Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Ajumuika na Wanznchi wa Zanzibar Katika Kisoma cha Hitma Kumuombea Rais wa Kwanza wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akijumuika na Wananchi wa Zanzibar katika dua ya Hitma ya kumuombea Rais wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, iliofanyika katika ukumbi wa Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui Zanzibar leo.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein leo ameongoza hitma ya kumuombea dua Rais wa Kwanza wa Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, iliyofanyika Afisi Kuu ya CCM Kisiwandui mjini Zanzibar.

Hitma hiyo, ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Awamu ya Pili Ali Hassan Mwinyi, Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Sita, Amani Abeid Karume na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd.

Viongozi wengine waliohudhuria katika hitma hiyo ni  Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabhi, Naibu Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Hassan Othman Ngwali, viongozi wa serikali zote mbili na viongozi wastaafu, viongozi wa vyama vya siasa, Masheikh kutoka Zanzibar na Tanzania Bara, Wabunge na Wawakilishi, wananchi kutoka maeneo mbali mbali pamoja na Mabalozi wadogo waliopo hapa Zanzibar.

Hitma hiyo ya kumuombea dua Marehemu Mzee Abeid Amani Karume  ambapo pia, ni miongoni mwa maadhimisho ya Siku ya Mashujaa ilitanguliwa na Qur-an tukufu, iliyosomwa na Ustadh Sharif Muhidin pamoja na hitma iliyohitimishwa na Sheikh Jafar Abdallah kutoka Masjid Noor Muhammad.

Mara baada ya hitma hiyo, Sheikh Fadhil Suleiman Soraga alitoa mawaidha na kumuelezea marehemu Mzee Abeid Amani Karume kuwa ni kiongozi aliyepigania maendeleo ya wananchi wa Zanzibar na kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ampe makaazi mema Peponi.

Katika mawaidha hayo, Sheikh Soraga alisisitiza haja ya kuendeleza na kudumisha amani na utulivu uliopo ikiwa ni miongoni mwa misingi madhubuti iliyoachwa na muasisi wa Mapinduzi Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume.

Aliongeza kuwa hadhara hiyo iliyohudhuria katika kisomo hicho huko katika Ofisi za CCM Kisiwandui mjini Zanzibar ni  udhibitisho wa wazi kuwa Wazanzibari na Watanzania wote kwa jumla wanathamini na wanatambua yale yoteyaliyofanywa na Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume.

“Yeye ndio mkombozi wetu kwani amefanya mambo mengi na sote tuko tayari  kushuhudia mema yote aliyoyafanya hapo siku ya kiama itakapofika mbele ya Mwenyezi Mungu (S.W)”alisisitiza Sheikh Soraga.

Baada ya kisomo hicho cha hitma ambacho hufanyika kila mwaka inapofika tarehe 7, Aprili, viongozi hao na wananchi waliohudhuria katika hitma hiyo walimuombea dua, marehemu mzee Abeid Karume katika kaburi lake lililopo pembezoni mwa afisi Kuu ya CCM Kisiwandui.

Dua hiyo iliongozwa na viongozi wa dini tofauti akiwemo Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Omar Kabhi kwa upande wa dini ya Kiislamu pamoja na Askofu  Charles Lundu kutoka Kanisa la Anglikana Zanzibar.

Viongozi na wanafamilia waliweka mashada ya maua katika kaburi la marehemu mzee Abeid Amani Karume akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Mzee Hamad Ussi Haji aliyeweka shada la maua akiwawakilisha wazee wa CCM.

Wengine walioweka mashada ya maua ni Meja Jenerali Sharif Sheikh Othman aliyeweka shada la maua kwa niaba ya Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Tanzania Jenerali Venance Salvatory Mabeyo, Balozi Ali Karume aliyeweka kwa niaba ya familia ya Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume na Balozi mdogo wa Msumbiji anayefanya kazi zake hapa Zanzibar Jorge Augusto  Menezes aliyewawakilisha Mabalozi wenzake wa hapa nchini.

Aidha, Mama Mwanamwema Shein aliungana na akina mama wengine katika hitma hiyo iliyofanyika katika Afisi ya CCM Kisiwandui, akiwemo mjane wa marehemu mzee Abeid Karume, Mama Fatma Karume,  Mama Shadya Karume na viongozi wengine wanawake wa kitaifa wakiwemo Mawaziri, Wabunge, Wawakilishi, viongozi wakuu wa vyama vya siasa na wananchi kutoka maeneo mbali mbali ya Zanzibar na Tanzania Bara.

April 7, 1972 ndiyo siku aliyouawa Rais wa Kwanza wa Zanzibar marehemu Mzee Abeid Amani Karume na wapinga maendeleo nchini ambapo hivi leo imetimia miaka 47 tokea utokee msiba huo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.