji huo ni sawa na
asilimia 89.2 ya makadirio. Matumizi kutokana na Misaada kutoka nje yalifikia
ni TZS 151 bilioni, nayo yakionesha ongezeko la asilimia 224.7 kutoka TZS 46.5
bilioni za mwaka jana.
41.
Mheshimiwa Spika, Ongezeko hilo limetokana zaidi na
kukwamuka kwa Mradi wa Ujenzi wa Jengo jipya la abiria katika Uwanja wa Ndege
wa Zanzibar ambapo katika Kipindi hicho, Benki ya Exim ya China inayofadhili
mradi huo kwa mkopo nafuu ilitoa Dola za Marekani 35.2 milioni sawa na takriban
TZS 78.9 bilioni.
b.
Deni la Taifa
42.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kufuatilia kwa
karibu mwenendo wa Deni la Taifa kwa dhamira ya kuhakikisha linaendelea kubaki
katika kiwango kinachohimilika. Aidha, Serikali inaendelea kuheshimu misingi
mikuu (Fiscal Responsibility Principles) kama ilivyotajwa katika Kifungu cha 5
cha Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Umma, namba 12 ya mwaka 2016.
43.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Deni, misingi hiyo
inayosimamiwa na Serikali ni pamoja na hii ifuatayo:
i.
Kuhakikisha kuwa Deni la Taifa ni himilivu;
ii.
Kuhakikisha kuwa
kwa Kipindi cha Muda wa Kati, Serikali inakopa kwa ajili ya matumizi ya Kazi za
Maendeleo na sio kugharamia kazi za Kawaida;
iii.
Kusimamia rasilimali na deni la umma kwa kutowabebesha
mzigo mkubwa kizazi kijacho; na
iv.
Kuwa na akiba inayotesheleza kuhudumia deni la nje.
44.
Mheshimiwa Spika, pamoja na kuzingatia misingi hiyo,
hadi kufikia Machi 2018, Deni la Taifa limekuwa na kufikia TZS 519.7 bilioni
kutoka TZS 377.1 bilioni mwezi Machi 2017, sawa na ukuaji wa asilimia 37.8.
Katika kiasi hicho, deni la ndani ni TZS 158.3 bilioni na deni la nje ni TZS 361.4
bilioni.
45.
Mheshimiwa Spika, kuongezeka kwa deni kumechangiwa na
sababu zifuatazo:
i. Kuanza tena kutolewa fedha za mkopo kwa
ajili ya ujenzi wa jengo jipya la abiria ambapo jumla ya Dola 35.2 milioni (TZS
78.9 bilioni) zimelipwa;
ii. Mkopo mpya wa Hati Fungani wa TZS 20.0
bilioni kati ya TZS 30.0 bilioni zilizoidhinishwa kukopwa ndani;
iii. Kuongezeka kwa kiwango cha malipo ya Kiinua
Mgongo kutokana na kuimarika kwa maslahi ya Wafanyakazi. Jumla ya TZS 17.7
bilioni zimelipwa kwa wastaafu 1075 kwa mwaka 2017/2018 ukilinganisha na TZS
15.3 bilioni zilizolipwa kwa wastaafu 1,604 kwa mwaka 2016/2017; na
iv. Kwa deni la nje, athari ya mabadiliko ya
kiwango cha kubadilishia fedha.
46.
Mheshimiwa Spika, pamoja na ongezeko hilo, thamani ya
deni letu (face value) ni sawa na asilimia 16.8 ya Pato letu la Taifa la mwaka
2017. Kigezo cha uhimilivu wa deni ni kuwa lisipindukie asilimia 50 ya Pato la
Taifa kwa thamani za sasa za deni (Present Value). Hivyo, kwa kiwango cha
asilimia 16.8 kwa Pato la Taifa, bado tuna kiwango kidogo cha kudaiwa, deni letu
linahimilika na tuna fursa zaidi ya kukopa tukihitaji, kwa ajili ya kuharakisha
maendeleo yetu. Hata hivyo, bado inakusudiwa kuendelea kutumia busara
(prudence) kwa Serikali kuingia katika madeni.
i. Mapato na Matumizi ya Mfuko wa Miundombinu:
47.
Mheshimiwa Spika, Jumla ya mapato yaliyopokelewa
kutokana na Mfuko wa Miundombinu kwa kipindi cha Julai hadi Machi 2018
yamefikia TZS 24.3 bilioni sawa na asilimia 89.0 ya lengo la TZS 27.3 bilioni
kwa kipindi hicho. Mapato hayo yamejumuisha makusanyo kutoka ZRB ya TZS 17.4
bilioni sawa na asilimia 89.2 ya makadirio ya TZS 19.5 bilioni na ya TRA ya TZS
6.9 bilioni sawa na asilimia 88.5 ya makisio ya TZS 7.8 bilioni.
48.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi, jumla ya
TZS 34.90 bilioni zilikadiriwa kutumika kwa miradi iliyoorodheshwa chini ya
Mfuko wa Miundombinu kwa mwaka 2017/18. Kwa kipindi cha mapitio, TZS 20.4 bilioni
zimetumika sawa na asilimia 58.5 ya makisio.
V.
MATARAJIO
YA MAPATO NA MATUMIZI MWAKA 2017/18
a.
Matarajio ya Mapato Julai – Juni 2017/2018
49.
Mheshimiwa Spika, utekelezaji wetu wa Bajeti kwa
kipindi kilichobakia cha robo mwaka unatarajiwa kuendelea kuchangiwa na sababu
tofauti zikiwemo zifuatazo:
i.
Shughuli za kiuchumi katika
kipindi hicho;
ii.
Utendaji wa TRA, ZRB
na Wizara zetu katika kukusanya mapato;
iii.
Utekelezaji wa miradi
na upatikanaji wa fedha kutoka kwa Washirika wa Maendeleo;
iv.
Mahitaji ya matumizi
muhimu kama yatakavyojitokeza.
50.
Mheshimiwa Spika, kutokana na sababu hizo, matarajio
ni kuwa tutaumaliza mwaka kwa kukusanya jumla ya TZS 881.4 bilioni, takriban
sawa na asilimia 85 ya makadirio ya mwaka. Kati ya kiasi hicho, mapato ya ndani
ni TZS 680.0 bilioni na mapato kutoka nje ni TZS 201.4 bilioni.
51.
Mheshimiwa Spika, kutofikiwa lengo la mapato
kunatarajiwa kuchangiwa na kiwango cha upatikanaji wa misaada (Ruzuku na Mikopo)
kutoka nje. Hali ya ukusanyaji wa mapato kutoka vyanzo vyetu vya ndani
inatarajiwa kuwa nzuri ambapo jumla ya TZS 680.0 bilioni zinatarajiwa
kukusanywa. Ikilinganishwa na lengo la kukusanya TZS 675.9 bilioni kwa mwaka huu
wa fedha, matarajio ya utendaji ni sawa na asilimia 100.6 ya lengo hilo. Aidha,
kwa utendaji huo kunajitokeza ukuaji wa mapato kwa asilimia 30.5 ikilinganishwa
TZS 521 bilioni zilizokusanywa mwaka uliopita, 2016/17.
52.
Mheshimiwa Spika, Kati ya makusanyo hayo, mapato yatokanayo
na kodi ni TZS 612.4 bilioni, sawa na asilimia 97.6 ya makadirio ya TZS 627.01
bilioni. Ikilinganishwa na makusanyo ya TZS 478.3 bilioni ya mwaka wa fedha
uliopita 2016/17, kiasi hicho cha mapato kitapelekea ukuaji wa mapato ya kodi wa
asilimia 28.04 baina ya miaka hiyo miwili.
53.
Mheshimiwa Spika, Kitaasisi, utendaji wa TRA unatarajiwa
kufikia asilimia 96.3 kwa kukusanya TZS 249.2 bilioni. Ikilinganishwa na mwaka
uliopita ambapo ilikusanya TZS 203.9 bilioni, mapato ya TRA yataongezeka kwa asilimia
22.2. Kwa upande wa ZRB, pia kunajitokeza ukusanyaji wa kuridhisha kwa kigezo
cha kufikia lengo na ukuaji wa mapato. ZRB inatarajia kukusanya TZS 342.2
bilioni sawa na asilimia 98.5 na sawa na ukuaji wa asilimia 35.2 kutoka makusanyo
ya TZS 253.5 bilioni yaliyopatikana mwaka uliopita 2016/17. Kodi ya Mapato
kutoka Serikali ya Muungano inayosimamiwa na Mhasibu Mkuu wa Serikali inatarajiwa
kufikia TZS 21.0 bilioni sawa na asilimia 100 ya lengo.
54.
Mheshimiwa Spika, kuhusu mapato yasiyokuwa ya kodi, utekelezaji
umeendelea kuonesha mwendo mzuri na wa kutia matumaini. Mapato haya yanatarajiwa
kufikia TZS 68.1 bilioni na hivyo kuwa asilimia 38.5 zaidi ya lengo la
kukusanya TZS 48.8 bilioni. Makusanyo hayo yanapelekea ukuaji wa asilimia 54.5
ikilinganishwa na TZS 43.8 bilioni zilizokusanywa kutoka kianzio hiki kwa mwaka
wa fedha uliopita.
55.
Mheshimiwa Spika, katika makusanyo hayo, Mapato ya
Mawizara yanategemewa kufikia TZS 51.4 bilioni sawa na asilimia 122.9 ya
makadirio ya mwaka ya TZS 41.84 bilioni; Gawio la Mashirika ya Serikali linatarajiwa
kufika TZS 3.2 bilioni sawa na asilimia 106.7 ya makadirio ya mwaka ya TZS 3
bilioni na Gawio la Benki Kuu ya Tanzania, ni TZS 13.5 bilioni sawa na asilimia
337.5 ya makadirio ya mwaka ya TZS 4 bilioni.
b.
Mfuko wa Miundombinu
56.
Mheshimiwa Spika, Kwa mwaka wa fedha 2017/18,
matarajio ya mapato ya Mfuko wa Miundombinu ni TZS 33.6 bilioni sawa na
asilimia 92.5 ya makadirio kwa mwaka huo. Kati ya kiasi hicho, TRA inatarajiwa
kukusanya TZS 10.0 bilioni sawa na asilimia 74.1 ya lengo la kukusanya TZS 13.5
bilioni na ZRB inatarajiwa kukusanya TZS 23.6 bilioni kati ya lengo la TZS 21.3
bilioni, sawa na asilimia 110.8
c.
Matarajio ya Matumizi, (Julai – Juni) 2017/2018
57.
Mheshimiwa Spika, Hadi kufikia Juni 2018, kwa ujumla,
matumizi yanatarajiwa kufikia TZS 865.1 bilioni sawa na asilimia 80.0 ya Bajeti
ya mwaka ya TZS 1,087.4 bilioni. Kati ya kiasi hicho, matumizi ya kazi za
kawaida yanatarajiwa kufikia TZS 559.2 bilioni wakati Matumizi ya maendeleo
yatafikia TZS 305.9 bilioni.
d. Matarajio
ya Mpango wa Maendeleo, 2017/18
58.
Mheshimiwa Spika, Kati ya TZS 305.9 bilioni
zinazotarajiwa kutumiwa na Serikali kwa ajili ya kugharamia utekelezaji wa
programu 27 na miradi 46 ya maendeleo, Serikali inatarajia kutumia jumla ya TZS
104.5 bilioni kutokana na mapato yake ya ndani na Washirika wa Maendeleo
wanatarajiwa kuchangia TZS 201.4 bilioni, zikihusisha Ruzuku ya TZS 45.5
bilioni na mikopo ya TZS 155.9 bilioni.
59.
Mheshimiwa Spika, katika Hotuba yangu ya mwaka jana
nilielezea dhamira ya Serikali ya kusawazisha deni linalodaiwa Shirika la Umeme
(ZECO) na Shirika kama hilo la Tanzania Bara (TANESCO). Deni hilo ni kutokana
na ununuzi wa umeme unaofanywa na ZECO kutoka TANESCO kwa ajili ya matumizi ya
visiwa vyetu, Pemba na Unguja. Nilieleza nia ya Serikali ya kuhakikisha kuwa
ZECO inalipa kwa ukamilifu Ankara zake zote mpya kwa bei iliyokubalika na pande
mbili ili kuzuia kurundikana zaidi kwa deni hilo. Nilieleza pia hatua ambazo
Serikali na ZECO zitachukua kumaliza kiasi kilichokuwa kimebakia.
60.
Mheshimiwa Spika, naomba kuliarifu Baraza lako tukufu
kuwa ZECO inaendelea kulipa kwa ukamilifu Ankara zote na hivyo kuepuka kuingiwa
deni jipya. Kwa mwaka huu tunaoumalizia, ZECO imelipa jumla ya TZS 18.5 bilioni
na hivyo kufanya jumla ya deni lililolipwa kufikia TZS 23.8 bilioni. Kwa upande
wake, Serikali imelipa jumla ya TZS 2.0 bilioni na kwa hivyo kufanya jumla ya
malipo kwa kipindi cha miaka miwili kufikia TZS 15.0 bilioni. Kwa mantiki hiyo,
ZECO na Serikali kwa pamoja wameshalipa TZS 38.8 bilioni na kubakisha deni la
TZS 26.8 bilioni. Itakumbukwa pia, ili kulimaliza haraka deni hilo, SMZ
imependekeza kwa Wizara ya Fedha na Mipango (SMT) kuilipa TANESCO moja kwa moja
TZS 18.0 bilioni inazoidai kupitia katika Kodi ya Mapato ya Wafanyakazi wa SMT
wananaofanyakazi Zanzibar ambazo hazijalipwa hapo kabla. Kwa upande mwengine,
Taasisi kadhaa za Serikali ya Muungano zinadaiwa na ZECO jumla ya TZS 1.7
bilioni ambapo itafanya jumla ya deni la SMT linalodaiwa kufikia 19,7 bilioni
ambazo kama zitalipwa TANESCO itabakiza deni la TZS 7.1 bilioni tu. Kwa nia njema ya kulimaliza deni hilo, katika
mwezi wa Oktoba mwaka jana, Serikali ilipendekeza kwa Serikali ya Muungano
kupitia Wizara ya Fedha na Mipango kulimaliza deni hilo kupitia katika madeni
ya marejesho ya Kodi ambayo Zanzibar inaidai SMT.
61.
Mheshimiwa Spika, mapendekezo hayo yakikubaliwa na SMT
yatasaidia katika maeneo kadhaa, Mosi, utasaidia kulimaliza deni lote kwa
mkupuo mmoja. Pili, utasaidia kupunguza athari za Kibajeti kwa SMZ; na tatu,
utapelekea SMZ kulipwa pesa zote inazodai hadi sasa kutokana na marejesho ya
Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) na Ushuru wa Bidhaa. Tunaendelea kufuatilia
ili kupata ridhaa ya SMT kwa nia ya kumaliza vyema suala la madeni hayo
yanayodaiana pande mbili za Jamhuri ya Muungano.
62.
Mheshimiwa Spika, katika Hotuba ya mwaka jana pia
nilieleza uamuzi wa Serikali wa kuanza na Ugatuzi wa madaraka kutoka Serikali
Kuu kwenda Serikali za Mitaa (Mabaraza ya Manispaa, Mabaraza ya Miji na
Halmashauri za Miji). Maeneo yaliyohusika na Ugatuzi huo ni pamoja na Elimu ya
Maandalizi na Msingi, Afya ya Msingi na Huduma za Ugani na nyenginezo katika
Kilimo. Nina furaha kulijuilisha Barza hili kuwa ugatuzi huo umeanzwa kama
ilivyopangwa na kwa ujumla umeendelea vyema.
63.
Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo ya mapitio ya
utekelezaji wa Bajeti ya mwaka tunaokaribia kumalizika wa 2017/18, naomba sasa
niwasilishe mapendekezo ya Bajeti kwa mwaka 2018/19 kama ninavyotakiwa na
Katiba yetu ya mwaka 1984 kama ilivyorekebishwa.
64.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya
fedha namba 12 ya mwaka 2016 na Kanuni za Baraza la Wawakilishi, maandalizi ya
Bajeti ya mwaka 2018/2019, yalitanguliwa na uwasilishwaji wa Mwelekeo wa Bajeti
katika Baraza la Wawakilishi mwezi Februari mwaka huu. Mwelekeo huo umekuwa Dira
ya utayarishaji wa Bajeti hii ambayo leo ninaiwasilisha mbele ya Baraza lako.
Mapendekezo ya Makadirio haya ya Mapato na Matumizi ya mwaka ujao (2018/2019)
ninayowasilisha leo hii yameongozwa na Mwelekeo huo ulioidhinishwa wa
Bajeti na mazingatio ya Vipaumbele vya
Taifa.
65.
Mheshimiwa Spika, makadirio haya ya Bajeti yametokana
na matarajio ya ukuaji mzuri wa uchumi kama nilivyoeleza kwa kina katika hotuba
yangu leo asubuhi. Kwa ufupi, tunatarajia ukuaji mzuri zaidi wa uchumi kwa
mwaka 2018 ambao utakua kwa kasi ya asilimia 7.7 itayotokana na kukua kwa sekta
za Huduma, Kilimo na Viwanda, utakaochangiwa zaidi na ukuaji rasilimali utaotokana
na ujenzi wa miundombinu.
VI.
MWELEKEO
WA MAPATO:
a.
Mapato ya Ndani
66.
Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kuwa wakati akizindua
Baraza la 9 la Wawakilishi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, alieleza nia ya Serikali ya
kuimarisha zaidi usimamizi wa mapato yetu na kuelekea zaidi kujitegemea katika
kuendesha mambo yetu badala ya kutegemea Wafadhili. Kuhusu mapato, Mheshimiwa
Rais alikumbusha kuwa ahadi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa wananchi, kama
ilivyobainishwa katika Ilani yake ya Uchaguzi ya mwaka 2015, ni kukusanya kiasi
cha TZS 800.0 bilioni ifikapo mwaka wa 2020.
67.
Mheshimiwa Spika, wazee wetu walishatuambia kuwa
ahadi ni deni na dawa ya deni ni kulipa. Na kwa deni hili, kulilipa kwake ni
kwa Serikali hii ya CCM kukusanya angalau TZS 800.0 bilioni kutokana na vyanzo
vya ndani ifikapo mwaka 2020.
68.
Mheshimiwa Spika, nina fakhari kubwa kulijuilisha Baraza
lako tukufu kuwa Serikali imedhamiria kutimiza ahadi hiyo na hivyo kulipa deni
lake kwa wananchi. Serikali inakusudia
kutimiza ahadi hiyo katika mwaka ujao wa fedha, 2018/19, mwaka mmoja kabla, badala
ya kusubiri mwaka 2020 kama ilivyoahidi.
69.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018/19, Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, katika awamu yake ya saba inayoongozwa na Dkt. Ali
Mohamed Shein, inatarajia kukusanya jumla ya TSZ 807.5 bilioni kutokana na vyanzo
vya ndani. Makadirio haya ni sawa na ongezeko la asilimia 18.7 kutoka mapato ya
TZS 680.0 bilioni yanayotarajiwa kukusanywa kwa mwaka wa fedha 2017/18 kama
nilivyoeleza awali.
70.
Mheshimiwa Spika, mchanganuo wa mapato hayo ni kama
ifuatavyo:
i.
Mapato yatokanayo na kodi ni TZS 727.5 bilioni;
ii.
Mapato ya Mawizara ni TZS 71.0 bilioni;
iii.
Gawio la Mashirika ya Serikali ni TZS bilioni 5; na
iv.
Gawio kutoka Benki Kuu (BoT) ni TZS 4 bilioni.
71.
Mheshimiwa Spika, Kitaasisi, mgawanyo wa jukumu la
kukusanya kiasi hicho cha mapato ni kama ifuatavyo:
i.
Mamlaka ya Mapato (TRA) imekadiriwa kukusanya jumla ya
TZS 301.1 bilioni ambapo Idara ya Forodha na Ushuru imekadiriwa kukusanya TZS 165.9
bilioni na Idara ya Kodi za Ndani TZS 135.2 bilioni;
ii.
Bodi ya Mapato
inatarajiwa kukusanya TZS 485.4 bilioni ikiwemo TZS 405.4 bilioni za Mapato ya
kodi, TZS 71.0 bilioni Mapato ya Mawizara na TZS 9.0 bilioni za Gawio la Benki
Kuu na Mashirika ya SMZ;
iii.
Ofisi ya Mhasibu Mkuu wa Serikali inatarajiwa kusimamia
upatikanaji wa TZS 21.0 bilioni zitokanazo na Kodi ya PAYE kwa wafanyakazi wa
Muungano waliopo Zanzibar.
b.
Mapato ya Nje
72.
Mheshimiwa Spika, pamoja na nia yetu ya dhati ya
kuharakisha kujitegemea, bado tutaendelea kushirikiana na Mataifa rafiki na
Mashirika ya Kifedha na ya Kibinaadamu ya Kimataifa katika kughramia Maendeleo
yetu. Kwa mwaka wa fedha 2018/19, Serikali inatarajia kupokea jumla ya TZS
464.2 bilioni kutokana na Mikopo na Ruzuku kutoka nje ya nchi. Kati ya kiasi
hicho, TZS 388.6 bilioni kinatarajiwa kutokana na Mikopo na TZS 75.6 bilioni ni
Ruzuku. Bado Serikali haitaingiza moja kwa moja Misaada ya Kibajeti (GBS)
katika mipango yake ya matumizi. Tutaendelea kutumia utaratibu wa Kibajeti wa
“100T” ili kukidhi haja ya matumizi pindi Misaada hiyo ikipokelewa katikati ya
mwaka.
VII.
MAPENDEKEZO
YA HATUA ZA KUIMARISHA MAPATO
73.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikuchukua hatua
maalum za kuweka utulivu wa mfumo wa kodi nchini kama njia mojawapo ya
kushajiisha uwekezaji na ulipaji wa Kodi kwa hiari. Kwa mara nyengine tena,
Serikali haipendekezi kupandisha kodi katika mwaka ujao wa fedha. Badala yake,
Serikali itaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha usimamizi na
ukusanyaji wa mapato. Kwa mustakabali huo, hatua zinazopendekezwa ni hizi
zifuatazo:
i.
Sheria ya Ushuru wa
Stempu namba 7 ya mwaka 2017
74.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitoza Ushuru wa
Stempu kwa bidhaa ambazo zimesamehewa Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
Miongoni mwa bidhaa hizo ni za vyakula muhimu kwa jamii yetu kama vile mchele
na unga wa ngano. Bidhaa hizo zilisamehewa VAT kwa dhamira ya kupunguza gharama
za maisha. Kwa lengo hilo hilo, Serikali inapendekeza kurekebisha Sheria ya
ushuru wa Stempu kwa kufuta Ushuru huo kwa uingizaji, usambazaji na uuzaji wa
bidhaa za mchele na unga wa ngano nchini ili kutoa unafuu zaidi kwa bei za
chakula.
75.
Mheshimiwa Spika, marekebisho mengine yanayopendekezwa
katika Sheria hii ni kufutwa kwa Ushuru wa Stempu kwenye tiketi za ndege
zinazotolewa na mashirika ya Kimataifa hapa Zanzibar kwa safari za nje ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lengo ni kuleta usawa wa kodi na Tanzania Bara
ambayo kwa sasa haitozi ushuru huo hivyo kuendelea kuutoza hapa Zanzibar
kunaathiri biashara hiyo.
ii.
Kufanya mapitio ya mfumo
wa misamaha ya ushuru wa stempu katika kuhaulisha mali (Transfer of property)
76.
Mheshimiwa Spika, Sheria ya Ushuru wa Stempu inataka
Ushuru huo utozwe hata pale ambapo mali inahama kutoka kwa mmiliki wake kwenda
kwa mtu mwengine kwa njia ya mirathi au kutoa kwa hiba bila ya kuwepo malipo
kutoka kwa anaepokea. Inapendekezwa kufuta Ushuru wa Stempu wakati wa uhaulishaji
mali (transfer of Property) bila ya malipo pale mali hizo zinapohaulishwa kwa
utaratibu wa urithi na baina ya mzazi au mlezi wa kisheria na mtoto au mume au
mke wa ndoa anapompa mwenza wake kwa hiba;
iii. Kuongeza Muda wa Kuwasilisha Ritani na Malipo
ya Kodi
77.
Mheshimiwa Spika, muda unaohitajika kuwasilisha Ritani
ya mauzo kila mwezi na muda wa kuwasilisha malipo ya Kodi Serikalini ni muhimu
kwa Walipakodi kutimiza matakwa ya Sheria na athari katika gharama za
kuwajibika kisheria. Kwa mujibu wa Sheria ya Usimamizi wa Kodi (TAPA) namba 7
ya mwaka 2009, kwa sasa walipakodi wanapaswa kuwasilisha Ritani kwa Kodi
mbalimbali si zaidi ya siku ya 10 ya mwezi unaofuatia mwezi wa mauzo. Aidha,
siku ya mwisho kufanya malipo ni tarehe 15 ya mwezi huo unaofuatia mwezi wa
mauzo. Baada ya mashauriano na Sekta binafsi, Serikali inapendekeza kubadilisha
tarehe hizo na kuzichanganya kuwa siku moja, tarehe 20 ya mwezi unaofuatia
mauzo kwa kuwasilisha Ritani na kufanya malipo.
78.
Mheshimiwa Spika, zaidi ya hatua hizo za kisheria,
Serikali pia itachukua hatua za kiutawala zenye lengo la kuimarisha ukusanyaji
wa mapato. Miongoni mwa hatua hizo ni hizi zifuatazo:
iv.
Kutoa Muongozo wa Kodi
ya Zuio (Withholding Tax)
79.
Mheshimiwa Spika, Wizara na Taasisi za Serikali
zimekuwa zikizuia Kodi za VAT na ya Mapato mbambali wakati wa malipo kwa wazabuni.
Imebainika kuwa bado si malipo yote yanayopaswa kuzuiliwa na kuwasilishwa ZRB
na TRA yanafanywa hivyo. Ili kurekebisha kazoro zilizopo, kwa mwaka ujao wa
fedha, Serikali itatayarisha na kutoa Muongozo wa Usimamizi na Ukusanyaji wa
Kodi ya Zuio (Withholding Tax Guideline) kwa Wizara, Idara na Taasisi mbali
mbali za Serikali. Hatua hii itaongeza mapato ya Serikali ya TZS 8.5 bilioni;
v.
Kuimarisha Usimamizi wa
Utoaji wa Leseni
80.
Mheshimiwa Spika, bado tuna tatizo la baadhi ya watu
kufanya biashara bila ya kusajiliwa na TRA na ZRB na hivyo kuikosesha Serikali
mapato yake. Serikali itasimamia mamlaka zote za utoaji wa leseni za biashara,
ikiwemo Serikali za Mitaa, kuhakikisha kuwa hakuna leseni zinazotolewa bila ya
Mfanyabiashara kusajiliwa na TRA na ZRB na kuonesha Hati ya kutodaiwa kodi (Tax
Clearance Certificate) kutoka TRA na ZRB. Matarajio ni kwua hatua hii itaiingizia
Serikali jumla ya TZS 4.5 bilioni;
vi.
Kodi ya Majengo
(Property Tax)
81.
Mheshimiwa Spika, matayarisho ya ukusanyaji wa Kodi
ya Majengo (Property Tax) yamefikia hatua kubwa. Serikali itaanza rasmi kutoza
kodi hiyo katika mwaka ujao wa Fedha (2018/19) kwa majengo ya biashara. Jumla
ya TZS 5.0 bilioni zinatarajiwa kukusanywa na kuhaulishwa kwenda Serikali za
Mitaa kwa kutumia vigezo maalum vya mgao vinavyokaribia kukamilishwa.
vii.
Kufanya mapitio ya
viwango vya Ada
82.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikifanya mapitio
ya viwango vya ada zinazotozwa katika huduma mbalimbali kwa lengo vya kuvifanya
viendane na mahitaji ya wakati. Serikali itaendelea na mapitio hayo katika
mwaka ujao wa Fedha, hatua ambayo inatarajiwa kuingiza jumla ya TZS 0.4
bilioni.
viii.
Kupunguza unafuu wa Kodi
ili kulinda Viwanda vya Ndani
83.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitoa unafuu wa
Ushuru wa Forodha na Kodi nyengine kwa uingizaji wa bidhaa muhimu za chakula
kama vile mchele, unga wa ngano na sukari. Hata hivyo, kufuatia kuimarika kwa uzalishaji
nchini kupitia kiwanda cha Unga wa Ngano cha “Zanzibar Milling Corporation” na
kufufuliwa Kiwanda cha Sukari cha Mahonda, inajitokeza haja ya kupunguza unafuu
unaotolewa kwa uingizaji wa bidhaa hizo muhimu ili viwanda vyetu viweze
kuhimili ushindani wa haki. Serikali inakusudia kupunguza unafuu unaotolewa
sasa wa ushuru wa uingizaji kwa dhamira ya kuupunguza au kuuondoa kabisa.
VIII. MWELEKEO WA MATUMIZI
84.
Mheshimiwa Spika, Serikali inakadiria kutumia jumla
ya TZS 1,315.1 bilioni katika mwaka wa fedha 2018/19. Matumizi haya
yanajumuisha matumizi ya kazi za kawaida ya TZS 702.2 bilioni na matumizi ya
kazi za maendeleo ya TZS 613.0 bilioni. Matumizi ya kazi za kawaida
yamezingatia matakwa ya misingi ya usimamizi wa fedha kama ilivyo katika
Kifungu cha 5(1)(b) cha Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Umma namba 12 ya mwaka
2016. Kifungu hiki kinaelekeza kuwa katika kipindi cha muda wa kati, matumizi
ya kazi za kawaida yasipindukie mapato ya ndani.
85.
Mheshimiwa Spika, katika matumizi ya kawaida, jumla
ya TZS 337.1 bilioni zinahitajika kwa ajili ya kulipa mishahara, posho
zinazoendana na mishahara pamoja na michango ya lazima, kwa ajili ya Mfuko wa
Hifadhi ya Jamii (ZSSF). Katika mwaka huo, kiasi cha TZS 15 bilioni zimetengwa
kwa ajili ya nyongeza za mwaka, upandishaji vyeo na ajira mpya. Kiasi hicho ni
sawa na asilimia 41.7 ya mapato ya ndani na hivyo kimezingatia matakwa ya
Kifungu cha 5(1)(d) cha Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Umma kinachokataza
matumizi ya mishahara na maslahi kwa wafanyakazi wa umma kuwa makubwa kwa
kuzingatia uwezo wa kuchumi.
86.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia mapato ya ndani
yanayotarajiwa ya jumla ya TZS 807.5 bilioni, matumizi hayo kwa ajili ya
mishahara yataacha salio la TZS 470.6 bilioni kwa ajili ya matumizi mengine. Aidha,
kati ya jumla ya mapato hayo yanayotarajiwa kutokana na vyanzo vya ndani, yamo mapato
yaliyokasimiwa matumizi maalum na hivyo kutoweza kugawanywa kwenye matumizi
mengine.
87.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018/19, mapato hayo
yenye matumizi maalum yanatarajiwa kufikia TZS 97.5 bilioni kama ifuatavyo:
i.
Fedha maalum zilizotengwa kwa ajili ya Mfuko wa Miundombinu, TZS 39.4 bilioni;
ii.
Asilimia 5 ya makusanyo inayobaki ZRB sawa na TZS 20.3 bilioni;
iii.
Makusanyo kwa ajili ya Mfuko wa Barabara TZS 15.8 bilioni;
iv.
Ada ya Bandari kwa mchango wa madawati inatarajiwa kuwa ni TZS 1.0
bilioni;
v.
Ada ya Kuendeleza Ujuzi (SDL), TZS 13.8 bilioni;
vi.
Marejesho kwa Idara ya Uhamiaji Zanzibar ya TZS 6.5 bilioni sawa na
asilimia 25 ya makusanyo yao; na
vii.
Ada ya Usalama ya Uwanja wa Ndege
kwa ajili ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege TZS 650 milioni.
88.
Mheshimiwa Spika, baada ya kuondoa kiasi hicho cha
TZS 97.5 bilioni zinabaki jumla ya TZS 373.1 bilioni ambazo ndio zinagaiwa kwa
ajili ya matumizi ya kuendeshea Serikali (Other Charges), Ruzuku kwa Taasisi
mbalimbali na kazi za maendeleo. Ugawaji wa fedha hizo umezingatia mambo ya
ziada yafuatayo:
i. Kuendeleza utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya Chama Cha
Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2015;
ii.
Maeneo ya vipaumbele vya Taifa kwa mwaka 2018/19 kama nilivyovibainisha
wakati nikiwasilisha Mpango wa Maendeleo leo asubuhi; na
iii.
Maagizo Maalum ya Serikali kwa mujibu wa vipaumbele vya Taifa yakiwemo ya
kutoa Elimu bure hadi Sekondari na kuongeza Bajeti ya Dawa na Vifaa tiba kama
nitakavyoeleza baadae.
89.
Mheshimiwa Spika, zaidi ya vigezo nilivyovitaja, ugawaji
wa fedha za maendeleo kwa mwaka 2018/19 umezingatia mambo ya ziada yafuatayo:
iv. Programu na miradi ya kimkakati (Flagship Projects)
iliyotajwa katika MKUZA III;
v. Programu na miradi yote ambayo Serikali ina dhima
(Commitment) kutoka kwa Washirika wa Maendeleo;
vi. Programu na miradi yote iliyokuwa haijakamilika
utekelezaji wa shughuli zake kwa bajeti ya mwaka 2017/18;
vii. Miradi inayogharamiwa kupitia Mfuko wa Miundombinu.
a.
Matumizi ya Mfuko wa Miundombinu
90.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi, jumla ya
TZS 39.4 bilioni zimekadiriwa kutumika katika kugharamia Miradi maalum ya maendeleo
hususan miradi ya kuimarisha Miundombinu. Miradi inayotarajiwa kugharamiwa na
Mfuko huo kwa mwaka 2018/19 ni kama ifuatavyo:

91.
Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia jumla ya matumizi ya
TZS 1,315.1 bilioni, mapato ya ndani ya TZS 807.5 bilioni na Misaada kutoka nje
ya TZS 464.2 bilioni pamoja na Mfuko wa Wafadhili (Basket Fund) wa TZS 3.4
bilioni, kunajitokeza matumizi kuzidi mapato kwa TZS 40 bilioni. Nakisi hiyo
inaombwa kuzibwa kupitia Mikopo ya ndani.
IX.
MAENEO
MENGINE MUHIMU YALIYOZINGATIWA
92.
Mheshimiwa Spika, katika mgawanyo wa rasilimali,
maeneno mengine muhimu yaliyozingatiwa ni pamoja na haya yafuatayo:
a.
Maendeleo ya Kiuchumi
93.
Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio yetu makubwa
katika kukuza uchumi wetu na hatimae ukuaji huo kupelekea maendeleo ya watu
wetu, bado tuna kazi kubwa sana mbele yetu kufikia katika maisha bora ya wananchi
ambayo Serikali ya CCM ingependa kuyaona. Tunaendelea kushuhudia Sekta za
kisasa zikichukua nafasi ya Sekta za asili kama vile Kilimo lakini bado kasi ya
mageuzi hayo inahitaji kuimarishwa zaidi. Mchango wa Sekta ya Kilimo katika
Pato letu la Taifa kwa mwaka 2017 ni asilimia 27. Pamoja na dhamira ya
kukiimarisha Kilimo ili kiwe cha kisasa na chenye tija, Sekta ya Viwanda na
Huduma zinapaswa kuimarishwa ili zitoe mchango mkubwa zaidi katika uchumi wetu.
94.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka ujao wa Fedha, sambamba
na kuendeleza jitihada za kushajiisha uwekezaji zaidi binafsi katika uzalishaji
viwandani, Serikali inatarajia kuanza ujenzi wa Eneo moja la Viwanda
(Industrial Park) na eneo la kuimarisha wazalishaji wadogo wadogo. Aidha, hatua
maalum za kuyaimarisha maeneo ya kusarifu
mazao ya Kilimo ya Kizimbani (Unguja) na Pujini (Pemba) zitachukuliwa.
95.
Mheshimiwa Spika, Nia ya Serikali ni kuwa maeneo hayo
yatumiwe na Wananchi pale wanapohitaji kusarifu na kuongeza thamani kwenye
mazao yao. Utaratibu huu unatarajiwa kuharakisha usarifu wa mazao kwa kuondoa
kikwazo cha gharama kubwa za kuwekezwa katika ujenzi wa viwanda. Kila mwenye
kuhitaji kusarifu mazao yake atakuwa na fursa ya kuyapelekea kwa ajili ya
kusarifiwa.
b.
Ajira
96.
Mheshimiwa Spika, eneo jengine linalopewa mkazo
maalum na Serikali ni upatikanaji wa ajira kwa vijana wetu. Sio siri kuwa nchi
nyingi zinazoendelea hasa za kusini mwa Jangwa la Sahara, ikiwemo Zanzibar,
zina changamoto kubwa ya kushajiisha upatikanaji wa ajira kwa nguvu kazi yake,
hususan vijana. Matokeo ya Utafiti wa Nguvu kazi wa mwaka 2014 yalionesha kuwa
kiwango cha ukosefu wa ajira Zanzibar ni asilimia 14.3, na tatizo likijokeza zaidi
kwa Vijana.
97.
Mheshimiwa Spika, kwa Vijana wa umri wa miaka 15 hadi
24, ukosefu wa ajira umepanda kutoka asilimia 17.9 mwaka 2006 hadi asilimia 27.
Hata hivyo, kwa kundi la vijana wa miaka 15 hadi 35, mafanikio yamepatikana kwa
kupungua ukosefu wa ajira kutoka asilimia 31.3 mwaka 2006 hadi asilimia 21.3
mwaka 2014. Pamoja na mafanikio hayo, kiwango hicho bado ni kikubwa na
kinahitaji juhudi maalum za kurekebisha.
98.
Mheshimiwa Spika, tatizo hili linachangiwa zaidi na
uchache wa nafasi za ajira zinazojitokeza kila mwaka ikilinganishwa na mahitaji
kutokana na wahitimu wanaomaliza masomo katika ngazi mbalimbali. Ili kurekebisha
hali hiyo, Serikali itachukua jitihada mbalimbali zikiwemo hizi zifuatazo:
a)
Kuendeleza juhudi za
kushajiisha uwekezaji binafsi nchini;
b)
Kuendelea kukuza ujuzi wa vijana wetu na kuwapatia
elimu bora ili waweze kuajirika;
c)
Kuimarisha mafunzo ya Ujasiriamali na amali ili
vijana wengi zaidi waweze kujiajiri na kuajiri wenzao;
d)
Kupitia upya utaratibu wa utoaji wa vibali vya Kazi
ili kuimarisha udhibiti kwa kuhakikisha kuwa wanaopatiwa vibali hivyo ni wale
tu wanastahiki na kwa nafasi ambazo vijana wa Kizanzibari hawana ujuzi wa
kuzifanya; na
e)
Kuendelea kuajiri vijana kwa kujaza nafasi
Serikalini zinazojitokeza kwa wengine kustaafu au mahitaji mapya.
99.
Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo, kuanzia
mwaka ujao wa Fedha, Serikali imeamua kuanzisha Programu Maalum ya Ajira kwa
Vijana. Lengo la Programu hiyo ni kuwasaidia vijana kuweza kujiajiri wenyewe
kwa kuwapatia mitaji kwa mapendekezo yao ya miradi katika sekta tofauti. Kwa
kuanzia, Serikali imetenga TZS 3.0 bilioni kwa ajili ya Programu hiyo.
Mazungumzo yanaendelea na Benki ya Dunia kuangalia uwezekano wa kupatikana
fedha zaidi kwa Programu hiyo. Programu hiyo inatarajiwa pia kunufaika na
matokeo ya mazungumzo yanayoendelea na nchi ya Abu Dhabi kutoka Umoja wa Falme
za Kiarabu ambayo imeahidi kusaidia jitihada za Serikali za kuleta ajira kwa
vijana kupitia Mfuko wake wa Khalifa (Khalifa Fund). Ahadi hiyo ni matokeo ya
ziara ya kufana na kidugu ya Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein katika Falme
hizo za Kiarabu.
c.
Utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia
100. Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu, nchi yetu ipo
katika harakati za utafutaji wa maliasili za Mafuta na Gesi. Maelezo ya kina
yametolewa na Mheshimiwa Waziri anaesimamia Sekta hiyo muhimu. Miongoni mwa
mambo yaliyokwishafanyika ni pamoja na haya yafuatayo:
a)
Kutungwa kwa Sheria
ya Mafuta na Gesi namba 6 ya mwaka 2016;
b)
Kuanzishwa kwa Mamlaka ya Kusimamia Shughuli
za utafutaji na undelezaji wa Mafuta na Gesi (ZPRA);
c)
Kuanza kazi za
utafutaji wa rasilimali hiyo kwa kutumia ndege, meli na vifaa vya nchi kavu
katika Kitalu cha Pemba/Zanzibar kwa mashirikiano na Kampuni ya Rak Gas kutoka
Ras Al Khaimah. Tayari kazi hizo zimekamilika isipokuwa utafutaji wa mafuta
katika nchi kavu kwa kisiwa cha Pemba ndio unaendelea; na
d)
Kutenga eneo la
Mangapwani kwa ajili ya ujenzi wa Bandari ya Mafuta na Gesi na Huduma nyengine
muhimu.
101. Mheshimiwa Spika, kwa mwaka ujao wa fedha jitihada
hizo zitaimarishwa zaidi kwa kuendeleza kazi ya utafutaji wa mafuta katika
Kitalu hicho na kutafsiri taarifa zilizokwishakusanywa. Aidha, Serikali
imetenga TZS 5.0 bilioni kwa ajili ya kuanza kazi ya uwekaji wa miundombinu ya
msingi katika eneo la Mangapwani. Kazi hizo ni pamoja na ujenzi wa barabara,
usogezaji wa umeme na maji.
102. Mheshimiwa
Spika, kwa upande mwengine, eneo hili la kiuchumi ni jipya kwa hapa kwetu
na lina mahitaji maalum ya utaalamu na uzoefu katika fani mbalimbali
zinazohusiana na mambo hayo. Kwa kuzingatia uhaba mkubwa wa utaalamu, hatua
ambazo Serikali inachukua kujenga haraka utaalamu ni pamoja na hizi zifuatazo:
a)
Kupitia Bodi ya
Mikopo ya Elimu ya Juu, imetoa kipaumbele katika kudhamini wataalamu wanaosomea
fani mbalimbali zinazohusiana na Mafuta na Gesi;
b)
Katika mikataba ya Ubia wa Mafuta (Petroleum
Sharing Agreements – PSA), kunatarajiwa kuwa na kiwango maalum kwa ajili ya
Kampuni hizo kutoa fedha za mafunzo ya wataalamu wazalendo; na
c)
Kwa mwaka 2018/19, Serikali
pia imetenga TZS 1.0 bilioni kwa madhumuni ya kuharakisha ujenzi wa utaalamu
huo.
d. Miundombinu
na Huduma za Jamii
103. Mheshimiwa Spika, mara nyingi nimekuwa nikieleza
umuhimu ambao Serikali inaweka katika kuendeleza miundombinu na huduma muhimu
za Elimu na Afya. Kwa mwaka ujao wa fedha, Sekta hizi tatu zimetengewa jumla ya
TZS 487.5 bilioni ambapo Afya ni TZS 93.3 bilioni, Elimu na mafunzo ya Amali
TZS 179.6 bilioni na ujenzi, Miundombinu na Usafirishaji TZS 214.6 bilioni.
104. Mheshimiwa Spika, kuhusu Elimu, baada ya mafanikio
yaliyopatikana kwa kusajili wanafunzi wengi zaidi katika Skuli za Maandalizi na
Msingi baada ya Serikali kufuta michango ya wazazi katika elimu ya ngazi hizo,
kuanzia mwaka ujao wa Fedha Serikali itafuta rasmi michango katika elimu ya
Sekondari. Hatua hii inaendana na dhamira ya Mapinduzi yetu matukufu ya Januari
1964 yaliyopelekea huduma ya elimu nchini kutangazwa kutolewa bila ya malipo,
bila ya ubaguzi kwa watoto wote.
105. Mheshimiwa Spika, Uwekezaji huu muhimu katika kukuza
watoto wetu utanufaisha watoto 256,048 wa elimu ya msingi na watoto 122,163 wa
elimu ya Sekondari kwa Takwimu za mwaka 2017. Serikali pia itaelekeza jitihada
zake katika kuimarisha ubora wa elimu na matokeo ya wanafunzi. Jitihada hizi
zitapata msukumo zaidi kutokana na mashirikiano na Washirika wa Maendeleo
hususan Benki ya Dunia na mashirika mengine ya Kimataifa.
106. Mheshimiwa Spika, eneo jengine muhimu kwa maisha ya
kila mwanaadamu ni siha, inayotokana na lishe bora, upatikanaji wa maji safi na
salama, kuishi katika mazingira mazuri na kwa kuzingatia tabia njema kama vile
kufanya mazoezi, na upatikanaji wa huduma bora za afya. Serikali inachukua
hatua mbalimbali katika kuimarisha mambo yote hayo kama zilivyoelezwa kwa kina
na Waheshimiwa Mawaziri wanaosimamia Sekta hizo.
107. Mheshimiwa Spika, kuhusu huduma za afya, kama
nilivyotangulia kusema Sekta hii imetengewa jumla ya TZS 93.3 bilioni mwaka
ujao wa fedha. Moja ya eneo muhimu lililopewa mazingatio maalum ni upatikanaji
wa dawa za lazima na vifaa tiba. Itakumbukwa kuwa hadi kwenye mwaka 2014,
tulikuwa tukitegemea sana wafadhili hasa ndugu zetu wa Denmark kupitia Shirika
lao la DANIDA na wa Marekani kupitia Shrika la USAID. Serikali ilifanya uamuzi
makhsusi wa kupunguza kutegemea washirika wa maendeleo kwa upatikanaji wa dawa
za lazima kwa Wananchi na hatua kwa hatua kuchukua yenyewe jukumu hili muhimu.
108. Mheshimiwa Spika, Sambamba na uamuzi huo, Bajeti ya
dawa muhimu na vifaa tiba kutokana na fedha za ndani za SMZ imeongezeka awamu
kwa awamu kutoka TZS 500 milioni mwaka 2014/2015 hadi kufikia TZS 8.0 bilioni
mwaka huu unaomalizika. Serikali kupitia Wizara ya Afya imefanya uchambuzi wa
kina wa mahitaji ya dawa za lazima na vifaa tiba na kubainisha kuwa jumla ya
TZS 12.7 bilioni zinahitajika kila mwaka kwa kukidhi mahitaji hayo.
109. Mheshimiwa Spika, nina furaha kulijuilisha Baraza
lako tukufu kuwa kwa mwaka ujao wa fedha, Serikali imeongeza tena bajeti ya
dawa na vifaa tiba na kutenga kiasi hicho cha TZS 12.7 bilioni katika Bajeti ya
Wizara ya Afya ili kukidhi mahitaji ya dawa za lazima kwa wananchi katika
hospitali zetu. Ni jukumu letu sote sasa kuhakikisha kuwa dawa hizo
zinanunuliwa kwa wakati, zinapatikana kwa wenye mahitaji na zinatumiwa vyema na
wanaopatiwa. Kinyume cha hayo, fedha nyingi zinazotumiwa na Serikali zitakuwa
zinapotea bila ya malengo yaliyokusudiwa.
110. Mheshimiwa Spika, katika Hotuba yangu ya Bajeti ya
mwaka jana nilieleza juu ya Mpango wa Serikali wa kuanza kutekeleza mageuzi ya
Serikali za Mitaa kwa lengo la kuongeza uwajibikaji wa umma kwa wananchi na
kusogeza huduma muhimu karibu yao. Nilibainisha kuwa majukumu yatakayohamishwa
kutoka Serikali Kuu kwenda Serikali za Mitaa (ugatuzi) ni pamoja na Huduma za
msingi za afya, elimu ya maandalizi na msingi na huduma za ugani na usimamizi
wa madiko katika Sekta ya Kilimo na Uvuvi.
111. Mheshimiwa Spika, mwaka wa kwanza wa utekelezaji wa
mageuzi hayo umeonesha matumaini mazuri na pia kubainisha kazi kubwa iliyo
mbele yetu katika kuhakikisha kuwa lengo la mageuzi hayo linafikiwa. Kwa mwaka
ujao wa fedha hatua zaidi zitachukuliwa katika kuimarisha mageuzi hayo kwa
maeneo ya kuanzia. Hatua hizo ni pamoja na kuhamisha wafanyakazi wa maeneo hayo
kutoka Serikali Kuu na kuhamishia Serikali za Mitaa sambamba na kuhamisha gharama
zao za mishahara, maposho na likizo. Serikali itaimarisha pia uratibu wa
mageuzi haya na kukabiliana na changamoto zozote zitakazojitokeza.
X.
SURA YA BAJETI
112. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia hali ya mapato na
matumizi niliyokwisha yaeleza hapo juu, Bajeti ya mwaka 2018/19 inatarajiwa
kuhusisha mapato ya jumla ya TZS 1,275.1 bilioni. Kati ya fedha hizo:
a. Mapato ya ndani ni TZS 807.5 bilioni; na
b. Ruzuku na Mikopo kutoka nje ni TZS 464.2 bilioni
c. Ruzuku ya TZS 3.4 bilioni ya Mfuko wa Wafadhili
(BF).
113. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi, jumla ya
TZS 1,315.1 bilioni zinatarajiwa kutumika kama ifuatavyo:
i.
Matumizi
ya Kazi za Kawaida TZS 702.1 bilioni, na
ii.
TZS
613.0 bilioni kwa kazi za Maendeleo.
114. Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia mapato ya TZS
1,275.1 bilioni na matumizi ya TZS 1,315.1 bilioni, kunajitokeza nakisi ya TZS 40.0
bilioni. Inapendekezwa kuwa nakisi hiyo izibwe kwa kukopa kiasi hicho cha fedha
kutoka soko la ndani.
115. Mheshimiwa Spika, kwa sura hii ya Bajeti,
kunajitokeza taswira ifuatayo:
i.
Mapato
yetu ya ndani ya TZS 807.5 bilioni yatakidhi haja ya kugharamia matumizi yetu
yote ya kazi za kawaida ya jumla ya TZS 702.1 bilioni;
ii.
Utekelezaji
wa Mpango wa Maendeleo utagharamiwa na vyanzo vifuatavyo vya fedha:
a) Mapato ya Ndani ya TZS 69.4 bilioni;
b) Mfuko wa Miundombinu TZS 39.4 bilioni;
c) Mikopo kutoka nje TZS 388.6 bilioni;
d) Ruzuku kutoka nje TZS 75.6 bilioni, na
e) Mikopo ya Ndani ni TZS 40.0 bilioni.
Sura kamili ya
Bajeti kwa mwaka 2018/2019 inaonekana katika jadweli hapa chini.

Chanzo: Wizara ya Fedha na Mipango,
Zanzibar
116. Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kwamba katika Bajeti
tunayoendelea nayo, tulitoa taarifa ya kupungua kwa utegemezi wa Bajeti kwa
ruzuku kutoka nje kutoka asilimia 11.1 mwaka 2016/17 hadi asilimia 7.3 mwaka
2017/18. Kutokana na mchango wa Ruzuku ya TZS 75.6 bilioni katika Bajeti ya TZS
1,315.1bilioni ya mwaka 2018/19, utegemezi wa Bajeti unatarajiwa kushuka zaidi
na kufikia asilimia 5.7 tu. Haya ni mafanikio mengine makubwa tunayoendelea
kuyapata ambayo yanapaswa kudumishwa.
XI.
SHUKRANI
117. Mheshimiwa Spika, nna deni kubwa kwa viongozi na
watendaji wote walioshiriki katika uandaaji wa Makadirio haya ya Mapato na
Matumizi kwa mwaka 2018/19. Uwasilishaji huu usingewezekana leo hii bila ya
mchango mkubwa wa maelekezo, miongozo na mawazo ya watu mbalimbali, Serikalini
na katika Sekta binafsi. Kwa ujumla wao, naomba uniruhusu niwashukuru sana wote
kwa namna walivosaidia na kufanikisha mimi leo hii kutimiza wajibu wangu wa
Kikatiba kwa dhamana niliyopewa ya Uwaziri wa fedha na Mipango. Naomba
uniruhusu niwataje wachache.
118. Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nishukuru sana
maelekezo na miongozo ya Mheshimwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Dira na upeo wa kuona mbali kwa Mheshimiwa
Rais, na utayari wake wa kutuongoza bila ya kinyongo na khiana na uzoefu wake
mkubwa katika uongozi wa Serikali ni faraja kubwa kwetu sote na kwangu mimi
binafsi.
119. Mheshimiwa Spika, kwa kauli hiyo hiyo, namshukuru sana
msaidizi wake mkuu, makamu wa pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi nae kwa kutusimamia
na kutuelekeza bila ya kuchoka. Tunajifunza mengi kutoka kwao, muda wote.
Shukran hizi pia ni kwa Baraza la Mapinduzi na Wajumbe wake wote. Utulivu
tunaoupata Wizarani na msaada mkubwa wakati wa maandalizi ya Makadirio haya
hauwezi kwenda bila ya kutambua na kuthamini mashirikiano ya Waheshimiwa
Mawaziri, Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu na Manaibu Waziri wote.
120. Pili, Mheshimiwa Spika, ni wewe binafsi Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid,
Naibu wako Mheshimiwa Mgeni Hassan Juma na Wenyeviti Mheshimiwa Shehe Hamad Mattar
na Mheshimiwa Mwanaasha Hassan Juma. Tunaelewa kazi ngumu ya kuliongoza Baraza
hili. Uweledi wenu umesaidia sana kuleta utulivu wa Baraza kwa kusimamia
wananchi wakiwakilishwa vyema na Wawakilishi wao, Waheshimiwa Wawakilishi
wakiiisimamia vyema Serikali na Serikali ikiwajibika kwa Wananchi kupitia
chombo hichi adhimu. Hakika hii si kazi nyepesi lakini mnaimudu na kuitekeleza
vyema.
121. Mheshimiwa Spika, tatu, naomba nimshukuru sana
Mheshimiwa Mohammed Said (Dimwa) na Waheshimiwa Wajumbe wote wa Kamati ya Kudumu
ya Bajeti ya Baraza lako hili. Tunapata na kuthamini sana mashirikiano makubwa
kutoka Kamati na Mwenyekiti wake. Miongozo na michango yao siku zote inaibua
fikra mpya na za kimaendeleo na tumekuwa tukiipokea na kuifanyia kazi kwa
dhati. Kwa uzito huo huo tunashukuru msaada na uelewa mkubwa wa Kamati ya
Fedha, Biashara na Kilimo na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC). Tunafanya kazi
na Kamati zote hizi, na nyengine zote, kwa maelewano yasioathiri majukumu ya
kila upande.
122. Mheshimiwa Spika, wapishi wa chakula chetu hiki kizuri
cha Makadirio ya Bajeti ni Watendaji. Naomba kumshukuru kwa dhati Katibu wa
Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dkt. Abdulhamid Yahya Mzee, Makatibu
Wakuu na watendaji wote walioshiriki katika maandalizi ya bajeti hii. Michango
na upeo wao umesaidia sana kuyaweka sawa makadirio haya na hivyo kuwezesha
kuwasilishwa Barazani leo hii.
123. Mheshimiwa Spika, pamoja na wote hao, bado kazi kubwa
ya uandaaji wa Makadirio haya imefanywa na Watendaji wa Wizara yangu, ya Fedha
na Mipango wakiwemo wa Tume ya Mipango. Nathamini na kushukuru sana uongozi na
msaada mkubwa wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bwana Khamis Mussa
Omar, Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango - Bwana Juma Hassan Reli, Naibu Katibu
Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango - Bwana Iddi Haji Makame, Mhasibu Mkuu wa
Serikali- Bi Mwanahija Almas Ali, na Kamishna wa Bajeti – Bwana Mwita Mgeni
Mwita. Kupitia kwao, nawashukuru sana watendaji wote wa Wizara, Tume ya Mipango
na Taasisi zilizo chini ya Wizara hususan, kwa mnasaba wa Mapendekezo haya,
Mamlaka ya Mapato (TRA) na Bodi ya Mapato (ZRB).
124. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kushirikiana na
Mataifa na Mashirika mbalimbali. Kwa namna moja au nyengine, mashirikiano hayo
yamesaidia sana katika kuharakisha maendeleo yetu. Kwa niaba ya Serikali ya
Mapinduzi, natoa shukran za dhati kwa nchi za Canada, China, Cuba, Denmark,
Falme za Kiarabu, Finland, India, Ireland, Japan, Korea ya Kusini, Kuwait,
Marekani, Misri, Norway, Oman, Saudi Arabia, Sweden, Ubelgiji, Uholanzi,
Uingereza, Ujerumani na Uturuki.
125. Mheshimiwa Spika, aidha, nashukuru sana msaada na
mashirikiano na mashirika ya: ACBF, ACCRA, AfDB, AGRA, BADEA, CARE
INTERNATIONAL, CDC, CHAI, CIDA, DANIDA, DFID, EGH, EU, EXIM Bank ya China, EXIM
Bank ya Korea, FAO, FHI, GAVI, GEF, GLOBAL FUND, IAEA, ICAP, IDB, IFAD, ILO,
IMF, IPEC, JICA, JSDF, KOICA, MCC, NORAD, OFID, ORIO-Netherlands, PRAP, SAUDI
FUND, Save the Children, SIDA, UN AIDS, UN, UNDP, UNESCO, UNFPA, UN-HABITAT,
UNICEF, UNIDO, USAID, WB, WHO na WSPA.
126. Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa kutoa shukran
maalum. Kwanza, kwa wananchi wote wa Jimbo la Donge. Wakati nipo hapa
nikitumikia wananchi wote wa Zanzibar, sitosahau Imani kubwa ya Wananchi wa
Donge kwangu. Kwa Imani na ridhaa yao ndio walinichagua kuwawakilisha katika Baraza
hili tukufu. Pili, ni shukran kwa familia yangu yote. Kutumikia wananchi mara
nyengine kunamaanisha sio tu kujitolea kwa muhusika, bali pia kunahitaji
ustahamilivu, ufahamu na kujitolea kwa familia nzima. Nashkuru sana uelewa na
ustahamilivu mkubwa wa familia yangu na kuniunga mkono muda wote.
XII.
HITIMISHO:
127. Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema awali, kwa mujibu
wa Katiba yetu ya mwaka 1984 na marekebisho yake, jukumu langu kama Waziri
mwenye dhamana ya Fedha ni kutayarisha na kuwasilisha makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka ujao wa Fedha. Kwa
sasa, mwaka huo ni mwaka 2018/19. Jukumu la kuidhinisha Makadirio hayo ya
Serikali ni la Baraza lako hili la Wananchi.
128. Mheshimiwa Spika, kwa mnasaba huo, na kwa heshima
kubwa, sasa naliomba Baraza lako tukufu liidhinishe Mapendekezo ya Makadirio ya
Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2018/19. Serikali inapendekeza
kukusanya jumla ya Shilingi Trilioni Moja, Bilioni Mia Tatu na Kumi na Tano na
Milioni Mia Moja (TZS 1.3151 Trilioni). Kati ya mapato hayo, mapato ya ndani ni
Shilingi bilioni mianane na saba na milioni Mia Tano (TZS 807.5 bilioni) na
Ruzuku na Mikopo kutoka Nje ni shilingi bilioni mia nne na sitini na saba na
milioni mia sita (TZS 467.6 bilioni) na shilingi bilioni arubaini (TZS 40.0
bilioni) ni mikopo ya ndani.
129. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa matumizi, kwa mwaka
huo wa 2018/19, nina heshima ya kuliomba Baraza lako liidhinishe matumizi ya
Shilingi Trilioni Moja, Bilioni Mia Tatu na Kumi na Tano na Milioni Mia Moja
(TZS 1.3151 Trilioni). Matumizi hayo ni TZS 702.1 bilioni kwa ajili ya kazi za
kawaida na TZS 613.0 bilioni kwa utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo.
130. Mheshimiwa Spika, Naomba kutoa hoja.
Dkt. Khalid S. Mohamed,
WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO,
ZANZIBAR.
20
JUNI 2018.
No comments:
Post a Comment