Habari za Punde

Hotuba ya kuakhirisha Mkutano wa 11 wa Baraza la tiza la wawakilishi




HOTUBA YA MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR, MHE. BALOZI SEIF ALI IDDI ALIYOITOA  KUAKHIRISHA MKUTANO WA KUMI NA MOJA WA BARAZA LA TISA LA WAWAKILISHI TAREHE 04 OKTOBA, 2018


Mheshimiwa Spika, Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwingi wa Rehma kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kufanikisha Mkutano huu wa Kumi na moja wa Baraza la Tisa ulioanza tarehe 19 Septemba, 2018 hadi leo tarehe 4 Oktoba, 2018 tunapouhairisha. Mkutano ambao tumeweza kujadili kwa kina taarifa za utekelezaji wa maagizo ya Kamati za Kudumu za Baraza letu Tukufu, kadhalika tumejadili Miswaada mitatu iliyowasilishwa Barazani pamoja na maswali yaliyoulizwa ambayo yaliweza kujibiwa kwa ufasaha kabisa.
Kwa ujumla shughuli zote tulizojipangia katika Mkutano huu zimeweza kukamilika kwa wakati muafaka na kwa ufanisi mkubwa.

Mheshimiwa Spika, Napenda kutoa pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohamed Shein kwa Uongozi wake mahiri na makini wa kuisimamia vyema Ilani ya Chama cha Mapinduzi pamoja na Serikali yetu ya Mapinduzi ya Zanzibar. Usimamizi wake huo umetuletea mafanikio makubwa ya kupigiwa mfano na sote ni mashuhuda wa hayo.  Kadhalika, nampongeza kwa ziara yake ya kikazi nchini Indonesia ambayo italeta manufaa makubwa ya kuinua uchumi wa nchi yetu katika Sekta ya Uvuvi, Sekta ya Utalii, Sekta ya Kilimo, Biashara na Viwanda, Afya pamoja na masuala ya Ushirikiano wa Kidiplomasia ambayo yameimarisha  uhusiano wetu baina ya Zanzibar na Indonesia, ushahidi wa hayo ni mapokezi mazuri aliyoweza kuyapata kutoka kwa ndugu zetu hao.

Mheshimiwa Spika, Napenda kuchukuwa fursa hii kukupongeza wewe mwenyewe binafsi Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza letu Tukufu, Naibu Spika Mheshimiwa Mgeni Hassan Juma pamoja na Wenyeviti wote wa Baraza kwa kuviendesha vyema vikao vyetu kwa hekima, busara na weledi mkubwa na kukifanya kikao hiki kumalizika kwa amani, salama na mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, Katika kikao hiki jumla ya maswali ya msingi 154 na maswali ya nyongeza ........yaliulizwa na yalijibiwa na Waheshimiwa Mawaziri.  Kadhalika katika mkutano huu jumla ya Miswada mitatu (3) imejadiliwa na kupitishwa kuwa Sheria na Baraza lako Tukufu. Miswada yenyewe ni:-
i        Mswada wa Sheria ya Kuweka Masharti Bora ya Usimamizi wa Mahakama, Kufafanua Utumishi wa Mahakama, Kuanzisha Ofisi za Mtendaji Mkuu wa Mahakama na Mrajis, Kuanzisha Mfuko wa Mahakama na Kuweka Masharti Mengine Yanayohusiana na Hayo.
ii       Mswada wa Sheria ya Kuanzisha Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Elimu na Kuweka Masharti ya Mkaguzi wa Elimu Pamoja na Mambo Mengine Yanayohusiana na Hayo.
iii                Mswada wa Sheria wa Kuanzishwa Wakala wa Serikali wa Uchapaji Zanzibar na Kuweka Masharti Bora Yanayohusiana Na Kazi, Uwezo, Uongozi na Mambo Mengine Yayohusiana na Hayo.

Mheshimiwa Spika, Ni imani yangu kwamba Miswada hiyo mitatu (3) tuliyoipitisha kwa kauli moja itasaidia kuimarisha Utawala bora ikiwemo uwajibikaji kwa watendaji wetu ili kukuza uchumi wa nchi yetu. Waheshimiwa Wajumbe wenzangu, Serikali inaahidi kuwa itaifanyia kazi michango yenu yote mliyoitoa wakati wa kujadili Miswada hii.  Nawaomba wananchi mtoe ushirikiano wenu wa karibu wakati Miswada hii itakapoanza kuwa Sheria.  Tutambue kuwa Sheria siku zote zinatungwa kwa ajili ya kusimamia haki za wananchi wake kwa maendeleo yao na Taifa lao kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika, Katika mkutano huu, Serikali iliwasilisha taarifa za Wizara zote za Serikali kuhusu utekelezaji wa maagizo ya Kamati Saba za Kudumu za Baraza lako Tukufu. Taarifa zenyewe ni kutoka:-

i.       Kamati ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa;
ii.         Kamati ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum;
iii.        Kamati ya Maendeleo ya Wanawake, Habari na Utalii;
iv.       Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo;
v.          Kamati ya Ardhi na Mawasiliano;
vi.         Kamati ya Ustawi wa Jamii;
vii.         Kamati ya Kuchunguza na Kudhibiti Hesabu za Serikali na Mashirika (PAC); na
viii.        Kamati ya Bajeti; 

Mheshimiwa Spika, Ninazishukuru Kamati zote kwa kuzipokea taarifa hizo na Waheshimiwa Wajumbe kupata fursa ya kuzichangia kwa umakini na uweledi ili kuleta ufanisi wa majukumu yetu.  Pia, nawaomba Waheshimiwa Mawazii kuzichukua hoja zote pamoja na mapendekezo yaliyotolewa na Wajumbe wa Baraza na kuzifanyia kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Wawakilishi wenzangu na wananchi wote wa Zanzibar, kwa mara nyengine tena tunatoa mkono wa pole kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wanafamilia na Watanzania wote kwa msiba mkubwa wa kuwapoteza Watanzania wenzetu wapatao 230 kutokana na ajali ya kupinduka kwa kivuko cha M.V. Nyerere huko Kisiwa cha Ukara, Mkoani Mwanza.  Tunamuomba Mwenyezi Mungu aziweke roho za Marehemu mahala pema peponi na wale wote walioumia wapate nafuu haraka.

Mheshimiwa Spika, uzoefu unaonyesha kuwa ajali nyingi zinazotokea nchini zinatokana na uzembe na ukiukwaji wa makusudi wa Sheria za Usalama wa vyombo vya usafiri. Nikiwa Msimamizi Mkuu wa Maafa hapa nchini natoa wito kwa watu wote wenye kumiliki vyombo vya usafiri kufuata sheria zote za usalama wa abiria ili kunusuru maisha ya wananchi wetu na mali zao.

Mheshimiwa Spika, Kama tunavyotambua kuwa mvua za Vuli kwa mwaka huu zinategemewa kuanza kunyesha mwezi wa Oktoba hadi Disemba. Hii ni kwa mujibu wa taarifa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, Kanda ya Zanzibar. Aidha, mvua tutakazozipata zinatarajiwa kuwa na kiwango cha wastani hadi juu ya wastani. Kwa hivyo, tunaomba wananchi kuchukua tahadhari za hali ya juu ikiwa ni pamoja na kuhama maeneo yote hatarishi, kuyatunza mazingira yetu, kushirikiana katika usafishaji wa mitaro ya maji machafu, kufunika karo kwa mifuniko madhubuti, kufuata maelekezo na kanuni zote za afya kama zinavyoendelea kutolewa na wataalamu wetu.  Kadhalika, tunapaswa pia kuwa karibu na watoto wetu wakati mvua zikiendelea ili kuwanusuru na maafa ya kuzama kwenye madimbwi au karo na hatimaye kupoteza maisha yao. Hivyo, tukumbuke wahenga walivyosema “tahadhari kabla l-athari.
Mheshimiwa Spika, Tutambue kuwa jamii inayowadhalilisha na kuwanyanyasa wanawake na watoto haiwezi kupata maendeleo endelevu. Hivyo, unyanyasaji na ukatili wa wanawake na watoto unaoendelea nchini unaweza kutishia amani, kuwakosesha uhuru wanawake na watoto na kuwapunguzia uwezo wa kushiriki kikamilifu katika shughuli zao za kijamii na kimaendeleo.

Mheshimiwa Spika, Vitendo hivi ni vya kinyama na aibu kwa jamii yetu yenye kufuata mila, silka, desturi, na utamaduni wa watu wastaarabu. Hivyo, tunaviomba vyombo vyote vinavyohusika na jamii nzima kuondoa muhali na kuchukua hatua kali za kisheria bila ya kujali dini, rangi, kabila au cheo cha mtu kwani tukumbuke Zanzibar bila ya unyanyasaji na udhalilishaji wa wanawake na watoto inawezekana iwapo kila mmoja wetu atatimiza wajibu wake kwa mujibu wa dhamana aliyopewa.

Mheshimiwa Spika, Kwa mara nyengine tena ninawasihi wananchi waachane na kujihusisha katika Uingizaji, Usambazaji, Uuzaji na Utumiaji wa dawa za kulevya.  Sote ni mashahidi wa athari kubwa zinazosababishwa na dawa za kulevya ambapo kundi kubwa la vijana ambao ndio nguvu kazi inayotegemewa na Taifa imeathirika na dawa hizo.  Serikali inaendelea na jitihada za mapambano dhidi ya dawa hizo na haitomuonea muhali au aibu mtu yeyote atakayeshindwa kutekeleza wajibu wake.  Zanzibar bila ya dawa za kulevya inawezekana, tutimize wajibu wetu. 

Mheshimiwa Spika, Serikali inasikitishwa kuona kwamba kuna baadhi ya Watendaji wasiokuwa waaminifu katika Taasisi zinazoshughulikia masuala ya ardhi ambao hukiuka taratibu za kiutumishi na maadili ya kazi zao na kuwa ni chanzo cha kusababisha migogoro.  Tunashuhudia kuwa kiwanja kimoja kuwa na nyaraka zaidi ya moja, na baadhi ya watendaji huchelewesha kwa makusudi utoaji wa hati za viwanja na kuwapa wasiostahiki na kutaka rushwa.  Vitendo hivi vinaisikitisha sana Serikali na kuitia aibu na lawama kwa wananchi wake.  Hivyo, ninawaagiza na kuwakumbusha Viongozi wenye dhamana wasijihusishe na kadhia hiyo watekeleze na kuwasimamia watendaji walio chini ya dhamana zao, ili kuwaondolea wananchi usumbufu na kuhakikisha kila mtu anapata haki yake kwa mujibu wa sheria na taratibu za ardhi.

Mheshimiwa Spika,
Maadili bora kwa Viongozi wa Umma ni jambo lisiloepukika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar haitakuwa tayari kuwavumilia viongozi wasio na maadili na kuwajibika ipasavyo kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.  Nina imani kuwa Serikali iliyopo madarakani inatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015-2020, ukurasa 234 (185) c kimeeleza:-
Lengo ni kurejesha dhamira ya kuwa na Viongozi wanaotumikia umma kwa maslahi ya umma na si viongozi wanaotumikia ofisi za umma kwa maslahi yao binafsi”
Tunawaomba Viongozi na Watendaji wote wa Umma wenye kutumia rasilimali za Ofisi za Umma kwa maslahi yao binafsi waache mara moja na pia naviomba vyombo vinavyohusika, Tume ya Maadili, ZAECA, Jeshi la Polisi na Vyombo vyengine vyote wasisite kuchukua hatua kwa watendaji hao ili kulinda na kutetea maslahi ya Taifa.
Mheshimiwa Spika, Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu 11(2) kimeandikwa “Kila mtu anastahiki heshima ya kutambuliwa na kuthaminiwa utu wake”.  Pia Baraza lako Tukufu linaendeshwa kwa kuzingatia misingi ya utawala bora ikiwemo uwazi, uwajibikaji pamoja na uhuru wa kuchagua au kuchaguliwa. Naomba nizungumzie kidogo kuhusu uhuru huu wa kuchagua na kuchaguliwa katika Kamati au mambo mengine ya Baraza, tunategemea kila mmoja akimthamini na kumuheshimu mwenziwe hivi ndivyo inavyotakiwa na ndivyo demokrasia ambayo wengi wetu huwa tunaihubiri katika Majimbo yetu.

Mheshimiwa Spika, ni jambo lisilopendeza na halikubaliki kidemokrasia kuwekeana chuki miongoni mwetu kwa sababu ya utekelezaji wa demokrasia hiyo.  Nasaha zangu kwenu tuachane na tabia hii ya kuchukiana na badala yake tujenge mshikamano miongoni mwetu Waswahili wanasema: “Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu”.  Mafanikio ya Baraza letu na Taifa letu yanategemea umoja na mshikamano wetu, Waheshimiwa Wajumbe.

Mheshimiwa Spika, siku za hivi karibuni katika Baraza letu umezuka mtindo wa kuzungumzia mambo binafsi yanayotokea mitaani na kuyageuza kuwa mambo ya kitaifa. Hali hii hatuwezi tukaichia kuendelea kwani inawanyima wananchi fursa ya kuzungumziwa mambo yao ya kimaendeleo yanayowahusu; ambayo yameainishwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Hivyo, tabia hii itakapoachiwa kuendelea tuelewe kuwa Baraza hili litakosa heshima machoni mwa wananchi tunaowawakilisha. Nikiwa Kiongozi wa Shughuli za Serikali ndani ya Baraza hili nasema sitokubali hata kidogo na ni lazima sheria na taratibu zifuate mkondo wake.
Mheshimiwa Spika, matatizo yote ya nchi yetu au watendaji wetu tunaweza kuyazungumza kwa kutumia lugha ya kawaida yenye hekma na busara na ujumbe uliokusudiwa ukafika Serikalini na kuchukuliwa hatua kwa ufanisi mkubwa. Naomba ieleweke kuwa kuzungumzia jambo lolote lile kwa kutumia lugha kali na wakati mwengine iliyobeba matusi haimaanishi hata kidogo unalolizungumzia una uchungu nalo. Na pale unapomtetea mtu kwa kutumia lugha hii ya ukali au matusi pia haionyeshi hata kidogo unayemtetea unampenda sana. 
Mheshimiwa Spika, ni vyema tukakumbuka mafunzo ya dini yetu ambapo Mwenyezi Mungu alimwambia Mtume wetu (SAW) katika Suratul Al – Imran, nanukuu:
         
          Na kama ungekuwa mkali na mwenye moyo
          mgumu bila ya shaka (watu) wangekukimbia”
Waheshimiwa Mawaziri, Wawakilishi Wapendwa na Watendaji wote wa Serikali tutumie lugha njema yenye busara na hekma katika utoaji huduma kwa wananchi au katika kukosoa, kushauri au kutekeleza jambo lolote ikiwa Serikalini au katika jamii, maneno mazuri humtoa nyoka pangoni na pia huleta upendo mapenzi na mshikamano na kufikia malengo tuliyojiwekea.
Mheshimiwa Spika, Wataalamu wanasema: “A civil servant isn’t accountable to the legislature and is not in a position to answer questions. Ministers are responsible and accountable for the affairs of their Department”. Kwa tafsiri isiyokuwa rasmi mtumishi wa serikali hawajibiki kwa Baraza hili na hawezi kujibu chochote endapo kutakuwa na maswali. Badala yake ni Mawaziri ambao wanawajibika kwa matendo yanayofanywa ndani ya Idara zao.  Waheshimiwa Wajumbe wajibu wetu ni kwenda kwa Waziri husika au vyombo vinavyohusika kisheria na kuelezea matatizo na kasoro zilizopo pamoja na ushahidi wake katika utoaji wa huduma au utendaji katika eneo hilo. Naamini Waheshimiwa Wawakilishi, Mawaziri wetu au watendaji wetu watakusikilizeni, na jambo au tatizo litachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi zilizopo.
Mheshimiwa Spika, kabla ya kumalizia hotuba yangu, napenda kuliweka jambo moja bayana ambapo ni hili la kuwaita baadhi yetu kuwa ni Wawakilishi wa Jimbo la Ikulu kama alivyoeleza Mhe. Mohamed Said Dimwa kuwa Ikulu hakuna Jimbo yuko Rais, kwa hiyo, wako Wawakilishi Wateule wa Rais tu. Waheshimiwa Wawakilishi wa nafasi za Rais kuendelea kusema Jimbo la Ikulu tunaweza kuwababaisha wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa mara nyengine tena,     nawashukuru Waheshimiwa Wajumbe kwa kutumia nafasi yao ya Kidemokrasia ya kuisimamia, kuishauri na kuihoji Serikali, jambo ambalo limeonesha nia thabiti mliyonayo ya kuitaka Serikali yenu kuwajibika ipasavyo kwa wananchi wake.  Kadhalika, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kujibu  maswali yote mliyoulizwa, mliweza kuyatolea ufafanuzi ambao uliwanufaisha Waheshimiwa Wajumbe pamoja na wananchi kwa ujumla. Nawaomba Waheshimiwa Wajumbe tuendelee kupendana, kuvumiliana na kushirikiana katika kuijenga nchi yetu kiuchumi na kijamii kwani mshikamano na umoja wetu ndio utakaoivusha nchi yetu kuelekea kwenye maendeleo endelevu.  Aidha, napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ufafanuzi wake alioutoa katika mambo mbali mbali yaliyohitaji ufafanuzi wa kisheria.

Mheshimiwa Spika, Napenda kuwashukuru wale wote waliotuwezesha kukamilisha shughuli zilizopangwa kwenye Mkutano huu wa Kumi na Moja wa Baraza la Tisa la Wawakilishi kwa ufanisi.  Pongezi hizo zaidi ziwafikie Watendaji wote wa Baraza hili la Wawakilishi wakiongozwa na Katibu, Ndugu Raya Issa Msellem.  Ni ukweli usiofichika kwamba tumeanza vizuri na ninaamini tutaendelea vizuri.  Mungu libariki Baraza hili, Mungu zibariki Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Pia nawapongeza Wakalimani wetu wa lugha ya alama ambao wamewawezesha Waheshimiwa Wawakilishi wenye ulemavu wa kusikia kufuatilia yote yaliyokuwa yakiendelea ndani ya Baraza.  Vile vile, nawashukuru Wanahabari kwa kufanya kazi nzuri ya kuwapatia habari wananchi wetu kwa shughuli zote ambazo zilikuwa zikiendelea kufanyika Barazani hapa.

Mheshimiwa Spika, Mwisho kabisa kwa mara nyengine tena nikupongeze wewe binafsi, Mhe. Naibu Spika na Wenyeviti wa Baraza kwa kuliongoza vizuri na kwa ufanisi mkubwa Baraza hili.  Hekima na busara zenu zimesaidia sana katika kuumaliza mkutano huu kwa salama na amani.   Mungu libariki Baraza letu la Wawakilishi, Mungu Ibariki Zanzibar na watu wake, Mungu Ibariki Tanzania.

Mheshimiwa Spika, Baada ya maelezo hayo, naomba sasa kwa heshima na taadhima kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu liakhirishwe hadi siku ya Jumatano tarehe 28 Novemba, 2018, saa 3.00 barabara za asubuhi panapo majaaliwa.

Mheshimiwa Spika, Naomba kutoa hoja.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.