Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein Ayafunga Maonesho ya Kimataifa ya Utalii Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa hafla ya Ufungaji wa Maonesho ya Kimataifa ya Utalii Zanzibar yaliofanyika katika Viwanja vya Hoteli ya Kitalii ya Verde Mtoni Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameridhia Maonyesho ya Utalii Zanzibar yaendelee kufanyika kila mwaka kwa lengo la kuendelea kuitangaza Zanzibar katika sekta ya utalii.

Dk. Shein alitoa kauli hiyo huko katika ukumbi wa Hoteli ya Verde, Mtoni, Mjini Zanzibar katika hafla ya utoaji wa zawadi kwa washindi walioshiriki vyema katika sekta ya utalii ikiwa ni hatua za kukamilisha Maonyesho ya Utalii Zanzibar ya mwaka 2018 yaliaoza tarehe 17 mwezi huu.

Hafla hiyo iliyokwenda sambamba na chakula maalum cha usiku ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Mama Mwanamwema Shein, viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali pamoja na wadau wa utalii wa ndani na nje ya Zanzibar.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alitamka kuwa ameridhia kuendelea kufanyika kwa Maoyesho ya Utalii Zanzibar kila mwaka kwani yana umuhimu mkubwa katika kuitangaza sekta ya Utalii hapa Zanzibar.

Rais Dk. Shein pia, alisisitiza haja kwa Wizara ya Habari, Utalii na Mambo ya Kale kufanya usajili katika Maonyesho hayo kwa kutumia njia za kisasa ili kurahisiha zoezi la shughuli zao hizo.

Aidha, Rais Dk. Shein alikichangia kikundi cha “City Band” ambacho kilitumbuiza katika hafla hiyo kwa kukipa TZS Milioni sita 6 ambapo na Mama Mwanamwema Shein kwa upande wake alikichangia TZS Milioni 4 na kufanya idadi ya TZS Milioni Kumi 10.

Pia, wageni wengine waalikwa walikichangia kikundi hicho kwa fedha taslim pamoja na huduma mbali mbali ikiwa ni pamoja na kutoa nafasi kutumbuiza katika hoteli mbali mbali hapa Zanzibar kwa lengo la kukipa moyo sambamba na kuweza kujiendeleza zaidi.

Akielezea kufurahishwa na Kikundi hicho, Rais Dk. Shein alitoa pongezo zake kutokana na uwezo mkubwa wa wanakikundi wa kuimba vizuri pamoja na kupiga ala kwa ustadi.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alitua fursa hiyo kutoa pongezi zake kwa Wizara ya Habari, Utalii na Mambao ya Kale kwa kufanikisha vyema Maonyesho ya Utalii hapa Zanzibar mwaka huu sambamba na wale wote waliosaidia kufanikisha hafla hiyo adhimu.

Dk. Shein pia, alitoa pongezi kwa mmiliki wa Hoteli ya Verde, Said Salim Bakhresa ambaye amejitolea kufanyika kwa maonyesho katika eneo lake hilo pamoja na hafla hiyo sambamba na uwamuzi wake wa pekee wa kujenga Hoteli hiyo ya kisasa katika eneo hilo ambalo hakuna aliyefikiria kuwa eneo hilo inaweza kuejngwa hoteli kama hiyo ya kisasa.

Alisema kuwa jitihada za mfanya biashara huyo ni kubwa sana na wananchi wa Zanzibar wanafurahishwa na juhudi zake hizo huku akitoa pongezi kwa wageni waliotoka sehemu mbali mbali za dunia ambao wamekuja kwa shughuli hiyo maalum ya maonyesho ya mwaka huu hapa Zanzibar.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliwapongeza Washindi wote waliopata zawadi katika hafla hiyo na kuwaeleza wale ambao mwaka huu wamekosa wasivunjike moyo wajiandae kwa mwakani hasa ikizingatiwa kuwa tayari amesharidhia kuendelea kufanyika kwa maonyesho hayo na miaka ijayo.

Katika kuwatia moyo wale ambao mwaka huu hawakupata nafasi, Rais Dk. Shein alisema kuwa “Mshindi hakati tamaa, na wale wanaokata tama kamwe hawashindi”, mkahawa bora kwa vyakula vya asili ambao ni Lukmaan, Mpishi bora ambaye ni Alankalee Mayaven kutoka Hoteli ya Melia Zanzibar.

Washindi wengine ni mshindi wa Shirika la ndege la ndani ambapo Coastal Aviation alifanikiwa kushinda, Shirika la Ndege la Kimataifa ambalo ni Oman Air, Kampuni bora ya kutembeleza  watalii ambayo ni Fishermen Tours and Travel, Melia Zanzibar iliibuka Hoteli yenye ukumbi bora wa mikutano, Best Western Plus Zanzibar iliibuka Hoteli inayotoa huduma ya makaaze nei nafuu.

Aidha, Hoteli bora katika maeneo ya Mji Mkongwe ni Park Hyatt Zanzibar na Hoteli ya Jaffeji House & Spa iliibuka mshindi wa Hoteli yenye urembo, Gold Zanzibar Beach House & Spa iliibuka Hoteli bora yenye fukwe huru na Park Hyatt Zanzibar iliibuka mshindi wa Hoteli bora yenye kutambulika zaidi, na sehemu yenye urithi ni kisiwa cha Prison Island na Kampuni bora katika kuiunganisha Zanzibar kama kituo cha Utalii ni Costal Aviation.

Nae Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo alitoa pongezi na shukurani wa Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuipa kipaumbe sekta ya utalii sambamba na juhudi kubwa anazozichukua katika kuhakikisha sekta hiyo inaimarika hapa nchini.

Alisema kuwa tukio Maonyesho ya Utalii Zanzibarla mwaka 2018 ni la kwanza kufanyika hapa nchini ambalo limeweza kuwashirikisha washiriki 152 na kuahidi kuwa endapo litaendelea washiriki zaidi wataongezeka ambao ni kutoka ndani na nje ya Zanzibar.

Waziri Kombo alitaja idadi ya waliotembelea katika maonyesho hayo ambao walifikia watu 4020 ambao wengi wao ni wananchi wa Zanzibar huku akitumia fursa hiyo kumpogeza mfanya biashara Said Salim Bakhresa kwa ushirikiano wake mkubwa alioonesha katika kufanikisha maonyesho hayo ya mwaka huu wa 2018 na fursa ya pekee aliyopewa.

Katika maelezo yake, Waziri Kombo alieleza jinsi ya mambo mbali mbali yaliyofanyika katika maonyesho hayo zikiwemo semina mbali mbali zilizowashirikisha wadau huku akitoa pongezi kwa wahisiriki wote wa ndani na nje ya Zanzibar ambapo pia, alipata fursa ya kutoa zawadi kwa washidi wa pili.

Katika hafla hiyo kikundi cha “City Band” kilitumbuiza na kuonesha umahiri wake mkubwa wa kuimba na kupiga ala hali ambayo iliifanya hadhira kushindwa kujizuia kutokana na nyimbo mwanana na zenye mvuto wa pekee.

Hafla hiyo ilihitimishwa kwa urushwaji wa fashfash maalum zilizoandaliwa kwa ajili ya shughuli hiyo katika viwanja vya Hoteli ya Verde ambapo Rais Dk. Shein na viongozi wengine alioambatana nao walijionea mapambo mbalimbali yaliooneshwa huku waalikwa wengi wakifurahia tukio hilo.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.