Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akiwahutubia Wahitimu wa Mahafali ya 14 ya SUZA katika Ukumbi wa Mkutano wa Dk. Ali Mohamed Shein, Tunguu leo wakati wa hafla hiyo.
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Chuo Kikuu cha Taifa (SUZA) kina
dhima kubwa ya kutoa taaluma bora inayoambatana na kufanya tafiti kwa lengo la
kuzipatia ufumbuzi changamoto zilizomo katika jamii.
Dk. Shein ambaye pia
ni Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) aliyasema hayo leo katika Mahafali ya 14 ya Chuo Kikuu hicho yaliyofanyika katika
ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein uliopo ndani ya Kampasi ya Chuo hicho kiliopo
Tunguu, Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.
Rais Dk. Shein alisema
kuwa kufanya tafiti mbali mbali ni miongoni mwa majukumu ya msingi ya vyuo
vikuu jambo ambalo hutoa mchango wa chuo kitaaluma na kupandisha hadhi ya ubora
wa chuo chenyewe.
Alikihimiza Chuo Kikuu
hicho kiendelee kushirikiana na Tume ya Sayansi na Teknolojia ya Tanzania
(COSTECH), ambayo ina wajibu wa kuwawezesha watafiti mbali mbali Tanzania Bara
na Zanzibar kufanya tafiti wanazozikusudia.
Dk. Shein aliongeza
kuwa Chuo Kikuu hicho kina wajibu wa kutafuta fedha za kufanya tafiti kutoka
vyanzo mbali mbali kwani utafiti ni miongoni mwa majukumu ya chuo hicho hasa
ikizingatiwa kuwa hakuna maendeleo bila ya utafiti.
Alieleza kuwa utafiti
ni ngazi muhimu kwa Wanachuo wa mafunzo ya Uzamili na Uzamivu ambao huwasaidia
kuhitimu masomo yao, na kukihimiza chuo hicho kujiandaa kuchapisha majarida ya
kitaaluma ambayo wahadhiri na wanachuo wa ngazi ya Uzamili na Uzamivu watapata
fursa ya kutuma makala zao zinazotokana na tafiti walizofanya.
Aidha, Rais Dk. Shein
aliutaka uongozi wa Chuo hicho kuwaweka sawa baadhi ya wahadhiri wachache ambao
hawatekelezi majukumu yao ipasavyo pamoja na wafanyakazi wote wanaojaribu
kufanya kazi zao kinyume na utaratibu.
Alisema kuwa
Wahadhiri, walimu na wafanyakazi wa namna hiyo hawatimizi wajibu wao vizuri na
hawachagii maendeleo ya Chuo kwani wafanyakazi wa namna hiyo hawana uzalendo “Si
wazalendo na hawastahiki wajigambe kuwa ni wahadhiri wa SUZA. SUZA ni chuo cha
watu wenye kuyapenda maendeleo ya viongozi wa baadae”,alisisitiza Dk. Shein.
Alisisitiza kuwa ili
mafanikio yapatikane ni vyema kukadumishwa umoja na mshikamano uliopo baina ya
wahadhiri, wafanyakazi, wanafunzi na washirika wote wa chuo hicho huku
akiwataka kujiepusha na mambo yanayoweza kuleta mifarakano.
Rais Dk. Shein
alieleza mategemeo yake kuwa uongozi wa
Wizara ya Afya utaendelea na utaratibu wa kuwaajiri madaktari wazalendo kwa
kushirikiana na Tume ya Utumishi Serikalini kwa lengo la kuzimarisha huduma za
afya ikiwemo kupunguza tatizo la uhaba wa madaktari katika hopsitali za hapa
nchini.
Alitumia fursa hiyo
kuipongeza Wizara hiyo ya Afya kwa kutekeleza agizo lake alilowataka
wahakikishe kuwa Hospitali ya Mnazi Mmmoja inatumika kwa kufanya mafunzo ya
mazoezi ya madaktari wanaohitimu yaani “Internship” kama ilivyoamuliwa tangu
mwaka 1977.
Akitoa nasaha zake Dk.
Shein alisisitiza haja ya kuitumia vyema rasilimali ya kuandaa wataalmu wa
Shahada za Juu za Lugha ya Kiswahili kwa kuwashirikisha Wazanzibari wanaoishi
nchi za nje kuweka mikakati maalum ya kuikuza lugha ya Kiswahili na kubainisha
uwezo wa kuwafundisha watu wa mataifa mengine.
Rais Dk. Shein
aliwataka wahitimu na wataalamu wa Kiswahili kufanya jitihada ili wajiandae kwa
kuzitafuta fursa zilizopo za mahitaji ya wataalamu wa Kiswahili badala ya kukaa
na kusubiri Serikali kwuatafutia fursa hizo.
Dk. Shein alitoa
pongezi kwa Chuo Kikuu hicho kwa mwaka
huu wa masomo ambapo Chuo Kitazindua udahili wa programu mpya mbili katika
ngazi ya Shahada ambazo ni Shahada ya Sayansi ya Uuguzi (DSc. Nursing) na
Shahada ya Sayansi za Kilimo.
Pia, Rais Dk. Shein
alieleza kufurahishwa kwake kwa kusikia taarifa za Makamu Mkuu wa Chuo hicho
kuwa upo mpango wa kuyafanyia matengenezo makubwa majengo ya Chuo kwa asilimia
75 na kujenga majengo mapya 12 ambapo Serikali imejiandaa kutekeleza Mpango huo
ili ufanikiwe.
Dk. Sheinj aliongeza
kuwa uongozi wa Chuo ni vyema ukaongeza kasi katika kufuatilia utekelezaji wa
Nyaraka za Maelewano (MoU) wanazoingia na Taasisi nyengine kwani chuo hicho
kimekwua kikishirikiana na vyuo mbali mbali duniani na kutiliana saini za
Maelelewano katika kushirikiana huko.
Alisisitiza kuwa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kutimiza wajibu wake ili iweze
kuyafanikisha malengo yaliyowekwa kwa kutumia fedha za Bajeti na mipango
mengine ambayo imeungwa mkono na nchi marafiki na washirika wa maendeleo.
Aidha, Dk. Shein
aliuhimiza uongozi na wanachuo wa Chuo Kikuu hicho kuendeleza masuala ya
michezo pamoja na uendelezaji wa midahalo kwani masuala hayo ni muhimu katika
vyuo kwa lengo la kuimarisha afya za wanachuo na kuwaongezea maarifa na masuala
mbali mbali ya kitaaluma.
Pia, Dk. Shein
aliwahimiza wahitimu wa Mahafali hiyo kuzichangamkia fursa zilizoandaliwa na
Serikali kupitia Mfuko wa Uwezeshaji Kiuchumi na Mipango mengine ili waweze
kujiajiri wenyewe na kuwataka kuwa na ndoto kubwa zaidi ya kujiajiri kuliko kusubiri
kuajiriwa na Serikalini.
Alieleza kuwa matajiri
na watu maarufu zaidi duniani wengi wao ni watu waliojiajiri wenyewe kwa
kujishughulisha na biashara, sanaa, michezo na shughuli mbali mbali za
ujasiriamali ambapo na wao wakiamua wanaweza kuwa miongoni mwa watu hao.
Katika Mahafali ya
mwaka huu ya Chuo Kikuu hicho zipo jumla ya fani za masomo 56 zenye wahitimu
1940 ambapo asilimia 58 ya wahitimu wote ni wanawake na asilimia 42 wanaume
ambapo pia kwa mara nyengine tena mwanamke ametokea kuwa mwanafunzi bora.
Nae Makamu Mkuu wa
Chuo cha (SUZA), Profesa Idrisa Rai, alisema
kuwa mahafali ya mwaka huu yameandika historia mpya kwa Chuo hicho kwa kutoa
wahitimu wa fani ya Udaktari hapa nchini.
Alisema kuwa
uanzishaji wa masomo hayo ni utekelezaji wa agizo la Rais Dk. Shein alilotowa
katika mahafali ya mwaka 2011 kwa lengo la kuhakikisha Zanzibar inajitegemea
kuwa wataalamu wa fani hiyo.
Nae Katibu Mkuu Wizara
ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Dk. Idrissa Muslim Hija kwa niaba ya Mwenyekiti
wa Baraza hilo, alisema kuwa mahafali ya mwaka huu yamepanua wigo kwa kuongeza
fani mbili zaidi tofauti na mwaka uliopita.
Dk. Idrissa alitumia
fursa hiyo kuwapongeza washirika wa maendeleo kwa juhudi na mchango wao mkubwa
katika kukiendeleza Chuo hicho kupitia nyanja tofauti.
Alizitaja taasisi na mashirika
hayo kuwa ni pamoja na Milele Foundation, UNICEF, World Bank, NORAD, DANIDA,
HUAWEI, Ubalozi wa Uturuki, Serikali ya Watu wa China pamoja na Falme za
Kiarabu.
Nae Waziri wa Elimu na
Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma aliipongeza Serikali wka juhudi kubwa
inazoendelea kuchukua katika kuiendeleza sekta ya elimu nchini, ikiwemo ya
Elimu ya Juu.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment